Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Wednesday 30 October 2013

WAKALA WA NYUMBA BORA ULIVYOJIZATITI


Mkuu wa Kitengo cha Mbinu za Ujenzi toka Wakala wa Taifa wa Utafiti wa Nyumba Bora na Vifaa vya Ujenzi(UNHBRA) Mhandisi Amri Juma akieleza kwa waandishi wa habari(hawapo pichani) namna wakala hao unavyosaidia kutoa elimu ya ujenzi wa nyumba bora,wakati wa mkutano uliofanyika katika ukumbi wa Idara ya Habari(MAELEZO) Leo Jijini Dar es Salaam.Kushoto ni Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Habari na Masoko toka Wakala hao Bw. Frimin Lyakurwa. Picha na Fatma Salum-MAELEZO

1.0 UTANGULIZI

NHBRA ni Wakala wa Taifa wa Utafiti wa Nyumba Bora na Vifaa vya Ujenzi (National Housing and Building Research Agency – NHBRA) ambao ulianzishwa kwa Sheria ya Wakala za Serikali Namba 30 ya Mwaka 1997 na kuanza shughuli zake rasmi 01 Septemba mwaka 2001. Wakala huu uko chini ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi.

NHBRU ilikuwa ni Kituo cha Utafiti wa Vifaa vya Ujenzi (Building Research Unit) ndani ya (Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi).

NHBRA inafanya kazi za utafiti pamoja na ushauri na ukandarasi katika kuwapatia wananchi wa Tanzania wenye kipato cha chini nyumba na makazi bora kwa gharama nafuu na ya kudumu ili kutimiza malengo ya MKUKUTA pamoja na malengo ya Maendeleo ya Mlenia (MDGs) Ambayo yanasimamiwa na UNHABITAT.

1.1       Dira
Kuwa kituo cha ufanisi uliotukuka katika nyumba za gharama nafuu na teknolojia ya uboreshaji makazi ya binadamu ifikapo Mwaka 2025.

1.2       Dhima
Kuwapatia watanzania huduma bora za vifaa na teknolojia ya ujenzi wa Nyumba Bora za Gharama nafuu kwa kutumia ubunifu ili kukidhi mahitaji ya wateja hivyo kuinua hali ya maisha kwa kila mtanzania.

2.0              JUKUMU KUU LA NHBRA
Kutafiti, Kukuza, Kushauri na Kushawishi Ujenzi wa NYUMBA BORA za Kudumu na za GHARAMA nafuu ili kuinua na kuboresha viwango vya nyumba pamoja na kuongeza ubora wa maisha ya wananchi vijijini na mijini. Mabadiliko hayo yamefanyika ili kuongeza ufanisi katika kuhudumia wateja.

3.0       MAJUKUMU YA WAKALA
Majukumu ya NHBRA kama Wakala wa serikali ni haya yafuatayo:
·         Kutafiti, kukuza, kushauri na kushawishi juu ya ujenzi wa nyumba za kudumu na za gharama nafuu ili kuinua na kuboresha viwango vya nyumba ili kuongeza ubora wa maisha ya wananchi vijijini na mijini kwa ujumla.
·         Kuhakikisha kuwa matokeo ya tafiti zake pamoja na habari za kitaalam kuhusu makazi vinapatikana kwa wananchi kwa wakati.
·         Kukuza na kuendeleza matumizi ya vifaa vya ujenzi vipatikanavyo katika maeneo ya ujenzi pamoja na teknolojia ya nyenzo za ujenzi wa nyumba bora zinazolinda mazingira.
·         Kuongeza mbinu za utaalam wa ujenzi wa nyumba bora za gharama nafuu.
·         Kutoa huduma bora za ushauri kuhusu ujenzi wa nyumba.

4.0 MAANA YA NYUMBA BORA
Tafsiri kuhusu nyumba bora ni nyingi na wakati mwingine hutatanisha. Hata hivyo wataalamu wengi wanakubaliana kuwa ufafanuzi sahihi wa nyumba bora sharti ujumuishe sifa zifuatazo:

  • Imara na ya kudumu
Nyumba bora haina budi kuwa imara na ya kudumu kutegemeana na uwezo wa kifedha. Uimara wa nyumba hutegemea sana vifaa vilivyotumika kujengea na pia uelewa wa ufundi uliotumika.

