Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Thursday 28 November 2013

ZITTO KABWE 'AMEFUNANIWA' KWEUPE

 Dk. Kitila Mkumbo na Zitto Kabwe


Na Daniel Mbega

NI kweli, ‘amefumaniwa’ kweupe safari hii. Ndiyo lugha pekee ambayo tunaweza kuitumia tunapolizungumzia suala la Naibu Katibu Mkuu wa Chadema na Naibu Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, Zuberi Zitto Kabwe, ambaye kwa sasa amevuliwa nyadhifa zote ndani ya Chama na hata Bungeni.
Uamuzi uliochukuliwa na Kamati Kuu ya Chadema dhidi ya Zitto Kabwe na Dk. Kitila Mkumbo (schoolmate wangu pale Pugu sekondari mwanzoni mwa miaka ile ya 1990) unaonekana kuwashangaza wengi, lakini kimsingi, pamoja na utetezi alioutoa yeye mwenyewe binafsi, au ule uliotolewa na Dk. Kitila, bado hawezi kukwepa lawama za ‘uhaini’ kama zilivyoitwa na viongozi wa Chadema.
Kilichotokea ni sawa na msaliti kwenye ndoa. Amefumaniwa akiisaliti ‘ndoa yake’, ambacho ni chama kilichomfanya afikie mahali alipo sasa, japokuwa anaweza kusema ni ‘juhudi zake binafsi’.
Mwanasheria wa Chadema, Tundu Lissu, amefafanua vyema, name nampongeza kwa weledi wake. Amesema kilichomuondoa Zitto ni waraka. Maana yake ni kwamba, kama vile ambavyo mwanandoa anaweza kufumaniwa na mwenzi wake akifanya usaliti dhahiri, na kwa kitendo hicho akaamua kudai ama kutoa talaka, ndivyo Chadema walivyofanya.
Uhaini ni usaliti, ni mapinduzi yasiyofuata utaratibu wa kuuondoa uongozi madarakani. Kama Dk. Kitila asingekiri kuutambua waraka huo na kwamba yeye alihusika kuuandaa, Watanzania tungekuwa na mawazo tofauti ya kuwataka Chadema wafanye upya uchunguzi wao kujua nani aliyehusika.
Dk. Kitila mwenyewe, wakati akitoa taarifa yake kwa wanahabari, alisema: Katika kikao cha Kamati Kuu ya CHADEMA kilichofanyika tarehe 20-22 Novemba 2013, pamoja na mambo mengine, kulijadiliwa waraka wa siri unaojulikana kama Mkakati wa Mabadiliko 2013. Waraka huu ulilenga kujenga hoja ya kufanya mabadiliko ya uongozi na kuanisha mikakati ya ushindi kwa mgombea mlengwa katika uchaguzi mkuu ndani ya CHADEMA. Nilikiri kuwa nilikuwa naufahamu waraka huu, na kwamba nilishiriki kuuandaa na kuuhariri, na kwamba mimi ni mmoja wa wanachama wanaoamini kwamba kuna haja ya kubadilisha uongozi wa juu wa chama katika uchaguzi ujao ndani ya chama.
“Zitto Zuberi Kabwe hajafukuzwa kwa sababu ya waraka huu kwa sababu yeye hakuhusika kwa namna yeyote kuandaa, ingawa alikuwa ni mlengwa mkuu. Yeye amefukuzwa kwa sababu ambazo yeye atazieleza na ambazo viongozi wa CHADEMA hawakuzieleza katika mkutano na waandishi wa habari,” alisema.
Kimsingi, Chadema wanasema Zitto Kabwe hakuvuliwa nafasi zake za uongozi kwa sababu ya mambo mengi aliyotuhumiwa nayo huko nyuma. Siyo kushindwa kuongoza kampeni za uchaguzi mkuu 2010 wala siyo kutohudhuria vikao vya chama huku akionekana kufanya shughulia zake.
Yawezekana pia kwamba uamuzi huo hauhusiani na tuhuma zilizopata kusambazwa huko nyuma kwamba alikuwa akiongoza kundi la PM-7, yaani Pindua Mbowe – 7 ambalo inadaiwa ndilo lililowagharimu akina Mtera Mwampamba, Juliana Shonza na wenzao mapema mwaka huu.
Aidha, Chadema wameongeza kwamba, Zitto hakuvuliwa nafasi hizo kwa tuhuma za hivi karibuni kwamba anashirikiana na Chama cha Mapinduzi na Usalama wa Taifa kukihujumu Chadema. Yote haya hayamo kwenye uamuzi uliofikiwa na Kamati Kuu. Kilichomo ni kuhusishwa kwake na waraka huo unaotajwa kwamba ni wa ‘kihaini’.
Yawezekana kabisa tukio la waraka huo wa ‘kihaini’ lilikuwa la 491 ndiyo maana Chadema wameshindwa kumsamehe Zitto. Si tunaambiwa tusamehe saba mara sabini? Lakini Chadema ndio wanaweza kuwa na majibu sahihi.
Zitto amesahau namna alivyompinga Chacha Wangwe mwaka 2008, akiwa mkono wa kazi wa Mwenyekiti Freeman Mbowe, wakati Wangwe aliposema chama hicho kinaendekeza ukabila. Zitto alikuwa anamchukulia Wangwe kama mhujumu wa chama, lakini maskini hakujua kwamba alikuwa anapambana na demokrasia ambayo leo hii imemgeukia mwenyewe.
Jambo pekee ambalo Zitto, Dk. Kitila na Samson Mwigamba wanapaswa ulifanya kwa sasa ni kuwa watulivu. Waswahili wanasema: “Ukitukanwa, funga kanwa!”. Wasikurupuke kuanza kuwatumia mamluki kuwajibia ama kuwapigia kelele maana kufanya hivyo kunazidi kuwaharibia badala ya kuwajenga. Ukitazama kwa jicho la tatu kwenye mitandao ya kijamii utayashuhudia haya, kwamba wapo baadhi ya watu wanaonekana dhahiri kwamba ni subjective badala ya kuwa objective. Wanadhani wanamsaidia Zitto, wakati kumbe wanamharibia.
Haya ndiyo majeraha ya siasa, ambayo hayana budi kutokea, lakini yanauma zaidi wakati mhusika anapofumaniwa katika mambo mazito kama haya, halafu akakosa namna ya kujitetea na kuwashawishi watu wamwelewe.
Pole sana kamanda Zitto na schoolmate wangu Dk. Kitila, ambaye naamini ulifanya kazi ngumu mwaka 2010 katika uteuzi wa wabunge wa viti maalum.

Wasalaam.
Mbega (0715-070109).

@@@@@@@@@@@@@@@@@@@@@@@@@@@@@

WARAKA ULIOWAONDOA ZITTO KABWE NA KITILA MKUMBO CHADEMA

MKAKATI WA MABADILIKO 2013

UTANGULIZI:
Taasisi tunayoizungumzia ilisajiliwa rasmi mwezi January 1993 na tokea wakati huo imeongozwa na wakuu wa taasisi wapatao wawili na aliyepo kwa sasa ni wa tatu. Wa kwanza aliongoza kwa miaka mitano tangu wakati huo 1993 hadi 1998 na kumwachia aliyefuata ambaye naye aliongoza kwa miaka mitano hadi mwanzoni mwa 2004 na kumwachia aliyepo sasa. Huyu aliyepo aliongoza kwa miaka mitano tangu mwaka 2004 hadi 2009 na kisha akachaguliwa tena mwaka 2009 kwa kipindi cha pili. Tunapenda kwa hatua ya mwanzo kabisa kutambua juhudi za wakuu wetu wote waliopita walizozifanya katika kuhakikisha taasisi yetu inakua kwa kutumia uwezo wote waliokuwa nao na katika mazingira yaliyowakabili. Mwaka 1995 chini ya mkuu wa kwanza tulipata wawakilishi watatu kwenye chombo chetu kikuu cha uwakilishi. Mwaka 2000 chini ya mkuu wa pili tukapata wawakilishi wanne pamoja na wa nyongeza mmoja na kufanya idadi kuwa watano. Mwaka 2005 chini ya mkuu wa tatu ambaye ndiye aliyepo hivi sasa, tulipata wawakilishi watano na wa nyongeza sita jumla wakawa 11. 2010 chini ya mkuu huyu huyu wawakilishi wakaongezeka na kuwa 23 na wa nyongeza 25 na kufanya idadi kuwa 48 kabla ya kupata mwingine mwaka jana na kufanya sasa wawe 49.

Tunapopongeza juhudi zao hizi tunahitaji pia kuwapongeza wakuu wetu wawili wa kwanza ambao kimsingi waliweka msingi mzuri sana wa kutong’ang’ania madaraka na badala yake kuachia mapema na kumwachia mwingine kidemokrasia bila vurugu. Hawakuwa madikteta na tunawapongeza sana. Walijitahidi sana kutokuwa wapenda madaraka na kimsingi walituwekea utamaduni ambao walitaka wote tuufuate na kujenga taasisi imara inayojali demokrasia na haki ya kila mwana taasisi. Ni kwa msingi huo waliamua kuandika kabisa katika mwongozo wetu kwamba kiongozi yeyote katika ngazi yoyote ya kuchaguliwa atakapogombea na kushinda ataongoza kwa kipindi kimoja cha miaka mitano na kisha ataweza kugombea na kuongoza kwa kipindi cha pili cha miaka mitano baada yapo hawezi kugombea tena katika nafasi ile ile aliyoitumikia kwa vipindi viwili. Ili kuonyesha kwamba walimaanisha kile walichokisema, wote wawili hawakuwahi kukaa madarakani kwa vipindi viwili vilivyoruhusiwa katika mwongozo bali wote wawili walikaa kipindi kimoja kimoja tu.

Lakini kuna matatizo yameanza kujitokeza na tusipochukua hatua haraka huko mbele tunaweza kupata shida kubwa. Tunapenda kuainisha matatizo hayo kwa uchache kama ifuatavyo:

Wakati tukiufanyia mwongozo wetu mabadiliko mwaka 2006 hatukugusa kipengele kinachomzuia kiongozi kuongoza kwenye nafasi moja kwa zaidi ya vipindi viwili vya miaka mitano mitano. Lakini wakati mwongozo unachapwa chini ya uongozi uliopo, kipengele hicho kiliondolewa kinyemela. Mambo yanayotokea hivi leo yanaonyesha dhahiri kipengele hicho kiliondolewa kwa makusudi kwa maslahi na kwa faida ya viongozi waliopo madarakani kwa sasa. Hiki kinaweza kuchukuliwa kama kitendo kidogo lakini kama viongozi wetu wanaweza kutokuwa waaminifu katika jambo kama hili, ni dhahiri hawawezi kuaminika na wanaweza kufanya mambo mengine makubwa na yenye athari zisizomithirika kwa taasisi yetu.

Ni dhahiri kwamba uongozi uliopo umeishiwa mbinu na kuakisi jambo la msingi sana ambalo waasisi wetu waliliona tangu mwanzo na kuamua kuweka kipengele cha ukomo wa uongozi kwenye mwongozo wetu. Kuchoka kwa uongozi wetu kunaonekana dhahiri katika mipango na mikakati ya taasisi ya miaka kadhaa. Mfano mwaka 2008 uongozi ulianzisha mkakati wa operesheni samaki mkubwa (maarufu kama Oparesheni Sangara). Huo ulifanyiwa kazi katika mikoa kadhaa na hatimaye ikafa kimya kimya. Baada ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2010 kulianzishwa matembezi ya maandamano ambayo nayo yalikuwa yakipeleka ujumbe kwa watu na yalipangwa kufanyika mikoa yote na wilaya zote.

