Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Tuesday 10 December 2013

NYUMBU WA SERENGETI NI RAIA WA TANZANIA

 

Na Daniel Mbega, Serengeti

HAWANA vyeti vya kuzaliwa, wala hawajulikani hata mahali gani wanapotupa makondo yao ingawa ukifuatilia unaweza kuyaona, lakini Nyumbu (Wildebeest) wanaopatikana katika Hifadhi ya Taifa ya Serengeti ni raia halali wa Tanzania.
Kwamba wanapatikana pia katika hifadhi ya Maasai Mara katika nchi jirani ya Kenya, katu hiyo haiwezi kuhalalisha uraia wao kwamba wanatokea huko.
Ni bahati mbaya tu kwamba wanyama hawana paspoti kama ambavyo hawana vyeti vya kuzaliwa, vingenevyo ushoroba (corridor) wanaoutumia ungewekwa kizuizi kama kile cha Sirari, Namanga, Tarakea, Holili na kwingineko hakika hati hizo zingethibitisha kwamba wanyama hawa huwa wanakwenda Kenya kutalii tu na kurejea tena nchini mwao Tanzania.
Kuweka mambo sawa ni kwamba, wanyama hawa wanapokwenda kwenye Hifadhi ya Maasai Mara, huwa wanakwenda kwenye 'fungate' kwa muda usiozidi miezi miwili na kisha kurejea kwao Tanzania kuendelea na maisha yao ya kawaida.
Maelezo haya yanathibitishwa na Mhifadhi Mkuu wa Hifadhi ya Serengeti, William Mwakilema, ambaye anasisitiza kwamba kauli zinazotolewa na wenzao wa Kenya kwamba wanyama hao wanapatikana nchini mwao na ni mali yao ni za upotoshaji mkubwa kimataifa.
"Achana na propaganda za Serikali ya Kenya inayojinasibu kwamba eti wanyama aina ya Nyumbu ni wa kwao kwa sababu wanapatikana kwenye Hifadhi ya Masai Mara. Huu ni uzushi mkubwa na unapotosha," anaeleza Mwakilema.
Mwakilema anasema, Nyumbu hao wanaosafiri kwa makundi makubwa kila mwaka ni 'raia' halali wa Tanzania kwa kuzaliwa na kwa nasaba.
Mhifadhi huyo anabainisha kwamba, wanyama hao, ambao ndiyo alama na nembo ya Serengeti, huzaliana kwenye hifadhi hiyo na kwamba wanatumia muda mrefu zaidi wakiwa Tanzania kuliko wanavyokuwa Kenya.
"Hivi tunavyozungumza ni kwamba wanyama hawa wamerejea Serengeti tangu mwezi Septemba mahsusi kwa ajili ya kuzaliana. Wanapatikana nchini Tanzania kwa kipindi kirefu cha mwaka kuanzia Septemba hadi mwanzoni mwa Julai ambapo huelekea Maasai Mara kwa kipindi kifupi tu," anafafanua Mwakilema.
Aidha, Mwakilema anasema, Nyumbu huelekea Maasai Mara kwa ajili ya kutafuta chakula tu kwa muda mfupi na kurejea, kwani wanayafahamu vyema makazi yao ya asili.

