Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Saturday 20 December 2014

ROSE MUHANDO, MARTHA MWAIPAJA, SOLOMON MUKUBWA KUWASHA MOTO

Solomon Mukubwa

Waimbaji mahiri wa muziki wa injili, Solomon Mukubwa, Rose Muhando na Martha Mwaipaja wataongoza shamrashamra za Tamasha la Krismasi katika mikoa ya Nyanda za Juu kusini.
Tamasha la Krismasi mwaka huu litafanyika katika mikoa ya Mbeya, Iringa na Ruvuma.
Mwimbaji Rose Muhando anayetamba na wimbo Wololo amesema anakusudia kufunga mwaka kwa staili ya aina yake na mashabiki wa muziki huyo katika mikoa yote atakayotumbuiza.
Rose atakayepanda jukwaani kuanzia Desemba 25, Agosti 3, mwaka huu alizindua albamu yake Kamata Pindo la Yesu yenye nyimbo za ‘Facebook’, ‘Bwana Niongoze’, ‘Wewe Waweza’, ‘Usiniache’, ‘Nibariki na Mimi’, ‘Usivunjike Moyo’ na ‘Kwema’.
Martha Mwaipaja apania kuburudisha
“Tamasha linafanyika siku maalumu ambayo Yesu Kristo amezaliwa, nitatoa huduma kwa njia ya uimbaji naomba wakazi wa mikoa yote mitatu wafike kwa wingi wale ambao hawanifahamu pia watanifahamu siku hiyo na wataguswa na kupata ujumbe uliotukuka,” anasema mwimbaji Martha Mwaipaja.
Mwimbaji huyo anasema kuwa amejipanga vilivyo ikiwa pamoja na kufanya maandalizi ya hali ya juu na akisisitiza kuwa atafanya makubwa katika Tamasha la Krismasi ambalo litakuwa la pili kufanyika.
Mwaipaja anasema kuwa anawaomba mashabiki wafike kwa wingi kwa sababu amepewa nafasi hiyo ya kulihubiri neno la Mungu kupitia uimbaji hivyo yupo kwa ajili yao ni vyema wakajitokeza kwa wingi kupata upako.
“Naimba kwa ajili ya kumtumikia Mungu, natoa huduma kwa njia ya uimbaji hivyo Watanzania wajitokeze siku hiyo muhimu ya kuzaliwa kwa Yesu naamini watafurahi kwa jinsi ninavyofanya maandalizi ya tamasha hili kubwa ambalo limepangwa kufanyika siku yenye Baraka za Mungu.”
Joshua Mlelwa hamtajuta
Mwimbaji anayekuja kwa kasi katika muziki wa injili,  Joshua Mlelwa amesema Watanzania watakaojitokeza katika tamasha hilo hawatajutia kuhudhuria kwa kuwa amewaandalia burudani adimu.
Mlelwa ambaye anatamba na vibao mbalimbali kikiwamo cha ‘Mambo Sawasawa’ anasema anafanya maandalizi yake ya kutosha ikiwamo kufanya mazoezi na timu yake mpya.
Anasema Watanzania watapata  vitu vipya siku hiyo kwa kuwa amepata muda wa kutosha kufanya maandalizi ya muda mrefu ukizingatia kuwa ana timu mpya atakayofanya nayo kazi ya kuhubiri neno la Mungu kupitia njia ya uimbaji. “Maandalizi yangu ni ya kutosha pamoja na mazoezi, sina cha kuwaeleza zaidi ya kupata kitu maalumu ambacho nimeawaandalia na timu yangu mpya ambayo iko vizuri,” anasema Mlelwa.
Anasema tangu ameanza muziki wa injili ni nyimbo nyingi ameimba lakini katika tamasha hili kuna nyimbo mpya ambazo ataimba, huku akisisitiza hasa kwa wakazi wa mkoa wa Iringa ambako hajahudumu muda mrefu.
