Kikosi mahiri cha Yanga. Kuanzia wa pili kutoka kushoto ni Daktari wa timu Sheki Mngazija, kipa Riffat Said, Said Mwamba 'Kizota', Willy Martin, Willy Mtendawema, Selemani Mkati, Issa Athumani 'Amiri Jeshi', Mtwa Kihwelu 'Dally Kimoko', Method Mogella 'Fundi', Steven Mussa, Mohammed Hussein 'Mmachinga', Abubakar Salum 'Sure Boy', Edibily Lunyamila, Zamoyoni Mogella 'DHL', David Mwakalebela 'MP', Steven Casmir Nemes na Kenneth Pius Mkapa.
Yanga ikipambana nchini Uganda mwaka 1993. Pichani ni Zamoyoni akihangaika uwanjani.
Na Daniel Mbega wa www.brotherdanny.com
MWAKA 1993
mashindano ya Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati yalifanyika jijini Kampala,
Uganda ambapo Tanzania Bara iliwakilishwa na mabingwa watetezi, Simba SC
pamojana mabingwa wa Bara, Yanga.
Mtandao wa www.brotherdanny.com unaendelea
kuwaletea uchambuzi wa kihistoria katika mashindano haya wakati tukielekea
kwenye michuano ya mwaka huu ambayo itaanza Jumamosi hii jijini Dar es Salaam.
Mwaka huo 1993 Yanga
iliweka historia katika mashindano hayo kwa kuwa timu ya kwanza ya Tanzania
kutwaa ubingwa huo katika ardhi ya kigeni, lakini pia iliweza kuwanyanyasa
wenyeji itakavyo kiasi kwamba mpaka leo wachezaji kama Edibily Lunyamila na
Said Mwamba Kizota bado wanakumbukwa huko.
Ni mwaka huo pia
ambapo mchezaji ghali aliyetokea Simba, Zamoyoni Mogella ‘Morgan’, alipachikwa
jina la ‘DHL’ akifananishwa na kampuni ya usafirishaji wa vifurushi. Hii
ilitokana na umahiri wake wa kutoa pasi za uhakika kwa wenzake pamoja na
kuiunganisha vyema timu.
Timu hii kwanza
iliondoka kwa mizengwe baada ya kukosa fedha za kuisafirisha hadi Mwenyekiti
Mtendaji wa Makampuni ya IPP, Reginald Mengi, alipojitolea kuisafirisha.
Yanga ilisafiri
kwa treni mpaka Mwanza, ambako ilipanda meli mpaka Jinja kabla ya kujipakia
kwenye basi lililowapeleka Kampala. Wafadhili wa Yanga, Abbas Gulamali,
Murtazar Dewji, Muhsin Hassanali, Mohammed Virani 'Babu' na Ramesh Patwa
walikuwa wameweka 'ka-mgomo baridi'.
Tofauti na Yanga,
Simba wenzao, wakiwa na mfadhili wao mkuu, Azim Dewji, walikwenda Kampala kwa
kutumia ndege ya kukodi, ambayo iliwachukua kutoka Mwanza hadi Kampala.
Kichekesho
kilikuwa wakati wa kurudi. Simba, ambayo ilitolewa mapema baada ya kufungwa na
Express ya Uganda na kuvuliwa ubingwa, iliondoka kwa njia iliyokujia Yanga;
yaani ilipanda basi mpaka Jinja kisha ikatumia usafiri wa boti hadi Mwanza
kabla ya kukwea gari moshi lililowafikisha Dar es Salaam. Yanga wao walirejea
kwa ndege moja kwa moja kutoka Kampala.
Kwa ujumla
mashindano ya mwaka huo yalikuwa hayatabiriki kutokana na kushirikisha timu
zenye uzoefu mkubwa na mashindano ya kimataifa.
Wasifu wa timu
hizo zilizoshiriki, ambazo zilikuwa nane ingawa moja ilijitoa, ni kama
ifuatavyo:
BATA BULLETS (Malawi): Ilikuwa klabu bingwa ya Malawi kwa mwaka
1992 na ndiyo ilikuwa moja ya timu mbili kubwa nchini humo. Nyingine ni Limbe
Leaf Wanderers. Timu hii mashuhuri mjini Blantyre ilikuwa inashiriki mashindano
haya kwa mara ya sita, ingawa haikuwahi kutwaa ubingwa mpaka sasa. Ilipata
kushiriki mwaka 1976, 1979, 1982, 1987 na 1992. Mwaka huu ilikuwa na wachezaji
sita mashuhuri wa timu ya taifa ya Malawi, kama golikipa George Waya, mlinzi
Gilbert Chirwa, kiungo Mabvuto Lungu (nahodha), winga Chancy Gondwe na
washambuliaji Brian Maulidi na Lawrence Waya.
EL-HILAL (Sudan): Hii ilikuwa El-Hilal ya 'bushi' kutoka Port
Sudan na siyo ile maarufu ya Omdurman. Hata hivyo, ndiyo iliyokuwa klabu bingwa
ya Sudan mwaka 1992. Nayo pia ilikuwa timu maarufu nchini humo na ilikuwa na
wachezaji kadhaa katika timu ya taifa.