Kumbukumbu zetu zinaonyesha kwamba yalikuwa yakianzia makao makuu ya mkoa na kwenda kwenye wilaya zote. Lakini kumbukumbu hizo zinaonyesha kwamba yalifanyika Mwanza, Musoma, Shinyanga, Kagera na mikoa ya Nyanda za Juu kusini (Mbeya, Iringa, Njombe na Rukwa) kisha nayo yakafa kifo cha mende. Kisha mwaka 2012 ikaanzishwa operation ya mabadiliko maarufu kama Movement for Change (M4C). Hiyo ilikuwa inakwenda kwenye mikoa na timu kama nne hivi ambazo kwa ujumla zilitathmini hali ya mtandao na uongozi wa taasisi, kuhamasisha umma kwa njia ya mikutano ya hadhara, kuingiza wanachama na kusimika uongozi na hatimaye kufanya mafunzo kwa viongozi. Hiyo ikafanyika Mtwara na Lindi, Morogoro na kisha ikaenda kufia Iringa. Mwaka huu viongozi wetu wamekuja na ugatuaji madaraka kutoka makao makuu ya taasisi na kupeleka madaraka kwenye kanda mbalimbali. Mkakati huu ulikufa kabla ya kuanza pale viongozi wakuu walipobadilisha maazimio ya kikao kikuu na kutekeleza matakwa yao ikiwa ni pamoja na kuleta suala la viongozi wa muda kwa muda mrefu badala ya kuajiri maofisa na wakahakikisha wanaweka watu wao kwenye uongozi wa muda. Kitendo hiki kwa peke yake, cha kufeli kwa kila mkakati unaoletwa na viongozi wetu katika hatua za utekelezaji unaofanywa na wao wenyewe waleta mkakati, ni kiashiria tosha kwamba uongozi uliopo umechoka.

Performance yetu kwenye chaguzi ndogo nayo ni ishara kwamba mabadiliko yanahitajika. Tangu uongozi huu uingie madarakani, kumefanyika chaguzi ndogo 8 za wawakilishi kwenye chombo kikuu, kati ya hizo tumeshinda 2 tu sawa na asilimia 25. Aidha baada ya mwaka 2010 kumefanyika chaguzi kadhaa za wawakilishi kwenye halmashauri. Mwezi Oktoba 2011, mwezi wa4 2012, mwezi Septemba 2012 na mwezi Juni 2013. Kote performance yetu imekuwa poor kupindukia. Mfano mwezi wa Juni 2013 tumepata viti 6 kati ya 22 (27%) na mwezi Septemba 2012 tulipata viti 7 kati ya 29 (24%). Ni dhahiri mabadiliko yanahitajika kwa kuwa wakuu waliopo wanatumia mbinu zile zile na kupata matokeo yale yale. Tunahitaji mbinu mpya. Kwa kifupi, ushindi ambao tumekuwa tukiupata katika chaguzi ndogo haulingani na ukubwa wa hamasa kwa taasisi yetu iliyopo mitaani. Hii ni kwa sababu tumekuwa tukitumia mbinu hizohizo katika kila chaguzi. Aidha, tu wepesi mno wa kuridhika na kujisifu kwa mafanikio madogo badala ya kukaa chini na kutafakari kwa kina mahala tunapojikwaa. 

Matumizi ya fedha za taasisi. Hakuna mtu anayejua hivi sasa fedha za chama zinatumikaje zaidi ya kakikundi ka watu watatu yaani mkuu kabisa, mtendaji mkuu na mkuu wa fedha kwenye taasisi yetu. Maamuzi ya vikao hayaheshimiki tena na mabwana hawa. Baada ya uchaguzi wa 2010 vikao halali vilielekeza kiasi na aina ya fedha ambazo hazitaguswa bali zitunzwe kwenye akaunti maalum kwa ajili ya uchaguzi wa 2015. Lakini leo si tu akaunti hiyo haina fedha bali hakuna akaunti yoyote yenye fedha. Watu watatu ndo wanaamua fedha zitumikeje. Mfano mwingine ni maamuzi ya kikao cha juu mno cha hivi karibuni kilichoamua kwamba kiasi cha fedha inayotoka serikalini kipelekwe kwenye mikoa na wilaya na kiasi kingine kipelekwe kwenye kanda. Leo ni mwezi wa tano maamuzi hayo hayajatekelezwa. Lakini kuna michango ya watu binafsi kama yule mtanzania mwenye asili ya kihindi, hizo nazo hazijulikani zimechukuliwa lini kwa mfumo gani, zikatunzwa wapi na hatimaye zimetumikaje. Hapo hatujataja fedha zinazopatikana kutoka kwenye fundraising events mbalimbali kama ile ya Dar es salaam na Mwanza. Hizo nazo hazijawahi kuonekana na walioendesha hizo fundraising, uaminifu wao kwenye masuala ya fedha ni questionable.

Taarifa za fedha. Tokea baada ya uchaguzi wa 2010 mpaka leo, hakuna kikao chochote kilichowahi kupokea na kujadili hadi mwisho ripoti ya mapato na matumizi ya fedha za taasisi. Kila kikao agenda hiyo inarushwa kiaina. Wanaojua mchezo huo ni watu watatu tu tuliowataja hapo juu na malengo ya kurusha hiyo agenda kila wakati na kukwepesha isijadiliwe pia wanayajua wao. Ni dhahiri tukiendelea na hawa watu tutafika 2015 tukiwa hatuna pesa hata ya kuweka mawakala kwenye vituo na tutapigwa tukiwa tumesimama. Kwa kiasi kikubwa mkuu aliyepo anatengeneza mazingira yaleyale ya mwaka 2005 na 2010 ya kutaka chama kiwe hakina hela ili ikifika wakati wa uchaguzi kimpigie magoti. Kisha atatoa pesa bila kumbukumbu zozote na mara baada ya uchaguzi anapeleka lundo la deni na kudai alipwe hela aliyekikopesha chama wakati wa uchaguzi. Alifanya hivyo katika chaguzi za 2005 na 2010. Wakati wote wa kampeni za mwaka 2010, kwa mfano, taasisi yetu ilihangaika sana kwa kukosa hata hela ya kununua maji kwa wajumbe wa ngome. Lakini ajabu ni kwamba baada ya uchaguzi mkuu wa taasisi na baadhi wa wapambe wake walilete deni kubwa la takribani shililingi milioni mia tano akiadi kuwa walikikopesha chama. Taasisi imewalipa pesa zote hizi kwa muda mwaka mmoja. Sasa anatengeneza mazingira hayohayo kwa ajili ya uchaguzi wa mwaka 2015. 

Mipango ya kukipatia chama mapato ya ziada kutoka nje ya chama. Wakuu waliopo hawana hata ndoto ya namna ya kupata fedha za ziada. Wanachokijua ni kukusanya ‘sadaka’ kwenye mikutano ya hadhara na kuwapatia kazi watu wanaoonekana kuwa matapeli eti waendeshe harambee za kuchangisha fedha kwa njia ya matukio. Mawazo mazuri kama lile la kuanzisha kampuni la uwekezaji la taasisi yetu litakalowekeza kwenye miradi mbalimbali, halijawahi kufanyiwa kazi, na hivyo uanzishaji wa miradi mbalimbali ya kuiingizia taasisi fedha imebaki ndoto ya mchana. Hatuwezi kufika hata siku moja bila fedha. Hata uchaguzi wa wenzetu wa hapa jirani juzi juzi wakuu wetu ingawa walishiriki lakini hawaonekani kama wamejifunza chochote.

Njia haramu za kubaki madarakani. Ili kuhakikisha wakuu wanabaki madarakani, wameanzisha vikundi vikundi ndani ya taasisi yetu. Siku hizi ni rahisi sana kuambiwa kwenye taasisi yetu eti huyu ni wa boss na huyu ni wa dogo. Na wale walio wa boss kwa kuwa boss ndo anashikilia raslimali za taasisi anatumia mfumo haramu kuwaneemesha watu wake kwa kutumia raslimali za taasisi na kuwakandamiza wote wanaoonekana wanapishana naye kimtazamo. Jambo hili limewaibua wachumia tumbo, wapenda madaraka, na vibaraka lukuki wanaokwenda kujipendekeza kwa wakuu wa taasisi kwa malengo ya kujinufaisha binafsi. Katika kufanya hivyo vibaraka hao wamekuwa wakiwaendea wakuu wa taasisi na kuwajaza maneno mabaya dhidi ya viongozi wenzao na kuzidi kuwafarakanisha viongozi wa juu.

Kuna mchezo umeanzishwa na wakuu wa taasisi unaitwa ulinzi wa chama uliogawanyika katika makundi mawili yaani visible na invisible. Visible ni ule unaoonekana ambao uko chini ya kikosi chetu chekundu ambacho kinajulikana kwa kila mtu lakini invisible wanajulikana kwa mkuu wa taasisi na mtendaji mkuu peke yake. Wanafanya kazi kwa maelekezo ya wakubwa hao wawili na hawajulikani kwa viongozi wengine wa juu. Ni hawa hawa ambao wanatumika vibaya pale wanapoleta taarifa za kiintelijensia ambazo zinawahusisha viongozi wasiopendwa na wakuu na usaliti dhidi ya taasisi. Hakuna kamati maalum inayowathibitisha maaintelijensia hao bali wakuu wenyewe wanawachukua wanaowataka. Ni katika mfumo huu wa kipuuzi mida eight amekuwa akitumika vibaya kwa kumshambulia mtendaji mkuu msaidizi hadharani kwa kutumia mitandao ya kijamii na wakuu wanafurahia na kumlipa pesa.

Udhaifu wa utendaji wa mtendaji mkuu. Mtendaji mkuu ni dhaifu mno na ni mara nyingi sana tumeshuhudia mkuu wa taasisi akifanya mambo ya kiutendaji kinyume na utaratibu kama vile yeye mwenyewe kuja kwenye kamati ya makatibu na wakurugenzi na kupangua mipango yao na ku-inject ya kwake na mtendaji mkuu kuadopt tu kana kwamba yeye hawezi kupanga mambo ya kiutendaji, hata tunapokuwa kwenye operesheni maalum tumeshuhudia mkuu wa taasisi ndo akipanga watendaji, posho zao na hata kusimamia matumizi ya pesa na shughuli mbalimbali za kiutendaji. Udhaifu wa mtendaji mkuu ni udhaifu wa mkuu wa taasisi kwa kuwa amemteua yeye mara mbili tena mara ya pili alileta jina moja mbele ya Baraza la juu kuonyesha kwamba aliridhika na utendaji wake kiasi cha kutotaka kumpambanisha na mwingine. Lakini baada ya kumpendekeza mara ya pili ndipo tumeshuhudia yeye kuingilia kati mara nyingi sana mambo ya kiutendaji kana kwamba anamfichia aibu mtendaji wake. Swali kwa nini alimteua tena? Jibu lake litakuwa rahisi tu kwamba ni kwa sababu mtendaji huyu ni passivekwa kila takwa la mkuu wake.

