Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Friday 30 October 2015

UCHAGUZI MKUU 2015: HUKU VILIO, KULE VICHEKO!

 
 Steven Wassira - Nje
Abbas Mtemvu - Nje
 Zitto Kabwe - Ndani
Bonna Kaluwa - Ndani


Na Daniel Mbega

UCHAGUZI mkuu umekwishapita, matokeo yametangazwa na tunashuhudia vilio na vicheko kutoka sehemu mbalimbali nchini – iwe kwenye udiwani, ubunge na hata urais.
Ingawa Chama cha Mapinduzi (CCM) kimeshinda viti vingi vya udiwani na ubunge, lakini binafsi nasema kimeshindwa vibaya kwa sababu safari hii tumeshuhudia ikipoteza halmashauri takriban 19 huku wapinzani wakizoa viti vingi vya ubunge kuliko ilivyowahi kutokea tangu kuanza kwa uchaguzi mkuu wa vyama vingi mwaka 1995.

Hili ni funzo kubwa kwa CCM, ambayo kama ilikuwa inadhani inaendelea kutawala kwa mfumo ule wa kizamani, inaweza ikapotea kabisa mwaka 2020 ikiwa haitafanya jitihada za makusudi kujikosoa, kujisahihisha na kutekeleza ahadi zake kwa vitendo.
Kinyume chake, chama hiki ambacho ni kikongwe kabisa barani Afrika, kinaweza kujikuta kikisukumwa pembeni kwa sababu Watanzania wameamka kidemokrasia na zaidi wanataka serikali inayowatumikia.
Najaribu kuangalia tu katika orodha ya wabunge wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania waliotangazwa baada ya uchaguzi wa Oktoba 25, 2015.

Vilio na vicheko
Ingawa CCM inachekelea kuyakomboa majimbo kadhaa yaliyokuwa yanashikiliwa na upinzani, hususan ya jijini Mwanza (Ilemela na Nyamagana), Kigoma Kusini, Kasulu na Lindi Mjini, lakini inalia kwa sababu imepoteza majimbo muhimu kabisa hasa ya mkoani Dar es Salaam.
Chama hicho kimepoteza jimbo jipya la Kibamba, lakini pia majimbo ya zamani ya Ukonga, Temeke na Kionondoni, huku ikishindwa kulikomboa Jimbo la Kawe ambalo limeendelea kushikiliwa na Halima Mdee wa Chadema wakati Jimbo la Ubungo limetua tena Chadema, safari hii chini ya mwanahabari-mwanaharakati Saed Kubenea.
Majimbo ya Kinondoni na Temeke yamenyakuliwa na CUF wakati majimbo ya Ukonga, Ubungo, Kawe na Kibamba yamechukuliwa na Chadema, huku CCM yenyewe ikichukua majimbo ya Kigamboni, Ilala, Mbagala na Segerea pekee.
Zaidi ya hayo, CCM imepoteza Jimbo la Same Mashariki, Moshi Vijijini, Siha, Babati Mjini, Arumeru Magharibi, Longido, Monduli, Iringa Mjini, Muleba Kaskazini, Buyungu, Kigoma Mjini, Bukoba Mjini na mengineyo.
Kwa ujumla, mpaka tunakwenda mitamboni, CCM ilikuwa imepoteza majimbo 42 Tanzania Bara, wakati ambapo mwaka 2010 ilipoteza majimbo 27 tu.
Wanaolia mmoja mmoja kwa CCM ni Namelock Edward Sokoine, Abasi Zuberi Mtemvu, Iddi Azzan, Mwakalebela Fredrick Wilfred, Balozi Khamis Sued Kagasheki, Christopher Chiza, Aggrey Mwanri, Anne Kilango Malecela, Dk. Cyril Chami, Said Mtanda, Murtaza Ally Mangungu, Steven Wasira, Dk. Steven Kebwe, Kisyeri Chambiri, Christopher Olonyhokie Ole Sendeka, Weston Godfrey Zambi.
Lakini kwa upande mwingine, wapinzani wanachekelea huku wakijifuta machozi, kwa sababu licha ya kuongeza majimbo, imejikuta ikipoteza majimbo mengine muhimu kabisa.
CUF imeongeza majimbo manne mwaka huu na kufikisha matano, lakini jambo baya ni kwamba, imepoteza Jimbo la Lindi Mjini ambalo limerejea CCM, huku ikishangilia kupata majimbo matatu katika mikoa muhimu ya Tanga na Dar es Salaam. Chama hicho kimeshinda ubunge Tanga Mjini, Kinondoni na Temeke, huku pia kikipata viti vipya Mtwara Mjini, Tandahimba, Kilwa Kaskazini, na Mchinga.
Chadema wamenufaika zaidi na ujio wa Edward Lowassa kwani wamepata viti 35 ukilinganisha na viti 22 vya mwaka 2010. Hii maana yake ni kwamba, bado kitaendelea kuwa chama kikuu cha upinzani bungeni, kwani kikipata na wabunge wa kuteuliwa kinaweza kufikisha wabunge 55.
Ikiwa Ukawa wataendelea na mshikamano wao huo wa sasa, basi wanaweza kutengeneza ngome imara bungeni kwa sababu watakuwa na wabunge pengine 100 hivi kutokana na ukweli kwamba, mpaka sasa wana wabunge 62 wa majimbo (Chadema 35, CUF 26 na NCCR 1).

