Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Saturday 24 October 2015

TUJIEPUSHE NA KURA ZA LIWALO-NA-LIWE!

Ikulu ya Tanzania

Na Mkimbu Lukule
Tangu kuanza harakati za uchaguzi Tanzania kumekuwa na tambo nyingi za kuwanadi wagombea.  Kila kundi likitaka mgombea wao ang’ae dhidi ya mwenzake.  Zimekuwepo mbinu na hadaa nyingi katika kufanikisha malengo haya ya kisiasa.
Wapo ambao wamekuwa wakifanya kampeni zao kwa kutoa ahadi lukuki ambazo zinalenga katika kuwaaminisha wananchi kuwa wakichaguliwa wataibadilisha nchi kwa haraka na kuifanya ifike katika kilele cha maendeleo.
Kampeni hizi zimeshuhudia pia kupakana matope, kusifiana na kupondana baina ya wapambe wa wagombea Urais.  Ni wazi kuwa kila upande unajaribu kuonyesha kuwa wapinzani wao hawajui, hawafai na hawawezi.  Kwamba ili maendeleo yapatikane ni lazima mgombea wanayemnadi achaguliwe kuwa Rais.
Mitaani nako kumeibuka hali ya sintofahamu na ushabiki.  Zimekuwepo kauli kuwa huu ni wakati wa ‘mabadiliko’. Kwamba iwe isiwe ni zamu yetu kuingia ikulu.  Kwamba hata likiwekwa jiwe au mbuzi na chama fulani, sisi tutalichagua jiwe au tutampigia kura mbuzi.
Ushabiki wa aina hii umeibua maswali kwa wadau mbalimbali wa demokrasia.  Tumeona wachambuzi wa kisiasa wakijitokeza kwenye vyombo vya habari na kujadili kuhusu hali hiyo.  Miongoni mwa wachambuzi hao yupo Johnson Mbwambo wa gazeti la Raia Mwema.
Mwambo amekuwa akiandika uchambuzi wa mara kwa mara kuhoji uhalali wa Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA) kumchagua Edward Lowassa,  mtu ambaye wapinzani wao yaani Chama Cha Mapinduzi, walimuengua kwa kigezo cha kukosa maadili na kuwa na kashfa nyingi za ufisadi.
Ukiachilia mbali Mwambo, Mchungaji Christopher Mtikila wa Chama cha Demokrasia (DP), mchambuzi wa kwenye mtandao wa Jamii Forums, Mwanakijiji,  aliyekuwa Katibu Mkuu wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo, Dkt. Wilbroad Slaa na aliyekuwa Mwenyekiti wa Chama Cha Wananchi (CUF), Prof. Ibrahim Lipumba nao wametoa kauli ambazo zimekinzana na uamuzi wa UKAWA kumsimamisha Lowassa.
Miongoni mwa sababu ambazo wadau hao wamezitoa ni kuwa, kabla ya Lowassa kujiunga UKAWA, ajenda kubwa ya vyama vya upinzani ilikuwa ni ufisadi na matumizi mabaya ya fedha za umma, lakini kujiunga kwa Lowassa kunasababisha wabadilishe ajenda.
Katika mazingira haya, viongozi hawa waliojitoa wameeleza kuwa hapo awali wakati wanaitengeneza UKAWA waliijenga kwa kanuni na misingi lakini lilipokuja suala la kumkaribisha Lowassa walijikuta wakivunja misingi waliyojiwekea. 
Mosi, Lipumba anasema kuwa Lowassa alikuwemo katika Bunge Maalum la Katiba lililobariki muungano wa Serikali mbili ambao UKAWA waliupinga na alikaa hadi mwisho wa bunge hilo.  Pili, Dkt. Slaa alisema kuwa CHADEMA walimtaja Lowassa katika orodha ya mafisadi wakubwa waliofilisi nchi na ameendelea kumshtumu Lowassa, kwa nyakati tofauti, kuwa amejihusisha na vitendo vya ufisadi mahala mbalimbali kwa nyakati tofauti.
