Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Wednesday 4 June 2014

RIWAYA TAMU: JUDITH...JUDITH...!

JUDITH…JUDITH…! 

INNOCENT A. NDAYANSE (ZAGALLO)

0755 040 520 / 0653 593 546 

PUUU! Mlango mkubwa wa nyumba ya mzee Ndayishimiye ulitikisika kwa kishindo. Kisha ukimya ukarejea. Mzee Ndayishimiye ambaye wakati huo alikuwa mezani na familia yake wakipata mlo wa usiku, walishtuka na kubaki wameduwaa.
Kwa kipindi cha wiki tatu mfululizo, matukio ya kutisha na kusikitisha yalishamiri jijini Kigali nchini Rwanda. Watu wengi waliuawa kwa kuvunjwa shingo, kupondwa na nyundo vichwani, kuchomwa moto na hata kwa risasi.
Yalikuwa ni mauaji yaliyoitikisa nchi nzima ya Rwanda, ukanda wa Maziwa Makuu, nchi wanachama wa Jumuia ya Afrika Mashariki, Afrika na hata dunia nzima. Mauaji hayo ya kimbari yalisababishwa na tatizo sugu la ukabila lililokuwa likiitawala ‘meli’ ya Rwanda.
Mtutsi alijiona kuwa yeye ni yeye ndani ya Rwanda. Nani mwingine anayetaka kuwa na sauti? Mhutu naye hakuwa amelala. Yeye pia aliamini kuwa ni yeye ndiye mwenye haki na raia halali wa Rwanda, kwamba Mtutsi ni mkimbizi tu!
Ni kutokuelewana huko ndiko kulikozua mzozo na hatimaye mapigano yaliyosababisha uadui mkubwa baina ya makabila hayo mawili makubwa nchini humo.
Usiku huu, saa 2.30, ndiyo kwanza Mzee Ndayishimiye alikuwa amerejea huku akitweta kwa woga. Hakuwa katika hali ya kawaida. Amani ilikosekana moyoni mwake. Tangu alipoingia humo ndani kwake, alitaka kumweleza mkewe hayo aliyoyashuhudia huko alikotoka lakini alijikuta akisita. Aliona kuwa ni mapema mno kulizungumzia hilo.
Fikra zake zilikuwa umbali wa nusu kilometa ambako alishuhudia rafikiye mpenzi, mzee Shomvi Niyonzima akiuawa kikatili pamoja na familia yake. Mzee Shomvi aliuawa kwa kufungiwa ndani ya nyumba kisha nyumba hiyo kuchomwa moto. Lilikuwa ni tukio lililomtisha na kumsikitisha sana mzee Ndayishimiye!
Alishuhudia nyumba hiyo ikiteketea huku sauti za vilio vya mkewe Shomvi na wanae waliokuwa ndani humo zikisikika! Vilio hivyo hivyo awali vilisikika kwa nguvu lakini hatimaye vilipungua taratibu na kuzidi kutia simanzi kwa kuwa moto ule ulizidi kuwaka na paa likatumbukia ndani, hali iliyotoa taswira ya kuwa hakuna kiumbe yeyote atakayenusurika.
Ilimuuma mzee Ndayishimiye!
Hali ya hewa ilikuwa imechafuka! Mzee Ndayishimiye naye sasa akakiona kifo kikimchungulia. Akajenga imani ya zahama hiyo kufika nyumbani kwake! Kwa mfadhaiko mkubwa kichwani mwake, akatembea kwa hatua ndefu hadi kwake ambako aliwakuta wanafamilia wake wakiwa ndiyo kwanza wakijiandaa kupata mlo wa usiku.
Bila ya kuwaambia chochote alijiunga nao mezani. Lakini mwonekano wake  ulimshangaza mkewe ambaye hakusita kumuuliza, “Baba Judi vipi, za huko ulikotoka?”
Mzee Ndayishimiye hakujibu, badala yake alitwaa tonge la ugali na kutowelea kwenye mboga kisha akalipeleka kinywani. Wala hakumtazama hata mkewe, hali iliyozidi kuwashangaza mama Judi na Judith ambaye ndiye aliyekuwa mtoto mwenye uwezo wa kupambanua mambo.
“Baba!”  Judith alimwita baada ya kumwona akiduwaa na tonge la pili mkononi bila ya kulipeleka kinywani.
Ndiyo, Mzee Ndayishimiye hakuwa timamu. Sasa alitoa macho pima, akawatazama mkewe na watoto wake kwa zamu huku kijasho chembamba kikimtoka kwenye paji la uso.
“Baba kwani kuna nini?” Judith alimuuliza kwa msisitizo, naye sasa akiacha kula na kumtazama kwa makini.
Mama Judith alipeleka mnofu wa nyama kinywani huku akimtazama mumewe kwa jicho kali na la udadisi. Akamgeukia mwanaye, Judith kisha akayarejesha tena kwa mumewe ambako alimkuta akimtazama Judith bila ya kupepesa, jicho nyanya!  
“Wamewamaliza!” hatimaye mzee Ndayishimiye alisema kwa sauti ya chini, nzito na iliyojaa fadhaa.
Mara Judith akayarudisha macho kwa baba yake. Akamtazama bila ya kutamka chochote. Walipokutanisha macho, mzee Ndayishimiye akaamua kumgeukia mkewe ambaye naye bado alikuwa akimtazama.
“Nini?” mkewe alimuuliza, sauti yake ikionyesha dhahiri jinsi alivyoipokea kauli ya mzee huyo kwa mshangao.
Kabla mzee Ndeayishimiye hajajibu, ndipo mlango wao ukalia puu! Ukatikisika kwa nguvu! Akili na macho ya wote yakahamia hapo mlangoni. Wakaduwaa! Macho yamewatoka pima! Kisha ukimya ukarejea!
Kisha tena, puu! kwa mara nyingine mlango ukagongwa na kutikisika zaidi. Pigo la tatu liliulazamisha mlango ufunguke! Wanaume wanne wenye silaha wakaivaa sebule hiyo.
Ndiyo, walikuwa ni wanaume wenye nyuso zilizotangaza shari, mavazi yao ya kijeshi yakiwa ni ishara kuwa wako kazini.
Mzee Ndayishimiye na familia yake wakaendelea kuwa katika hali ileile, wameduwaa, na zaidi, kila mmoja alikuwa katahayari!

Wale wanaume wakawasogelea wanafamilia hao bila ya kutamka chochote. Kisha wakatulia. Wakatazamana. Mara mmoja wao akainua bunduki na kumlenga mzee Ndayishimiye kifuani. Ilikuwa ni kama vile mchezo fulani wa kuigiza. Askari huyo alitulia kwa sekunde chache na kumgeukia mwanzake ambaye alionekana kama kiongozi wa msafara. Wakatikisa vichwa kwa pamoja kama ishara ya kukubaliana.

Inaendelea kesho...

No comments:

Post a Comment