Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Thursday 26 June 2014

RIWAYA TAMU: JUDITH…JUDITH…! - 13

INNOCENT A. NDAYANSE (ZAGALLO)

0755 040 520 / 0653 593 546 

 UTANGULIZI
Judith amekutana na wanaume wawili ambao anatambua kwamba ni Watanzania na wako na lori la mizigo. Anakubali kuwa nao ili tu afanikishe azma yake ya kutoroka mikononi mwa Makella. Makella naye anazidi kuchanganyikiwa na hata anapokutana na mkuu wake anaonekana mwenye mawazo. Je, Judith atafanikiwa kufika salama Tanzania? Vipi Makella atachukua uamuzi gani? Ungana na msimulizi wako …

Muda mfupi baadaye walikuwa pamoja, Luteni Kasa akinywa bia na Makella akinywa maji.
“Uko kazini?” hatimaye Luteni Kasa alimwanza.
“Ndiyo,” Makella alijibu, kisha akafuatisha hadithi nzima ya operesheni dhidi ya Watutsi mchana kutwa lakini akiepuka kuuweka bayana ukweli wa kilichomsibu dakika chache zilizopita.
Ok, lakini siyo vizuri kujiamini kiasi cha kutembea peke yako eti kwa kuwa una silaha,” Luteni Kasa alimwonya. “Ni vyema kama mngekuwa wawili, watatu hivi. Ukiwa peke yako kama hivi, adui akikuona na silaha atakuwahi.”
“Ni kweli, lakini kuna sababu iliyonifanya niwe peke yangu.”
“Sababu gani?”
“Namfuatilia  shushushu mmoja wa Kitutsi.”
“Shushushu?!”
“Ndiyo. Tena ni mwanamke!”
“Mwanamke?!” Luteni alimkazia macho Makella. Akairejesha mezani glasi ya bia iliyokuwa mikononi. Kisha akaongeza, “Una hakika kapita hapa au unabahatisha?”
“Taarifa nilizonazo zinanifanya niamini kuwa amepita hapa!” Makella alisisitiza.
Kimya kifupi kilitawala. Luteni Kasa akamtumbulia zaidi macho, Makella. Kisha: “Nina zaidi ya saa nzima niko hapa nje. Huyo mtu kapita muda gani?”
“Siyo zaidi ya robo saa.”
“Kavaaje?”
“Fulana ndefu ya bluu na sketi nyeusi.”
“Kichwani?”
“Ana nywele ndefu zilizomwagika hadi mabegani.”
Tabasamu la mbali likamtoka Luteni Kasa. Akasema, “Nadhani nimemwona.”
“Afande, umemwona?” Makella akamtolea macho.
“Ndiyo, na nadhani ni mwenyewe.”
“Yuko wapi?”
“Hapa hakukaa,” Luteni Kasa alijibu kwa utulivu. Akaongeza, “Kawaulize hao madereva teksi. Nadhani watakuwa na jibu la kukuridhisha.”
Makella aligugumia maji na kuitua chupa mezani ikiwa tupu. Kisha akanyanyuka na kutoa saluti nyingine, saluti ambayo  kama ile ya awali, hii pia Luteni Kasa alionyesha kutoijali, zaidi alitamka neno moja tu: “Asante.”
Makella akatoka. Moja kwa moja hadi kwenye teksi ambayo dereva wake alikuwa nje, kaegemea bodi. Akazungumza naye kwa kifupi tu na kuambiwa kuwa mwanamke huyo alikodi teksi na kuelekea mashariki mwa nchi.
“Labda anakimbia hizi vurugu,” dereva huyo alimalizia.
“Teksi hiyo imeelekea kule mpakani?”
“Inawezekana.”
Makella alifikiri kidogo kisha akauliza, “Una mafuta ya kutosha?”
Full tank.”
Ok, twende. Chaji yako utaileta hapa kwa afande, Luteni Kasa. Sawa?”
Haikuwa rahisi kwa dereva huyo kupinga amri ya Makella. Kwa siku hiyo, kila askari wa jeshi alikuwa na sauti. Kama dereva huyo angekataa, isingemwia vigumu Makella kumshindilia risasi na kumchukua dereva mwingine. Angeweza, na asingetokea mtu yeyote wa kumuuliza chochote!
 
