Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Monday 30 June 2014

RIWAYA TAMU: JUDITH…JUDITH…! - 17



INNOCENT A. NDAYANSE (ZAGALLO)


0755 040 520 / 0653 593 546 

UTANGILIZI
Judith ameingia ndani ya Jiji la Dar es Salaam na Baraki anampangishia chumba cha gesti Magomeni. Kunapokucha anamuaga kwamba anakwenda kazini lakini anamwambia wazi kuwa ameoa ingawa anamtoa hofu asiwe na wasiwasi. Lakini baadaya Baraki kuondoka Judith anagundua kwamba hana nguo, hivyo anatoka nje mapokezi kuomba msaada. Je, nini kitaendelea? Ungana na msimulizi wako …

 Judith hakutaka Swaumu awe rafiki wa karibu. Ni ugeni wake tu uliomfanya aambatane naye. Kwa mtazamo wa haraka haraka alimwona Swaumu kuwa ni mwanamke ambaye hajatulia. Yuko macho juu-juu. Maswali mengi, udadisi usiokoma. Kichwani mwake hakumwona kuwa ni mtu anayefaa kwa ushirikiano wowote baina yao. Akaamua kujihadhari naye, lakini kwa namna ambayo Swaumu mwenyewe hatamshtukia.
Jioni ilifika, usiku ukaingia. Baraki hakuonekana. Lakini ilipotimu saa 4 usiku Judith akamwona Yohana, mhudumu wa gesti akimjia na simu mkononi. “Simu yako,” alimwambia huku akimpatia simu hiyo.
Alikuwa ni Baraki aliyepiga. Judith alipoipokea na kusikiliza, akapokea taarifa kutoka kwa Baraki kuwa kwa siku hiyo hatafika kwa kuwa amekuta matatizo katika familia yake.
“Kesho mchana tutawasiliana, sawa?” Baraki alimalizia.
“Sawa,” Judith alijibu kwa unyonge.
Usiku huo Judith akaamua kupiga pasi nguo zile alizonunua mchana kisha akaziweka juu ya kiti kilichokuwa chumbani humo. Angeziweka wapi wakati hakuwa hata na kijibegi kidogo? Baada ya hapo akalala. Usingizi haukumjia mapema. Alikuwa akiwaza jinsi atakavyomudu kuishi katika nchi hiyo ngeni ilhali hana hata ndugu huku pia ubalozi wa Rwanda ukiwa hauna taarifa yake. Akaendelea kuwaza na kuwazua, jibu asilipate. Hatimaye akaamua kufumba macho na kuulazimisha usingizi.
Dakika kumi baadaye alipitiwa na usingizi bila ya kujitambua, akazinduka asubuhi. Sasa akapiga moyo konde na kuamua kutoka, aukague mji huo mkubwa wa Dar es Salaam, labda huenda akapiga hatua moja nzuri katika kuhangaika huko.   
Na sasa hakutaka kumshirikisha mtu yeyote hususan yule Swaumu ambaye jana walikubaliana kuwa leo watakwenda wote kwenye maduka ya kubadilisha pesa. Hata huyu mhudumu wa mapokezi naye hakupaswa kujua ni kipi kinachoendelea.
Hivyo, mara tu baada ya kuoga, alivaa nguo nyingine kisha akaondoka kimya-kimya, machoni mwa wapita njia wenzake akionekana kuwa ni mwanamke wa kuvutia. Ndani ya pochi ambayo nayo aliinunua jana kule sokoni, kulikuwa na pesa kidogo za Tanzania, shilingi 9,000 zikiwa ni masalia ya zile 30,000/- alizoachiwa jana na Baraki.
Alitembea huku akiwafuata watu wengine walioonekana kuwa na haraka, wengi wao wakiwa wamevalia kinadhifu, hali iliyompa hisia kuwa huenda walikuwa wakielekea kule ambako watu hupaita ‘mjini.’ Na wengi kati ya watu hao walikuwa ni wanawake. Akaendelea kuwafuata.