Matumizi mabaya ya madaraka yanayoweza kuhusishwa na ufisadi. Taasisi yetu inayo kamati ya tenda ambayo iko chini ya kamati ya makatibu na wakurugenzi. Lakini uzoefu unaonyesha kwamba kamati hii haifanyi kazi imezimwa kimya kimya na wajumbe wote wa kamati ya tenda kwa kuwa ni wachumia tumbo wanaojigonga kwa wakuu, wamekubali kuzimwa. Leo ikidaiwa kamati hiyo ilete nyaraka za mchakato wa manunuzi ya magari, pikipiki, vifaa vya kueneza taasisi, set ya televisheni iliyofungwa ofisini kwa mtendaji mkuu, hawana. Manunuzi haya yote yote yanafanywa na wakuu hasa hasa mkuu wa taasisi bila utaratibu wowote jambo ambalo ni hatari na linarahisisha matendo ya kifisadi. Bila aibu, mkuu wa taasisi ndio amekuwa mnunuzi wa vifaa vyote vya chama nje ya nchi kwa bei anayoijua mwenyewe na ambaye haihojiwi popote. Huu ni mfano wa wazi wa mgongano wa kimaslahi jambo ambalo ni hatari kwa kiongozi mkubwa wa taasisi kama yetu inayojitambulisha katika kupinga vitendo vya ufisadi na uvunjifu wa maadili ya uongozi kwa ujumla. 

Makubaliano ya kifisadi na mtu binafsi anayeuza vifaa vya kueneza taasisi. Hakuna kikao chochote cha juu kilichojadili ama kilichowahi hata kupewa taarifa tu kwamba sasa kuna mtu binafsi kapewa tenda ya kuuza vifaa vya taasisi na taasisi inanufaika vipi na mauzo hayo na kwa nini vifaa muhimu vya taasisi vinauzwa. Jambo hili linajulikana kwa wakuu tu.

Mifumo ya uteuzi wa maofisa wa makao makuu ya taasisi imevurugwa na siku hizi wakuu wa taasisi hasa mtendaji mkuu anateua na kutimua ofisa anavyotaka na mara nyingi bila hata kamati ya makatibu na wakurugenzi kujua. Mambo haya yanafanyika mbele ya macho na masikio ya mkuu wa taasisi jambo ambalo linazidi kuthibitisha kwamba mkuu na mtendaji mkuu wanajuana na wanafanya kwa kulindana.

NANI TUMUUNGE MKONO KUCHUKUA NAFASI YA MKUU: Baada ya utangulizi huo unaoonyesha kinagaubaga kwamba tunahitaji mabadiliko, hatua iliyofuata ilikuwa ni kuangalia nani anaweza kuleta mabadiliko tunayohitaji. Ni vema ikazingatiwa kwamba mtu ambaye tungemuunga mkono lazima awe ni mtu mwenye uwezo mkubwa kuliko tunayetaka kumtoa. Awe ana qualities za kiuongozi na zaidi sana awe na uwezo wa kupambana na mkuu aliyeko. Tukileta mtu asiyefahamika sana kwenye mifumo ya taasisi yetu hata kama angekuwa mzuri kiasi gani hatachagulika na mkuu aliyeko atarudi kwa urahisi na kuendelea kuididimiza taasisi.

Katika kuchunguza ndani ya taasisi tuliridhika kwamba mtendaji mkuu msaidizi ana sifa zote tulizozitaja hapo juu ingawa kila mwanadamu ana udhaifu wake. Ni dhahiri pia kwamba udhaifu wa mtendaji mkuu msaidizi unarekebika kuliko wa mkuu aliyepo. Kwa ujumla mtendaji mkuu:

Ni kiongozi anayeweza kuongoza taasisi bila kujenga makundi akijali zaidi kazi ya taasisi kuliko maslahi binafsi.
Ameonyesha kwa vitendo kwamba hana maslahi binafsi kwa kuwa tumeshuhudia akifanya kazi nyingi za taasisi bila kudai malipo kwa njia ya posho ama vinginevyo.

Anaheshimika na viongozi wa ndani na nje ya taasisi jambo ambalo ni la muhimu sana kwa ustawi wa taasisi na kwa yeye kuwa mkuu wa taasisi tunatarajia wakubwa wengi sana kutoka nje ya taasisi yetu kuiamini na hata kujiunga nasi katika kuhakikisha tunafanikisha lengo la taasisi.

Ni msomi wa kiwango cha juu na mwenye uwezo mkubwa katika kuchanganua mambo ya kiuchumi, kisiasa, kijamii, kimichezo, nk jambo ambalo ni muhimu sana kwa kuwa ni hatari kuwa na kiongozi asiye na ujuzi wa kutosha kwenye masuala kama hayo.
Ndani ya taasisi anakubalika kwa makundi yote ya vijana, wazee na akina mama. 

Uongozi wa sasa wa taasisi yetu umefanya tuonekana kwamba taasisi yetu ipo kwa ajili ya kuvuruga amani ya nchi. Yote hii ni kwa sababu tumekuwa hatuna mbinu mpya za mapambano zinabadilikabadilika zaidi ya maandamano ya kila mara. Kwa kuzingatia utamaduni wa watanzania wa kupenda amani, kuna haja ya kufuta hii taswira na njia rahisi ni kubadilisha uongozi wa taasisi haraka iwezekanavyo. 

Uelewa wake wa mambo ya kiuchumi ni muhimu sana kwa taasisi kwa sasa. Tunahitaji kuja na vyanzo vipya vya mapato ikiwa tunahitaji kufanikiwa. Mkuu aliyepo si kwamba ameishiwa bali hana mbinu za maana za kuiimarisha taasisi kimapato kwa ajili ya malengo yake ya mbele.

Exposure kubwa na kukubalika katika siasa za kimataifa. Tunahitaji kiongozi ambaye anazifahamu siasa za kimataifa na anayeweza kuungwa mkono na viongozi wengi wa kimataifa. Ni hatari kutegemea utaweza kufanikisha malengo kama ya taasisi yetu bila mpango kabambe wa kuungwa mkono na jumuia ya kimataifa. Mpaka hivi sasa hakuna mpango wowote wala hata mchakato wa maana kuwa connected na jumuia ya kimataifa. Kiongozi wetu mkuu wa sasa yupo ‘too local’ na hana mawasiliano yeyote ya maana na viongozi wengine katika kanda na kimataifa. Ndio maana mkuu huyo na mtendaji wake mkuu wamekuwa hawaonekani katika matukio makubwa ya kimataifa. Hata katika kutoa maoni katika mambo makubwa ya kitaifa na kimataifa viongozi hawa hawapo. Kwa kifupi kwa sababu ya aina ya viongozi tulio nao, nafasi ya taasisi yetu katika nyanja za kimataifa haipo! 

Aina na staili ya uongozi wa sasa wa taasisi yetu ni kina kwamba nchi hii haipo hadi taasisi yetu itakapochukua dola. Yaani tunafanya mambo kama kwamba tutaanza upya kabisa tukichukua dola. Ni kwa sababu tumegombana na kila mtu katika utawala wan chi, vikiwemo vyombo vya ulinzi na usalama. Ukweli ni kwamba tutavihitaji vyombo hivi kabla na baada ya kuingia madarakani na ni ndoto kudhani kwamba tutakabidhiwa nchi kwa kugombana na kila mtu. Ni kwa sababu ya mtazamo kama huu ndio maana wakuu wetu wa sasa hawaonekani kabisa katika shughuli za kitaifa kama vile sherehe za uhuru wan chi, n.k. 

Uwezo wa kuwaunganisha wasomi wa kada mbalimbali, wafanyabiashara wakubwa, watumishi wa umma na sekta binafsi, nk katika kupata muunganiko wa mawazo na kutoka na sera murua zinazogusa kila sekta. Hili la kuwashirikisha litaenda sambamba na kutoa elimu kwa wote waelewe na watuunge mkono. Tunasema hivi kwa kuwa watu wa kada mbalimbali hawajaelewa sera zetu juu ya mambo yanayowahusu mfano wafanyabiashara wakubwa, wawekezaji, wakulima, watumishi, wanafunzi,nk na hivyo hawajawa tayari kutuunga mkono. Kile kinachofanywa wakati wa uchaguzi kwa njia ya ilani ya uchaguzi na elimu kutolewa kwa njia ya kampeni majukwaani hakitoshi. Tunahitaji watu wajue tumeunda think tank kwa ajili hiyo na baadaye wajue nini kimetokana na think tank hiyo ili wajadili na kutoa maoni na hatimaye tutoke na kitu kinachokubalikwa na wananchi wote. Na tuna imani hilo tunayempendekeza ana uwezo nalo.

Kubwa zaidi ni kwamba alishaiangalia taasisi yetu na kuona mambo yanayohitaji mabadiliko na kujiangalia yeye na kuridhika kwamba ataweza kuleta mabadiliko tunayoyahitaji na ndipo mwaka 2009 aliamua kujitosa kuutafuta ukuu wa taasisi yetu kabla ya kuombwa kumwachia aliyepo.

SWOT ANALYSIS:
Kwa kutumia uchambuzi huu hapa chini wa uimara, udhaifu, fursa na vitisho ama vikwazo dhidi ya mtu tunayempendekeza, utaweza kutuonyesha kama tunayempendekeza ataweza kushinda vita iliyo mbele yetu. Kama SWOT inavyotaka, tutaangalia sifa njema alizonazo tunayemtaka ambao ndio uimara wake, tutaangalia pia udhaifu wake, tutaangalia fursa alizonazo na mwisho tutazingatia vitisho ama vikwazo vilivyopo. Ni muhimu tukaeleza kwamba katika SWOT analysis tunajikita kwa mambo yanayohusika moja kwa moja na uwezekano wa tunayemtaka, kuchaguliwa. Kwa hiyo kwa mfano utakuta kwamba katika sehemu hii hatutazungumzia sifa njema alizonazo tunayemtaka kama kiongozi lakini sifa hizo zikawa hazina ushawishi wa kuwafanya wajumbe wa kikao cha uchaguzi kumchagua.

Uimara wa tunayemtaka:
Ingawa si mmoja wa waasisi wa taasisi yetu, lakini ni mwana taasisi mkongwe akiwa amejiunga na taasisi yetu miaka miwili tu tangu ianzishwe na mwaka mmoja tangu isajiliwe rasmi na serikali.

Zaidi ya kuwa mwanataasisi mkongwe, hajawahi kujiunga na taasisi nyingine hapo kabla. Alijiunga na taasisi hii kabla hata haijajulikana kwa watu na alibaki kuwa mwana taasisi mwaminifu hata pale taasisi zingine zilipoonekana kuwa imara na maarufu zaidi ya hii.

Kutokana na vipengele ‘a’ na ‘b’ hapo juu, hakuna mtu hata mmoja anayeweza kusema mtu huyu alikuja kwenye taasisi yetu kwa ajili ya kutafuta maslahi kama vile uwakilishi kwenye chombo chetu kikuu cha uwakilishi hapa nchini.

