Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Sunday 27 July 2014

KWA NINI ZITTO KABWE ANAFAA KUWA RAIS 2015

NINAAMINI kwamba makala haya yataniletea upinzani mkubwa sana kwa baadhi ya watu ambao hawataki kusikia mtu akisema Mbunge wa Kigoma Kaskazini (CHADEMA), Kabwe Zitto, anafaa kuwa rais.
Kwa bahati mbaya, wengi hawamfahamu vizuri au taarifa walizonazo zinatokana na wale wenye chuki binafsi naye.
Ni muhimu kwa taifa letu kuwa na mijadala mipana kuhusu watu wanaotaka kugombea nafasi kubwa na nyeti hapa nchini kama urais. Rais hawezi kuchaguliwa eti kwa vile ametoka katika chama fulani, dini fulani, ana mwonekano mzuri au kabila fulani.
Rais anachaguliwa kutokana na ajenda anazoleta mezani. Barack Obama alikuja na sera za mabadiliko (change) na atahukumiwa kwa hilo. Ni lazima tujiulize, wagombea wetu watakuja na hoja gani mezani?
Kwa nini Zitto Kabwe?
Katika mojawapo ya maandishi yake, mwanasiasa na mwandishi wa iliyokuwa Urusi, Leon Trotsky, alipata kusema kwamba kiongozi mzuri ni yule mwenye uwezo wa kuandika mawazo yake.
Kwamba ni hatari sana kwa taifa kuwa na kiongozi ambaye hawezi kueleza kwa maandishi ya walau kurasa tatu mawazo yake kuhusu mambo mbalimbali.
Trotsky alikuwa ni mwandishi mzuri na pengine aliandika hivi ili aonekane kama mbadala sahihi wa Vladmir Lenin kuliko Stalin.
Hata hivyo, ukiangalia mifano mbalimbali, utaona ukweli wa mawazo haya ya Trotsky. Julius Nyerere ameandika mara ngapi kuhusu masuala mbalimbali? Thomas Jefferson miongoni mwa marais mahiri kabisa wa Marekani alikuwa mwandishi mzuri.
Angalia maandiko ya Rais wa zamani wa Senegal, Leopord Sedar Senghor. Nilikuwa msomaji mzuri wa makala za Thabo Mbeki katika gazeti la chama cha ANC wakati alipokuwa Rais wa Afrika Kusini.
Na hadi sasa, huwa nafurahia sana kusoma makala za Yoweri Museveni kila anapoandika iwe katika vitabu au magazeti. Hata kama hukubaliani na kiongozi kwenye masuala fulani fulani, inasaidia kama unaona anawaza nini.
Miongoni mwa watu wanaotajwa kuwania urais wa Tanzania, ni Zitto Kabwe pekee ambaye anaandika mara kwa mara kwenye magazeti na mitandao mbalimbali.
Makala zake nyingi zina mwelekeo wa kiuchumi lakini huwezi kulaumu kwa sababu kitaaluma ni mchumi. Hata hivyo, ameandika pia mambo kuhusu mtazamo wake kisiasa na kijamii.
Natoa changamoto kwa wenzangu mniambie mmeona makala za akina nani wengine wanaotajwa kuwania urais zilizotoka katika magazeti au mtandaoni katika siku za karibuni.
Obama alikuwa hafahamiki sana lakini watu walimfahamu kwa kazi zake bungeni na za kiuandishi wakati alipokuwa mwanafunzi katika Chuo Kikuu cha Harvard. Alikuwa miongoni mwa waandishi wa jarida la chuo.
Unamchaguaje mtu ambaye hawezi kukaa chini na kutafakari kuhusu lolote na kutoa mchango wake kuhusu jambo analolifahamu? Huo ni uchoyo wa kitaaluma.
Zitto pia, pengine, ndiye mwanasiasa ambaye anaweza kufiti kwenye mazingira mengi ya kijamii kuliko wengi wa wanasiasa nchini.
Nimemuona kwenye mikutano au mijadala ya kisomi katika vyuo vikuu ambako alipokewa vizuri tu. Nimemuona katika mijadala ya asasi za kijamii ambapo alifiti vizuri tu (kabla ya kuingia kwenye siasa kindakindaki alifanya kazi za kiharakati).
Nimemuona akizungumza vijijini kwao mkoani Kigoma na ungemuona sawa tu na wananchi hao. Nimemuona mpirani akishabikia klabu ya Simba au timu ya taifa kama shabiki mwingine yeyote.
Nimemuona akichanganya na wale wanaoitwa celebrities katika muziki na filamu na nikamuona amepokewa vizuri tu kiasi cha kuimba nao wimbo wa kumchangia msanii Sajuki aliyekuwa akiumwa.
