Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Saturday 20 December 2014

MGANDA KIDEDEA SPIKA BUNGE AFRIKA MASHARIKI

Naibu Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki wa Tanzania,Dk Abdalah Sadala (kushoto) akimpongeza Spika mpya wa Bunge la Afrika Mashariki (EALA), Daniel Kidega aliyechaguliwa jana jijini Arusha. Picha na Peter Saramba 
Na Peter Saramba, Mwananchi
Arusha. Dan Kidega (41), ndiye Spika mpya wa Bunge la Afrika Mashariki (Eala), baada ya kupitishwa kwa kauli moja kutokana na kukosa mshindani.
Kidega, raia wa Uganda, msomi wa shahada ya sheria kutoka Chuo Kikuu cha Makerere Uganda, anakuwa mbunge wa nne Eala kushikilia nafasi ya Spika wa Bunge hilo lililoanza tangu mwaka 2002.
Spika mpya anachukua wadhifa huo uliobaki wazi baada ya aliyekuwa Spika, Dk Margaret Zziwa kuondolewa madarakani kwa matumizi mabaya ya madaraka.
Awali, kikao cha Bunge kilichoanza Saa 9:30 alasiri jana, kilitarajiwa kuwapigia kura wabunge wawili kutoka Uganda ili kumchagua mmoja kuwa Spika, lakini Mbunge Chris Opoka-Okumu akajitoa kabla ya zoezi la kura kuanza.
“Kwa sababu Mheshimiwa Kidega (Dan), ndiye mgombea pekee katika nafasi ya Spika, kikanuni anakuwa mshindi wa moja kwa moja katika nafasi hii na kinachofuata ni zoezi la kumwapisha kuwa Spika,” alisema Naibu Katibu wa Bunge, Alex Obatre, ambaye ndiye msimamizi wa uchaguzi.
Awali juzi, wabunge wanne kutoka Uganda walichukua fomu za kuwani nafasi hiyo, lakini hadi Bunge linaanza, wagombea walisalia wawili pekee ambao ni Opoka na Kidega.
Wengine waliochukua fomu lakini wakaishia hatua za awali ni Mike Sebalu na Suzan Nakaukhi.
Kiti cha Spika wa Eala kinashikiliwa kwa kupokezana miongoni mwa wabunge wa kuchaguliwa kutoka nchi tano wanachama wa EAC.
Tanzania ndiyo ilikuwa ya kwanza kushikilia nafasi hiyo kupitia kwa Abdulrahaman Kinana aliyefuatiwa na Abdirahin Abdi wa Kenya, aliyepokewa na Zziwa aliyeng’olewa kwa matumizi mabaya ya madaraka, upendeleo na kauli za kuudhi kwa wabunge na watumishi wa Eala.
Uganda ndiyo yenye zamu ya kushikilia nafasi hiyo, ndiyo maana hata baada ya Zziwa kung’olewa, nafasi hiyo ikajazwa na mbunge kutoka nchini humo.
CREDIT: MWANANCHI

No comments:

Post a Comment