**********
KICHWA cha Judith kilikuwa kizito. Aliuhisi uzito huo kutokana na mambo yaliyoisumbua akili yake. Kumbukumbu ya mauaji yaliyotokea usiku huo, saa chache zilizopita zilimganda akilini. Hakujisikia kuwa yu binadamu wa kawaida, wala hakuwa na hamu ya kuendelea kuishi. Kuuawa kwa wazazi wake na wadogo zake kulimwathiri kisaikolojia kwa kiwango kisichokadirika.
Isitoshe, ni muda mfupi tu uliopita alipomtoroka Makella huku akiwa amemwibia dola 2,000 za Marekani, tendo aliloamini kuwa lingeweza kumletea matatizo zaidi, hata kuyahatarisha maisha yake.
Kwa hali hiyo, alihitaji usalama, na usalama huo uwe wa uhakika. Hapo alipo, bado hakujiona kuwa yu katika sehemu nzuri kwa usalama wake. Lakini afanye nini? Hakuwa na la kufanya. Akalazimika kusubiri muda ambao Baraki ataamua waondoke huku kimoyomoyo akiomba Mungu, Makella asitokee.
Alikunywa bia  huku akiilazimisha nafsi yake kutii utomasaji wa Baraki katika chuchu za matiti yake na wakati mwingine mkono ukivuka hadi mapajani ambako ulitulia na kuyapapasa-papasa.
Japo eneo waliloketi halikuwa na mwanga, hata hivyo halikuwa likistahili kuchukuliwa kuwa ni maficho kamili, eneo ambalo mtu yeyote mwingine ambaye angefika hapo angeshindwa kuwaona.  Kwa vyovyote vile, mtu ambaye angelisogelea eneo hilo kwa umbali wa hatua tano kutoka kwenye meza hiyo, kama anamfahamu Judith, angeweza kumtambua. Ni taswira hiyo ambayo Judith hakuipenda, na hakuipenda kwa kuwa alihofia kukutwa hapo na Makella.
Mara Baraki aliacha kumpapasa. Akaitazama saa yake na kusema, “Nadhani huu ni muda mwafaka. Saa nne! Twende na bia zetu garini, na nyingine ziko hukohuko. Sidhani kama tutazimaliza.”
Yalikuwa ni maneno ambayo Judith aliyahitaji, zaidi ya hizo bia au jambo jingine lolote. Hakuhitaji bia, alihitaji kuwa mbali na Makella. Hakumhitaji Baraki, alihitaji kuwa mbali na Makella! Aliyahitaji maficho!
Kwa furaha ambayo ilifurika moyoni na kufanikiwa kutoiweka hadharani, aliitwaa chupa na kuipeleka kinywani. Safari hii hakunywa, alimimina! Alipoitua chupa hiyo mezani, ilikuwa tupu. Sasa akamtazama Baraki kwa namna nyingine kabisa, macho yake yakitoa shukrani za dhati.
Baraki akiwa hayajui yaliyomo moyoni mwa Judith, alivutiwa na macho hayo, akamvuta na kumbusu shavuni. Hakuishia hapo, akajaribu kupenyeza ulimi kinywani mwa Judith, jaribio ambalo safari hii Judith hakulizuia, akafuata ule usemi wa ‘mtaka cha uvunguni.’  Wakakutanisha midomo yao na kudumu katika busu hilo kwa sekunde kadhaa, Baraki akipata burudani halisi ilhali Judith akiwa katika starehe bandia.

Itaendelea kesho…

No comments:

Post a Comment