Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Monday, 6 July 2015

KOMBE LA KAGAME: PENATI ZAINYIMA YANGA UBINGWA MBELE YA EL MERREIKH


Kikosi makini cha Yanga. Waliosimama kutoka kushoto ni Charles Boniface Mkwasa, Dotto Rutta Mokili, Hamisi Ramadhan Kinye, Joseph Fungo, Ahmad Amasha 'Mathematician', Abeid Mziba, Edgar Fongo na Muhidin Mohammed Cheupe. Waliochuchumaa ni Lawrence Mwalusako, Athumani Juma Chama, Isihaka Hassan 'Chukwu', Omar Hussein 'Keegan',  Juma Mkambi, Allan Shomari, Mohammed Yahya 'Tostao', Abubakar Salum. (Naomba mnisahihishe jamani).


Na Daniel Mbega wa www.brotherdanny.com
Mashindano ya Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati, maarufu kama Kombe la Kagame, mwaka huu yanafanyika jijini Dar es Salaam. Blogu ya www.brotherdanny.com inakuletea mfululizo wa dondoo mbalimbali za kihistoria kuhusu michuano hiyo tangu mwaka 1974 ilipoanza.
Leo tunaangalia jinsi Yanga ilivyoukosa ubingwa huo jijini Dar es Salaam baada ya kutolewa kwa penati kwenye fainali na mabingwa wa Sudan El Merreikh mwaka 1986.
Mwaka 1986 mashindano hayo yalianza rasmi Januari 11 katika miji ya Dar es Salaam na Mwanza hapa Tanzania yakishirikisha jumla ya timu 10. Tanzania Bara kama mwenyeji wa mashindano hayo, iliingiza timu mbili, ambazo zilikuwa Yanga (mabingwa wa Tanzania Bara) na Majimaji waliokuwa washindi wa pili. Timu nyingine zilikuwa Small Simba (Zanzibar), Silver Strikers (Malawi), Wagad (Somalia), AFC Leopards (Kenya), El-Merreikh (Sudan), Mufulira Wanderers (Zambia), KCC (Uganda) na mabingwa watetezi, Gor Mahia pia ya Kenya.
Timu hizo zilikuwa zimepangwa katika makundi mawili; kundi A lilikuwa mjini Dar es Salaam na timu za Yanga, Small Simba, Leopards, KCC na Silver Strikers, na kundi B lilikuwa Mwanza na timu za Wagad, Majimaji, Gor Mahia, Mufulira Wanderers na El-Merreikh.
Yanga ilitolewa katika mchezo wa fainali na El-Merreikh kwa penati 4-2 baada ya kutoka sare ya mabao 2-2 hadi muda wa nyongeza. Hadi kufikia fainali, Yanga iliifunga KCC bao 1-0 Januari 11, ikaifunga Small Simba 2-1 Januari 13, ikafungwa na Leopards bao 1-0 Januari 16 kabla ya kutoka sare na Silver Strikers.
Kwenye nusu fainali, Yanga iliifunga Mufulira Wanderers kwa penati 4-2 baada ya kutoka suluhu hata katika muda wa nyongeza kwenye Uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza.
El Merreikh ilishika nafasi ya pili kwenye Kundi B nyuma ya Mufulira Wanderers. Katika mechi zake, Mereikh ilitoka suluhu na Mufulira, ikaifunga Maji Maji bao 1-0, ikatoka sare ya bao 1-1 na Gor Mahia kabla ya kuichabanga Wagad kwa mabao 5-1.
Katika nusu fainali, Merreikh iliichapa AFC Leopards bao 1-0 katika muda wa dakika 120. Hata hivyo, Leopards ilishika nafasi ya tatu baada ya kuifunga Mufulira bao 1-0.
Katika mchezo wa fainali dhidi ya El-Merreikh, Yanga ilibidi ijilaumu yenyewe kwa kushindwa kuyalinda mabao yake mawili ambayo yalifungwa na Aboubakar Salum 'Sure Boy'. El-Merreikh ilisawazisha mabao yote kupitia kwa Issa Sabah El-Kier na Ibrahim Mohammed.
Kama ulikuwa hujui tu ni kwamba, mashindano haya ndiyo yaliyomfanya Abubakar Salum akaitwa ‘Sure Boy’ kutokana na umahiri aliouonyesha.
Kwa upande wa penati, wachezaji Aboubakar Salum na Charles Boniface Mkwasa waliipatia Yanga penati mbili na Adil Amin, Kamal Abdelghani, Hamid Breima (kipa) na Atif Fadel Almoula waliifungia El-Merreikh. Lawrence Mwalusako na Muhidin Mohammed Cheupe walikosa penati za Yanga na Gamal Ibrahim alikosa penati kwa upande wa Merreikh baada ya kipa Joseph Fungo kuipangua penati hiyo. Yanga hawakumalizia penati ya tano kwa kuwa tayari walikwishatolewa. Hivyo, Wasudan wakawa mabingwa wa fainali hizo za 13.
Aidha, katika mashindano hayo, mchezaji Aboubakar Salum wa Yanga alichaguliwa mfungaji bora baada ya kutikisa nyavu mara nne.
Wachezaji waliomfuatia kwa kufunga mabao matatu kila mmoja ni Gamal Ibrahim na Ibrahim Mohammed El-Hak wote wa El-Merreikh.
Wachezaji waliofunga mabao mawili kila mmoja ni Celestine ‘Sikinde’ Mbunga (Majimaji), Fredrick Kashimoto (Mufulira Wanderers), Young Chimodze (Silver Strikers), Peter Ouma (AFC Leopards), Henry Bwire Namudeche (Gor Mahia) na Adil Amin (El-Merreikh).
Waliofunga bao moja kila mmoja ni Mohammed Mkandinga (Majimaji), Abbas Magongo, Abbey Nassur, Benny Oloo na Hesbone Omolo (Gor Mahia), Ali Duale na Kamal Sheikh (Wagad), Alfred Ngwata, Ian Banda na Lewis Nhlane (Silver Strikers), Mosses Mulamba, Wilberforce Mulamba, Michael Amwayi na Patrick Shim (AFC Leopards), Abeid Mziba, Mohammed Yahaya ‘Tostao’, Edgar ‘Fongo’ Mwafongo, Omari Hussein ‘Keegan’ na Dotto Rutta Mokili (Yanga), Joseph Sekitto na Charles Masiko (KCC), Hussein Ally (Small Simba), Emmanuel Munaile, Jackson Manda, Ashtons Melu na Kennies Mubanga (Mufulira Wanderers) na Sami Ezedin, Suleiman Makien na Issa Sabah El-Kier (El-Merreikh).

