Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Sunday 13 October 2013

MKUYU: MALKIA WA MITI YOTE





*Baadhi wanauita mti mtakatifu, wengine wanasema wa mashetani

Na DANIEL MBEGA

TANGU utotoni tulizowea kuambiwa kwamba mti wa mbuyu ni wa mashetani na tusithubutu hata siku moja kukaa karibu pindi mvua inaponyesha kwa sababu radi linaweza kuupiga na kuugawanya katikati. Hata hivyo, bado tuliendelea kukwea na kuchuma matunda yake nyakati za kiangazi.
Tuliambiwa kwamba wachawi hupendelea kuweka maskani yao kwenye miti hiyo ya mibuyu, ambayo ni miongoni mwa miti mikubwa na inayoweza kukua na kumea katika maeneo yenye ukame, kama Dodoma na Singida kwa hapa Tanzania.
Lakini ukiachilia mbali mbuyu, pia wazee wetu walikuwa wakitukataza tusipendelee kucheza kwenye miti ya mikuyu, ambayo inatajwa kwamba ndiyo ‘malkia wa miti yote’. Sababu kubwa waliyotuambia ni kwamba miti hiyo ni ya miungu na ndiyo maana inapendelea kuota sehemu zilizotulia kwenye mapito ya maji huku ikiwa inaongoza kwa kuwa miti pekee yenye mizizi mingi.
“Ninyi hamuoni, hata nyakati za kiangazi mti unaonekana umependeza, tofauti na ule mbuyu. Ule mbuyu ni mti wa mashetani, lakini huu ni mti wa miungu. Msije mkathubutu hata siku moja kuukata ama kuuchezea, miungu ikikasirika mtapata shida,” nakumbuka mzee mmoja alipata kutuambia wakati tukiwa wadogo, zaidi ya miaka thelathini iliyopita.
Kweli hatukuwa tukiikata miti hiyo, lakini daima tulipendelea kucheza chini ya vivuli vyake na kukwea kuchuma matunda yake mazuri kuyatazama, matamu kuyala, lakini yakiwa yamejaa wadudu wengi ambao unalazimika kuwaondoa kabla ya kuyala.
Huo ndio mkuyu, mti ambao ni wa ajabu ambao si wengi wanaoufahamu kutokana na kutoota kila mahali kama ilivyo miti mingine. Tena basi si mti wa kupandwa, bali hujiotea wenyewe, hasa katika maeneo ya kitropiki, ingawa baadhi ya jamii yake inaweza kuota kwenye maeneo ya joto.
Tunaambiwa kwamba mti mashuhuri wa mkuyu (Ficus carica) asili yake ni Asia na Mashariki ya Kati lakini umefanikiwa kumea hata katika maeneo mengine, ukiwa unazaa matunda matamu sana, ambayo kama unaweza kuhudumiwa kama yalivyo matunda mengine, huwezi kukuta wadudu ndani ya matunda yake yenye majimaji mengi.
Wataalamu wa mambo ya kale wanasema kwamba mti huu wa mkuyu unaweza kuwa mmoja kati ya mimea iliyowahi kutunzwa na binadamu (katika sehemu nyingine mikuyu inatunzwa, hasa kwa watu wenye maeneo makubwa, kwa sababu miti hii huchukua maeneo makubwa sana kutokana na mfumo wao wa mizizi kuwa yenye kutambaa). Mkuyu unatajwa ndani ya Biblia, wakati Adam na Eva wanapotumia majani yake kujistiri baada ya kuona wako uchi ndani ya Bustani ya Eden.
Ukristo siyo dini pekee ambayo imeupa mkuyu nafasi kubwa kama unavyotajwa pia katika Injili. Jamii nyingine ya mkuyu au mtini wa Kiasia, Ficus religiosa, unachukuliwa kama mti mtakatifu na Wahindu, Wajaini, na Mabuddha. Inasemekana Buddha Mkuu, Siddhartha Gautama, alipata ufunuo wakati alipokuwa ameketi chini ya mti mtakatifu wa mkuyu, ambao pia unajulikana kama bo au pipal. Waislamu pia wanaichukulia miti mingine ya jamii ya mkuyu kama mitakatifu.
Kwa hakika, kati ya miti yote duniani, mikuyu (Ficus) ndiyo miti pekee ambayo ukuaji wake umetandwa na utata utata na hata uchavushaji wake ni wa ajabu. Jaribu kufikiria mti ukiwa umejaa mizizi inayofanana na nyoka, ikiwa imejiviringisha na kuchomoza kwenye shina ama matawi ya mti mkubwa na kutanda kila sehemu na hata kuinyonga miti mingine ya jirani yake.