Ni mvumilivu sana. Katika jitahada za wakuu waliopo kuhakikisha wanaendelea kukalia viti vyao, wamejitahidi sana kumpaka matope lakini amevumilia. Mahali ambapo wengine wangeshakata tamaa na kuhama taasisi, yeye alibaki kuvumilia mpaka imefikia wana taasisi wa ngazi za chini waliokuwa wanadanganywa kwamba mtu huyu ni msaliti, wameanza sasa kushtuka.
Ana historia nzuri ya utendaji uliotukuka ndani na nje ya chombo cha uwakilishi.

Ana uwezo mkubwa wa uelewa wa mambo mbalimbali ya uchumi, jamii, utamaduni, michezo, nk. Uwezo wake unachagizwa si tu na elimu yake ya darasani bali pia vipaji na akili ya kuzaliwa.

Ni mzalendo wa hali ya juu anayeipenda nchi yake kwa moyo wa dhati. Amethibitisha hilo kwa namna anavyolitetea taifa letu katika medani za kimataifa na jinsi anavyolipigania ndani dhidi ya mafisadi na wasiolitakia mema taifa letu. Ni mwakilishi pekee aliyekuwa tayari kukosa mishahara ya miezi kadhaa kwa kuamua kusimamia ukweli kwamba kuna ufisadi ulifanyika mpaka akasimamishwa uwakilishi wake kwa mikutano kadhaa ya chombo chetu cha uwakilishi.

Katika kuzidi kuonyesha alivyo mzalendo tunaweza kusema hapa kwamba ni kiongozi pekee kutoka upande huu ambaye ameonekana sana kwenye mambo ya kitaifa kwa mfano kulipigania taifa letu katika mambo ya kimchezo, kutumia gharama zake kwenda nje ya nchi na kujifunza mambo mbalimbali yanayoweza kulisaidia taifa katika sekta nyeti kama mafuta, gesi na madini, nk bila kusahau kwamba amekuwa ndiye mwakilishi pekee aliyeongoza katika kuibua kashfa nyingi na nzito za ubadhirifu ndani ya serikali hata kufikia mawaziri kadhaa kufukuzwa kazi.

Mambo hayo tuliyoyataja kwenye vipengele ‘e’, ‘f’, ‘g’ na ‘h’ yamemfanya kuwa kiongozi wa kwanza kuwa maarufu sana katika taasisi yetu aliyewapiku hata viongozi wa serikali kwa umaarufu. Hii ya umaarufu ni sifa muhimu sana linapokuja suala la uchaguzi. 

Uwezo wake wa kujieleza kwa kujenga hoja pale anapopewa nafasi. Hata pale anapokuwa amepakwa sana matope na wenzake, anapopewa nafasi ya kujieleza huweza kuwashawishi watu wengi wanaomsikiliza. Hii itamsaidia sana siku ya kujieleza mbele ya kikao cha uchaguzi ambapo ataweza kupangua hoja zote dhaifu za kumpaka matope.

Ana uwezo wa kuchangamana na makundi yote ambapo vijana humwona kama mwenzao, wanawake humwona kama mtetezi wao wakati wazee humwona kama kijana mwenye busara anayeweza kuelekeza kama kiongozi.

Ana mahusiano mema na mazuri na viongozi wa ngazi za chini kutokana na ziara nyingi alizozifanya na kukutana na viongozi wa ngazi za chini akiwa katika kuijenga taasisi hii. Mahusiano haya mazuri yanachagizwa na jinsi anavyotumia muda wa kuongea na viongozi wa ngazi za chini kuzungumza kwa lugha ya upole na kuelekeza viongozi wenzake bila kuwaonyesha dharau.

Si mtu wa kujipenda nafsi na katika kupambana umaskini wa watu badala ya umaskini wake, alifikia kuzikataa posho wanazolipwa wawakilishi wakati wakitekeleza majukumu ambayo kwayo wanalipwa na kuiomba ofisi ya chombo hicho kuzipeleka posho hizo kwa watu maskini. 

Ana limu nzuri sana aliyoipata katika vyuo vinavyoeleweka kitaifa na kimataifa
Ni kijana na hii ni taswira njema kwa sababu taasisi yetu inaungwa mkono sana na vijana

Udhaifu wa tunayemtaka:
Maneno yake mara nyingine hayazingatii anayazungumza katika mazingira gani na hivyo kuwasha masikio ya wanataasisi jambo linalompunguzia kukubalika kwake taratibu.

Kama ilivyo kwa maneno, kuna matendo pia ambayo mara nyingine huyafanya bila kuzingatia mazingira na wasikilizaji wake na hivyo kupunguza imani ya wana taasisi kwake.

Hali ya ndoa ya tunayemtaka kutoeleweka msimamo wake

Kuna wakati tunayemtaka hu-respondkwa taharuki kubwa dhidi ya mashambulizi yanayoelekezwa kwake jambo linalomfanya achukue maamuzi yasiyo sahihi kwa wakati huo. Kwa kifupi kuna wakati tunayemtaka huonekana kufanya maamuzi kwaemotion zaidi badala ya kutulia kwanza na kutafakari kwa kina ikiwa ni pamoja na kutafuta ushauri kwa wenzake kabla ya kurespond.

Jambo lililoelezwa katika ‘d’ hapo juu humfanya tunayemtaka wakati mwingine kuonekana ana jazba sana kwa sababu akishataharuki na kuchukua maamuzi akingali kwenye taharuki huwa ni rahisi sana kuonekana anajibu mapigo kwa jazba sana.

Ustahimilivu: yaliyotajwa katika ‘d’ na ‘e’ hapo juu yanaashiria tunayemtaka si mstahimilivu sana sifa ambayo inahitajika sana kwa kiongozi.

Uwazi:
 Katika taasisi zetu hizi ni muhimu sana kuepuka kufanya mambo yote wazi wazi hata kama ni mema ama ni haki ya mhusika ama si makosa katika jamii tuliyomo. Kuna mambo ambayo ni haki ya mtu mfano mahusiano binafsi ya kimapenzi, kuwa na marafiki wa damu kutoka upande mwingine wa utawala, nk. Lakini mambo hayo ni muhimu wakati mwingine ama kwa kiwango fulani yakafanywa kwa siri kuepuka mitazamo potofu kwa unaowaongoza.

Fursa alizonazo tunayemtaka:
Utamaduni wa taasisi yetu wa kubadilisha wakuu wa taasisi kila baada ya vipindi vifupi ili kuleta maono mapya kwenye taasisi unampendelea tunayemtaka.

Udhaifu ulioonyeshwa na uongozi uliopo chini ya mpinzani wetu katika kutekeleza program mbalimbali za taasisi nyingi zikiwa zimebuniwa na wao wenyewe, pia ni fursa kwa tunayemtaka.

Udhaifu mkubwa ulioonyeshwa na uongozi uliopo kwenye ugawanyaji wa raslimali za taasisi kama vile fedha za ruzuku, michango mbalimbali ya wahisani na hata vifaa vya uenezi.

Kujitokeza kwa tunayemtaka kutaonekana kama fursa kwa wanataasisi kufanya mabadiliko makubwa na kuua kabisa ile propaganda ya kwamba taasisi yetu ni ya kabila fulani ama eneo fulani kwa kufanya reference kwa uongozi wa taasisi.

Hoja ya uongozi uliopo kushindwa kabisa kusoma taarifa za fedha tokea 2010 ikifahamika kwa wapiga kura inaweza kuwa machinjio kabisa ya uongozi uliopo na kumpa fursa kubwa tunayemtaka.

Imani ambayo wana taasisi wengi wanayo kwake. Utafiti mdogo unaonyesha kwamba bado jina la tunayemtaka linatamkika sana midomoni mwa wanataasisi pale wanapotajwa viongozi wa juu wa taasisi yetu. Hii inaonyesha bado wana taasisi wanayo imani kubwa kwake na kwa hiyo atakapopata fursa ya kupangua matope aliyopakwa atakuwa na nafasi kubwa ya kuchaguliwa.

Mpinzani wetu hana historia nzuri ya utendaji uliotukuka ndani na nje ya chombo cha uwakilishi. Hakuonyesha utendaji wowote wa pekee alipokuwepo kwenye chombo mwaka 2000 -2005 na hata alipopewa uongozi wa upande wetu ndani ya chombo tokea 2010 hadi leo 2013 hajafanya lolote la kutukuka ndani ya chombo hicho.

Mpinzani wetu hana uwezo mkubwa wa uelewa wa mambo mbalimbali ya uchumi, jamii, utamaduni, michezo, nk. Si tuelimu yake ya darasani ni ya magumashi bali pia vipaji na akili ya kuzaliwa havijaonekana katika maisha yake.

Uzalendowampinzani wetu unatia shaka akiwa hajaonyesha lolote la maana katika kulitetea taifa letu kimataifa. Ingawa ameshapata nafasi lukuki ya kwenda nje ya nchi lakini mara zote akifika huko ni kuiponda tu nchi yake. Ingawa anayo majukwaa ya kufanya hivyo akiwa ameshakuwa mwakilishi mara mbili kwenye chombo chetu lakini hatujawahi kumsikia akiibua kashfa mahsusi ya ufisadi na kuisimamia zaidi ya yeye mwenyewe wakati fulani fulani kutuhumiwa kwa ufisadi mfano pale alipokopa kwenye shirika la umma na kugoma kulipa mkopo.

Katika kuzidi kuonyesha uzalendo hafifu wa mpinzani wetu tunaweza kuangalia jinsi ambavyo mpinzani haonekani kwenye mambo ya kitaifa. Hii ni fursa kwa tunayemtaka. 

Mpinzani wetu si maarufu akilinganishwa na tunayemtaka na hivyo kumpa fursa zaidi tunayemtaka kumshindani mpinzani wetu kwenye uchaguzi. 

Uwezo wa mpinzani wetu wa kujieleza kwa kujenga hoja pale anapopewa nafasi ni mdogo sana.

Mpinzani wetu hajazoea ushindani na changamoto. Ni mtu aliyezaliwa kwenye utajiri na anadhani pesa ni kila kitu. Ukimnyang’anya pesa ukamwambia ashindane kwa hoja hawezi na ndo maana anajaribu sana kuhakikisha anaingia mwenyewe ulingoni bila kupingwa. 

Kutokana na tuliyoyasema hapo juu kwenye ‘m’ ni dhahiri kwambapale mpinzani wetu anaporushiwa kombora la kashfa anakuwa mzito kujieleza hata kama anapewa nafasi ya kufanya hivyo na hii ni fursa muhimu kwa tunayemtaka.

Mpinzani wetu ni mgumu sana katika kuchangamana na makundi yote ambapo vijana humwona kama si mwenzao kiumri na kifedha, wanawake humwona kama malaya anayependa kutumia miili yao kujistarehesha wakati wazee humwona kama mtu anayedhalilisha hata nafasi aliyopewa kwa kufanya uhuni waziwazi hata kuvunja ndoa si ya kwake tu bali hata za watu wengine.

