Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Monday 26 January 2015

KAZI IMEKWISHA ESCROW!

 
Profesa Sospeter Muhongo akitangaza kujiuzulu wadhifa wake wa uwaziri wa Nishati na Madini Jumamosi, Januari 24, 2015

Na Sophia Yamola
KAZI imekwisha. Waziri wa Nishati na Madini Prof. Sospeter Muhongo amejiuzulu, Baraza la Mawaziri nalo limebadilishwa.

Haya yote yanadhihirisha kukamilika kwa kazi ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) iliyotoa mapendekezo na Bunge kutoa maazimio ya kumtaka Rais Jakaya Kikwete amfukuze kazi waziri huyo, kutokana na kutajwa kwenye kashfa ya akaunti ya Tegeta Escrow.
Lakini Profesa Muhongo naye amesema amemaliza kazi katika wizara hiyo aliyoiongoza kwa kipindi cha miaka miwili na nusu baada ya ‘kutimuliwa’ kwa William Ngeleja.
Kujiuzulu kwa Prof. Muhongo kunaonekana kuhitimisha kilio cha wananchi na watunga sera waliotaka waziri huyo kuwajibishwa, japo kwa muda mrefu hakuwa tayari.
Akizungumzia kujiuzulu kwake, Prof. Muhongo alisema ameamua kuchukua uamuzi huo ili mambo mengine ya kitaifa yasonge.
“Mambo mengi yanaonekana kusimama kwa sababu mijadala mingi ndani ya serikali ni Escrow, ndani ya chama (CCM) ni Escrow, hata Bungeni mjadala ni huo huo tu.
Akizungumza na waandishi wa habari mwishoni mwa wiki iliyopita, kabla hajachukua uamuzi huo alisema inatakiwa ifike mwisho juu ya sakata la Escrow kwani wananchi wanahitaji kufanya shughuli za maendeleo kuliko kuendeleza malumbano ambayo hayana faida.
“Inatakiwa tufike mwisho kuhusu sakata la Escrow, inawezekana mimi ndio tatizo juu ya mambo yote haya. Yapo mambo mengi ya msingi ambayo yanahitaji kusonga mbele, sasa nimeona bora nipishe,” alisema.
Hata hivyo, alionya kwamba Watanzania wanapaswa wajue kwamba kwenye sakata hilo kuna mvutano wa kisiasa, ubinafsi, wivu, chuki, fitna za kisiasa, biashara na mvutano wa mambo ya kisiasa.
Alisema baada ya kutafakari kwa kina ameamua kwamba maslahi ya Taifa yawe muhimu kuliko cheo cha mtu mmoja.
Alisema yote hayo yamemkuta kwa sababu haingiliki kwa rushwa, hajawahi kupewa rushwa wala sio rahisi na haiwezekani.
Akizungumzia kuhusu wafadhili kusitisha misaada ya fedha, Prof. Muhongo alisema lazima ifike mahali nchi iache kuwa tegemezi kwa wafadhili na badala yake isimame yenyewe.
“Ukitaka utu wako utambuliwe ni lazima ujitegemee, Mwalimu Julius Nyerere (Rais wa kwanza wa Tanzania) aliwahi kusema lazima kama Taifa lijitegemee, hawa wafadhili kila mwaka huwa hawakosi sababu, mwaka juzi bei ya umeme ilipopanda walitishia kusitisha misaada, mwaka jana sakata hili la Escrow na mwaka huu wataibuka na kitu kingine,” alisema.
Alisema hata hizo fedha ambazo wahisani wanaahidi kuzitoa kwa miaka 10 mfululizo, hakuna hata mwaka mmoja walishatoa kwa asilimia 100, badala yake huishia asilimia 60.
Kabla hajatangaza uamuzi wake huo wa kuachia ngazi, Prof. Muhongo alielezea mafanikio yaliyopatikana kwa kipindi cha miaka miwili na nusu aliyokaa wizarani hapo toka ateuliwe kushika wadhifa huo.
