Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Wednesday 27 August 2014

NAWAKUMBUSHA TU: SABABU NI MOJA, NYERERE ALIMCHUKIA MALECELA KWA KUKUBALI HOJA YA TANGANYIKA BUNGENI


 MAMBO YALIVYOKWENDA 

WAZIRI Mkuu alipohisi kuwa baadhi ya mawaziri walikuwa wanaunga mkono hoja ya Serikali ya Tanganyika,
(i) Alimwarifu Rais na kupendekeza ifanyike Semina kama mbinu ya kupinga hoja hiyo. Hii ilikuwa hatua sahihi.
(ii) Alipaswa kumshauri Rais kuitisha kikao cha Baraza la Mawaziri, ili wale watakiwe kuweka msimamo na mkakati wa pamoja wa kupinga hoja ya Serikali Tatu. Hakufanya hivyo; lilikuwa kosa.
(iii) Baada ya Rais na mimi kusema na Wabunge, na kupinga hoja ya Utanganyika, Waziri Mkuu alipoona kuwa mawaziri wahusika bado wanaendelea na msimamo wao, angeitisha kikao cha Baraza la Mawaziri, ili mawaziri hao watakiwe kueleza msimamo wao Serikali inayo kanuni ya msimamo wa pamoja wa Kabineti nzima.
Katika suala kubwa kama hili Waziri Mkuu, Msimamizi wa Shughuli za Serikali Bungeni, akijua kuwa baadhi ya wenzake walikuwa wanaendelea kuunga mkono hoja ya Serikali Tatu, alikuwa na haki na wajibu wa kudai kanuni hii ya msimamo wa pamoja ifuatwe. Rais angetazamiwa kumuunga mkono. Lingekuwa jambo la ajabu sana kama baada ya maagizo ya Kamati Kuu ya Chama, na Rais mwenyewe kuipinga hoja ya Serikali Tatu Bungeni, angemgeuka Waziri Mkuu wake anayeendeleza msimamo huo, na hivyo akamfedhehesha na kujifedhehesha yeye mwenyewe kwa kukubaliana na msimamo wa mawaziri wapinzani.
(iv)(a) Kama mawaziri wapinzani wangeamua kubadili msimamo wao, Baraza zima la Mawazili lingekwenda Bungeni na kupinga kwa pamoja hoja ya Utanganyika.
(b) Kama mawaziri wapinzani wangekataa kubadili msimamo wao, (na mimi siamini kuwa angetokea hata waziri mmoja ambaye angefanya hivyo), basi ama mawaziri hao wangejiuzulu na kueleza sababu zao, au Rais angewafukuza na kueleza kwa nini. Angeteua mawaziri wapya wenye msimamo wa Chama, na Serikali ingekwenda Bungeni mawaziri wake wale wakiwa na msimamo mmoja na mkakati mmoja wa kupinga hoja ya Utanganyika.
Basi kama Wabunge wahusika wangeng'ang'ania hoja yao ijadiliwe, Serikali ingeipinga kwa pamoja, ingeungwa mkono na wabunge walio wengi, wa Bara na Visiwani, na hoja hiyo ingekufa kifo cha kawaida. Na huo ndio ungekuwa mwisho wa ngoma hizi.
Viongozi wetu walijua hivyo. Wabunge wale, pamoja na wabunge wenye hoja walijua hivyo: siyo kwamba Serikali ikipinga hoja haitapita; bali wote waliamini na walitazamia kuwa Serikali itaipinga hoja ya Serikali Tatu, na hoja hiyo haitapitishwa na Bunge.
Badala yake Serikali ikaamua kusarenda. Viongozi wetu waheshimiwa, kwa sababu wanazozijua wao wenyewe, ambazo mpaka sasa hawataki au hawawezi kulieleza Taifa, wakaona kuwa hoja ya Utanganyika haizuiliki; wakakubali kushindwa, wakajitolea. Wakaamua kumshauri Rais wetu. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Jemadari Mkuu wa Majeshi yetu, aliyechaguliwa na Watanzania akaapishwa kwa Katiba ya Nchi yetu na Msahafu wa Mwenyezi Mungu ailinde Tanzania; wakamshauri akubali hoja ambayo wanafahamu kuwa ikitekelezwa, itavunja nchi yetu.
