Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Monday 16 December 2013

NYAYO ZA CHIFU MKWAWA (14)

Mto Ruaha uliokauka, siyo mbali na eneo la vita Lugalo.

Na Daniel Mbega

KUANGUKA kwa ngome ya Mtemi Isike huko Tabora kulizidi kuidhoofisha Himaya ya Wahehe kwa sababu Chifu Mkwawa hakuwa na mshirika yeyote kati ya watawala wa jadi waliomzunguka.
Baada ya kumuua Mtemi Isike, Wajerumani walifanikiwa kuwateka askari wa Kinyamwezi (walugaluga) na kuwaingiza kwenye jeshi lao ambalo sasa lilikuwa limejiimarisha zaidi.
Mwaka 1893 Gavana von Soden, ofisa pekee wa kiraia katika historia ya utawala wa Ujerumani katika Koloni la Afrika Mashariki, aliondoka kurejea Berlin baada ya miaka kadhaa ya kupingana na wasaidizi wake wa kijeshi pamoja na wakubwa wake kule Ujerumani. Nafasi yake ikachukuliwa na Friedrich Radbod Freiherr von Schele.
Maagizo aliyopewa ni kuhakikisha anakomesha uvamizi wa misafara na kumwadabisha Chifu Mkwawa huku wakiwa na mkakati wa kuanzisha mapambano makali dhidi ya Wahehe na kuitwaa ardhi yao yenye rutuba. Lakini alitambua kwamba, wenyeji wote wa maeneo ya jirani walikuwa wanaendelea kuwahofia Wahehe.
Mashushushu wa Kijerumani wakati huo walikuwa wameanza kuondoka katika ngome yao iliyokuwa katika Koloni la Waingereza na Wamisri (Sudan ya sasa) na Koloni la Ureno Afrika Mashariki (Msumbiji) kwa sababu maeneo hayo yalikuwa yameanzisha ushirikiano na Waingereza na wareno.
Katika kulipa kisasi cha mwaka 1891 na kampeni zilizofuatia, serikali ya Ujerumani mjini Dar es Salaam ikawatuma majasusi wake huko Aden, Cairo, Massawa, na Zanzibar, ambao waliwasiliana na vyanzo vyao huko ‘Msumbiji’, ‘Sudan’, na kwenye Himaya ya Ottoman wakitaka msaada wa namna ya kufidia hasara waliyoipata. Baada ya majadiliano Waingereza walituma askari wa Misri kufidia askari wa Kisudani waliokufa kule Lugalo na mahali pengine na Wataliano wakawaruhusu Wajerumani kuwaandaa wapiganaji huko Massawa, bandari maarufu kwenye Koloni la Wataliano Afrika Mashariki (Eritrea ya sasa).
Lakini baadaye wakaanzisha harakati za kuwatumia watu wa pwani waliokuwa wakiishi jirani na Koloni la Ujerumani Afrika Mashariki. Wengi kati ya hawa walikuwa Waislamu, ambao walitumia Kiswahili kama lugha ya mawasiliano jeshini, ambayo waliona ni silaha ya kusambaza dini ya Uislamu. Wajerumani pia, kama ilivyoelezwa hapo awali, wakawatumia wapiganaji wa jadi kama Wanyamwezi wa Tabora, ambao walionekana kuwa hazina kubwa ya wapiganaji.
Wanyamwezi, ambao ndio walikuwa wapiganaji wa jadi wengi zaidi kwenye jeshi la Mjerumani, walikuwa wameendeleza tu ushiriki wao wa awali kwani ndio waliokuwa wanaongoza kwa upagazi, ambapo kote walikuwa akifanya kazi kwa ujira. Ndiyo maana haikushangaza hata baada ya ujenzi wa Reli ya Kati mwaka 1910 iliyochukua nafasi ya wapagazi, Wanyamwezi wengi wakajiunga na jeshi la Mjerumani.
Hadi mapema mwaka 1894, Jeshi la Mjerumani lilikuwa na wapiganaji karibu 2,000, likiwa limefidia mara mbili zaidi ya askari waliopotea Lugalo, na Schele alikuwa na uhakika kwamba alikuwa na jeshi ambalo lingeweza kuibomoa Himaya ya Uhehe.
Jaribio la kwanza la Wajerumani kuibomoa Himaya ya Uhehe lilifanyika mapema mwaka 1894 huko Image wakiwa na hadhari yasitokee kama yale ya kule Lugalo na Kilimatinde. Jeshi la Mkwawa katika mapigano ya Image, ambako wakeze pia walikuwa wametekwa na Wajerumani, yaliongozwa na kaka yake, Chifu Malangalila Gamoto na kufanikiwa kuwakomboa.

Kwa bahati mbaya, pamoja na kufanikiwa zoezi hilo la ukombozi, Malangalila Gamoto alijeruhiwa vibaya kwa risasi. Chifu Mkwawa akaagiza kaka yake apelekwe Ubena ambako ndiko alikokuwa anatawala, lakini walipofika eneo la Mbweni akafariki dunia. Mwili wake haukuzikwa kwa sababu za kimila. Mahali hapo pamejengwa mnara.
Tutaendelea...

No comments:

Post a Comment