Alisema aliongoza jahazi kwa kupeleka umeme vijijini kwa gharama za kuunganisha za Shs. 27,000 ambapo matarajio ni kwamba, hadi kufika Juni mwaka huu vijiji 500 vitakuwa vimepata umeme huku akiamini siku za usoni matatizo ya umeme hayatakuwepo.
Akizungumzia mafanikio mengine yaliyopatikana akiwa wizarani hapo ni kubadili Shirika la Umeme (Tanesco), kuanza kujiendsha kibiashara tofauti na ilivyokuwa awali, mradi wa bomba la gesi kutoka Mtwara hadi Dar es Salaam kukamilika kwa asilimia 99 na tayari wameshaanza majaribio ya awali.
Mafanikio mengine ni kusuka upya Shirika la Madini (Stamico), ambapo hivi sasa mgodi wowote unapoanzishwa serikali inakuwa na hisa, huku kampuni kubwa zikitakiwa kulipa kodi asilimia 30 na malipo kwa Halimashauri (service levy) Dola za Kimarekani 200,000.
Alisema, Stamico kwa sasa ndio mlezi wa wachimbaji wadogo, lakini kazi kubwa aliyoifanya ni kuwanyang’anya wawekezaji ambao walikuwa hawaendelezi maeneo yao ya uchimbaji wa madini kwa miaka 15 hadi 20.
Sakata la uchotwaji wa fedha za akaunti ya Tegeta Escrow kiasi cha Shs. 306 bilioni liliibuliwa Bungeni mwaka jana na Mbunge wa Kigoma Kusini (NCCR), David Kafulila, ambapo mara baada ya majadiliano makali Bunge liliazimia kuwajibishwa kwa mawaziri Prof. Muhongo, Prof. Anna Tibaijuka, na Mwanasheria Mkuu wa Serikali Jaji Frederick Werema, kutokana na sakata la uchotaji wa fedha katika akaunti ya Tegeta Escrow, iliyokuwa Benki Kuu (BoT) kwa kutaka mamlaka ya uteuzi kutengua uteuzi wao.
Mbali na hao alikuwemo Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini, Eliakim Maswi na Bodi ya Wakurugenzi wa Tanesco.
Hata hivyo mwanasheria Mkuu alitangaza kujiuzulu, Prof. Tibaijuka alifutwa kazi, Katibu Mkuu Nishati na Madini uchunguzi unaendelea, Bodi ya Wakurugenzi imeundwa upya, huku wengine wakifikishwa mahakamani.
Pamoja na kuwa mmoja kati ya watu walioshiriki kuandaa mapendekezo ya Bunge ya kumtaka waziri Muhongo aondoke, Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe alimsifu kiongozi huyo na kusema kuwa amewajibika kwa kuwa makosa yamefanyika chini yake.
Zitto ambaye ni Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC), amemsifu Muhongo kuwa ni kiongozi mwenye uwezo wa kipekee ambaye amefanya mambo makubwa yatakayomfanya akumbukwe.

Baraza la Mawaziri
Rais Kikwete alifanya mabadiliko ya Baraza la Mawaziri saa chache baada ya kujiuzulu kwa Muhongo, ambapo George Simbachawene ndiye aliyemrithi waziri huyo katika Wizara ya Nishati na Madini.
Mawaziri wengine ni Mary Nagu (Ofisi ya Rais, Mahusiano na Uratibu); Christopher Chiza (Ofisi ya Rais, Uwekezaji na Uwezeshaji); Dk. Harrison Mwakyembe (Ushirikiano wa Afrika Mashariki); William Lukuvi (Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi); Steven Wasira (Kilimo, Chakula na Ushirika); Samuel Sitta (Uchukuzi); na Jenista Mhagama (Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Uratibu na Bunge).
CREDIT: DIRA YA MTANZANIA

No comments:

Post a Comment