Ufundi duni unaweza kuifanya nyumba iliyojengwa kwa vifaa madhubuti na ghali isiwe imara. Ni vizuri kuhakikisha vinatumika vifaa bora vya ujenzi kwa kujenga nyumba bora.

Nyumba imara hudumu kwa muda mrefu zaidi. Faida za nyumba bora, imara na ya kudumu ni:
i)        Huokoa fedha na muda kwa kutoifanyia matengenezo na ukarabati wa mara kwa mara, (Nyumba yoyote ikichakaa kupita kiasi ni lazima kujenga nyingine).
ii)      Huhimili misukosuko mingi na kuwafanya wakazi wake wawe na usalama zaidi.

  • Gharama nafuu
Nyumba bora na ya gharama nafuu ni ile mtu anayoweza kuijenga au kununua kulingana na kipato chake. Iwapo gharama zitakuwa kubwa mno ni wazi kuwa dhana ya nyumba za gharama nafuu haitakuwepo. Ni vyema basi jitihada zifanyike ili kupunguza gharama zote zisizo za lazima kwa kutumia vifaa vinavyopatikana katika sehemu ya ujenzi pamoja na teknolojia yake.

  • Kukidhi mahitaji
Nyumba bora lazima iwe na uwezo wa kukidhi mahitaji na shughuli za kila siku katika maisha ya binadamu. Nyumba ni mahala pa kulala, kupikia, kula chakula, kupumzika, kustarehe na shughuli nyingine kama kusoma, kucheza, kuabudu, kuzaa, na kulea watoto. Nyumba hutumika kwa kuhifadhi vitu, kulinda siri na kutoa faragha inayotakiwa. Kutokana na hayo, ni muhimu kuwa na picha kamili ya nyumba unayotaka kujenga  kabla ya kuanza ujenzi kwa kuzingatia shughuli mbali mbali zitakazofanyika ndani yake.

  • Masharti ya kanuni za afya
Afya bora ni sharti muhimu kwa maisha ya binadamu. Nyumba mbovu au ujenzi mbovu wa nyumba unaweza kuathiri maisha na afya ya watu wanaoitumia. Kwa mfano nyumba ambazo sakafu, kuta, na paa zake zinakuwa na unyevunyevu kila wakati zinaweza kuhatarisha afya ya watumiaji. Ni vizuri nyumba iwe na madirisha ya kuingiza na kutoa hewa pamoja na mwanga wa kutosha. Nyumba ambazo hali ya hewa ya ndani aidha ni baridi au joto sana nazo pia huweza kuathiri afya za watumiaji.

Pamoja na hayo yote nyumba bora haina budi iwe na choo safi. Mara nyingi watu husahau kuwa choo ni sehemu ya nyumba. Nyumba kama haina choo inakuwa haijakamilika na hivyo kutostahili kuitwa nyumba bora. Ni muhimu sana kuwepo choo ndani au nje ya nyumba kutegemeana na mchoro wa nyumba na uwezo wa mtu. Hili linatakiwa lizingatiwe tangu awali ili kukidhi masharti muhimu ya afya.

  • Kuheshimu mila na desturi
Nyumba bora lazima itilie maanani mfumo wa maisha ya watu, yaani ikidhi mila na desturi za watumiaji. Kwa mfano nyumba za watu wa maeneo ya pwani hazina budi ziwe na baraza ya mbele kwa ajili ya wanaume kupumzika na kuongea, na sehemu ya uani kwa ajili ya akina mama kufanyia shughuli zao. Pia kuna makabila mengine hayashirikiani vyoo na wakwe au watoto n.k, Hayo lazima yazingatiwe katika usanifu na ujenzi wa nyumba.

  • Hali ya kuvutia, kupendeza na kumpa raha mtumiaji
Nyumba bora lazima iwe ya kupendeza kwa mtumiaji, na hata watu wengine wanaoiona. Hii itatokana na kusanifiwa, kujengwa vizuri na kutunzwa vizuri. Ni vema kutumia ushauri wa wataalam wa usanifu majengo, wahandisi na hata wakadiriaji gharama za ujenzi. Wataalam hawa na wengineo wapo NHBRA, taasisi za ujenzi na makampuni mengine.