MALINDI (Zanzibar): Ndiyo iliyokuwa klabu bingwa ya Zanzibar na
ilikuwa ikishikilia ubingwa wa Jamhuri ya Muungano baada ya kuinyang'anya Yanga
mwaka 1992. Malindi ilikuwa inashiriki kwa mara ya kwanza mashindano haya baada
ya kutofanyika mwaka 1990, ambapo pia ilikuwa bingwa wa Zanzibar. Mwaka 1993
ilikuwa na wachezaji kadhaa mashuhuri wa timu ya taifa ya Zanzibar, kama vile,
Seifu Bausi, Rashid Tall, Ally Bushiri (kipa), Hamad Hilika, Juma Bakari
Kidishi na Amour Aziz.
EXPRESS (Uganda): Ilikuwa mshindi wa pili wa ligi na bingwa wa
Kombe la Uganda. Timu hii ndiyo yenye wapenzi wengi kuliko zote nchini humo.
Iliimarika zaidi wakati wa amani baada ya kuvunjwa na utawala wa Idd Amin Dada,
ambaye aliamini kuwa klabu hiyo ilikuwa ikitumiwa na kabila la Baganda
kumhujumu. Ilipata kushiriki mashindano haya mwaka 1975, 1976 na 1988. Express ilikuwa
na wachezaji sita katika timu ya taifa ya Uganda iliyoifunga timu ya pili ya
Tanzania Bara, Kakakuona, mjini Mwanza katika mchezo wa fainali ya Kombe la
Chalenji mwishoni mwa mwaka 1992. Wachezaji hao ni George Ssemogerere, Robert
Aloro, Umar Senoga, Issa Sekatawa, Richerd Kirumila na Issa Sewanyana.
SIMBA (Tanzania): Ndiye aliyekuwa bingwa mtetezi. Ilikuwa
inatetea taji lake kwa mara ya pili mfululizo baada ya kufanikiwa kulitetea
huko Zanzibar mwaka 1992. Simba ndiyo ilikuwa timu ya kwanza kutwaa ubingwa huo
mjini Dar es Salaam, mwaka 1974. Safari hii ilikuwa inashiriki kwa mara ya kumi
baada ya mwaka 1974, 1975, 1977, 1978, 1980, 1981, 1985, 1991 na 1992. Ilikuwa
na wachezaji watatu kwenye timu ya taifa, golikipa Often Martin, Abuu Omar na
Mbuyi Yondani.
VILLA SC (Uganda): Ndio waliokuwa mabingwa wa Uganda. Ni timu
ambayo kwa wakati huo ilikuwa ikitamba sana na kutawala ligi nchini humo kwa
miaka kadhaa. Timu hii ilianzishwa wakati wa utawala wa Idd Amin baada ya
kuvunjika kwa Express ambayo Amin hakuipenda. Imewahi kutwaa ubingwa wa Afrika
Mashariki na kati mwaka 1987 wakati mashindano hayo yalipofanyika Uganda kwa
mara ya mwisho kabla ya mwaka 1993. Safari hii ilikuwa inashiriki kwa mara ya
saba baada ya kushiriki katika miaka ya 1983, 1985, 1987, 1988, 1989 na 1991.
Villa, ambayo mwaka 1991 ilifikia fainali za Klabu Bingwa Afrika na mwaka 1992
ilifikia fainali za Kombe la CAF, ilikuwa na wachezaji wazuri nchini humo,
ambao ni Paul Hasule, William Nkemba, Suleiman 'Sula' Katto, Godfrey Higenyi na
Idd Batambuze.
YANGA (Tanzania): Ilikuwa klabu bingwa ya Tanzania Bara na
mojawapo ya timu mbili mashuhuri nchini Tanzania, lakini ikiwa na wapenzi wengi
kuliko zote. Kabla ya wakatihuo, iliwahi kuwa bingwa wa Afrika Mashariki na
Kati mwaka 1975. Mwaka 1993 ilikuwa inashiriki kwa mara ya nane baada ya
kushiriki katika miaka ya 1975, 1976, 1982, 1984, 1986, 1988 na 1992. Ilikuwa
na wachezaji sita kwenye timu ya taifa, ambao ni nahodha wa timu ya taifa,
Salum Kabunda, Willy Martin, Edibily Lunyamila, Willy Mtendawema, Said Mwamba
'Kizota' na golikipa Riffat Said.
NKANA RED DEVILS (Zambia): Siyo tu ilikuwa klabu bingwa nchini Zambia,
bali pia ilikuwa klabu 'numero uno', yaani nambari wano, nchini humo, ambapo
hata Rais wa nchi hiyo, Frederick Chiluba, alikuwa mmoja wa wapenzi wake
wakubwa. Nkana, ambayo wakati huu ilikuwa klabu ya kulipwa, ilikuwa inaumiliki
ubingwa wa Zambia kama mali yake na mwaka 1990 ilifikia fainali za Klabu Bingwa
Afrika. Mwaka 1993 ilikuwa inashiriki kwa mara ya tatu mashindano ya Klabu
Bingwa Afrika Mashariki na Kati. Ilipata kushiriki mwaka 1984 na 1985 na
ilikuwa na wachezaji mashuhuri wa timu ya taifa ya nchi hiyo, kama Eston Mulenga,
Kelvin Mutale na Numba Mwila, ambaye baadaye alifariki kutokana na ajali ya
ndege. Hata hivyo, timu hii ilijitoa katika dakika za mwisho.