Mpinzani wetu hana mahusiano mema na mazuri na viongozi wa ngazi za chini kutokana na dharau nyingi anazozionyesha pale anapokukutana na viongozi wa ngazi za chini akiwa katika kuijenga taasisi hii. Hutumia muda mwingi kuwaponda viongozi wenzake hata kufikia kutamka mara nyingi kwamba kama kiongozi hawezi kujigharamia nauli na malazi ya kutoka mahali fulani kwenda mahali fulani kwa siku kadhaa hafai kuwa kiongozi bila kujali kwamba kuna viongozi wetu wana moyo na taasisi hii na ndo wameifikisha hapa ilipo lakini hawana uwezo wa kifedha na hivyo kauli kama hizo za mkuu huyu huona kama anawadharau kwa kuwa yeye ni tajiri. Hii imemfanya kutopendwa na viongozi wengi wa ngazi ya chini hivi sasa na kutoa fursa ya pekee kwa tunayemtaka. 
Mkuu aliyepo amekuwa na mkakati unaoitwa kuondoa watu wa zamani. Jambo hili linawaudhi sana viongozi wa ngazi za chini ambao wanaona kama baada ya kuifikisha taasisi mahali ilipo kwa sasa wanaonekana hawana maana tena. Wengi wamefikia kuapa kwamba kama mwendo ni wa kuwaondoa watu wa zamani basi na yeye ni wa zamani lazima aondoke.

Mpinzani wetu amejionyesha dhahiri kujipenda na kujijali nafsi bila kujali watu wa hali ya chini. Matukio mawili yanamwacha uchi katika hili pale alipolitangazia taifa kwamba wawakilishi wetu wote hawatachukua posho za vikao halafu yeye na wengine wote wanazichukua hadi leo na kumwacha mtendaji msaidizi peke yake. Na la pili linalofanana na hilo ni pale alipotangaza kutotumia gari la serikali ambalo ni la kifahari kisha akalirudia kimya kimya.

Kuwepo muhtasari wa kikao cha wazee ambacho mwaka 2009 kilimshauri tunayemtaka ajitoe na kumwachia mkuu aliyepo na kumtaka mkuu aliyepo kumwachia tunayemtaka katika uchaguzi ujao na wote wakasaini makubaliano hayo, nayo ni fursa muhimu sana kwa tunayemtaka.

Mkuu aliyepo anaamini kwamba ameshamsambaratisha tunayemtaka na hivyo kwa sasa amebweteka na hiyo inatupatia sisi fursa kuendelea kuimarisha mtandao wetu.

Kwa kuwa ni mwislamu. Hii ni fursa katika kupata kuungwa mkono na wanachama waislamu ambao wamekuwa na kigugumizi wakidhani waislamu hawatakiwi katika uongozi wa taasisi yetu.

Elimu ndogo na duni aliyenayo mpinzani wetu ambaye ndiye mkuu wa taasisi yetu kwa sasa. Kwa sasa ni kiongozi pekee katika nchi yetu anayeongoza taasisi kubwa asiye na elimu ya shahada huku taasisi yetu ikiwa inaongoza kwa kuwa na wasomi waliobobea katika kila nyanja. Hii ni kejeli hasa kwetu sisi ambao tumekuwa tukiwasema wenzetu kwamba ‘akili ndogo’ inaongoza akili kubwa. Kimsingi tumekuwa tukijisema kwa kukubali kuongozwa na mtu mwenye akili ndogo. 

Mkuu wa sasa kutokuwa na msimamo thabiti katika mambo ya msingi. Rejea swala la maandamano ya kumshinikiza Kawambwa ajiuzulu na kujitoa katika mchakato wa katiba. 

Vikwazo dhidi ya tunayemtaka:
Sisi wenyewe tunaoandaa mkakati huu hatuna uhakika kama tunayemtaka yuko tayari na yuko serious na business hii, na kwa hiyo huenda tusifanye kwa nguvu zetu zote ikiwa hatutapata nafasi mapema ya kukutana na mhusika na akatuhakikishia kwamba yuko serious.

Utayari wa mhusika mkuu kutekeleza yale tunayokubaliana. Inapotokea baada ya kukubaliana sisi na yeye akapata ushauri tofauti na ukauona uko more genuine, basi tuwasiliane kwamba nimeshawishika kufanya hivi badala ya vile tulivyokubaliana kwa sababu hizi ama zile. Hii haitatukatisha tamaa tofauti na kama tutakuwa tunapanga hivi halafu yeye anafanya vile bila maelezo yoyote
Kitendo cha mkuu aliyepo kung’ang’ania kuendelea nayo ni kikwazo kwa kuwa baada ya kuwa madarakani kwa miaka yote hiyo lazima amejipatia watu wanaomhusudu ama kumpenda ama kumkubali na kuwepo wengine wanaoogopa tu kwamba mkuu aliyepo akitoka taasisi itakufa hata kama hawana sababu yoyote.

Tunatazamia mkuu aliyepo atafanya vitendo vingi zaidi vya haramu katika kumdhibiti tunayemtaka pale tunapoelekea kwenye uchaguzi wenyewe.

Raslimali za taasisi kutumiwa na viongozi waliopo katika kumsaidia mkuu aliyepo wakati wa kwetu anatumia raslimali zake za mfukoni.

Propaganda chafu zilizokwishapigwa dhidi ya tunayemtaka zimepunguza imani ya wanataasisi kwa tunayemtaka kwa kiasi fulani
Baadhi ya mambo ambayo amekwishayasema ama kuyatenda nayo yameshawapunguzia imani kiasi fulani wanataasisi mbalimbali.
Kutoonekana sana kwenye operations za taasisi yetu pia kumewapa wasiwasi baadhi ya wanataasisi.

Muhtasari wa SWOT analysis unaonyesha kwamba strength na opportunities za tunayemtaka ni nyingi sana zikilinganishwa na weaknesses zake na threats dhidi yake. Aidha ukichambua zaidi utaona kwamba weaknesses za tunayemtaka nirepairable na vikwazo dhidi yake pia ni rahisi kuvikabili na kuvisambaratisha. Tukishamaliza maandalizi ya mkakati huu tukaonana na mhusika mkuu na kumpa ushauri akatulia na kufanya kazi, mkuu aliyepo hatafua dafu. Tunahitaji kutekeleza mkakati huu kwa siri kubwa ili mkuu aliyepo aendelee kubweteka na ndiyo maana hata lugha iliyotumika ni ndani hapa ni ya pekee. Tunahitaji tunayemtaka asionekane kama kuna kitu anafanya na tunafurahi kwamba kuna wakati alitangaza kwamba hana nia ya kugombea tena waliopo wanatosha. Ikitokea vyombo vya habari vikamuuliza tena hiyo ndiyo iwe kauli yake ili kuendelea kumfanya mkuu aliyepo asihangaike na hivyo kuja kummaliza kirahisi. Aidha katika utekelezaji wa mkakati kama tutakavyoeleza hapo baadaye, tunayemtaka atajitenga mbali asionekane hata kuwa karibu na sisi. Vikao vyetu na yeye vitafanyika mara chache sana na mahali pa faragha kupita kiasi ikiwezekana hata nchi jirani. 

Mkakati huu hautatakiwa kupatikana kwenye komputa zaidi ya tatu yaani ya mchapaji ambaye ni M3, ya M3 na ya MK mwenyewe. Hata hivyo email zitakazotumika kusafirisha mkakati huu kutoka kwa M3 kwenda kwa M1 hadi kwa MK hazitakuwa zile za kawaida za hao watu bali mpya kabisa zilizofunguliwa kwa makusudi haya tu na kwa majina fictitious. Aidha kila atakayekuwa na mkakati huu kwenye computer yake anatakiwa kuliwekea file hilo password ili hata mtu wa karibu naye anayeweza kufungua computer yake asiweze kulifungua file hilo. Pia email address hazitatolewa kwa sms bali kwa kupiga na kuambiana spelling za address.

MTANDAO WA USHINDI:
Mtandao wa ushindi utakuwa kama ifuatavyo. Kwenye ngazi ya kitaifa tutakuwa na kamati yenye members watatu tu. M1 ndiye atakayekuwa anawasiliana na tunayemtaka ambaye ataitwa MM (Mhusika Mkuu). Tumepanga kwamba kusiwe na mawasiliano mengi kati ya kamati na mhusika mkuu kuepuka tracking ya wapinzani wetu. M1 ni mtu wa karibu na MM kwa hiyo mawasiliano yao hayataweza kutiliwa shaka na mtu yeyote hata wangewasiliana mara nyingi kiasi gani. Hata hivyo, linapokuja suala la mkakati huu tunasihi mawasiliano yawe kwa kuonana uso kwa uso ama kwa simu na si sms. M1 ndiye atakayewasilisha mambo yote yanayotoka kwenye kamati ya kitaifa na endapo kuna haja ya MM kukutana na kamati ya kitaifa, mipango yote ya kikao itafanywa na M1 kwa usiri mkubwa. M2 ni mtu ambaye yuko kwenye ofisi kuu za taasisi yetu wakati M3 ndiye mchapaji wa mkakati huu. 

Kamati hii imefanywa kuwa na members wachache sana wenye uelewa mpana wa mambo na wenye elimu nzuri ili kuhakikisha kazi inafanyika kitaalam na kwa uhakika sana. Kamati ya kitaifa itapeleka mapendekezo yake kwaMM na yeye pia ataleta ushauri wake kwa kamati kama mishale inavyoonyesha. Chini ya kamati ya kitaifa kutakuwepo waratibu wa kanda zote kumi watakaojulikana kama MK1 – MK10. Hawa watatafutwa na kusimikwa na kamati ya kitaifa kwa kushauriana na MM kwa utaratibu utakaokubalika na pande zote yaani MM na kamati ya kitaifa. Chini ya waratibu wa kanda kutakuwapo waratibu wa mikoa yote 30 (MMK1 – MMK30) ambao watapatikana kwa utaratibu ule ule wa kuwapata waratibu wa kanda. Isipokuwa pale ambapo inakuwa ngumu, itabidi kamati ya taifa isaidiane na waratibu wa kanda kuwapata waratibu wa mikoa lakini kamati itashauriana na MM kabla ya kuwasimika rasmi hao waratibu wa mikoa.Mtandao utakuwa kama inavyoonyeshwa kwenye mchoro ufuatao:

NAMNA YA KUFANIKISHA MKAKATI:

Kazi itagawanywa katika awamu tatu:
Awamu ya kwanza ni kuanzia sasa mpaka uchaguzi wa ngazi ya matawi utakapoanza. Katika awamu hii kazi ni kuhakikisha kwamba mtandao mzima umekamilika mpaka kwenye ngazi ya mkoa. Kazi nyingine itakayofanyika ni kwa waratibu wa mikoa kuendelea kuspot makada kwenye wilaya na mikoa ambao tayari wana mtazamo tulio nao ama ambao wanaweza kuingiziwa kirahisi mbegu hii ya mabadiliko na wakawa tayari na wana uwezo na sifa za kushinda uongozi kwenye wilaya na mikoa yao bila kusahau sifa ya kuwa waaminifu wenye uwezo wa kutunza siri. Kulingana na muda hii ni kazi inayotakiwa kufanyika sasa lakini kwa uangalifu mkubwa. Ni muhimu kukumbushana hapa kwamba katika awamu hii hakuna anayetakiwa kujua mpango mzima zaidi ya kamati ya kitaifa na MMili kuhakikisha uwezekano wa mkakati wetu mapema kwa wapinzani wetu unakuwa minimized to almost zero.