Sura ngeni tupu
Bunge la 11 linatarajiwa kutumia muda kwa wajumbe wake kuzoeana, kwani takwimu zinaonyesha kwamba, walio wengi ni wageni kabisa japokuwa wapo baadhi ambao wamerejea.
Kwa kuangalia takwimu, inaonysha kwamba 95 ya wabunge wa mwaka huu ni wapya kabisa, ambao watahitaji muda kidogo wa kujifunza Kanuni za Bunge wakati wenzao wengine tayari wamekwishazielewa na watakuwa wakijikumbusha tu.

Uwiano
Bunge la safari hii halina ule uwiano wa jinsi katika nafasi za uchaguzi, kwani takwimu zinaonyesha kwamba, kuna wabunge 19 tu wanawake walioshinda kwenye majimbo, ambapo kati yao 13 ni wa CCM na waliobaki wa Chadema.
Kama Katiba Mpya hasa Rasimu ya Pili ingepitishwa, maana yake Bunge la 11 lingekuwa na wanawake wachache zaidi, lakini sasa kwa kutumia Katiba ya Mwaka 1977, bado wataongezeka wabunge 72 ambapo kati yao 62 ni wa Viti Maalum na 10 wa ‘Kapu la Rais’.

Matokeo ya ajabu
Katika uchaguzi wa mwaka huu, kumekuwepo na matokeo ya ajabu kwenye ubunge, hasa baada ya kushuhudia wanasiasa kama Wasira, Dk. Didas Masaburi, Mwanri, Dk. Chami, Abbass Mtemvu, Christopher Chiza na Hezekiah Wenje waking’olewa katika nafasi zao.
Lakini pia ni uchaguzi ulioshuhudia wanasiasa wapya wakiibuka kutoka kusikojulikana na kufanya vizuri zaidi.
Wengi kati yao ni kutoka upinzani, baadhi yao ni pamoja na Gibson Ole Mesiyeki (Arumeru Magharibi), Wille Qambalo (Karatu), Saed Kubenea (Ubungo), Bonna Mosse Kaluwa (Segerea), Abdallah Mtolea (Temeke), Maulid Mtulia (Kinondoni), Antony Mavunde (Dodoma Mjini), Sanda Edwin (Kondoa Mjini), Cosato Chumi (Mafinga Mjini), Bilago Samson (Buyungu), Dk. Godwin Mollel (Siha), Nangejwa Kaboyoka (Same Mashariki), Hassan Bobali (Mchinga) na Emmanuel Papiani (Kiteto).
Hii inaonyesha kwamba demokrasia imekua na Watanzania wanazidi kukomaa kisiasa hasa katika kipindi hiki ambacho serikali ya awamu ya nne imejitahidi kuweka uwazi katika masuala mengi ikiwemo utawala bora.

Kwa mantiki hiyo, ni dhahiri siasa zikifanywa kwa uadilifu, uwazi na uaminifu wananchi wanaweza kushuhudia maendeleo katika huduma mbalimbali za kijamii.

CREDIT: UWAZI MIZENGWE

No comments:

Post a Comment