Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Tuesday 19 August 2014

ALBINO WAZUA TAFRANI POLISI BUGURUNI


Dar es Salaam. Watu wenye ulemavu wa ngozi (albino), jana walizua tafrani Kituo cha Polisi Buguruni, wakipinga dhamana kwa mshtakiwa, Ombeni Swai (34), mkazi wa Tabata Matumbi anayekabiliwa na kesi ya kutoa vitisho vya kumuua mwenzao.
Tafrani hiyo ilianzia katika Mahakama ya Mwanzo Buguruni baada ya mshtakiwa huyo kusomewa mashtaka na Karani wa Mahakama, Edwin Wandanda na kisha Hakimu Mfawidhi, Benjamin Mwakasonda aliyekuwa akiisikiliza kusema dhamana ya mshtakiwa iko wazi.
Ingawa mshtakiwa alishindwa kutimiza masharti ya dhamana, albino waliokuwapo mahakamani hapo hawakufurahishwa na kitendo cha kuwapo kwa nafasi ya dhamana kwa mshtakiwa wakidai kwamba ameshatoa vitisho vya mauaji dhidi yao.
Baada ya kulalamika mahakamani hapo waliandamana hadi kituoni hapo ambako mshtakiwa alikuwa amepelekwa hali iliyosababisha polisi kituoni hapo kutumia risasi za baridi kuwatawanya na kusababisha taharuki kwa wafanyabiashara na wakazi wa eneo hilo.
Mwandishi wetu alishuhudia baadhi ya watu wakiwa wamesimama, wengine wakikimbia ovyo huku polisi wakiwa silaha.
Kamanda wa Mkoa wa Polisi Ilala, Mariam Nzuki alisema vurugu hizo ziliongezeka baada ya kundi la vijana wa sokoni kuungana nao.
Alisema baada ya polisi kuona hivyo, walitumia mabomu ya machozi kuwatawanya na kumpeleka mtuhumiwa katika Mahabusu ya Segerea.
Hati ya mashtaka
Mshtakiwa anadaiwa kuwa Agosti 16, mwaka huu maeneo ya Buguruni kwa Mkanda alitishia kuua kwa maneno watu wenye ulemavu wa ngozi katika maeneo hayo.
Hati hiyo inadai kuwa mshtakiwa alimtishia kwa maneno mlalamikaji, Mwinyiusi Issa kuwa atamuua kama anavyoua albino.


Mengi ajitolea
Wakati hayo yakitokea, Mwenyekiti Mtendaji wa Kampuni za IPP, Reginald Mengi amejitolea kuwasomesha watoto wawili wa albino Suzan Mungi, aliyekatwa kiganja cha mkono na watu wasiojulikana wilayani Igunga mkoani Tabora.
Akizungumza jana, Mengi alisema amesikitishwa na tukio hilo ambalo mume wa Suzan, Mapambo Mashili aliuawa wakati akijaribu kumtetea ili asifanyiwe ukatili huo.
“Sina mamlaka ya kuwaadhibiti wahalifu hawa lakini naahidi kutoa Sh10 milioni kwa mtu atakayewezesha kukamatwa kwao, Serikali inapaswa kuwashughulikia wahusika wote yaani wanaofanya ukatili huo, wanaohitaji viungo hivyo na waganga wa kienyeji,” alisema.


Imeandikwa na Kelvin Matandiko, Beatrice Moses, Ismail Gass na Salim Shao
CHANZO: MWANANCHI: http://www.mwananchi.co.tz/habari/Kitaifa/Albino-wazua-tafrani-Polisi-Buguruni-/-/1597296/2423706/-/ahsvaaz/-/index.html

No comments:

Post a Comment