Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Saturday 28 June 2014

RIWAYA TAMU: JUDITH…JUDITH…! - 15

INNOCENT A. NDAYANSE (ZAGALLO)

0755 040 520 / 0653 593 546 

UTANGILIZI
Judith ameondoka mpakani na kuingia Tanzania baada ya kukutana na Baraki. Makella naye anahangaika kumtafuta kila kona na anafika mpakani baada ya kuelekezwa na dereva wa teksi kwamba amekwenda huko. Anapofika hapo anabuni uongo kwamba Judith ndiye aliyehusika na tukio la kutungua ndege iliyomuua Rais, uongo ambao ofisa wa mpakani anaupinga. Je, nini kitaendelea? Ungana na msimulizi wako …

SIKU iliyofuata, wakati jua linakaribia kuzama, lori aina ya Fuso lilikuwa likiingia katika mji wa Biharamulo, mkoani Kagera, nchini Tanzania.
“Itabidi tulale hapa,” Baraki aliwaambia  Livingstone na Judith. Kisha akamgeukia Judith: “Unaionaje Tanzania? Kuna vurugu kama kule kwenu?”
Badala ya kujibu, Judith alitabasamu kidogo na kuyaepuka macho ya Baraki ambayo yalikuwa yamemganda, akisubiri jibu.
“Naamini utaipenda Tanzania,” Baraki aliendelea. “Kama nilivyokwambia jana, huku hakuna mauaji ya kikabila kama kule kwenu.  Tuna makabila zaidi ya mia moja na ishirini, na makabila kati ya matano au sita ni makubwa  sana  kama ilivyo huko kwenu kwa makabila ya Kihutu na Kitutsi. Lakini huku Tanzania ukabila hauna nguvu. Mtu wa kabila moja anaweza kuoa au kuolewa na wa kabila jingine. Kule kwenu inawezekena hiyo?”
Judith alikataa kwa kutikisa kichwa.
“Inasikitisha,” Baraki alisema kwa sauti ya chini.
Yalikuwa ni maneno yaliyomwingia vizuri Judith. Alielewa na akashangaa. Kwake, haikumwingia akilini kuwa anaweza kumchojolea nguo Mhutu, iweje aolewe naye?! Eti Watanzania wao hawana utamaduni wa kujali ukabila. Mmakonde anaweza kuolewa na Msukuma, Muha akamwoa Mchaga, na kadhalika na kadhalika. 
Hata hivyo, mawazo hayo yalipeperuka haraka kichwani mwake pale Makella alipomjia tena akilini. Hakuhofia kuwa huenda akavuka mpaka na kuingia  Tanzania katika harakati zake za kumsaka, bali alizidi kuumia moyoni pale kumbukumbu ya jinsi Makella na wenzake walivyodiriki kunyanyua bunduki na kuwamiminia risasi baba, mama na wadogo zake watatu usiku wa siku iliyopita.
Kwa mbali alihisi machozi yakilenga machoni. Akaharakisha kuyafuta kwa namna ambayo Baraki hakutambua. Kwa ujumla hakuiona haja ya kila mtu kuyajua masaibu yaliyompata. Kila mtu, hata huyu Baraki! Ajue ili iweje?  Na kwani akijua atamsaidiaje?
Akiwa ni msichana mwenye umri wa miaka 22, tayari alikuwa na uwezo wa kupambanua baya na zuri. Alikuwa na uwezo kuamua chochote kwa hiari yake, mradi aijue faida au madhara yake.
Alihitaji kumtoroka Makella, na kwa hilo amefanikiwa. Suala kuwa hawa wasamaria wema walistahili kujua yaliyomsibu, hakuona kuwa lilistahili. Dola 2,000 zilizokuwa ndani ya bukta aliyoivaa ndani ya sketi zilimtia matumaini ya kutotetereka kimaisha japo yuko ugenini.
Saa 2 usiku Baraki alikuwa akiegesha gari kando ya nyumba ya wageni ambayo walikuwa na mazoea ya kufikia kila walipofika mjini humo. Ni Kyaka Guest House.
Usiku huo ukawa ni mtihani mwingine kwa Judith, mtihani ambao hakujua kama ataushinda ilhali yuko ugenini na yuko na watu ambao kwake ni wageni kabisa. Kilichomtorosha kule Kiyovu Hotel ni kutokubali kufanya mapenzi na Makella. Lakini huyu mfadhili wake, Baraki ameonyesha bayana tangu kule mpakani kuwa anamhitaji kwa ajili ya kustarehe naye kimwili.
Akatae? Na akikataa Baraki atachukua hatua gani? Kwa vyovyote uhusiano utavunjika. Na matokeo ya kuvunjika kwa uhusiano huenda pia kukamfanya Baraki atoe taarifa katika Idara ya Uhamiaji kuwa kuna Mnyarwanda mmoja aliyeingia nchini kinyume cha sheria.
Hadi wakati Baraki alipokuwa akifunga mlango wa gari na kumshika mkono Judith wakielekea ndani ya gesti hiyo, bado Judith hakuwa akijua uamuzi aliostahli kuchukua kama ataombwa penzi na Baraki.
Baraki alichukua vyumba viwili; kimoja kwa ajili ya Livingstone, na kingine kwa ajili yake na Judith.
Moyo wa Judith ulikuwa mzito pale alipokaribishwa chumbani na Baraki. “Tutakuwa pamoja, mpenzi,” Baraki alimwambia huku akimtazama kwa macho yaliyozungumza bayana uchu dhidi yake. Akaongeza, “Naamini utakuwa usiku mzuri kwako na kwangu, usiku utakaoiliwaza mioyo yetu kwa kiwango kikubwa, eti?”
Yaleyale! Judith aliwaza kwa uchungu. Afanye nini? Akahisi kitu kikimshawishi kutoleta ukaidi wowote kama Baraki atataka penzi. Jambo moja tu lilimtia faraja; kufanikiwa kumtoroka Makella. Kufanya mapenzi leo na Baraki haitakuwa mara ya kwanza kwake maishani. Tayari alishafanya tendo hilo na kijana mmoja huko Gisenyi, kijana ambaye alimwondolea usichana wake na wakaendelea kufanya hivyo mara kadhaa kabla kijana huyo hajakumbwa na mauti ya ghafla katika sekeseke lilelile la ukabila miezi takriban sita iliyopita.
Lakini kwa kijana yule, Judith alifanya mapenzi kwa kuridhia. Na ni kwa itikadi hiyo ya kufanya mapenzi na mtu ampendaye, ndiyo maana aliamua kumtoroka Makella. Pamoja na hayo, kumtoroka Makella akiepuka kumvulia nguo, na kumkatalia Baraki, ni mambo mawili tofauti.
Makella alikuwa ni muuaji; aliwaua baba, mama na wadogo zake na pia alikuwa ni  wa kabila la Wahutu. Huyu Baraki siyo Mhutu, ni Mtanzania. Isitoshe, Baraki amemfadhili kwa kiwango kikubwa, ufadhili ambao hata yeye mwenyewe haujui uzito wake. Kumvulia nguo Baraki hakuona kuwa ni kosa, zaidi atakuwa naye amelipa fadhila. Kwa ujumla bado aliuhitaji ufadhili wa Baraki, na aliuhitaji ufadhili wa Watanzania. Dola 2000 alizokuwanazo, hakuona kuwa ni kinga madhubuti katika nchi hii ngeni. Bado aliihitaji roho yake!

Itaendelea kesho…


No comments:

Post a Comment