Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Tuesday 23 December 2014

DODOMA MABINGWA COPA-COCA-COLA

Wachezaji wa timu ya Dodoma wakifurahia baada ya kukabidhiwa zawadi zao za ubingwa wa michuano ya Copa Coca Cola baada ya kuibuka mabingwa wa mashindano baada ya kuichabanga Kinondoni mabao 3-0. (Picha kwa hisani ya issamichuziblog).

TIMU ya Mkoa wa Dodoma wametawazwa rasmi kuwa mabingwa wapya wa michuano ya Copa-Coca- Cola kwa vijana wenye umri chini ya miaka 15, baada ya kuibuka na ushindi mnono wa mabao 3-0 dhidi ya timu ya Kinondoni, katika mchezo uliofanyika Uwanja wa Karume jijini Dar es Salaam.

Katika mchezo huo ambao ulihudhuriwa na mashabiki wengi kutoka jijini Dar es Salaam, Dodoma ambao ndiyo mara ya kwanza kuingia fainali kwenye michuano hiyo, walionekana kuwa na njaa ya ushindi tangu dakika ya kwanza huku wakipeleka mashambulizi ya nguvu na yaliyokuwa na madhara langoni mwa Kinondoni.

Alikuwa ni Pius Raphael ambaye aliiandikia Dodoma bao la kwanza dakika ya sita, baada ya kupiga mpira wa adhabu na kupenya moja kwa moja langoni mwa Kinondoni, Timothy Joseph aliiandikia Dodoma bao la pili kwa kichwa dakika 26 baada ya kuunganisha mpira uliopigwa na Pius Raphael.

Raphael kwa mara nyingine tena akihitimisha karamu ya mabao kwa kuifungia Dodoma la tatu dakika ya 35 kutokana na mpira wa kona aliopiga na kuingia moja kwa moja langoni.

Kabla ya kuingia fainali ya michuano hiyo Dodoma waliweza kuzitoa timu ngumu za Morogoro katika hatua ya robo fainali na Kigoma hatua ya nusu fainali huku Kinondoni, wakizitoa timu za Simiyu.

Akizungumza mara baada ya mchezo huo Kocha Mkuu wa Dodoma, Mussa Furutuni alisema maandalizi ya muda mrefu waliyofanya ndiyo sababu kubwa ya mafanikio na ushindi kwa timu yake na kuongeza kuwa kutopewa nafasi kubwa ya ushindi kwa timu za mikoani ilikuwa ni chachu ya ushindi kwa timu yake.

"Tumeweza kukaa kambini kwa muda wa miezi sita kwa sababu ya maandalizi ya michuano hii kwa nini tusishinde? Ni haki yetu kabisa kuwa mabingwa," alisema Furutuni.

Kwa upande wake kocha wa Kinondoni, Everist Katomondo alisema wameshindwa kihalali mchezo huo na mchezo ulichezeshwa bila ya upendeleo wowote.

Katika mchezo wa fainali kwa upande wa wasichana timu ya Kinondoni, iliwafunga ndugu zao wa Ilala kwa changamoto ya mikwaju ya penati mara baada ya kufungana mabao 2-2 katika muda wa kawaida.

Mchezo wa kutafuta mshindi wa tatu ulizikutanisha timu za Kigoma na Kusini Pemba, Kigoma walishinda kwa mabao 3-1.

Baada ya michezo yote kumalizika wachezaji mbalimbali waliweza kutwaa tuzo za michuano hiyo.

Kwa upande wa mchezaji bora kwa wasichana, Zubeda Mohamedi wa Kinondoni alitwaa tuzo hiyo wakati Mwami Ismail wa Kigoma akitoka upande wa wavulana na wote walizawadiwa sh. 500,000.

Kipa bora alikuwa Suleza Saadi kutoka Zanzibar huku, Abdallah Mbarouk pia kutoka Zanzibar akitunukiwa kuwa mwamuzi bora.

Tuzo kwa timu yenye nidhamu ilikwenda kwa Mbeya upande wa wasichana na kupata sh. 500,000 wakati kwa upande wa wavulana ikipewa Tanga na kuzawadiwa sh. milioni moja.

Temeke ilikuwa mshindi wa tatu kwa upande wa wasichana na kupewa sh. 2,000,000 na Kigoma kwa upande wa wavulana walipewa sh. 3,000,000.

Kwa upande wa mshindi wa pili timu ya wasichana ya Ilala ilizawadiwa sh. 3,000,000 wakati kwa upande wa wavulana Kinondoni ikipata sh. 5,000,000.

Mabingwa wa michuano hiyo kwa upande wa wasichana, Kinondoni walizawadiwa sh. 5,000,000 huku Doodma wakizawadiwa 8,000,000 kwa upande wa wavulana.

Akizungumzia michuano hiyo Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Jamal Malinzi alisema wachezaji wote bora wa michuano hiyo tayari wameshachaguliwa na wanatarajia kuanza kambi mjini Bagamoyo huku akisisitiza kuwa nia ya mashindano hayo ni kukuza vipaji na kuwanyooshea vidole wote walioleta wachezaji waliozidi umri.

Naye Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo Dkt. Fenella Mukangara, alisema amefurahishwa na vijana kwa kuonesha soka safi na lenye kuvutia pamoja na kuipongeza TFF na Coca-Cola kwa kutoa ushirikiano katika kuhakikisha taifa linasonga mbele katika nyanja ya michezo.

CREDIT: MAJIRA

No comments:

Post a Comment