  • Rasirimali na kitega uchumi
Nyumba bora ni kitu cha thamani kwa kuwa inaweza kuwa kitega uchumi. Hii ni pale ambapo mmiliki anaweza kupangisha na kupata pesa kutokana na kodi inayolipwa na mpangaji, au mwenye nyumba kuishi kwenye nyumba yake na kuepuka gharama za kulipa kodi kama angekuwa amepanga nyumba kwa mtu mwingine. Pia nyumba inaweza kutumika kama rehani unapotaka kuchukua mkopo kutoka katika benki, hata kuuzwa kwa ajili ya mahitaji ya haraka.

5.0 VIFAA VYA UJENZI VYENYE GHARAMA NAFUU
Katika ujenzi wa nyumba, gharama ya vifaa huchukua takribani asilimia 70 ya gharama za nyumba. Hii ni pamoja na kuwa vifaa vya ujenzi ni vizito na usafirishaji wake mpaka sehemu za ujenzi ni ghali. Tafiti zilizopo zimeonyesha kuwa katika baadhi ya maeneo tunayojenga tunaweza kutumia malighafi zilizopo eneo la ujenzi pamoja na utaalamu wa malighafi na hivyo kupunguza gharama za usafiri wa vifaa na hatimaye kupunguza gharama za ujenzi.
Vifaa bora na vya kudumu ambavyo vinapatikana katika maeneo tunamoishi ambavyo vyanzo vyake vimeshafanyiwa uchunguzi ili kuweza kuwa na utaratibu mzuri wa ununuaji, usafirishaji, uhifadhi na utumiaji na pia utumiaji wa teknolojia rahisi na sahihi kwa mpangilio mzuri wa utekelezaji wa shughuli zote za ujenzi hupunguza gharama za ujenzi kwa kiasi kikubwa.

6.0 VIFAA BORA VYENYE GHARAMA NAFUU VILIVYOTAFITIWA NA NHBRA
Matofali ya kufungamana ya udongo-saruji: Ni matofali yanayotengenezwa kwa kutumia udongo ambao huchanganywa na saruji kwa kiasi kidogo ili kuuimarisha udongo, kisha kuyafyatua kwa kutumia mashine maalum ili kupata umbo la kufungamana. Ni vizuri kutambua udongo wako na vipimo vya saruji inayohitajika.
Vigae vya kuezekea: Vigae hivi hutengenezwa kwa kutumia mchanganyiko wa mchanga, saruji na nyuzi za katani ambazo hukatwa kwa urefu wa sentimita 2-3 kisha mchanganyiko huu huwekwa katika mashine ya kutengenezea vigae ambayo huendeshwa kwa betri ya gari. Kwahiyo mashine hii inaweza kutumika hata katika maeneo yasiyo na umeme hususani vijijini.

7.0 KAZI ZILIZOFANYIKA NHBRA
(i)           Kuvielekeza vituo vya uzalishaji na urekebishaji wa mashine zinazotumika katika uzalishaji wa vifaa vya Ujenzi vipatikanavyo hapa nchini.

·      Mashine 81 za kufungamana zilitengenezwa katika Kituo cha NHBRA kwa kushirikiana na MM Foundry kwa kipindi husika.

(ii)         Kuendesha semina za uhamasishaji wa ujenzi wa nyumba bora za gharama nafuu katika wilaya tatu.

·      Semina za uhamasishaji wa ujenzi wa nyumba bora za gharama nafuu zilifanyika kwa viongozi wa Wilaya ya Arusha Vijijini na kwa vijiji vya Engorora watu 23 na Likamba watu 27

·      Semina za uhamasishaji zilifanyika mkoani Tabora, katika kata kumi (10) ambazo ni Isevya, Ipuli, Mtendeni, Ng`ambo, Kanyenye, Chemchem, Cheyo, Kariakoo, Kiloleni na Tambukareli

·      Pia Biharamulo Mkoani Kagera kuzunguka mgodi wa Tulawaka.

·      Mafunzo kwa vitendo yalifanyika Mkoa wa Tabora, wilaya ya Tabora Mjini

(iii)       Kuendesha mafunzo kwa vitendo kuhusu teknolojia rahisi ya ujenzi wa nyumba katika wilaya tatu (3) moja kila wilaya.

