Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Tuesday 17 December 2013

TEMBELEA HIFADHI ZETU UWAONE HAWA: YANGEYANGE

Yangeyange mweupe.

 Yangeyange fuata-ng'ombe.
 Yange tumbo-kahawia.
 Yangeyange Kulasitara.
 Yangeyange njano.

Na Daniel Mbega (Mhifadhi Asilia)

SEKTA ya Utalii, hasa utalii wa ndani ndiyo huchangia kwa kiasi kikubwa mapato ya Taifa katika sehemu nyingi duniani, kwani ni sekta ambayo haihitaji mtaji mkubwa sana wa Serikali kuiendesha.
Hii inatokana na ukweli kwamba, mtaji uliopo ni wa asili kwani kuna vivutio vingi kama wanyama, ndege, mimea na mbuga nzuri ambazo macho ya binadamu yeyote anayependa kubadilisha mtazamo wake yangependa kuvinjari.
Hata hivyo, wananchi wengi wa Tanzania wameonekana kutokuwa na utamaduni kwa kwenda kutembelea vivutio vyetu vya asili vya utalii, badala yake wengi wao wako tayari kununua mikanda mingi ya filamu za Kimagharibi na kupoteza muda mwingi kuangalia.
Hii ni mbaya kwa sababu siyo tu tunawajengea utamaduni mbovu hata watoto wetu, bali tunaikosesha Tanzania mapato ya ndani huku tukijenga hisia mbovu kwamba mbuga za wanyama ziko kwa ajili ya Wazungu pekee, jambo ambalo siyo sahihi.
Kama hatukuepuka tabia hii, ipo siku tutakuja kujikuta tuna kizazi ambacho hakiifahamu sura halisi ya Tembo, zaidi ya kuendelea kuwatazama kwenye picha za kawaida tu, wakati nafasi ya kwenda kuwaona ‘laivu’ tunayo na tunakuwa na shingo ngumu kubadilika.
Tanzania tunavyo vivutio vingi vya utalii, lakini katika safu hii, ambayo inalenga zaidi kuwahamasisha Watanzania kupenda utalii wa ndani, leo hii tutawazungumzia ndege jamii ya Yangeyange.
Yangeyange ni ndege wakubwa wa jenasi mbalimbali katika familia ya Ardeidae wenye miguu mirefu, shingo ndefu na domo refu na jembamba. Hupinda shingo yao wakiruka angani. Ndege hawa ni weupe au weusi au rangi hizi mbili (pengine kijani au buluu). Ndege hawa wana majina mengine ya kienyeji (mwenye nayo naomba anitumie kwa jina la kabila yake kwa ujumbe wa sms kupitia namba ya simu hapo chini tafadhali).
Spishi nyingine huitwa ngojamalika, kulasitara au dandala. Yangeyange wengine hupenda kula samaki, wengine hula wadudu na wanyama wadogo kama vyura na mijusi. Hujenga matago yao kwa matawi juu ya miti, matete au mafunjo.
Yangeyange ama Egret au Heron wanatoka katika Himaya (Kingdom) ya Wanyama (Animalia), Faila ya Chordata (Wanyama wenye ugwe wa neva mgongoni), Ngeli ya Aves (Ndege), Oda ya Ciconiiformes (Ndege kama makorongo), Familia Ardeidae (Ndege walio na nasaba na koikoi), Jenasi ni za (Bubulcus Bonaparte, Butorides Blyth, na Egretta T. Forster).
Pamoja na kujua aina na jamii ya ndege hawa, lakini hapa tutaangalia zaidi Yange Fuatang’ombe (Cattle Egret). Yange Fuatang’ombe ni familia ya Heron wasiokula nyama, yaani cosmopolitan ambao wanapatikana katika ukanda wa Tropiki na kanda za joto.
Ndege hawa wako katika jenasi ya Bubulcus. Asili yao I sehemu za Bara Asia, Afrika na Ulaya, na wameweza kusambaa sehemu mbalimbali duniani. Ukienda katika jamii za wafugaji utawaona ndege hawa, mara nyingi wakiwa wanawafuata ng’ombe kwa ajili ya kula kupe.
Lakini zaidi wanapatikana katika maeneo ya hifadhi kama Ziwa Manyara na kwingineko, na kwa hakika ni ndege wazuri mno kuwaangalia.
Ndege hawa wana urefu wa kati ya sentimeta 88–96 (Inchi 35–38) kwa kuzingatia upana wa mabawa yake kutoka ncha moja hadi nyingine; urefu wao halisi ni kati ya sentimeta 46–56 (Inchi 18–22) na wanaweza kuwa na uzani wa gramu kati ya 270–512 (wakia 9.5–18.1). Midomo yao imechongoka sana, lakini huwa hawaleti madhara wanapodonoa kupe na inzi kwenye ng’ombe.
Kwa ujumla, ndege hawa wana uhusiano mzuri na binadamu na mifugo yao, na wanasaidia kuwashambulia wadudu wenye madhara kwa mifugo hiyo, hasa kupe na inzi.
Mara nyingi malisho yao ni wadudu kama panzi, inzi, buibui, vyura, na hata minyoo. Kwa nyakati nyingine wanaweza kula matunda.
Ukiwa katika hifadhi za wanyama mara nyingi utawaona ndege hawa wakiwa migongoni mwa wanyama kama pundamilia, nyumbu na hata nyati, wakidonoa wadudu ambao huwashambulia wanyama hao.
Kwa kifupi, ndege hawa wana manufaa makubwa kwa binadamu hasa wafugaji, kwani husaidia kupambana na wadudu wenye madhara kwa mifugo, wadudu ambao wanaweza kusababisha magonjwa hatari ya mifugo kama Ndigana.
Ni vyema Watanzania wakajenga utamaduni wa kutembelea mbuga na hifadhi zetu na kushuhudia raslimali za asili zilizopo badala ya kudhani mbuga hizi ni maalum kwa ajili ya wazungu.

* Mwenye maoni, au anayewajua ndege hawa kwa majina ya kienyeji, anitumie kupitia namba 0715 070109, au e-mail: brotherdanny5@gmail.com.

No comments:

Post a Comment