Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Thursday 5 June 2014

RIWAYA TAMU: JUDITH…JUDITH…! - 2


INNOCENT A. NDAYANSE (ZAGALLO)

0755 040 520 / 0653 593 546 

Mauaji ya kinyama ya Rwanda yanaanza ambayo ndiyo yaliyozua vita ya kimbari. Mzee Ndayishimiye anashuhudia watu wengine wakiuawa. Lakini mara anaona akivamiwa na askari wenye bunduki ambao wanamuelekezea mtutu kifuani. Wakakonyezana kwa ishara. Je, nini kitaendelea? Fuatilia riwaya hii ya kusisimua….

Mara mlipuko mkubwa ukaitawala sebule hiyo. Risasi mbili zikazama kifuani mwa mzee Ndayishimiye. Akakata roho huku akishangaa vilevile, macho kayakaodoa, akiwatazama watu hao ilhali hawaoni!
Mchezo haukuishia hapo! Ukahamia kwa wanafamilia wengine. Alianzwa Martha, binti wa pili kuzaliwa, ambaye alikuwa akikimbilia kwenye miaka 18. Huyo alilishwa risasi ya kichwa!
John, Abel na Ndiyokubwayo ambao walikuwa na umri wa kati ya miaka saba na kumi, wao kabla hata hawajajua ni kipi kilichotokea, risasi kadhaa zikazama miilini mwao.
“Mungu wangu wee!” mke wa mzee Ndayishimiye aliomboleza, na kilikuwa ni kilio chake cha mwisho; mmoja wa wanaume wale hakumchelewesha, alimmiminia risasi mbili usoni, risasi zilizokifumua kisogo na kuumwaga ubongo nje huku mwenyewe akiuangukia mwili wa mumewe taratibu.
Aliyebaki hai ni Judith, ambaye kwa wakati huo aliduwaa, huenda hata akili yake haikuwa na uwezo wa kufikiri chochote. Aliyakodoa macho akiwatazama wageni hao ilhali hawaoni! Tonge la ugali alilokuwa amelishika kabla ya uvamizi huo lilibaki limetulia mkononi vilevile!
“Simama!” mmoja wa wale watu alimwamuru.
Alisikia, hakuelewa. Kwa jumla alikuwa ameathirika kisaikolojia kwa kiwango kikubwa. Alikuwa nusu mfu! Kilichofuata siyo amri tena bali kono la mtoa amri lilimshika kwenye ukosi wa blauzi na kumnyanyua kimsobemsobe, akaburutwa akipelekwa nje.
Ikawa ni kama tamthilia fulani isiyopendeza akilini mwa Judith.
********
JUDITH alikuwa ni binti ambaye tayari alitosha kuyavuta macho ya mwanamume yeyote mpenda wanawake wazuri. Kifua chake kidogo, kilichoyabeba matiti yenye ukubwa wastani yaliyovutia, kilikuwa kivutio machoni mwa wengi.  Mapaja makubwa,  na miguu minene iliyomeremeta, pia zilikuwa ni taswira kuwa muumba aliikamilisha kazi yake kwa upendo na labda hisia za wanadamu wengine zikawa ni kwamba ameifanya kazi yake kwa upendeleo.
Isitoshe, kichwa chake ambacho hakikustahili kuitwa kidogo au kikubwa kilifunikwa na nywele nyingi nyeusi tii, nywele zilizomwagika hadi mabegani na kuuongeza mvuto ambao wengi wa mabinti wa rika lake hawakuwa nao.
Macho yake yaliyorembuka muda wote kama yabembelezayo, pua ndefu na mdomo mdogo ulioyahifadhi meno meupe yaliyopangika vizuri, ni  miongoni mwa vigezo vilivyompandisha katika chati ya juu kiasi cha kuwapagawisha wanaume wengi, Wahutu kwa Watutsi.
Makella ni mmoja wa wanaume waliomtazama Judith kwa ‘macho mia.’ Akiwa ni mzaliwa wa mchanganyiko wa makabila hayo mawili makubwa nchini Rwanda, Makella alijisikia kumpenda na zaidi kumtamani Judith. Naye, kama wanaume wengine waliomtamani na kumhitaji  Judith, hakumwachia hivihivi; alimtamkia maneno mawili, matatu lakini akaambulia majibu yasiyomridhisha, na zaidi yalikuwa ni majibu ya kumkatisha tamaa:
“Shaa…hivi unaniona-aje?”
“Sina muda wa kupendana na mtu…”
“Nina malengo yangu ya maisha kwanza kwa miaka mitatu hivi mbele…”
“Sijui nina ugonjwa gani…sijui kupenda ni nini…labda mpaka nikaombewe kanisani…” na kadhalika na kadhalika.
Ndiyo, yalikuwa ni majibu ya kumkatisha tamaa, lakini hakuwa mtu wa kukata tamaa wala  kukubali kushindwa. Alijali kuwa mtu mwenye uvumilivu, asiye na papara, akiamini kuwa ipo siku atafanikiwa. Mama yake Makella alikuwa ni wa uzao wa Kitutsi na baba, Mhutu. Lakini hadi Makella anafikisha umri wa kuijua historia ya wazazi wake, wenyewe walikwishafariki kitambo kutokana na uhasama na mapigano hayohayo ya kikabila.
Makella akatunzwa na baba yake mdogo hadi alipofikia hatua ya kuwa jasiri asiyeogopa chochote wala kumwogopa yeyote. Aliweza kuua kwa risasi, kisu, panga hata kwa mikono!
Katika mfumo huo wa maisha, kikafikia kipindi ambacho alimsahau Judith kwa muda, Judith ambaye ni mwanamke pekee aliyetokea kumwingia moyoni tangu siku alipomtia machoni kwa mara ya kwanza, siku ambayo timu ya taifa ya soka ya Rwanda (Amavubi) ilipocheza na timu ya taifa moja la ukanda wa Afrika ya Magharibi katika Uwanja wa Amahoro.

Ni mchana huo wa maafa, siku ambayo ilianza kwa sekeseke la risasi kurindima huku na kule, visu kuchomwa kwa hawa na wale, mapanga na kila aina ya silaha kutua miilini mwa raia wengi, ndipo kumbukumbu kuhusu Judith ilipomjia Makella.

Itaendelea kesho...

No comments:

Post a Comment