Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Sunday 13 October 2013

WEWE NI MTUMWA WA NGONO?!

Picha kwa hisani ya enrichmentjournal.ag.org


Ngono: Ni neno linalozungumzia kwa mapana mambo mengi yakiwemo kutazama picha za ngono, kujichua (masturbation) na mambo mengineyo. Lakini kwa baadhi ya Waamerika, wingi wa ngono katika utamaduni wao umekuwa mtego, ambao ni mgumu kuukwepa.

Mwandishi wa habari wa CBN, Gailon Totheroh, anatuambia jinsi uambukizo wa watumwa wa ngono unavyoweza kuwafanya waathirika wakajidhuru na namna Mungu anavyoweza kuleta matumaini mapya.
Utumwa au uraibu wa ngono (sexual addiction) - baadhi wanauita ugonjwa uliojificha. Wengine wanauita "dhambi isiyozungumza."
Wakati watu wengi huweka taswira ya wanyama waliopagawishwa na mapenzi, ukweli wa utumwa wa ngono uko tofauti. Wengi wa waathirika siyo wahalifu kifikra na siyo kwamba wazembe.
Ni nani hawa watumwa wa ngono? Jibu linaweza kukushangaza. "Utumwa wa ngono huathiri mipango yote ya maisha," anasema Dk. Douglas Weiss, Mmarekani ambaye ameegemea zaidi katika ushauri wa watumwa wa ngono. "Nina watu wengi sana, wengine ni wanafunzi wa seminari, madaktari, maseneta na wanamichezo. Hebu fikiria mwenyewe wengine, wataalamu wa mahesabu wenye CPA zao, mafundi wa kompyuta - mtu yeyote anaweza kuwa mtumwa wa ngono, kwa sababu ndiyo njia ambayo tumekuzwa nayo tangu tukiwa watoto na tuliendelea nayo mpaka kwenye balehe. Siyo inatokea wakati tukiwa na umri wa miaka 40."
Na wengine wanasema kwamba hiyo ndiyo sababu watu wasishangae kuhusu kashfa za ngono zinazotokea kwenye Ikulu ya nchi hiyo (White House).
Dolly Kyle Browning, muathirika ambaye alisoma darasa moja na Bill Clinton, rais mstaafu wa Marekani, katika shule ya juu kabla ya kwenda chuo kikuu. Mwanamke huyo anasema kwamba walikuwa na uhusiano wa kimapenzi kwa miaka 30 na kwamba mnamo mwaka 1988, aliwahi kuzungumza naye kuhusu uraibu wa ngono.
"Hivyo nikamuuliza, utumwa huu wa ngono umehatarisha malengo yako ya maisha na yeye alihuzunika sana na huo ndio ulikuwa ukweli, lakini bila kuliacha hilo lielee, nikamwambia, 'Umeshawahi kufikiria kwamba unaweza kuwa mtumwa wa ngono?' " anakumbuka Browning. "Naye akaitikia kwa kutikisa kichwa na kusema, 'Najua mimi ni mtumwa wa ngono na ninajitahidi kushinda.' "
Katika kadhia yake ya kujisalimisha kwa Paula Jones, Bill Clinton alikana katu katu kwamba hajawahi kuwa na uhusiano wa kimapenzi na Browning na kutokana na namna alivyojitetea, inaonekana kwamba Wamarekani hawako tayari kuafiki tuhuma hizo. Lakini Browning anaamini kwamba wastani wa Wamarekani wengi hawajui utumwa wa ngono unajihusisha kwa namna gani.
"Kama wangepambana na kweli wote, kitu ambacho ni kugumu kuliko kawaida, mawazo yao yangeasi," anasema mwanamke huyo ambaye tayari amekwishapatiwa tiba ya utumwa wa ngono. "Hawaelewi chochote, lakini sasa mwathirika wa ngono anaelewa, na kwa mtu wa kawaida, tabia hii inaonekana kuwa mbali sana na haisadikiki, hawawezi kusadiki."