Lakini viongozi wetu waheshimiwa baada ya kusarenda kwa aibu hivyo, hawataki kukubali matokeo ya kusarenda kwao. Wanaendelea kutuongoza katika kikao kile kile cha Bunge Waziri Mkuu huwezi ukamshauri Rais wako kupinga, halafu baada ya siku chache tu, wewe, huyo huyo umshauri Rais huyo huyo kukubali hoja hiyo, ambayo juzi tu ulimshauri na kumwomba kupinga, na akapinga; na bado ukabaki na wadhifa wako.
Ama ushauri wako wa awali haukuwa sahihi, na wajibu wako ni kujiuzulu; au ulikuwa sahihi, lakini ukashindwa kuutetea na wajibu wako ni kujiuzulu. Huwezi kuendelea kuongoza Serikali. Ama umwachie Waziri Mkuu mwingine anayeweza kutetea msimamo wa awali; au umwachie mwingine anayeweza kumpa Rais ushauri huu wa pili. Wewe huyo huyo huwezi kushindwa kuutetea ushauri wako wa awali, halafu umshauri Rais akubali ushauri ulio kinyume cha ule wa kwanza, na utazamiwe kuwa huo sasa utautetea. Utakuwa Saulo aliyeona mwangaza akageuka kuwa Paulo!
Lakini hata yeye wale aliokuwa akiwatesa awali waliendelea kuwa na mashaka naye kwa muda mrefu sana, mpaka akasaidiwa kwa miujiza ya Mwenyezi Mungu. Katika siasa hatuwezi kutegemea miujiza hiyo. Lazima tuhukumu kwa kutumia akili zetu za kawaida.
Ushauri wa pili, ambao ni kinyume cha ule ushauri wa kwanza, ulitakiwa utolewe na Waziri Mkuu mwingine, baada ya kujiuzulu kwa Waziri Mkuu aliyetoa ushauri wa kwanza. Hii ndiyo maana ya kuwajibika.
Kwa maana ya kwanza ya kujiuzulu, yaani maana ya kuacha kazi, Waziri Mkuu hajajiuzulu, maana bado ana cheo hicho; hajakiachilia au kukisarenda. Lakini kwa maana ya pili ya kujiuzulu: yaani maana ya kukata tamaa, na kukubali kuwa Utanganyika hauzuiliki, na hoja ya Serikali Tatu haipingiki, Waziri Mkuu alikwisha kujiuzulu zamani pale alipotishwa au alipoambiwa: 'Wenzake wale wamekwisha kukubali kwamba hoja ya Serikali Tatu haizuiliki na wao wataiunga mkono; na wewe usipobadili msimamo wako ukakubaliana nao utaachwa katika mataa:', hakulazimika kusarenda - kutupa silaha chini.
Alikuwa na hiari ya kuendelea kutetea msimamo wa Chama; Maagizo ya Kamati Kuu, na kauli ya Rais wake mbele ya Wabunge. Alikuwa na hiari ya kuwakumbusha Wabunge waheshimiwa hotuba yake ya tarehe 30, Aprili, 1992; na msimamo wa Chama chao kuhusu suala la Serikali Tatu. Alikuwa na hiari kuamua kuachwa katika mataa. Hakufanya hivyo. Badala yake aliamua kusarenda. Aliacha msimamo wa Chama na, Rais wake, akakubali msimamo wa Wabunge wenye hoja ya Utanganyika.
Huwezi kujiuzulu kwa maana hii ya kusalimu amri, kukubali kuwa umeshindwa, halafu usilazimike kujiuzulu kwa maana ya kuiacha hiyo kazi iliyokushinda. Ukisha kubwaga silaha lazima ukubali kuwa mateka. Waingereza wana msemo: huwezi kula kekiyo kisha ukabaki nayo. Na akina mama wa Kiswahili husema: Uliyataka mwenyewe, mambo ya kuolewa!
Kujiuzulu, kwa maana ya kuacha kazi, ni matokeo tu ya kujiuzulu kwa maana ya kushindwa kazi. Kazi hii imekushinda, ondoka! Hiyo ndiyo maana ya kuwajibika.

REJEA: NYERERE, J.K.; UONGOZI WETU NA HATMA YA TANZANIA (1994)

No comments:

Post a Comment