Awamu ya pili ni kipindi kuanzia uchaguzi wa matawi mpaka uchaguzi wa mikoa unapokamilika. Katika awamu hii tutasaidiana na waratibu wa kanda na mikoa kuhakikisha makada tuliowaspot kwenye wilaya wanapanga safu zao kwenye kata ili kuhakikisha watakaochaguliwa kwenye kata ni watu wao ili waje wawachague kwenye wilaya.Vivyo hivyo kwa makada tuliowaspot kwenye mikoa wahakikishe wanaochaguliwa kwenye wilaya ni wale makada wetu ili nao waje wawachague kwenye mikoa yao. Hapa ndipo kwenye kazi kubwa ya mkakati wetu na hapa ndipo tutakapohitaji kuingia gharama zaidi kwa ajili ya kuhakikisha zoezi hilo linafanikiwa kwa asilimia angalau 80.

Awamu ya tatu ni kuanzia baada ya kukamilika kwa uchaguzi wa mikoa hadi uchaguzi wa kitaifa utakapoitishwa. Katika kipindi hiki kwa ustadi mkubwa tutakuwa tukiwaandaa makada wetu waliochaguliwa tayari kuja kufanya mabadiliko makubwa kitaifa. Ni wakati huu ambapo tutawaingizia mkakati taratibu lakini kwa ustadi mkubwa tukijikita hasa kwenye kuonyesha kwa nini tunahitaji mabadiliko. Ni katika kipindi hiki ambapo kwa ustadi mkubwa tunaweza kuwaspot wale waliochaguliwa ambao hatukuwaandaa na kuwaingizia pia mbegu ya mabadiliko ili kuwawin na kuwarecruit kwenye mkakati.

Aidha katika awamu zote tatu kazi ya kuianalyze ofisi kuu itakuwa non stop kwa kuzingatia kwamba mabadiliko ya wakurugenzi na maofisa yatakuwa yanatokea na watu nao watakuwa wanabadilika kimtazamo. Analysis ya ofisi kuu ni kuhakikisha tunajua nani na nani wako na sisi na nani na nani wako against na pia nani na nani wanaweza kupandikiziwa mbegu kwa ustadi na wakaungana nasi.


MAHITAJI YA KUFANIKISHA MKAKATI:
Raslimali watu. Tunahitaji watu waaminifu watatu kwenye ngazi ya kitaifa ambao tayari wapo. Tunahitaji watu waaminifu kumi kwenye kanda ambao tutawatafuta na pia waaminifu wengine 30 kwenye mikoa yote thelathini.

Fedha. Tunahitaji fedha kwa ajili ya mawasiliano kati ya wanakamati na wale wa ngazi ya chini. Aidha tunahitaji fedha kwa ajili ya gharama za usafiri pale tutakapohitaji kwenda kwenye kanda na mikoa husika kwa ajili ya kusimika watu hao tunaowahitaji.

MAPENDEKEZO MAHSUSI NA HITIMISHO:

Katika kuhitimisha tunapendekeza mambo mahsusi yafuatayo:

Kuhusu Bajeti: 
Tunapendekeza kwamba bajeti ya mkakati huu isipangwe hivi sasa. Ni muhimu tu sote kuelewa kwamba wakati wenzetu wanatumia raslimali za taasisi kujijenga na kutekeleza mkakati wao wa ushindi, sisi tunapaswa kuingia mifukoni. Kwa kila kila mmoja wetu atakuwa budget conscious ili kuepuka matumizi makubwa ya pesa. Hata hivyo, kwa kuzingatia kwamba lazima pesa inahitajika ni muhimu M1 na MM kujaribu kuangalia namna ya kuraise pesa na kushauri. Otherwise, tutakapokuwa tunahitaji kufanya hatua yoyote ama jambo lolote tutakuwa ndo tunapiga hesabu za funds tunazohitaji kwa jambo husika na kuingia katika utekelezaji.

Kuhusu mwenendo wa MM kuanzia sasa: 
Ni maoni yetu pia kwamba kuanzia sasa MM aenende katika mwenendo ambao utarahisisha ushindi. Mfano tunapendekeza afanye yafuatayo kuanzia sasa:

Apunguze ukaribu na viongozi wa serikali na wa chama tawala na awe crical zaidi na utendaji wa serikali nje na ndani ya bunge. 
Ashiriki kikamilifu katika shughuli za taasisi yetu zikiwamo vikao vyote vinavyomhusu, operesheni mbalimbali, chaguzi ndogo, nk.
Aendelee kushusha ‘nondo’ ndani ya chombo chetu cha uwakilishi na kuendelea kuwa juu ya wawakilishi wengine katika hoja mbalimbali zenye maslahi ya kitaifa.

Ajitahidi kudhibiti jazba hata pale anapokuwa amebambikiziwa tuhuma nzito namna gani. Atulie, ashauriane na wazee ili kuona namna nzuri ya kujibu tuhuma zinazomkera. Tukumbuke kwamba wakati mwingine kukaa kimya ni jibu zuri zaidi kuliko hoja nzito.
Sambamba na ‘iv’ hapo juu, adhibiti sana emotion ili kuhakikisha kila kitu kinachofanywa ama kuzungumzwa kinachomgusa asikimbilie kuongea na vyombo vya habari ama kwenye mitandao ya kijamii bali afuate kile tulichokizungumza kwenye kipengele cha ‘iv’ hapo juu.

Kuhusu mapambano ya kuchafuana kwenye mitandao ya kijamii:

Katika hili sisi hatukuona haja ya kufanya hivyo kwa sababu mbili:
Imani yetu kwamba taasisi yetu ni kubwa kuliko watu kwa hiyo ni muhimu kuzingatia kwamba hatuiui taasisi katika mapambano haya. Tukiendekeza mashambulizi kwa njia ya mitandao ya kijamii hatutakuwa na ngao ya kuwakinga watu wa kawaida (wanataasisi na wasio wanataasisi) dhidi ya kujikuta wakiamini kwamba taasisi hii nayo haina jipya ni sawa tu na ile tunayotaka kuitoa. 

Tutakuwa tumeiua taasisi na mkakati huu hautakuwa na maana sana kama lengo ni kufanya mabadiliko ya uongozi wa taasisi tu lakini malengo ya taasisi ya mwaka 2015 yasitimie!

Kujikita kwenye mashambulizi kupitia mitandao ni kuzidi kuwashtua wakuu waliopo kwamba bado tuko serious na mkakati wa kuwatoa na kuwafanya wafanye kazi zaidi huku wakiendelea kumpaka matope MM kwamba ndiye anayerusha makombora hayo kwenye mitandao kwa kusudi la kuhujumu taasisi maana hiyo ndo lugha yao. Hatukatai kwamba wakuu wanajua kabisa kwamba bado MM ana nia ya kumvaa mkuu aliyepo lakini tunajua kwamba kwa sasa wanaamini wamemdhoofisha na hana madhara tena. Ndiyo maana tunataka kutekeleza mkakati wetu kwa siri sana ili wafikiri MM amekata tamaa kumbe ndo anakuja na mkakati mzito zaidi.

Hata hivyo, ni muhimu kukumbushana kwamba wenzetu hawatanyamaza kwa sababu eti sisi tumeacha kuwashambulia kwenye mitandao ya kijamii. Lazima wataendelea! Wataendelea kumchafua MM kwa kupitia wapuuzi kama yule kichaa wa ‘ars’ na kundi lake. Nini tutakuwa tunakifanya sasa? Tutahakikisha tuko busy kupost mambo mema na mazuri yatakayokuwa yakifanywa na MM kila wakati na kuzidi kusambaza sifa zake njema kila inapotokea nafasi. Atakayefanya kazi hiyo ni sisi wengine wala si yeye! Pia tutahakikisha kila post ya kumchafua inapatiwa majibu bila kutumia ID yake inayojulikana. Ni vema aidha akatupatia majibu na sisi kuyapost ama afungue ID mpya kabisa ambazo hazijawahi kuwepo kwenye mitandao halafu ndo awe anazitumia kujibu lakini kwa kuzingatia tuliyokwishayazungumza hapo juu yaani kutofanya kwa emotion na kuepuka jazba lakini pia kushauriana na watu wa karibu kabla ya kutoa majibu kwa jambo lolote linalomhusu.

Kuhusu kamati ya kitaifa (hususan M2 & M3):
Tulikubaliana kwa kauli moja kwamba katika kutekeleza mkakati huu tunahitaji members hawa wawe wametulia kimaisha. Inakuwa vigumu kwa mfano kumtaka member aende mahali fulani kwa makusudi ya mkakati huu wakati hajui familia yake nyumbani anaiacha inakula nini. Tuliona kwamba M3 tayari hana kazi kwa sasa tena kwa kufanyiziwa na wakuu waliopo. Ni katika mwendelezo huo huo tunamwona M2 naye akiwa ukingoni kupigwa nje na kuachwa mtupu na wakuu waliopo katika kile wanachokiita wao reshuffle ya ofisi kuu. Kwa sababu hiyo tukapendekeza kwamba MM kwa kushirikiana na M1 kwa hatua ya kwanza wanaweza kutafuta kiasi cha sh. 2m kila mmoja tukijua kwamba kama members hawa wawili wakisaidiwa milioni mbili mbili wanaweza kuanzisha projects ambazo zitawasustain hata kama hawana ajira. Kwa hatua ya baadaye tutasaidiana kuona kama hawa members wanaweza kusecure good employments mahali, provided hazitawazuia kufanya siasa.
https://mail.google.com/mail/images/cleardot.gif


HII NAYO NI RIPOTI YA SIRI JUU YA ZITTO KABWE

Friday, 8 November 2013 

RIPOTI YA SIRI JUU YA ZITTO KABWE
CHADEMA
UCHUNGUZI WA MWENENDO WA KISIASA WA ZITTO Z. KABWE NDANI NA NJE YA CHADEMA.
UTANGULIZI:Tangu mwaka 2008 mwenendo wa kisiasa wa Zitto Zuber Kabwe ulianza kutiliwa shaka na wanachama wa CHADEMA ndani na nje ya chama, Hili lilipelekea kuibuka maneno ya chini kwa chini kuwa anakisaliti chama.
Hilo liliilazimu timu ya kijasusi ya chama kuanza kufuatilia nyendo zake kwa ukaribu zaidi usiku na mchana ili kujiridhisha pasipo kuacha chembe ya mashaka. Ifahamike kuwa chama kina idara ya ulinzi na usalama wa chama na viongozi wake yenye uwezo wa kufuatilia nyendo za majasusi wa nje na viongozi na wanachama wake popote walipo kwa masaa 24. Baada ya kujiridhisha kuwa mwenendo wake ni wa mashaka, bila kusita timu ya ujasusi ilianza kazi rasmi ya ujasusi dhidi ya nyendo zote za Zitto Zuberi Kabwe.

MAMBO YALIYOFANYIWA UCHUNGUZI DHIDI YA ZITTO KABWE.
Kumfuatilia yeye binafsi nyendo zake.
Kufuatilia mawasiliano yake ya simu.
Kufuatilia mawasiliano yake ya barua pepe.
Kufuatilia pato lake nje ya kazi zake halali za kibunge.