Ukweli kwamba waathirika wengi wa utumwa wa ngono ni watu wenye familia zao, kazi zao na hata ni waumini ama viongozi wa dini unaweza kuwashangaza watu wengi na kuleta matatizo makubwa kwa wahusika wenyewe na jamii kwa ujumla.
Fikiria, unaweza kumkuta baba mzima mwenye familia yake na fedha zake akitangatanga na watoto wadogo, tena wale wa shule, huku akimwacha mama watoto wake akiwa hajui lolote. Mama mzima mwenye fedha na maisha ya hali ya juu, anamwacha mumewe na kutafuta vijana ili wakidhi kiu yake ya mapenzi, kwa madai kwamba mumewe amechoka na akifika mshindo mmoja yuko taabani kabisa! Vijana wanakwenda kujiunga na kwaya kanisani kwa sababu tu ya kumpata binti fulani, na wengine hufikia hata hatua mbaya zaidi kwa kuamua kutangaza wameokoka ili wawe karibu tu na msichana mwenye msimamo anayemcha Mungu kwa bidii. Mapadre wanasema kwamba hawaruhusiwi kuoa, lakini kutokana na utumwa wa ngono unaowasakama utakuta ama wanafanya mapenzi na watawa wa kike au kutafuta wanawake wa pembeni, na tayari kuna mashauri mengi hapa Tanzania ya aina hiyo. Wapo wachungaji wengi wa Kondoo wa Bwana ambao wamekwishashikwa ugoni ama wakiwa na wake za watu au wake zao kuwafumania na wahudumu wa kanisa. Wapo mashekhe ambao pamoja na kuwa na wake wanne kama dini ya Kiislamu inavyoelekeza, lakini utakuta wana vimada zaidi ya sita mitaani!
"Ni ule upande wenye giza," anasema Weiss. "Ni upande ule wa kuzifurahisha tamaa zao za mwili ambazo zimetengana na fikra zao za kawaida, mpaka watakapokamatwa au kufumaniwa au kitu fulani kilete dunia hizi mbili pamoja na kuleta mgongano."
Kwa upande wa Jerry, utumwa wake wa ngono ulitokana na mambo mengi: makahaba, picha za ngono, klabu za usiku ambako wanawake wanacheza uchi na kupendelea kuchukua wanawake tofauti kila siku, ambao kwa Kiingereza wanaitwa (one-night stands). Lakini utumwa wa ngono haumaanishi kwamba mpaka ufanye mapenzi na mtu mwingine. Unaweza kuwa unajichua mwenyewe, kutazama picha na sinema za ngono na mambo mengine.
Baraza la Taifa la Utumwa wa Ngono la Marekani (National Council on Sexual Addiction) linaielezea hali hiyo kama tabia za mapenzi zinazozidi na kuhamasisha zaidi.
"Kwamba mtu hatimaye huanzisha uhusiano na tabia hiyo na wataifanya tabia hiyo katika kuleta madhara makubwa," anasema Dk. Deborah Corley wa Sante Center mjini Dallas.
Mwathirika "ataendelea kufanya ngono nje" pamoja na uwezekano wa kuipoteza familia yake au kupoteza kazi. Waathirika mara nyingi hupoteza maelfu ya fedha katika vitendo vyao, wakiziacha familia zao zikiteseka kwa kukosa msaada wa kifedha. Nyumba ndogo, kama wenyewe wanavyoita, hutaka kutimiziwa haja zao haraka sana bila kujali hali ya kipato ya mwanamume husika, na matumizi yao mara nyingi ni makubwa kuliko ya nyumbani kwako. Waathirika mara nyingi hupenda kutumia fedha ili kununua mapenzi na kuwaonyesha hao vimada kwamba wanawajali, lakini wakisahau kwamba huko nyumbani moto unawaka na paka kalala mekoni! Aibu na hatia huchukua nafasi haraka katika raha zao na baadaye huanza kujilaumu kwa vitendo hivyo, ambavyo hata hivyo huwa ni vigumu kwao kuviacha.
