Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Friday 6 December 2013

LEO NIMEKUTANA NA ABUNUASI SERENGETI

Ndugu zangu,
Bado safari yetu inaendelea. Kama nilivyowaeleza hapo awali, leo hii tulikuwa kwenye Hifadhi ya Taifa ya Serengeti, ambayo ni ya pili kwa ukubwa nchini Tanzania baada ya Ruaha.
Hata hivyo, hiki ndicho kitovu kikuu cha mapato ya serikali yatokanayo na utalii kutokana na kupokea watalii wengi zaidi, ambao wanavutiwa na kuhama kwa makundi ya nyumbu.
Tumekutana na Mhifadhi Mkuu, William Mwakilema, ambaye ameeleza mengi nasi tukamuuliza mengi kuhusiana na mafanikio pamoja na changamoto zinazowakabili. Nawaahidi nitawaletea siku chache zijazo kwa undani zaidi.
Tumetembelea baadhi ya maeneo na kuona wanyama wengi. Hata hivyo, aliyenivutia ni mnyama aitwaye Abunuasi ambaye kwa Kiingereza anaitwa Springhare au Rodent. Mnyama huyu, ambaye kwa jina la kisayansi anajulikana kama Pedetes capensis ambaye anapatikana zaidi Afrika, hasa Kusini na Mashariki mwa bara hilo. Anatokea kwenye jenasi ya Pedetes, familia ya Pedetidae, kundi dogo la Anomaluromorpha na Oda ya Rodentia.
Huyu niliyemuona usiku huu, yaani nusu saa iliyopita, anafahamika kama East African springhare, au kwa jina la kitaalamu Pedetes surdaster. Nimeambiwa na mhifadhi Miraji aliyekuwa anatuongoza kutupeleka mahali pa kulala kwamba, mnyama huyo huonekana zaidi nyakati za usiku na ni nadra sana kumuona. Pengine nina bahati ya mtende kuota jangwani.
Wanyama hawa wana kawaida ya kulala mchana kwenye mashimo. Wanakula majani, mizizi na mbogamboga, na mara moja moja hula wadudu.
Utamtambua Abunuasi kutokana na mwendo wake, kwani anapenda kurukaruka kwa kutumia miguu yake ya nyuma. Yaani yuko kama Kangaroo, ingawa yeye ni mdogo sana.
Kwa kweli nimefurahi sana mwenzenu, maana nakumbuka mara ya mwisho kumuona ilikuwa takriban miaka 33 iliyopita wakati nikiwa nachunga ng'ombe wa familia enzi hizo.
Nitaendelea kuwapa dondoo mbalimba za yale ninayoyaona.

Ndugu yenu,
Daniel Mbega

No comments:

Post a Comment