SEHEMU YA KWANZA 2008
Chombo chetu cha ujasusi tulichokipandikiza kwa siri katika nyendo zote za Zitto Kabwe na ndani ya vikao vya mwanzo kabisa vya Zitto na viongozi serikalini, nahata vile vikao muhimu  vya idara ya ujasusi ya chama cha mapinduzi (ccm), kinatupa fursa ya kuweka msingi wa kuimarisha chama cha CHADEMA na kutenda haki kidemokrasia kwa maslahi ya chama na Taifa kwa ujumla:
Mnamo Jumatatu ya tarehe 16/6/2008 saa 09:46 asubuhi, Mh Zitto Kabwe kupitia simu yake ya kiganjani namba +255754787550 alipokea simu kutoka kwa Ramadhani Ighondu mwenye namba +255717760473 ambaye ni afisa Usalama wa Taifa anayefanya kazi ikulu hivi sasa. Alijitambulisha kuwa yeye ni Usalama wa Taifa  ametumwa na mkuu wake wa kazi aje aongee na Zitto, Maelezo ya msingi katika simu hii ilikuwa ni bwana Ramadhani Ighondu kuomba miadi ya kuonana kutokana na agizo la mkuu wake wa kazi.
Siku sita baadae yaani Jumatatu ya tarehe 23/6/2008 saa 07:52 asubuhi, Zitto alipigiwa tena simu na Ramadhani Ighondu akimkumbusha maongezi yao waliyo fanya siku 6 zilizopita na kumuomba siku hiyo jioni waonane, ingawa Zitto alionekana kusita kidogo lakini baadae alikubali, Walikubaliana wakutane Sea Cliff  Hotel, ilipofika jioni ya siku hiyo Zitto akiwa na marafiki zake wawili Omar Lyasa na Abdalah Said walifika Sea Cliff Hotel wakaketi na kuagiza vinywaji, Baada ya kama dakika kumi hivi Zitto alipokea simu ikimuelekeza alipo bwana Ramadhani Ighondu kisha Zitto akawaambia marafiki zake wamsubiri kidogo, akaondoka kuelekea aliko elekezwa…..
Mashariki mwa lango kuu la kuingilia Sea Cliff Hotel mita kama tatu tu kuna mlango mdogo unaoelekea kwenye vyumba maalumu (VIP), chumba namba 8 ndicho Zitto alichokuwa anaelekezwa kwa simu kuingia, chumba hiki kina meza moja na sofa zilizo zunguka meza ile zenye uwezo wakukaliwa na watu watano hadi sita, Ndani ya chumba kile Zitto anakutana na watu watatu ambao ni Steven Wasira, Ramadhani Ighondu na Abdalla Punja (hawa wote ni TISS)
Mazungumzo yao ndani ya chumba hiki yalianza maramoja, akianza Mr Ighondu kueleza sababu za wao kumuita Zitto, kikubwa ilikuwa ni “bwana Zitto, serikali (ikulu) inakutaka uache kuibana na kuishurutisha hasa kwa hili suala la Buzwagi”. Tunaomba kujua shida yako kubwa ni nini?” Ighondu alihoji, Katika majibu yake Zitto anajibu,  “Mimi napigania haki za watanzania, nimechaguliwa na wanakigoma na watanzania wameniamini ni wawakilishe hivyo”, Lakini mashambulizi ya ushawishi yalipozidi Zitto alilegeza msimamo wake.
Katika kikao hiki kilichochukua masaa mawili, Zitto anaonekana kusita sana na anaomba apewe muda akafikirie aliyoitiwa, wote wanaafiki na kukubali ombi la Zitto na kikao kinaahirishwa.
Siku tatu tu baada ya kikao cha Hotel ya Sea Cliff, yaani tarehe 27/6/2008 Zitto anakutana na Naibu Mkurugenzi wa TISS Ndugu Jack Zoka jijini Arusha, hiki sio kikao chao maalumu bali wamekutana kwa mara ya kwanza wote wakiwa kwenye shughuli za kitaifa, Katika mazungumzo yao wanaonekana ni watu wanaofahamiana japo si kwa undani, Baada ya maongezi ya dakika kadhaa wakiwa wamesimama, Mr Zoka alimuuliza “Vipi vijana wangu walikupa ujumbe, umefikia wapi?” Zitto aliitikia kwa kucheka na kusema “yap nipo tayari, lakini nihakikishieni usalama wangu” Katika maongezi haya, Zoka anasikika akisema“Ondoa shaka” Kisha Mr Zoka anamuagiza Zitto kuwa kesho kutwa yake aende kwa Charles Kimei (Mkurugenzi CRDB Benki) pale Makao makuu, atayakuta maagizo yake huko.
Tarehe 30/6/2008 majira ya saa 12:22 za alasiri, Zitto akiwa ameongozana na kijana mmoja aliyetambuliwa kwa jina la Rajabu Abdala anaingia eneo la CRDB Benki mtaa wa Azikiwe, na kwenda moja kwamoja kuonana na Bw Kimei, baada ya salamu haikuchukua muda mrefu, Zitto akapelekwa katika moja ya vyumba maalumu vya bank hiyo kwenye jengo hilohilo la Azikiwe, baada ya kufika katika chumba hicho Zitto alihamaki kuwakuta watu wawili katika chumba hicho, mmoja alikuwa ni mfanyakazi wa bank hiyo aliyetambuliwa kwa jina la Maselina K. Kombe na mwingine hakuwa mgeni machoni mwa Zitto, alikuwa ni Ramadhani Ighondu yule wa TISS waliyekuwa naye kwenye kikao cha awali kule Sea Cliff  Hotel wiki chache zilizopita, Zitto alikabidhiwa Briefcase nyekundu iliyokuwa imesheheni pesa halali za kitanzania kiasi cha Shilingi milioni 250.
Wakati hayo yakitendeka yule kijana aliyekuja na Zitto alikuwa kwenye gari aina ya Toyota Mark 11 No T 134 AAB yenye rangi nyeupe na vioo vyeusi (Tinted). Baada ya makabidhiano yaliyochukua kama dakika 10 tu, Mr Ighondu alimwambia Zitto, “tunataka utulivu, mengi mazuri yanakuja utafurahia kijana,” Na kisha Zitto akatoka na begi lake (Briefcase) na kuingia nalo katiga gari ile na kutokomea.
Uchunguzi umeonyesha kuwa pesa ile aliyokabidhiwa ndugu Zitto, ilitoka katika akaunti Namba 0J56708968923 yenye jina la Shani Maya, ambapo inaonyesha kuwa akaunti hii ilifunguliwa CRDB tawi la azikiwe tarehe 25/6/2008 saa 10:14 asubuhi, kisha tarehe 27/6/2008 iliingizwa kiasi cha pesa za kitanzania milioni 400. Na tarehe 30/6/2008 pesa hizo zilitolewa zote na akaunti hii ilifungwa. Madhumuni ya pesa hii kutoka CRDB kwenda kwa Zitto yanathibitishwa na kikao cha 23/6/2008 pale Hotel ya Sea Cliff kuwa ni kupunguza kasi ya Zitto kuibana serikali hasa anapo kuwa bungeni. Na kweli kasi yake iliyozoeleka kwenye kuibana serikali akiwa bungeni ikapungua na kuweka msingi wa ujenzi wa mashaka juu ya mwenendo wake wa kibunge.