Amekusanya pia wasanii wa mkoa wake na kutoa wimbo wa kuhamasisha maendeleo ya mkoa huo uitwao Leka Tutigite.
Kwenye hili, Zitto amefuata wosia wa mwanafalsafa Conficus aliyeasa kwamba kiongozi ni lazima awe karibu na jamii na asionekane amejitenga nayo.
Katika dunia hii iliyo kijiji, unahitaji rais anayefahamu mawazo na hisia za makundi mbalimbali ya kijamii. Unahitaji pia rais ambaye makundi mengi kadri iwezekanavyo yanaweza kujihusisha na harakati zake.
Majuzi hapa, katika gazeti hili hili, Zitto ameandika makala kuhusu namna Mkoa wa Lindi unavyoweza kuwa Sri Lanka ya Tanzania. Angeweza kuandika kuhusu Kigoma lakini akaandika kuhusu rasilimali za mkoa wa Lindi usio wake.
Hili lilionyesha namna anavyofikiri kama Mtanzania na si kama Mha. Lakini pia ameonyesha namna gani anafahamu matatizo ya Watanzania kiuchumi na utatuzi wake.
Tusisahau pia kwamba Zitto amejikita zaidi katika usomi wa masuala ya madini na nishati. Ninaamini kwamba huko tuendako tunahitaji rais mweledi katika masuala hayo. Huko tuendako, gesi na mafuta yatakuja kuwa rasilimali muhimu zaidi hapa nchini. Nani miongoni mwa wanaotajwa ana uelewa wa mambo haya kuliko Zitto?
Mimi pia ni miongoni mwa wale wanaoitwa romantics katika siasa. Kwamba Zitto ni mtoto wa mkulima. Hatokani na familia zile za “uchifu mamboleo” zinazoanza kujitengeneza hapa nchini.
Za mtoto wa rais mstaafu anayetaka urais. Za mke wa waziri ambaye ni mbunge wa viti maalumu. Bado wapo miongoni mwetu wanaotamani wanasiasa waliojitengeneza wenyewe. Tunaitwa romantics. Zitto anaangukia katika kundi hili la waliojitengeza wenyewe.
Katika umri wake, Zitto ametengeneza urafiki na kufahamiana na watu ambao wanasiasa wengine hata hawawajui. Tumeona mara ngapi Zitto akikutana na watu kama Mahathir Mohamed, yule mwanasiasa aliyeibadili Malaysia kutoka nchi masikini hadi tajiri?
Tumemuona akikutana na akina Keneth Kaunda. Ninafahamu ana mawasiliano ya karibu na Raila Odinga. Zitto anaaminika na karibu wakuu wote wa vyombo vya usalama nchini. Unahitaji mgombea anayeaminika na vyombo nyeti kama hivyo.
Ninafahamu kwamba kuna viongozi wa juu na waliomzidi umri Zitto hapa nchini ambao walikuwa hawafahamiani na viongozi mashuhuri wa kitaifa wa Tanzania na walikutanishwa nao kupitia kwa mwanasiasa huyu.
Watu wengi hawafahamu lakini Zitto ni mwanajumui wa Afrika (Pan Africanist). Huko nyuma ilikuwa miongoni mwa sifa muhimu za mtu kuwa kiongozi. Umujumui, pamoja na mambo mengine, unampa fahari mtu mweusi. Unampa fursa ya kufahamu mtu mweusi alikotoka.
Kwangu mimi, hii ni sifa nzuri kwa kiongozi wa nchi ya kiafrika. Tuliwapenda kina Nyerere na Nkrumah kwa sababu walikuwa wanajumui wazuri. Waliweza kuzungumza na wazungu na kueleza msimamo wao pasipo waoga.
Kama una rais mpenda uzunguni, anayetamani kuwa mzungu na asiyejua nini kilio cha mwafrika, unategemea nini kutoka kwake. Kwangu mimi, uanajumui unamfanya kiongozi kuwa mzuri.
Zaidi ya nusu ya Watanzania wana umri chini ya miaka 30. Itapendeza zaidi kama mtu mwenye maono, elimu, umri na kipawa cha Zitto akawa kiongozi wa taifa la namna hiyo badala ya kuwa na Rais ambaye anawakilisha asilimia 20 ya Watanzania kiumri.
Hebu tumchambue Zitto Kabwe wakti ungalipo. Lakini, kama atawania urais mwaka 2015, na kama Allah atanijalia uzima, kwa chama chochote au kama mgombea binafsi, ana uhakika wa kura yangu.
Nimefungua mjadala
- See more at: http://www.raiamwema.co.tz/kwa-nini-zitto-anafaa-kuwa-rais-2015#sthash.PdqEx9sd.o3jjMDqa.dpuf

No comments:

Post a Comment