Uhamaji wa Nyumbu
Hakuna mahali popote duniani ambako kuna uhamaji wa Nyumbu kama wa Serengeti kuelekea Maasai Mara ambao umekuwa miongoni mwa Maajabu Saba ya Dunia na hakika ndio umeifanya Serengeti kushika nafasi ya kwanza katika Maajabu Saba ya Asili ya Afrika mwezi Machi 2013.
Zaidi ya nyumbu milioni 2 huhama kutoka Hifadhi ya Taifa ya Serengeti nchini Tanzania kuelekea Hifadhi ya Maasai Mara nchini Kenya kutafuta malisho kati ya kipindi cha Julai na Oktoba.
Wanapohama ni lazima wakatize kwenye Mto Mara ambako hukumbana na mamba ingawa wengi hunusurika.
Mwakilema anasema, wanyama hao wanapatikana katika Mfumo-asili wa Serengeti (The Serengeti Ecosystem), unaochukua eneo la kilometa za mraba 40,000 huku wengi wa nyumbu hao wakiwa wale wenye manyoya meupe (Connochaetes tuarinus mearnsi) ambao wanapatikana pia katika sehemu ya Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro kwa upande wa kusini; Hifadhi ya Serengeti na Maswa Game Reserve pamoja na Hifadhi za Jamii zinazopakana.
Mwanzo wa safari hizi za uhamaji ni kuzaliwa kwao, kama anavyosema Jonathan Scott, mwandishi na mpigapicha wa Afrika Mashariki, ambaye ametumia miaka 30 akizunguka Serengeti na Maasai Mara. Na mwisho wao pekee ni kifo, bila kujali wamefia Tanzania au Kenya.
Nyumbu wanazaa kati ya Januari na Machi katika uwanda mpana wa Serengeti ambapo kipindi hicho huwa kunakuwa na chakula na maji ya kutosha. Ikitokea hali ikawa ni ngumu, nyumbu anaweza 'kuahirisha kuzaa' mpaka chakula na maji vipatikane.
Kwanini wanazalia Tanzania? Mbali ya kuwa Serengeti ndiyo makazi yao ya asili, lakini wanyama hao, na wengine wengi, hupenda kuzalia huko kwa kuwa ardhi ina madini ya kutosha ya fosforasi ambayo ni virutubisho muhimu kwa majani, hivyo kuwafanya ndama wanaozaliwa kupata nguvu muda mfupi baada ya kula majani hayo.
Mwakilema anasema, katika kipindi cha uzazi, Nyumbu wanaweza kuzaa ndama 8,000 kila siku, hivyo kuonyesha ni kwa nini hifadhi hiyo inao wanyama hao wengi zaidi.
Kutokana na tabia yao ya uhamaji, nyumbu huwa hawana uhusiano wa kudumu. Majira ya nyumbu kupandana ni wakati nyumbu madume wanapotengeneza himaya na kuwavutia majike.
Himaya hizi ndogo huwa zinaanzia meta za mraba 3,000, ambapo ndani ya kilometa moja ya mraba kunaweza kuwepo himaya 300. Madume yanalinda himaya zao zisiingiliwe na wengine na kuwaita majike.
Kwa kawaida nyumbu huzaa mwishoni mwa kipindi cha masika, na ikitokea muda wa kuzaa umefika huku mvua zikiendelea kunyesha, basi wanaweza kuahirisha kwa muda mpaka mvua ziishe.
"Mimba hutungwa kati ya mwezi Mei na Julai, kwa hivyo utaona kabisa kwamba hata wakati wanapokwenda Maasai Mara huwa tayari majike wana mimba. Sasa unawezaje kusema kwamba hawa ni nyumbu wa Kenya?" anahoji Mwakilema na kuongeza kwamba wanyama hao wanabeba mimba kwa muda wa miezi nane na tisa.

Uainishaji wa kisayansi
Nyumbu wanatokea katika Himaya ya Wanyama (Animalia); Faila (Phylum) ya Chordata na Faila ndogo ya Vertebrata (Wanyama wenye ugwe wa uti wa mgongo); Ngeli ya Mammalia; Oda ya Artiodactyla; Familia ya Bodivae na Familia ndogo ya Alcelaphinae; Jenasi ya Connochaetes Lichtenstein, 1812.
Spishi zake ni kama nyumbu weusi (Connochaetes gnou) wanaopatikana Afrika Mashariki, hasa Tanzania na nyumbu wa bluu (Connochaetes taurinus) wanaopatikana Afrika Kusini.
Connochaetes ni neno la Kigiriki, yaani konnos, ambalo maana yake ni 'ndevu', na khaite ni 'nywele zinazoning'inia'.
Nyumbu mkubwa kabisa ana urefu wa meta 1.27–1.47 (futi 4.17–4.82) kuanzia begani na anakuwa na uzito wa kati ya kilogramu 120–270.

Uongo wa Wakenya
Taarifa mbalimbali zinadaiwa kusambazwa na Wakenya kwamba nyumbu walioko Serengeti wanatokea Kenya, propaganda ambazo zinalenga kuwahadaa watalii ili waone kwamba hawana haja ya kuja Serengeti, eneo ambalo Januari 2013 limetangazwa na UNESCO kuwa la Urithi wa Dunia.
Kama walivyowahi kudanganya watalii kwamba Mlima Kilimanjaro uko Kenya, lakini wakashindwa kuwapandisha kileleni kwa kuwa mlima huo hauko kwao, sasa wameanza propaganda nyingine ya kutaka kuwadanganya walimwengu kuhusu nyumbu wa Serengeti.
"Napenda kuwaambia walimwengu kwamba, huu ni uongo, nyumbu hawa kwao Tanzania na siyo Kenya. Watalii waachane na propaganda hizi, waje Serengeti wataona makundi makubwa ya wanyama hawa," anasisitiza Mwakilema.
Huko nyuma Wakenya pia walikuwa wakiwahadaa watu kwamba madini ya Tanzanite, ambayo ulimwenguni kote yanapatikana Tanzania tu, kwamba yanatoka Kenya.

Hii ni baada ya kuwa wananunua madini hayo na kwenda kuyapaki Kenya kabla ya kuyasafirisha Ulaya, kama walivyokuwa wanafanya kwa kahawa inayolimwa Arusha na Kilimanjaro.

No comments:

Post a Comment