Japokuwa watu wengi wanaufahamu mti wa mkuyu ambao ni wa kale (Ficus carica), aina mbalimbali za jamii ya mikuyu hustawi kwenye maeneo ya kitropiki. Ukuaji wake na mifumo yake ya mizizi inaweza kufananishwa na miti inayoonekana kwenye filamu za "Tarzan" au "Rambo". Kuna jamii ya miti hii ambayo iliwahi kupandwa katika jimbo la Florida na kusini mwa California nchini Marekani, na ukiangalia ndiyo miti ambayo imetumika katika filamu hizo ambazo mara kadhaa wahusika wanatumia mizizi yake inayoning’inia kubembea huku wakiwashambulia adui zao.
Miti hii ambayo iko katika kundi (genus) la Ficus, katika familia ya Mulberry (Moraceae), ndiyo yenye jamii kubwa zaidi ikiwa na aina ya miti 1,000. Miti inayoifuatia kwa kuwa na jamii nyingi ni ile ya jamii ya mikungugu yenye miiba maarufu kama Acacia (ambayo ina jamii 800), Mikaratusi ama Eucalyptus (500), na Cassia (500).
Pamoja na kuambiwa na wazee wetu kwamba miti hiyo ni ya miungu, lakini pia nakumbuka kwamba mahali ambako miti hiyo iliota ama ilikuwa ni vyanzo vya maji au sehemu iliyopitisha maji kama mto, au sehemu iliyokuwa na uoto mzuri na ardhi yenye rutuba.
Kama iliota sehemu za nyikani, basi tuliamini kwamba ikiwa utachimba kisima mahali hapo maji hayakuwa mbali sana, na ndivyo ilivyokuwa, hasa kwa sisi ambao tulikuwa tukiishi katika maeneo kame kama yale ya mikoa ya kati.
Hata hivyo, hivi sasa miti hii, ambayo tuliiheshimu kwa kuona kwamba ni miti ya miungu, imeanza kutoweka baada ya wananchi kuamua kuikata kwa matumizi mbalimbali. Ile hofu kwamba ikikatwa inaweza kuleta madhara haiwasumbui wengi na wanaona kama vile zilikuwa hekaya tu za wazee wetu.
Kitu kimoja ambacho hawakielewi ni kwamba, wazee wetu walikuwa na maana kwamba, miti hiyo ilikuwa vyanzo vikubwa vya maji na dalili nyema kwamba nchi ilikuwa na neema, hivyo kuikata kulimaanisha kwamba janga la ukame lingeweza kuibuka.
Janga hilo sasa liko dhahiri kwa sababu baada ya kukatwa kwa miti mingine yote kwenye misitu, na waheshimiwa hawa kuigeukia mikuyu, hivi sasa maeneo mengi ni makavu na hata mvua imekuwa ikinyesha kwa bahati, kwa sababu ile miti ambayo ilikuwa ikivuta mawingu ya mvua haipo tena.
Kwa hakika, kama wana mazingira wakifanya utafiti wa kutosha, na kama kuna uwezekano wa kuipanda miti hii, basi inaweza kusaidia kutunza mazingira na kuwa kivutio cha mvua katika maeneo mengi, hasa yenye ukame.
Faida yake ni kubwa, kwamba pamoja na kuwa vyanzo vya maji na vivutio vya mawingu ya mvua, lakini matunda yake ni chakula kizuri sana kwa ndege, wanyama wa porini na hata binadamu.
Tunaambiwa kwamba matunda ya mkuyu yana viiniisho kama wanga, hamirojo, sukari, mafuta na protini kibao, hivyo ni mazuri sana kuliwa. Kwa sisi tuliowahi kuyala wakati wa utotoni tunaujua utamu wake, lakini linaweza kuwa jambo geni kwa wale ambao hata mti wenyewe hawaujui.
Tunda la mkuyu linachukuliwa kama tunda, lakini kwa hakika hilo ndilo kama ua la mkuyu. Linaweza kutajwa kama ni tunda bandia ama tunda linalojipogolesha, ambapo ua na mbegu hukua pamoja na kufanya tunda.
Pengine uwezo huu wa kutoa maua ambayo ni matunda, tofauti na miti mingine, ndiyo yaliyowafanya hata wazee wetu waone kwamba huu ulikuwa ni mti wa miungu, tofauti na mbuyu ambao maua yake yanaonekana mpaka matunda yanapokomaa.
Yote kwa yote, kinachotakiwa kufanyika kwa sasa kwa wizara ya Maliasili na Utalii, kwa kushirikiana na Wizara inayohusika na Mazingira, ni kuilinda miti kama hii ambayo kuwepo kwake kuna faida kubwa kwa mazingira yetu na sisi wenyewe kwa ujumla. <Mwisho>.

No comments:

Post a Comment