Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Saturday 14 December 2013

NYAYO ZA CHIFU MKWAWA (12)


Kaburi walimozikwa makamanda wa jeshi la Wajerumani waliouawa na Chifu Mkwawa pale Lugalo.

Na Daniel Mbega

KAMA tulivyoona huko nyuma, Wajerumani walionekana wema kuliko Mkwawa, ambapo makabila mengi yaliyoizunguka Himaya ya Uhehe yaliyokuwa yakinyanyaswa hapo kabla yaliona kwamba Wazungu hao ndiyo kimbilio lao na wangeweza kuwatetea dhidi ya Mkwawa.
Wazungu kwa kiasi kikubwa wanaipotosha historia katika kuhalalisha kile wanachodhani Waafrika watakiona ndicho bora zaidi. Katika historia ya Mkwawa, wanadai kwamba, utajiri ambao Chifu Mkwawa aliurithi kutoka kwa baba yake Munyigumba ulikuwa ni wa dhulma, kwamba waliupata kwa kupora misafara, kama walivyofanya Wangoni na Wasangu.
Na itakumbukwa kwamba, Mkwawa aliendelea kuivamia misafara ya Wajerumani katika Njia ya Kati kadiri alivyoweza, hali ambayo baadaye ikasababisha mapigano mengine katika Kijiji cha Munisagara Desemba 7, 1892 ambapo pamoja na Wahehe kushindwa, lakini walifanikiwa kukiteketeza Kijiji cha Kondoa kwenye Bonde la Mukondoa karibu na ngome ya Wajerumani ya Kisaki.
Lakini siyo siri kwamba, ushindi wa Wahehe dhidi ya Wajerumani Agosti 1891 ulisikika kila pembe ya Afrika Mashariki ambapo Waafrika waliuzungumzia sana. Lakini mwishoni mwa mwaka 1892 na mwanzoni mwa 1893 kulikuwa na kila dalilia kwamba Wajerumani wangeweza kutawala kwa sababu nguvu zao dhidi ya Wahehe zilikuwa zimeimarika na kutanua mpaka wao.
Wasagara, ambao awali walikuwa wameishi kwa hofu ya Mkwawa na kumpelekea zawadi kila wakati ili asiwapige, sasa waliishi jirani na kambi za Wajerumani na wakaanza kuubeza uwezo wa Wahehe waziwazi.
Wasangu nao, ambao waliwahi kuwa tishio kwa Wahehe, Wabena na makabila mengi katika miaka ya 1850 na 1860, walinyanyaswa mno tangu enzi na Munyigumba na Mkwawa baada ya Wahehe kuimarika na kuwageuzia kibao katika miaka ya 1870 na 1880. Kutoka na Wajerumani kupenya upande wa kaskazini na mashariki mwa Uhehe, inaelezwa kwamba Chifu Merere Towelamahamba (Merere III) wa Usangu waligeuka kuwa washirika wakubwa wa Wajerumani upande wa kusini ambapo waliweza kuwaelekeza Wajerumani mahali gani na wakati gani wa kumshambulia Mkwawa.
Hata Wakinga na Wabena ambao awali walionekana wanyonge wakaanza kugomea amri za Wahehe kwa matarajio kwamba Wajerumani na Wahehe wangeweza kupigana na kuuana wenyewe. Wakati wa Vita vya Lugalo, Wabena walikuwa wamewatoa wanamgambo zaidi ya 1,000; lakini sasa miaka miwili baadaye walikuwa wameanza kukataa hata kupeleka chakula.
Kibaya zaidi kwa Mkwawa ni kwamba, mgawanyiko ulitokea katika utawala wake chini ya kaka yake Mpangile (ambaye baadaye ndiye aliyechukua nafasi ya Mkwawa kama ‘Chifu wa Wahehe’.
Kuzungukwa na Wajerumani pamoja na usaliti wa watawala wengine kama Wasangu, Wabena na Wasagara kuliifanya Himaya ya Uhehe iyumbe na kupunguza uimara wa Mkwawa, hali hiyo ikawahamasisha Mpangile na wenzake kutumia madaraka yao na kuweka maazimio kadhaa ya kisiasa ya kula njama na Wajerumani ili kumsaliti Mkwawa.
Wakati ambapo matukio ya miaka ya 1892 na 1893 yalionekana taratibu yanamgeuzia kibao Mkwawa, Chifu Merere Towelamahamba wa Usangu, kwa upande mwingine, aliiona fursa ya kuingia kwa Wajerumani na vita yao dhidi ya Himaya ya Uhehe. Wasangu, ambao Mkwawa hakuwahi hata kuingia nao maridhiano yoyote, walikuwa wameshikwa na mshangao – wakaona fursa kubwa ya kutumia uvamizi wa Wajerumani kwa faida yao. Jamie Monson aliwahi kuandika katika kitabu chake, “Wajerumani walionekana kama washirika muhimu wenye nguvu na walinzi kwa jamii nyingi katika kanda ya kusini. Wakafanya ushirika na watawala wa jadi kwa kuungana kidiplomasia.”

Merere alikuwa mmoja wa watawala werevu sana kati ya ‘washirika’ wa Wajerumani. Tom von Prince alikutana naye zaidi ya mara moja kwa amri kutoka makao makuu Dar es Salaam kukamilisha baadhi ya makubaliano na Wasangu, ambao walionekana kuwa washirika wazuri kutokana na mahali walikokuwa wakiishi magharibi mwa Uhehe pamoja na uhasama wao wa muda mrefu uliokuwepo dhidi ya Mkwawa na watu wake. Gavana von Soden pia akatumia fursa ya kuingia kwa Wamisionari wa Jumuiya ya Wainjilisti ya Berlin (Berlin Evangelical Mission Society), kufungua mazungumzo na Merere na kudumisha uhusiano wa ‘kirafiki wa kiserikali’.
Tutaendelea...

No comments:

Post a Comment