Wote hawa wanaompinga Lowassa, wanasema kuwa haikuwa tatizo kwa UKAWA kumpokea Lowassa ila kitendo cha kumpokea na moja kwa moja kumkaribisha na kumpa nafasi ya kuwa mgombea Urais, kimeibua udhaifu mkubwa wa wapinzani hao.  Kwamba hadi kufikia hatua wapinzani wao wanafanya mchakato wa kumpata mgombea Urais wao walikuwa bado hawajaweza kuwa na mtu ambaye alikuwa na vigezo stahiki vya kusimama katika nafasi hiyo kubwa ya Urais.
Jambo la kushangaza UKAWA inaundwa na vyama vya kisiasa vyenye nguvu ambavyo baadhi ya wagombea wake kwa nyakati tofauti wamesimama dhidi ya CCM na kusababisha ushindani mkali.  Aliweza kufanya hivyo Prof. Lipumba, aliweza kufanya hivyo Dkt. Slaa na walipata kura nyingi.
Kutokana na sintofahamu hii ndipo inapoibuliwa hoja ya kuwa Je, kuna baadhi ya wanasiasa wanaounda UKAWA walipokea fedha ili kufanikisha Lowassa awe mgombea Urais? Ama ni ushawishi gani wa kisera na kimkakati, mgombea huyo aliingia nao Ukawa na kusababisha apewe dhamana hiyo?
Kwa upande wa wana mabadiliko wanatetea ujio huo wa Lowassa kwenda UKAWA wakisema kuwa kutokana na mzingira yaliyopo, ujio wa Lowassa ukawa na kuteuliwa kwake katika nafasi ya kugombea Urais ni vitu ambavyo visingeweza kuepukika.
Hoja yao ni kuwa CCM imekuwepo madarakani miaka mingi na imefanya mabaya mengi na kwamba imefika wakati kuwa wapumzishwe kwa njia yoyote ile.  Katika hili wapo wengi miongoni mwao yupo Freeman Mbowe-Mwenyekiti wa CHADEMA Taifa, Peter Msigwa- mbunge wa Chadema Iringa mjini, Tundu Lissu-mbunge wa CHADEMA Singida, Jenerali Ulimwengu – mchambuzi wa gazeti la Raia Mwema na wengineo.
Watoa hoja hii ya mabadiliko wanaeleza kuwa kwa hali ya nchi ilivyo sasa wanaamini kuwa ni wakati pekee wa kuing’oa CCM kwasababu imegawanyika.  Ni wazi maelezo yao yanarejea kujiengua kwa waliowahi kuwa mawaziri wakuu wawili Tanzania kupitia CCM, Lowassa na Frederick Sumaye ambao wamejiunga Ukawa.
Ukiyapitia maelezo ya ‘wanamabadiliko’ ni kama vile wanasema kuwa kabla ya kuja kwa Lowassa UKAWA na vyama vilivyoungana havikuwa na uwezo wa kusimamisha mgombea mwenye nguvu ya kushinda katika ngazi ya Urais. 
‘Wanamabadiliko’ wameamua kuachana na ajenda ya ufisadi na badala yake wameeneza falsafa mpya kuwa nchi imechoshwa na utawala wa chama kimoja kwa maana hiyo inahitaji mbadala wa fikra.  Hata hivyo, wanashindwa kujibu swali la Je, kuwachukua wagombea walioshindwa kura za maoni kwenye vyama vyao ndiyo kuleta fikra mpya?
Kutokana na hali hiyo nchi imeingia katika sintofahamu kubwa ambapo vijana na wananchi wa kawaida wamejikuta wakiburuzwa na falsafa na misemo ambayo hawaielewi.  Watu wanalishwa neno ‘mabadiliko’ lakini hawaelewi mapana ya dhana ya neno hilo la mabadiliko. Wanaenda kulingana na upepo wa kisiasa ambao hawaujui hatma yake.
Wakati huu nadhani kwa wanasiasa ni wakati wa kuvuna walichopanda, kama mtu alipanda bangi atavuna bangi. Kiongozi tunayemtaka ni yule ambaye uwajibikaji wake na uadilifu wake utakuwa chachu kwa Watanzania wenyewe kujiletea maendeleo, kwani nchi haiendelezwi kwa hela za mtu binafsi.

Mwandishi wa makala hii ni msomaji wa blog hii, anapatikana kwa barua pepe 
mkimbulukule70@gmail.com

No comments:

Post a Comment