Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Friday 13 December 2013

NYAYO ZA CHIFU MKWAWA (11)



Na Daniel Mbega

BAADA ya ushindi wa Lugalo, Chifu Mkwawa hakutulia, bali aliendelea kuimarisha himaya yake pamoja na jeshi lake. Lakini pia kipindi hicho Wajerumani nao walikuwa wakipanga mikakati ya namna ya kuisambaratisha himaya hiyo.
Kitendo cha kupigwa kwa jeshi lao imara lenye silaha kali, tena na wapiganaji wenye mikuki na mishale tu, kiliichanganya Berlin kwa sababu hakikuwahi kutokea hapo kabla. Hivyo Gavana Julius Freiherr von Soden aliyekuwa anaongoza koloni hilo la Afrika Mashariki alikuwa katika presha kubwa kutoka kwa wakubwa wake kuhusiana na namna atakavyomshinda Mkwawa.
Gavana huyo alijitahidi kukabiliana na presha ya Wahehe waliokuwa wakkivamia misafara yake hadi miaka miwili baadaye alipoondoka nchini. Wajerumani walikuwa na mbinu ya kuidhoofisha himaya ya Wahehe kwa mazungumzo, siyo kwa vita, kwa sababu walitambua kwamba hiyo ingeweza kuwagharimu tena.
Historia inaeleza kwamba, uamuzi wa Von Soden wa kutotumia jeshi kupambana na Mkwawa ulimfanya aonekane gavana bomu kati ya magavana wote walioongoza koloni hilo, lakini hiyo ilitokana na historia yake. Yeye ndiye alikuwa gavana pekee aliyetokea uraiani, kwani aliyemtangulia von Wissmann na wafuasi wake wa baadaye walikuwa makamanda wa jeshi.
Katika kipindi hicho cha Von Soden, Mkwawa naye alifanya majaribio kadhaa ya mazungumzo na Wajerumani akituma ujumbe wake Dar es Salaam. Mazungumzo hayo yalichukua muda wa miezi kadhaa kupitia kwa wawakilishi wake, lakini hayakuwa na mafanikio kwa sababu watawala wa Kijerumani walikuwa na mashaka na msimamo wa Mtawala huyo wa Wahehe kwamba angeweza kuwabadilikia. Kwa kifupi, hawakumwamini.
Pamoja na Von Soden kuwa na nia njema ya kufanya mapatano, maofisa wengine wa Kijerumani walikuwa na mawazo kwamba hakukuwa na haja yoyote ya kufanya mazungumzo na mtawala wa Kiafrika ambaye alikuwa ameidhalilisha Ujerumani kama alivyofanya Mkwawa.
Luteni Tom von Prince (baadaye Kapteni baada ya kuiangusha Kalenga) aliwahi kusema: “Tangu kuangushwa kwa kikosi cha Zelewski, hasa nikiwa askari wa jeshi lile la zamani, haja yangu kubwa ilikuwa kulipa kisasi kwa kudhalilishwa kwa jeshi letu, na tangu hapo nikaweka mkakati, sikuhitaji kuingia kwenye vita yoyote, sikufanya chochote ambacho kingeweza kuingilia kati mpango huu.”
Wajerumani wakati huo walikuwa na mashaka kwamba watawala wa Kiafrika, hususan Mkwawa walikuwa wameanza kuonyesha upinzani wa wazi, hasa Mtemi Isike wa Tabora na Mbunga wa Ungoni ambao himaya zao zilipakana na Uhehe. Chifu mmoja wa Usagara aliwahi kutamka wazi, “Watu hawa (Wahehe) ndio pekee walioweza kuoga mchanga wa damu ya Mzungu ambao ‘bomba zao za moto’ ziliwafanya wengi washindwe kujitetea. Na kweli, vijiji vingi vilivyokuwa jirani na boma la Wajerumani viliendelea kutoa msaada kwa Mkwawa na Himaya yote ya Uhehe mpaka pale Kalenga ilipoangushwa.
Sababu za Mkwawa kutochukua uamuzi wa kuwafukuzia Wajerumani baada ya vita vya Lugalo zinatajwa kuwa nyingi, ingawa kubwa zaidi, kwa mujibu wa waandishi wa zamani wa historia Erick Mann, Alison Redmayne, na wengineo, ilikuwa ni kupoteza askari wake wengi. Vikosi vya Mkwawa havikuwahi kuvamia eneo lililokuwa likikaliwa na Wajerumani. Katika vita vya Lugalo, Mkwawa alipompoteza makamu kiongozi wa Kalenga, Ngosi Ngosi Mwamugumba.
Pia inaonekana kwamba, Mkwawa alitegemea mazungumzo ya amani dhidi ya Isike wa Wanyamwezi, Chifu Songea wa Wangoni, na Mbunga wa Wandebele na wengineo yangeweza kuweka umoja na kuwapiga Wazungu. Kwa maana nyingine, Mkwawa ndiye mtu pekee aliyeanzisha umoja ambao leo hii tunajivunia na kama machifu wenzake wangetambua azma hiyo, pengine Wajerumani wangeweza kuondolewa kwa nguvu hata kabla ya jaribio la Vita vya Maji Maji vya mwaka 1905 hadi 1907. Kama mpango wa Mkwawa ungefanikiwa, Wajerumani wangepigwa kuanzia Tabora hadi Songea, ambapo ungeligawa koloni hilo katikati.
Mbali ya mkakati huo mkubwa, Wahehe walilazimika kupambana na Wajerumani ambao walikuwa amejitanua kutoka kaskazini hadi mashariki: kasi ya kuongezeka kwa Avadaliki (kama Wajerumani walivyokuwa wakiitwa na Wahehe) ilimaanisha kwamba Wahehe wangeweza kuzuiwa kwenye msafara wa wafanyabiashara kutoka Bagamoyo hadi Tabora. Ili kudumisha fursa ya uchumi, na hatimaye heshima ya utawala, Wahehe wakaendelea kuvamia misafara hiyo. Miongo kadhaa nyuma, juhudi zao za kuvamia misafara hiyo zilikuwa zimelenga kuteka watumwa, fedha, silaha, na kudumisha hadhi yao. Kwa ujumla, himaya hiyo kubwa ilikuwa imefanya uvamizi wa misafara kama ndiyo njia yao kuu ya uchumi ambayo watawala wa kigeni walikuwa wakkiitegemea.
Taarifa zinasema kwamba, Mkwawa pia alikuwa na hofu ya uasi ndani ya jeshi lake. Wakati ambapo Vita vya Lugalo vilikuwa vimewafanya Wakinga, Wasagara, Wabena na makabila mengine kuwa ‘watwana’ na kwamba Wahehe ndio waliokuwa na sauti zaidi, lakini kwa kuangalia hali ya baadaye, kuendelea kuwepo kwa kambi za Wajerumani katika maeneo ambayo awali yalitambuliwa kwamba ya Wahehe yaliwapa fursa makabila hayo kuasi, japo siyo moja kwa moja, huku wakimwita Mkwawa ‘chinja chinja’.
Wajerumani sasa walionekana wema kuliko Mkwawa, na Wasagara pamoja na makabila mengine ambayo yalikuwa yakinyanyaswa na Wahehe waliona kwamba Wazungu hao ndiyo kimbilio lao na wangeweza kuwatetea.
Tutaendelea..

No comments:

Post a Comment