·      Mafunzo kwa vitendo yalifanyika kwa Mafundi Sanifu wanne (4) kutoka Mamlaka ya Uendelezaji Mji (CDA) Dodoma.

  • Mafunzo kwa vitendo yalifanyika Mkoa wa Lindi katika Wilaya ya Kilwa kwa wanakijiji 72 katika jumla ya vijiji sita (6) navyo ni Somangandumbo, Somangasimu, Mtyambuko, Miumbu, Pungutini na Kinjunbi.
  • Kuzalisha matofali, vigae pamoja na mashine zake kwa wingi ofisini NHBRA ili wananchi waweze kupata huduma hizi toka NHBRA na hivyo kutengeneza ajira kwa vijana.
  • Ujenzi wa nyumba za mfano hutumika vijana wa maeneo husika ili waendeleze teknolojia hii.

8. UBORA WA VIFAA VYA UJENZI
NHBRA inajitahidi kutoa elimu kwa wananchi ili waweze kujua vifaa bora vipatikanavyo katika maeneo yao, pia ambavyo vinaweza kuzalishwa katika maeneo wanamoishi wananchi kwa ubora unaofaa. Hii itasaidia kupunguza matumizi ya vifaa visivyo na ubora au vyenye ubora duni, pamoja na kuwezesha vikundi kujipatia ajira. Mojawapo ya kazi za NHBRA ni kutoa mafunzo ya uzalishaji na matumizi bora ya vifaa vya ujenzi vinavyopatikana karibu na maeneo ya ujenzi na bila kuathiri mazingira.

9. MIKAKATI YA KUJITANGAZA
Mikakati ya kujitangaza inaendelea kufanyika kwa kujitangaza katika vyombo mbalimbali vya habari kama vile magazeti, redio, televisheni pamoja na kushiriki maonesho mbalimbali yanayofanyika hapa nchini kwa nyakati tofauti.

Mpaka sasa kuna mikakati ya kuunda na kuimarisha vikundi vya vijana wa kujitegemea watakaojishughulisha na uzalishaji wa vifaa, mashine pamoja na ujenzi kuanzia ngazi ya kata. Hawa watakuwa wawakilishi wa NHBRA katika maeneo yao. Mifano halisi ni vikundi vya uzalishaji na ujenzi huko Pwani, Namtumbo-Songea, Somanga-Lindi, Manispaa ya Tabora na Tulawaka-Biharamulo. Vikundi hivi vitaweza kutumiwa na yeyote katika miradi ya ujenzi wa nyumba za gharama nafuu.

10. MAFANIKIO YA NHBRA
  • Ubunifu na utengenezaji wa matofali ya kufungamana ya udongo – saruji (Tanzanian type) na mashine zake.
  • Vigae vya kuezekea nyumba vya mchanga – saruji na mashine zake.
  • Tumejenga nyumba za mfano katika sehemu mbalimbali za Mkoa wa Dar es salaam.
  • Ujenzi wa vyumba 72 vya biashara huko Ipogolo – Iringa.
  • Ujenzi wa nyumba za kuishi wafanyakazi wa halmashauri ya Wilaya ya Ruangwa Mkoani Lindi, nyumba za kuishi polisi huko Singida, Songea na Ukonga – Dar es salaam.
  • Ujenzi wa nyumba za watu binafsi katika sehemu mbalimbali.
  • Kutoa semina za uhamasishaji na mafunzo kwa vitendo karibu mikoa yote ya Tanzania bara.
  • Ujenzi wa nyumba za kuishi wafanyakazi wa halmashauri ya Wilaya ya Mvomero Mkoani Morogoro.
  • Majarida mbalimbali ya kitaalam kuhusu tafiti zilizokwisha kamilika.
  • Uanzishaji na ulezi wa vikundi vya vijana wajasiriamali vya kuzalisha vifaa vya ujenzi vilivyotafitiwa, na wa kujenga kwa kutumia vifaa hivyo huko Namtumbo-Songea, Tabora Manispaa, Tulawaka-Biharamulo, NHBRA –Dar es salaam.

No comments:

Post a Comment