Kundi A
      AFC Leopards   2-1 Young Africans
      AFC Leopards   1-1 Silver Strikers
      AFC Leopards   1-0 Kampala City Council
      AFC Leopards   2-0 Small Simba
      Young Africans 3-1 Silver Strikers
      Young Africans 1-0 Kampala City Council
      Young Africans 2-1 Small Simba
      Silv. Strikers 2-2 Kampala City Council
      Silv. Strikers 1-0 Small Simba
      Kampala CC     2-0 Small Simba

 1.AFC Leopards    4  3  1  0  6- 2  7  [Kenya]
 2.Young Africans  4  3  0  1  7- 4  6  [Tanzania]
 3.Silver Strikers 4  1  2  1  5- 6  4  [Malawi]
 4.Kampala CC      4  1  1  2  4- 4  3  [Uganda]
 5.Small Simba     4  0  0  4  1- 7  0  [Zanzibar]

Kundi B
      Mufulira Wand. 0-0 El Merreikh
      Mufulira Wand. 2-0 Maji Maji
      Mufulira Wand. 1-0 Gor Mahia
      Mufulira Wand. 1-0 Wagad
      El Merreikh    1-0 Maji Maji
      El Merreikh    1-1 Gor Mahia
      El Merreikh    5-1 Wagad
      Maji Maji      1-0 Gor Mahia
      Maji Maji      2-1 Wagad
      Gor Mahia      3-0 Wagad

 1.Mufulira Wand.  4  3  1  0  4- 0  7  [Zambia]
 2.El Merreikh     4  2  2  0  7- 3  6  [Sudan]
 3.Maji Maji       4  2  0  2  3- 4  4  [Tanzania]
 4.Gor Mahia       4  1  1  2  4- 3  3  [Kenya]
 5.Wagad           4  0  0  4  2-11  0  [Somalia]

Nusu fainali
      AFC Leopards   0-1 El Merreikh     [baada ya dakika 120]
      Mufulira Wand. 0-0 Young Africans  [baada ya dakika 120, 2-4 pen]

Mshindi wa tatu
      AFC Leopards   1-0 Mufulira Wanderers

Fainali
      El Merreikh    2-2 Young Africans          [aet, 4-2 pen]


KUMBUKUMBU HIZI ZIMEANDALIWA NA MTANDAO WA www.brotherdanny.com. Ukirejea weka chanzo tafadhali cha habari.

No comments:

Post a Comment