Mwimbaji huyo alizitaja baadhi ya nyimbo anazotarajia kuimba katika tamasha hilo inalofanyika katika  uwanja wa Sokoine Mbeya, Desemba 25 wakati Iringa litafanyika Desemba 26 katika Uwanja wa Samora pia, litahitimishwa katika Uwanja wa Majimaji wilayani Songea Mkoa wa Ruvuma Desemba 28. Nyimbo atakazoimba ni pamoja na ‘Kaa salama’, ‘Bam bam’, ‘Yesu ni yeye Yule’, ‘Ni Wewe’ na ‘Haleluya Ameni’.
“Wito wangu kwao wajitokeze kwa wingi kwenye tamasha ambalo linafanyika kwa mwaka mara moja, kwa siku ambayo Yesu anazaliwa, waje wapate vitu freshi vya moto kabisa hakuna kujiuliza mara mbilimbili hawatajutia kuhudhulia,’ anasema.
Mwasabwite kuitoa ‘Mungu Amenihurumia’
“Hapa nilipo mimi ni kwa neema ya Mungu, vile nilivyo mimi ni kwa neema ya Mungu, nimetoka mbali toka mbali toka mbali nimetoka mbali...Ni kwa neema tu na rehema, ni kwa neema tu na rehema...”
Hayo ni baadhi ya maneno katika wimbo ‘Ni kwa Neema na Rehema’ uliomtambulisha kijana Edson  Mwasabwite ambaye kwa sasa ana albumu mbili mojawapo ni kwa Neema na Rehema yenye nyimbo nane ikibebwa na wimbo huo.
Desemba 7 mwaka huu alizindua albamu yake ya ‘Mungu Amenihurumia Asilimia 100’ yenye nyimbo 11.
Tumaini Njole ampa tano Msama
Mwimbaji Tumaini Njole amempa tano, Mkurugenzi wa Msama Promotions Alex Msama kwa nia yake njema anayoionyesha ya kuisaidia jamii kupitia Matamasha ya Krismasi na Pasaka.
Anampongeza Msama kwa kuanzisha matamasha mbalimbali yanayofanyika katika maeneo mbalimbali nchini, kuwa nia na lengo lake ni kupiga vita maovu yanayofanyika kwa jamii.
Msanii huyo mpaka sasa amesharekodi albamu mbili mpaka sasa ambazo ni Pokea Sifa (Mvua za baraka) ikiwa imebeba nyimbo nane na  Sema na Yesu ambayo nayo imebeba nyimbo nane.
Solomon Mukubwa apania kufanya makubwa
Mwimbaji wa nyimbo za injili na mchungaji kutoka nchi jirani ya Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo (DRC) na mwenye makazi yake nchini Kenya, Solomon Mukubwa amepania kufanya shoo ya nguvu katika Tamasha la Krismasi.Ameeleza kuwa katika suala la kumsifu Mungu daima huwa hafanyi utani hivyo siku hiyo atahakikisha kila mmoja atakayefika kuondoka na baraka zake.
Solomon anasema kuwa kipaji chake cha uimbaji amepewa na Mungu ingawa ameweza kuongeza jitihada ili kuweza kufanikisha kipawa hicho.
Anaeleza kuwa pamoja na kuonekana kuwa muimbaji mkubwa, lakini nyimbo zake zimetokana na waimbaji wa injili waliopo Tanzania kwani wana nafasi ya kwanza katika soko la muziki huo Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) na Afrika kwa ujumla.Mwimbaji huyo mwenye ndoto nyingi ikiwemo ya kutaka kufungua kituo cha watoto yatima nchini Tanzania anasema kuwa anaipenda nchi hii kiasi cha kuwa tayari kutoa msaada kwa wahitaji mara kwa mara.“Watanzania hawana mioyo ya kinafiki ni wakarimu, wacheshi na wenye upendo ndiyo sababu mimi napenda kuwa Tanzania na kutoa misada ikiwemo kuweka kituo cha kulea watoto yatima” alisema Mukubwa.

No comments:

Post a Comment