Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Thursday 30 July 2015

LOWASSA JIHADHARI TAFADHALI, SIYO KILA AKUPIGIAYE MAKOFI ANAKUSHANGILIA!

 Edward Lowassa akionyesha kadi yake ya uanachama wa Chadema baada ya kujiunga na chama hicho juzi Jumanne Julai 28, 2015.
Anawaaga CCM? Hapana. Hapa ni wakati wa mikutano yake ya kutafuta wadhamini alipokuwa katikaharakati za kuomba kugombea urais kupitia chama hicho.
Lowassa na mkewe Regina wakionyesha kadi zao za uanachama wa Chadema.

 Lowassa akiwa katika mkutano wa ndani wa Chadema Jumatatu Julai 27, 2015 huko Bahari Beach Hotel, siku ambayo Chadema ilitangaza rasmi kumkaribisha.
Lowassa akiwa pamoja na viongozi wa Ukawa Julai 28, 2015 kwenye Hoteli ya Bahari Beach siku aliyotangaza kujiunga rasmi na umoja huo kupitia Chadema.
 Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe, aiteta jambo la Lowassa katika mkutano huo na waandishi wahabari.
 Lowassa akiteta jambo na Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi (CUF), Profesa Ibrahim Lipumba. 
Lowassa akifafanua mambo mbalimbali baada ya kukabidhiwa kadi ya uanachama wa Chadema.
 Lowassa akikumbatiana na Profesa Lipumba.
 Wafuasi wa Chadema wakiwa na bango.