Hizo ndizo timu
zilizokuwa zinashiriki mashindano hayo, ambayo 'yalimwinua mnyonge (Yanga)
kutoka mavumbini' na kutwaa ubingwa kwa mara ya pili baada ya kipindi cha miaka
18, huku watani wao wa jadi, Simba, wakiwa hoi.
Timu hizo
zilikuwa katika makundi mawili; kundi A lilikuwa na Yanga, Villa na Malindi
baada ya Nkana kujitoa, na kundi B lilikuwa na Simba, Express, El-Hilal na Bata
Bullets.
Sasa tuangalie
namna mashindano hayo yalivyoendeshwa Januari 16 hadi Januari 30, Yanga
walipotawazwa kuwa mabingwa. Michezo ya Nkana sitaiandika humu kwa kuwa timu
hiyo ilijitoa.
Wafungaji:
Mbali ya Yanga
kutwaa ubingwa, pia mshambuliaji wake hatari, Said Mwamba Kizota alichaguliwa
kuwa mfungaji bora wa mashindano hayo baada ya kuzifumania nyavu mara sita. Pia
alichaguliwa kuwa nambari 9 bora wa mashindano.
Katika ufungaji,
Kizota alifuatiwa na Mathias Kaweesa wa Villa aliyefunga mabao matano. Issa
Sekatawa wa Express alifunga mabao manne wakati Mabvuto Lungu wa Bata Bullets
alifunga mabao matatu. Waliofunga mabao mawili kila mmoja ni George Akena
(Villa) na Robert Aloro (Express), wakati waliofunga bao moja kila mmoja ni
Edward Chumila (Simba), Amour Nassoro (Malindi), Chancy Gondwe (Bata Bullets),
David Odowa (Express) na Mohammed Hussein na Edibily Lunyamila (Yanga).
Kundi A
16/01/1993: Nakivubo
Villa 1-0 Malindi
Mfungaji: Mathias Kaweesa 65’
20/01/1993: Nakivubo
Villa 3-1 Yanga
Wafungaji: George Akena sekunde ya 30,
Mathias Kaweesa 23’ na 57’/ Said Mwamba Kizota 45’
22/01/1993: Yanga
2-1 Malindi
Wafungaji: Said Mwamba 78’, 82’/ Amour
Nassoro pen. 31’
1.Nakivubo Villa 2
2 0 0 4- 1 4
[Uganda]
2.Yanga 2
1 0 1 3-
4 2
[Tanzania]
3.Malindi 2
0 0 2 1-
3 0
[Zanzibar]
Kundi B
17/01/1993: Express
FC 2-2 Bata Bullets
Wafungaji: Robert Aloro 4’na Issa Sekatawa 40’/Mabvuto
Lungu 8’ na Nelson George 66’
19/01/1993: Simba
SC 1-0 Hilal
Mfungaji: Edward Chumila 53’
21/01/1993: Express
FC 2-0 Hilal
Mfungaji: Issa
Sekatawa 3’, 13’
21/01/1993: Bata Bullets
0-0 Simba SC
23/01/1993: Bata
Bullets 2-0 Hilal
Wafungaji: Mabvuto Lungu 10’ na Chancy Gondwe
17’
25/01/1993: Express
FC 2-0 Simba SC
Wafungaji: David Odowa 63’ na Issa Sekatawa 72’
1.Express FC 3
2 1 0 6-
2 5
[Uganda]
2.Bata Bullets 3
1 2 0 4-
2 4
[Malawi]
3.Simba SC 3
1 1 1 1-
2 3
[Tanzania]
4.El Hilal 3
0 0 3 0-
5 0
[Sudan]
Nusu fainali
27/01/1993: Nakivubo
Villa 3-0 Bata Bullets
Wafungaji: Mathias Kaweesa 12’, 63’, Mzee
Josam og. 26’
28/01/1993: Express
FC 1-3 Yanga
Wafungaji: Robert Aloro 88’/Said Mwamba 10’, 31’
na Mohammed Hussein ‘Mmachinga’ 18’
Mshindi wa tatu:
30/01/1993:
Express 0 vs Bata Bullets 1
Mfungaji: Mabvuto Lungu 110’
Fainali
30/01/1993: Yanga
2-1 Nakivubo Villa
Wafungaji: Said Mwamba 6’ na Lunyamila 44’/ George
Akena 2’.
KUMBUKUMBU
HIZI ZIMEANDALIWA NA MTANDAO WA www.brotherdanny.com.
Tafadhali ukirejea weka chanzo cha habari.


No comments:
Post a Comment