Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Monday 31 March 2014

HUYU NDIYE ABUNUASI!


Ndugu zangu,
Tembea uone, na hasa unapoona mazingira ya asili. Kwa bahati nzuri sisi wengine tulizaliwa porini, maana siyo vijijini, kwa sababu wakati huo hata Vijiji vya Ujamaa vilikuwa havijaanza bado. Huku mjini nilikuja wakati nasoma - muda wote ni Bush, kuchunga ng'ombe na kukutana na hayawani aina kwa aina.
Kwa maana hiyo nimebahatika kuyasawiri mandhari ya asili kabisa ambayo babu zetu walirithishwa na Mwenyezi Mungu mwenyewe. Kufukuzana na mbwa mwitu, mbeha na fisi ilikuwa ni sehemu ya maisha yangu enzi hizo miaka ya 1970. Miungurumo ya simba ilikuwa kama vinubi nyakati za usiku, wakati mwingine walikuja mpaka nyuma ya boma wakivizia ng'ombe wetu.
Wapo wanyama wengi tuliokuwa tukiwaona, walikuwa kama jirani zetu, wengine kama tuliwinda, basi ilikuwa ni kwa ajili ya kitoweo tu, vinginevyo tulipishana nao mwituni bila shida.
Lakini wengi kati ya wanyama hao ni mnyama aitwaye Abunuasi ambaye kwa Kiingereza anaitwa Springhare au Rodent. Mnyama huyu, ambaye kwa jina la kisayansi anajulikana kama Pedetes capensis ambaye anapatikana zaidi Afrika, hasa Kusini na Mashariki mwa bara hilo. Anatokea kwenye jenasi ya Pedetes, familia ya Pedetidae, kundi dogo la Anomaluromorpha na Oda ya Rodentia.
Kwa sasa wanyama hawa, ambao wanafahamika zaidi kama East African springhare, au kwa jina la kitaalamu Pedetes surdaster, wametoweka na ni nadra sana kukutana nao. Mnyama huyo huonekana zaidi nyakati za usiku na ni nadra sana kumuona. 
Lakini baada ya miaka zaidi ya 30 tangu nimuone kwa mara ya mwisho, hatimaye niliweza kumuona Desemba 6, 2013 usiku, pale katika Hifadhi ya Taifa ya Serengeti, ya pili kwa ukubwa nchini Tanzania na ndicho kitovu cha utalii na pato la taifa katika sekta hiyo. Pengine nilikuwa na bahati ya mtende kuota jangwani.
Wanyama hawa wana kawaida ya kulala mchana kwenye mashimo. Wanakula majani, mizizi na mbogamboga, na mara moja moja hula wadudu.
Utamtambua Abunuasi kutokana na mwendo wake, kwani anapenda kurukaruka kwa kutumia miguu yake ya nyuma. Yaani yuko kama Kangaroo, ingawa yeye ni mdogo sana.
Kwa kweli nimefurahi sana mwenzenu, maana nakumbuka mara ya mwisho kumuona ilikuwa takriban miaka 33 iliyopita wakati nikiwa nachunga ng'ombe wa familia enzi hizo.
Nitaendelea kuwapa dondoo mbalimba za yale ninayoyaona.

Ndugu yenu,
Daniel Mbega

No comments:

Post a Comment