Na Daniel Mbega

KUNA wahubiri wengine na watoa mawaidha huwa wanajisahau. Wanatumia muda mwingi kueleza mambo mengi kwa wakati mmoja na kuwafanya watu wasahau yaliyotangulia kusemwa. Kwa vile siyo busara kuondoka ibadani wakati wa mahubiri, wengine huamua kuketi lakini mawazo yao yakiwa mbali.
Sasa sikiliza kisa hiki cha mhubiri aliyetumia muda mwingi kuzungumza mambo mengi kiasi cha kumchanganya mmoja wa waumini wake. Alipomaliza akawauliza waumini ambao walikuwa kimya wakati akihubiri:
"Nani anataka kwenda Mbinguni?" Watu wengi wakanyoosha mikono huku wakipiga vigelegele "AMEN!".
Akauliza tena: "Nani anataka kwenda motoni?" hakuna aliyenyoosha mkono.
Lakini kulikuwa na muumini huyu mmoja ambaye muda wote wa mahubiri alikuwa ametulia tuli 'akisikiliza' kwa makini. Ajabu ni kwamba, hakunyoosha mkono mahali popote katika maswali yale mawili yaliyoulizwa.
Mhubiri akamsogelea akiwa na kipaza sauti akitaka kujua kama huyo bwana amemwelewa ama alikuwa na mawazo gani.
Akamuuliza: "Mpendwa, hukunyoosha mkono kati ya wanaotaka kwenda Mbinguni, wala hukunyoosha mkono kati ya wanaotaka kwenda motoni. Sasa wewe unataka kwenda wapi?"
Muumini akajibu, “Nataka kwenda nyumbani, Eboh!”
Naam. Kwa muda sasa siasa za Tanzania zimekubikwa na agenda moja tu hasa tunapoelekea kwenye uchaguzi mkuu.
Mjadala mkubwa kwenye mitandao ya kijamii kama twitter, whatsapp, facebook au telegram ni kuhusu kuondoka kwa kada wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Edward Lowassa na kujiunga na Chadema, hivyo kuwa na nafasi ya kugombea urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa).
Magazeti ndiyo usiseme, kwani yameigeuza agenda hiyo mtaji wa biashara tangu alipoenguliwa na chama chake kule Dodoma wakati wa kuwania uteuzi wa kugombea urais.
Vyama vya siasa vya upinzani vilimsubiri muda mrefu ili ‘vimkabidhi mikoba’ ya kuwania urais kwa matumaini kwamba lazima vitashinda vikimsimamisha.
Hoja zilizo nyuma ya mijadala mbalimbali ni kwamba, mwanasiasa huyo anakubalika kila kona ya nchi, watu wa rika zote wanamkubali na wengi waliamini kwamba ndiye angekuwa rais wa awamu ya tano.
Kuishi kwa matumaini ni jambo jema, na kuziishi ndoto zako ni vyema pia, lakini wakati mwingine ni vyema kukubaliana na uhalisia, vinginevyo zitakuwa ni ndoto za Alinacha kuoa binti wa Sultan huku akipiga teke kapu lake la urembo!
Umati mkubwa ambao Lowassa alikuwa akiukusanya tangu Mei 30, 2015 alipotangaza nia ya kuwania urais pale Arusha, na umati ambao ulikuwa ukijitokeza kila mahali alikokwenda kukusanya saini za wadhamini umewatia kiburi wananchi wengi kwamba kumbe anaweza kushinda hata kama atasimama upande mwingine.
Kila mmoja ana mtazamo wake, siwezi kupingana naye na sitegemei kama kuna mtu atapingana na mtazamo wangu, kwa sababu ni wangu na hauwezi kuwa wa mwingine!
Ninaamini kwamba Watanzania wengi walikuwa wanapenda Lowassa ateuliwe na CCM siyo kwa sababu ya busara na uwezo wake wa uongozi, bali walitaka kuleta mabadiliko kwa kumpata walau kiongozi dikteta kidogo ili awashikishe adabu wale wote ambao ‘wamezowea kazi’ na kuendelea na fungate hata pale shela linapohitaji kufuliwa.
Lowassa, kama binadamu mwingine yeyote, ana uwezo na udhaifu wake. Katika uwezo, wengi wanamkubali kwa sababu anaweza kuchukua maamuzi magumu hata kama yataigharimu serikali. Lakini udhaifu wake ni katika kashfa ambazo anahusishwa za uporaji wa mabilioni ya shilingi za walipa kodi hata kama hakuhusika moja kwa moja.
Pengine hiyo ya pili ya udhaifu wake, ikiwa ni pamoja na kujilimbikiza mali nyingi zisizo na maelezo, ndiyo iliyosababisha Kamati Kuu ya CCM ikamwengua mapema, hatujui!
Ninachopenda kumshauri Lowassa, kwa nia njema tu kabisa, ni kutulia badala ya kuendelea kuwa na ndoto za urais, kwa sababu naamini wapo waliomshauri usiku na mchana aende upinzani akagombee kwa vile katika umri wa miaka 62, hawezi kusubiri miaka mingine 10 ndipo ateuliwe na CCM.
Kwa yale machache ambayo aliyafanya na kumwezesha ‘kupendwa’ na wengi kiasi cha mikutano yake ya kutafuta wadhamini kufurika, yanatosha na angeweza ama kuendelea na mbio za ubunge ama kutulia na kuachana na presha hizi zisizo na kikomo.
Kwa hali ilivyo sasa, nakumbusha tu kwamba, yawezekana hata umati ule mkubwa uliokuwa ukimfuata kila kona haupo tena na kuna uwezekano mkubwa umati huo ulikuwepo kutokana na uzito wa pochi! Si wanasema silaha pesa, kisu mzigo bwana?
Kama Mzee Lowassa anadhani wale waliokuwa wanamfuatilia kila mahali ni dalili ya yeye kushinda, nachelea kusema kwamba anajidanganya. Wengi waliletwa na njaa zao. Si tumeelezwa kwamba hata waendesha boda boda nao walikuwa wakijaziwa mafuta ili kupamba misafara hiyo!?
Ukweli kwamba siyo kila anayekupigia makofi anakushangilia, ndio ujumbe wangu kwa Mzee Lowassa. Kumbuka tu hata kisa cha mtoto wa mbu, ambaye kila alikopita alisikia makofi Pwaa! Pwaa! Aliporudi kwa mamaye akamwambia: “Mama, aisee binadamu wananipenda kweli, kila ninakopita wananishangilia kwa kunipigia makofi!” Mamaye akamwambia: “Mwanangu jihadhari. Una bahati umenusurika, makofi hayo siyo ya kheri, wanataka kukuua lakini wamekukosa!”
Wengi walipiga vigelegele kwa nguvu ili usije ukawasahau katika ufalme wako, au wengine walishangilia kwa sauti ili hata posho yao iongezeke.
Hata huko alikokwenda, ni vyema akawa makini zaidi na kuchukua tahadhari, maana jambo lililo wazi ni kwamba, hao hao waliomwita fisadi, leo hii ndio wanaompigia nderemo na vifijo, wakiimba nyimbo na mapambio kwamba anafaa.
Ninachokiona ni kwamba, hao jamaa wanatambua uchu wa madaraka ya urais alionao Lowassa licha ya kashfa za ufisadi, lakini wenyewe pia wana uchu wa kuongoza Dolan a kuing’oa CCM madarakani, hivyo wanaona njia rahisi ni kumtumia Lowassa ambaye ‘ana mtaji wa wafuasi ndani na nje ya CCM’ ili waweze kutimiza ndoto zao.
Hao jamaa, ikiwa Lowassa ‘atawasaidia’ kuing’oa CCM, baadaye watamtosa kwa kisingizio kwamba ni mzee na pia mgonjwa!
Kuthubutu kwenda upinzani kwa dhamira ya kuingia Magogoni kuna mawili – ukibahatika unaweza ukalamba turufu, lakini ukikosa na kulamba galasa itakuwa mbaya zaidi hata kwa heshima uliyojijengea.
Wakati mwingine historia inasaidia. Tulimshuhudia Augustine Mrema mwaka 1995 alipokwenda upinzani baada ya kutimuliwa CCM. Kila kona ilikuwa Mrema! Mrema! Na yote hiyo ilitokana na juhudi zake alizozifanya akiwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi pamoja na kushikilia cheo cha ajabu cha Naibu Waziri Mkuu, ambacho kilianzishwa na kufutwa katika awamu ya pili.
Huyo bwana alipamba vichwa vya habari vya magazeti, ambayo wakati huo yalikuwa yanahesabika kama vidole vya mkono, gari lake likasukumwa bila hata kuwashwa kwa mwendo mrefu, lakini mwisho wa siku akaangukia pua.
Mzee Lowassa mshahara bado unao, ulinzi bado unao kwa cheo chako cha uwaziri mkuu. Bado Mungu amekujaalia amali nyingi ambazo hata utakula kila siku sidhani kama zitamalizika leo au kesho, kwa nini urais iwe dili kubwa? Kuna nini Ikulu kiasi cha watu kukushawishi uvae jezi za timu pinzani?
Tafadhali usiniulize ninataka kwenda wapi, kwa sababu nitakwambia tu “Nataka kwenda nyumbani!”
Alamsiki.


0656-331974

No comments:

Post a Comment