Alikumbuka kuwa jana, wakati akiwa na Swaumu wakienda sokoni, aliyaona mabasi madogo ya abiria yenye maandishi ubavuni: CITY BUS. Alitaka ayatumie magari hayo kumfikisha huko panapoitwa ‘mjini.’ Akaendelea kuwafuata hao watu wengi ambao baadhi yao walikuwa na mabegi madogo mikononi.  
Robo saa baada ya kuianza safari hiyo, akajikuta akitokea Barabara ya Rashid Kawawa. Akaivuka na kushika Barabara ya Chemchemi. Hatimaye alijikuta akiibukia katika kituo cha daladala cha Magomeni Mapipa ambako alikuta idadi kubwa ya watu wanaosubiri usafiri.
Daladala zilikuja, daladala zikaondoka. Yeye hakukurupuka kupanda. Hakujua ni wapi alikopaswa kwenda na pia hakuwa na haraka. Akaendelea kuwatazama abiria wakikimbilia kila daladala iliyoingia. Kuna zilizokwenda Posta, nyingine Kariakoo, Muhimbili na hata Kivukoni.
Hatimaye aliamua kupanda daladala lililokwenda Posta, bila ya kupajua huko Posta na kama atafanikiwa kutimiza malengo yake.
Aliteremkia Posta Mpya. Akavuka barabara bila ya kumuuliza mtu yeyote, jambo lolote. Moyoni mwake alipanga kutafuta duka la kubadilisha pesa, lakini aliamua kuwa makini kwa kuwa alijua fika kuwa thamani ya pesa alizonazo ni kubwa hivyo kama watu wengine wangefahamu huenda ingekuwa hatari kwa upande wake. Kuna vibaka, matapeli na majambazi. Yeyote kati ya hao anaweza kumfanyia unyama kwa kujitwalia pesa hizo kwa njia moja au nyingine.
Akaifuata Barabara ya Jamhuri, akitembea kwa kujiamini kama vile ni mwenyeji wa eneo hilo . Huko mbele akajikuta akikumbana na Mtaa wa Zanaki. Hapo akasita. Sasa akajiwa na wazo la kuachana na Mtaa wa Jamhuri.
Akapinda kushoto na kufuata Mtaa wa Zanaki. Hakufika mbali, mara akaliona duka lenye bango kubwa ukutani: SAKA BUREAU DE CHANGE. Akasimama na kulitazama kwa sekunde chache kisha akalifuata. Dakika ishirini baadaye alikuwa akitoka ndani ya duka hilo huku akiwa na pesa za Tanzania, shilingi 2,000,000 na ushei. Akasimama kando ya barabara akiwa hajui ni wapi alikopaswa kwenda na kipi alichopaswa kufanya.
Akatulia kando ya barabara hiyo, nje ya duka hilo huku akiwa ameduwaa. Dakika mbili baadaye akapata uamuzi wa kukodi teksi. Japo alikuwa mgeni, lakini hakuwa mtu wa kushindwa kuzitambua teksi za jijini Dar, ambazo zilikuwa na utambulisho rasmi. Akaipungia mkono teksi  ambayo ilimtii.
“Magomeni,” alimwambia dereva teksi akiwa ameshaingia garini.
“Magomeni ipi?”
Lilikuwa ni swali ambalo Judith hakulitarajia. Hakuijua vizuri Magomeni na vitongoji vyake. Amwambie ni Magomeni ipi? Hata hivyo hakutaka kuudhihirisha ugeni wake kwa huyu dereva. Akamjibu, “Nitakuelekeza mbele ya safari.”
Walipofika jirani na Bondeni Hotel, Judith akakikumbuka kile kituo cha daladala alichopandia wakati anakuja Posta. Akamwambia dereva akate kulia. Dereva akatii. Walipofika jirani na kituo hicho, akamwamuru asimame.
“Ni kiasi gani?”
“Elfu saba.”


Itaendelea kesho…

No comments:

Post a Comment