"Aibu, hatia ya kufanya mambo niliyokuwa nikiyafanya vilikuwa havielezeki," anasema Jerry. "Njia pekee ambayo niliifahamu katika kukabiliana na aibu, hatia na maumivu ni kuendelea kufanya vitendo hivyo."
"Ukitambua kwamba ni kitu ambacho hupaswi kukifanya," anasema Browning. "Ukitambua kwamba siyo vizuri kwako - ni kitu ambacho hakika ni vigumu kukiacha. Najua inaonekana kama uendawazimu, hakika ni uendawazimu."
Uga wa saikolojia umekuwa mgumu kukubali kwamba utumwa wa ngono ni uraibu kama ilivyo kwa pombe na dawa za kulevya, lakini wataalamu wanasema unaweza kubomoa maisha ya watu katika njia na kiwango kile kile kama pombe na dawa za kulevya.
"Utumwa wa ngono siyo ni kiasi gani au mara ngapi mtu anafanya mapenzi," anasema Weiss. "Utumwa wa ngono ni kuhusu mtu fulani kutumia mapenzi ili kukidhi haja zake za kiakili. Wanatumia kama kimbilio - kupambana na msongo wa mawazo. Wanatumia kupambana na maumivu yaliyopita. Wanatumia ili wapendwe - wakubalike. Wanakimbilia kwenye ulimwengu wa kufikirika badala ya ulimwengu halisi. Ni kama kuwa katika ukuta wa kioo. Naweza kuuona ulimwengu, lakini huwezi kuugusa na wala wenyewe hauwezi kukugusa. Na hivi ndivyo ulivyo utumwa huu."
"Unataka kuafikia watu, lakini huwezi," anasema Terry, ambaye zamani alikuwa mwathirika. "Unakuwa umekwama na unajiona kama maisha yako yamepotea na ubomolewa."
Ni kitu gani kinachosababisha utumwa huu? Kama uraibu mwingine, wanasaikolojia wengine wanaamini kwamba ubongo wa baadhi ya watu umeachiliwa huru kwa ajili ya uraibu, iwe pombe, dawa za kulevya chakula au ngono.
Tatizo jingine kubwa ni unyanyasaji wa kimapenzi, ambao tutauona huko mbele. Asilimia 82 ya waraibu wa ngono wameshawahi kunyanyaswa kimapenzi wakati wakiwa watoto. Deborah Corley, mkurugenzi wa The Sante Center mjini Dallas, Texas, anasema waathirika wanaweza kuwa wanajaribu kutanzua mkanganyiko unaozunguka manyanyaso hayo.
Tiba za uraibu wa ngono, kama ni nilivyoelezea hapo awali, zipo za aina nyingi. Kuna Programu ya Hatua-12 kama Sexaholics Anonymous au Freedom Groups ya Doug Weiss ambazo zinawasaidia waathirika kupambana na tatizo hilo na kuishi maisha ya uponaji na matumaini.
Baaa ya kujaribu kwa miaka kadhaa uacha baadhi ya utumwa wake, Dolly Kyle Browning alipata msaada wa kiroho mwaka 1998.
"Niliamka asubuhi moja na kusema, 'Hii inatosha: unatakiwa kuamua.' Utaendelea kuishi maisha ya kumpendeza Mungu au utaendelea kufanya mambo yale yale? Punguza," anakumbuka. "Ndiyo, natakiwa kuwa na bwana mmoja na, unafikiria kuolewa. Bado siyo sahihi."
Na Dolly, kama walivyo watu wengi wenye tatizo kama lake, walikuja kutambua kuhusu Mungu. "Nilitambua kwamba Alikuwepo muda wote. Nilikuwa ninafanya mambo mengine tofauti."
"Ni kama ukombozi wa kudumu," anasema Terry. "Nina matumaini makubwa sana, hata pamoja na hofu ambayo nimekuwa nikipambana nayo. Ninaona Mungu akiendelea kunivuta nitoke na hakika naona kama kuna matumaini makubwa ya baadaye nikiwa Naye."
Tutaendelea na mjadala…
Niandikie: brotherdanny5@gmail.com

No comments:

Post a Comment