SEHEMU YA PILI 2009
Mnamo Jumatatu ya tarehe 30/11/2009 saa 04:30 asuhuhi wakati wa maandalizi ya uchaguzi wa  mkuu wa 2010,  idara ya ujasusi ya CCM ilikutana kwa siri pale Moven Pick/SERENA Hotel, ndani ya idara hii wakiwamo Jack Zoka, Wilson Mkama, Kingunge Ngombale Mwiru, Jakaya Kikwete, Nape Nnauye, Fred Kimati, Steven Wasira, Ramadhani Ighondu, Martin Palakyo, Mwigulu Nchemba, Ahamed Msangi na Abdalla Punja. Katika kikao hiki yalijadiliwa mengi sana, lakini kubwa lilikuwa nikukabiliana na vyama vya upinzani hususani CHADEMA, zilipangwa mbinu nyingi sana juu ya Chadema. Mbinu hizo ni kama ifuatavyo:
Kuwanunua wagombea ubunge na Udiwani (Mtakumbuka wagombea wetu kadhaa walikuja kununuliwa na chama kina ushahidi kwenye hili).
Kuwanunua VIONGOZI wajuu wa CHADEMA.
Kutumia TISS kutisha wagombea na wanachama wa Chadema (Hii ilikuwa ni kuwakamata au kuvuruga mikutano).
Kuwaua baadhi ya wafuasi wa Chadema, viongozi wa Chadema na wabunge.
Lakini walitilia mkazo zaidi njia ya kwanza, ya pili na ya tatu ambapo kikao kilijiridhisha kuwa mmoja wa VIONGOZI wa Chadema ambae ni Zitto Kabwe ni mtu wao ambaye wamesha anza kumtumia, kikubwa liandaliwe fungu tu kwa ajili yakuanza mikakati yao, Waliafikiana mambo mengi kwaajili ya uchaguzi wa mwaka ambao ungefuata, na wakakubaliana mambo kadhaa ambayo walimuagiza Mr Zoka akamwambie Zitto nini cha kufanya ili kupunguza nguvu ya upinzani.
Kwa upande wake Zoka alikiambia kikao kuwa Zitto amemthibitishia kuwa yeye ana wafuasi wa kutosha ndani ya chama ambapo watamuunga mkono kwa lolote hivyo kikubwa ni pesa tu. Lakini kwanza kikao hicho kilimtaka Mr Zoka amwambie Zitto kuwa taarifa zote zinazoihusu Chadema na za kila vikao vya ndani vya chama zinatakiwa pia ziifikie timu hiyo ya kijasusi ya CCM, pili walitaka Zitto apunguze ushiriki katika majukwaa ya chama na shughuli nyingine za chama. Baada ya kikao sasa ulikuwa ni utekelezwaji wa maadhimio yao.
Zoezi la kikao cha tarehe 30/11/2009 linaonyesha kuzaa matunda hasa baada ya kubainika mawasiliano ya karibu sana kati ya Zitto na Jack Zoka,  Kwamfano: Jumamosi ya tarehe 6/12/2009 saa 03:43 asubuhi Zoka kupitia namba yake ya simu +255756809535alimpigia simu Zitto kupitia simu yake ya kiganjani ambayo ni +255754787550, wakati wa mawasiliano yao haya ya simu Zitto alikuwa Tabata na maongezi yao yalihusu kikao cha 30/11/2009 na kile walichoamua timu ya kijasusi ya chama (CCM) na matakwa yao kwa Zitto. Ndani ya maongezi yao yaliyochukua dakika 68, Zitto anasema, “Mr kazi hii ni nzito, vipi mmeongeza hela? Isije kuwa kama ile ya mwaka jana.” Anajibiwa na Zoka kuwa “ondoa shaka una dili na Jamhuri, hela sio tatizo”
Lakini zaidi Zitto anamshauri bwana Zoka kuwa utaratibu wa uchukuaji wa pesa ubadilike, “Mr Jack ile staili ya uchukuaji pesa kule CRDB mwaka jana ilinitisha kidogo halafu hii isije ikabumburuka vyombo vya habari vipo makini kweli sasa hivi” Anajibiwa na Bwana Zoka kuwa “Tunazo njia nyingi sana ambazo si TAKUKURU wala polisi wanaoweza kubaini, tusikilize sisi, tutakacho kuambia ujue ni salama, Haya Mr (Zitto) wewe unayajua mazingira vizuri katika nchi moja ya Ulaya?, au unaweza kutafuta mtu unae mwamini huko ili atumiwe yeye hiyo pesa na awe wa kuaminika ili tumtumie kwa vipindi hivi vyote, kisha uifuate huko au uangalie mwenyewe njia sahihi ya kuichukua huko”  Suala la kumpata mtu Ulaya lilionekana kama zito kidogo kwa Zitto, kwani aliomba wawasiliane kesho yake ili awe na jibu la uhakika.
Tarehe hiyo hiyo 6/12/2009 ya Jumamosi saaa 23:05 usiku, Zitto kupitia simu yake ya mkononi namba  +255754787550, alipiga namba +4915739444853, kimaongezi walionekana ni watu wanafahamiana sana, alikuwa anaongea na mwanamke, waliongea mengi lakini kubwa lilikuwa ni Zitto kuomba kupitisha hela yake kwenye akaunti ya huyu mtu. Mwanamke huyu alihoji kama pesa hiyo ni nyingi na haina madhara? Lakini alijbiwa sio nyingi na haina madhara kwakuwa inatoka serikalini na chama tawala, Mwanamke huyo alizidi kuhoji zaidi, “sasa vyombo vya dola vya hapa Berlin vikinihoji nitasema nimepata wapi?”  Anajibiwa kuwa “Darling  huniamini? Nimesoma na wewe na nimefanya kazi  na wewe, lakini huniamini? Utasema umelipwa nchini Tanzania kwa kazi yako”, kisha katika maongezi ya hapa na pale dada akakubali na baada ya dakika kumi akamtumia akaunti namba 033B 33093101 Berliner Bank German.
Baada ya kuipata akaunti hii Zitto hakuchelewa, akaipeleka kwa Mr Zoka kwa njia ya ujumbe wa maandishi (sms), baada ya dakika 5, Zoka akampigia simu Zitto kupitia namba+255756809535 nae Zitto akapokea kupitia namba +255754787550, na mazungumzo yao yaliyochukua dakika 6 yakaendelea,  Zoka aliuliza swali kuwa “Mwenye akaunti hiyo huko Ujerumani unamwamini na unamjua vema?” Majibu ya Zitto yalikuwa “Ondoa shaka Mr Jack nafanya kazi ya hatari na wewe, siwezi kukuangusha au kujiangamiza, huyu mtu nimesoma nae na ninamfahamu in and out” Zoka akajibu “ok”.
Jumatano ya tarehe 16/12/2009 majira ya saa 13:12 za mchana kwa Ujerumani akaunti namba 033B 33093101 Berliner Bank, ziliingizwa dola za kimarekani 266,000 pesa hizi katika uchunguzi zimebainika kuwa zilitoka Tanzania katika Benki ya NMB tawi la NMB House jiji Dar katika akaunti namba 2231604658 yenye jina la TSA, hii ni moja ya akaunti za siri za TISS, ambapo wao ndio huzisimamia akaunti zao zote kwa kutumia mawakala (TISS) walio ndani ya benki hiyo.
Kujiridhisha kuwa pesa hiyo ilifika Ujerumani, kunabainishwa na mawasiliano ya barua pepe kati ya Zitto Kabwe na  yule mwanamke wa kijerumani aliyemtumia akaunti ya benki, anafahamika kwa jina la Andrea Cordes, mawasiliano yaliyofanywa tarehe 17 alhamisi saa 20:34 usiku ambapo Andrea kupitia barua pepe yake acodes@gmail.com anamwandikia Zitto kupitia barua pepe ya Zitto iitwayo zittokabwe@gmail.com ,  Andea anasema “Hey sweet, mzigo yako imefika, can we talk?”  Ujumbe huu unajibiwa na Zitto saa 21:03 usiku huo kwakusema, “I’m so sorry my darling, nimechelewa kukujibu, I will call you soon”
Saa 23:23 Zitto Kabwe kupitia simu yake ya kiganjani namba +255754787550, alimpiga Andrea Codes kupitia namba +4915739444853akimweleza kuwa anashukuru kwa mzigo kumfikia, lakini anataka kumpa utaratibu wa kuichukua hiyo pesa, ambapo alimweleza kuwa atakuwa anaichukua kidogo kidogo kila mwezi kwa njia ya Western Union kuanzia dola 20,000 hadi dola 50,000, wakati huo Andea Codes atakula kamisheni ya dola 25,000.
Uchunguzi wa ndani umebaini pesa hiyo ilitumwa kwa Zitto ndani ya miezi 8 kwa vipindi tofauti kupitia Western Union kama alivyoomba, na alikuwa anachukulia maeneo tofauti tofauti hapa jijini Dar, vilevile uchunguzi umebaini kuwa mwanamke huyu ni Mjerumani aliyewahi kuishi Tanzania na amezaa mtoto mmoja hapa Tanzania,  Mwanamke huyu anaitwa Andrea Cordes, anaishi Mechernich Ujerumani, mtaa namba 134, nyumba namba 141,  anafanya kazi UN Women Nationales Komitee Deutschland e.V.  Shirika ambalo shughuli zake huendeshea pia Tanzania. Katika uchunguzi zaidi imebainika kuwa akaunti aliyomtumia Zitto ni ya kwake binafsi, katika ushahidi tuliobaini kupitia  benki iitwayoBerliner Bank yenye Code No Hardenbergstraße 32, 10623 iliyopo mjini Berlin nchini Ujerumani.

SEHEMU YA TATU 2010
Uhusiano usio wa kawaida na wa karibu wa Zitto na viongozi wa ccm, serikali na wale wa Usalama wa Taifa uliendelea kushamiri hasa kipindi cha kampeni na kipindi cha uchaguzi mkuu wa 2010, Mfano tarehe 7/9/2010 siku ya jumanne saa 11:21 asubuhi, Ahmed Msangi kupitia namba yake ya simu  ya kiganjani +255784277884, alimpigia Zitto kupitia simu ya kiganjani  namba  +255754787550 waliongea mambo mengi japo kwa muda mfupi, na jambo kubwa lilikuwa ni “vipi kuna kipya ndani ya Chadema?” Zitto alijibu “yapo mengi lakini hayana impact kwa ccm” Msangi anajibu “Ok mr nikutakie siku njema”
Lakini mawasiliano  ya simu yaliyochukua mda mrefu zaidi yalikuwa kati ya Zitto na Zoka yaliyofanywa tarehe  10/9/2010 siku ya ijumaa saa 07:04 jioni na mazungumzo yao yalichukua dakika 71, Mazungumzo haya yalifanywa wakati huo Zitto akiwa katika hoteli ya  Blue Pearl Ubungo, Mr Zoka alitaka kujua mambo kadhaa kuelekea Uchaguzi mkuu, kwanza alimuuliza “Mr Zitto umejiandaaje, una timu ya kazi?” Zitto akajibu “nipo fiti kiakili na kimwili na nina timu ya kutosha, ondoa shaka juu yangu, kama ipo hiyo hela tumeni tu Ujerumani kwenye ile akaunti, na ningeomba kukutana na mwenyeti wenu (rais JK)” Zoka lijibu “hilo halina tabu nitalifikisha sehemu husika bwana Zitto”,
Uchunguzi umebainisha kuwa akaunti namba 033B 33093101 Berliner Bank ya German iliendelea kuingizwa pesa kwa nyakati tofauti kutoka Tanzania kupitia NMB akaunti namba 2231604658  yenye jina la TSA ambayo ni moja ya akaunti za siri za TISS.
Mfano: tarehe 29/9/2010 siku ya juma tano, kiasi cha dola 250,000 kiliingizwa kwenye akaunti hii  033B 33093101 ya Ujerumani, kutoka akaunti namba 2231604658 NMBTanzania,
Tarehe 06/01/2011 siku ya alhamisi, kiasi cha dola 240,000 kiliingizwa kwenye akaunti hii  033B 33093101 ya Ujerumani, kutoka akaunti namba 2231604658 NMB Tanzania,
Tarehe 21/6/2011 siku ya jumanne, kiasi cha dola 240,000 kiliingizwa kwenye akaunti hii  033B 33093101 ya Ujerumani, kutoka akaunti namba  2231604658 NMB Tanzania,
Tarehe 09/12/2011 siku ya ijumaa, kiasi cha dola 255,000 kiliingizwa kwenye akaunti hii  033B 33093101 ya Ujerumani, kutoka akaunti namba 2231604658 NMB  Tanzania,
Tarehe 02/02/2012 siku ya alhamisi, kiasi cha dola 260,000 kiliingizwa kwenye akaunti hii  033B 33093101 ya Ujerumani, kutoka akaunti namba 2231604658 NMB Tanzania,
Tarehe 14/05/2012 siku ya jumatatu, kiasi cha dola 250,000 kiliingizwa kwenye akati hii  033B 33093101 ya Ujerumani, kutoka akaunti namba 2231604658 NMB Tanzania,
Tarehe 13/12/2012 siku ya alhamisi, kiasi cha dola 255,000 kiliingizwa kwenye akati hii  033B 33093101 ya Ujerumani, kutoka akaunti namba 2231604658 NMB Tanzania,
Uchunguzi umebainisha kuwa pesa zote zilimfikia Zitto kwa njia ya Western Union akitumiwa dola 50,000 mpaka dola 20,000 kati ya wiki mbili mpaka mwezi mmoja.

SEHEMU NNE: MATUMIZI YA PESA HIYO

Uchunguzi umezidi kubaini kuwa kuanzia mwanzoni mwa mwaka 2011, kutoka kuugwa mkono na wanachadema kama mwanasiasa makini, Zitto aliamua kuunda kundi la uasi ndani ya chama. Baadhi ya waliounda kundi hili ni:
Zitto Z. Kabwe +255754787550/756809535/713730256
Juliana Shonza +255714669850/756359073
Habib Mchange +255762178678
Mtela Mwampamba +255718037358/755178927
Gwakisa  Burton +255713316790
Eddo Makata +255757149043/655148758
Greyson Nyakarungu +255755023503
Adams Chagulani +255767137831
Deogratius Kisandu +255655025609
John M. Shibuda  +255754465597
Kitila Mkumbo +255754301908
Exaud Mamuya  +255767160685
Ben Saanane +255768078523

Timu ya upelelezi imebaini kuwa kundi hili lilikuwa linapokea fedha kutoka kwa Zitto kwa njia ya M-Pesa, Uchunguzi umebaini kuwa kuanzia 2011 kundi hili lilianza kutumiwa pesa na Zitto kwa njia ya M-Pesa kila mwezi, ambapo kila mwanakundi alikuwa akipokea kati ya 150,000/= mpaka 200,000/= , na ilipofika mwishoni mwa mwaka 2012 kundi hili sasa likawa linalipwa karibu kwa wiki,

Takwimu za malipo ya wafuasi wa kundi hili kutoka kwa Zitto kwa mwaka 2012 zinaonyesha walilipwa kwa njia ya  M-PESA  No+255756809535 hii ni namba mojawapo ya Zitto Zuberi Kabwe:
Tarehe 25/2/2012 saa 10:09 asubuhi, Zitto Kabwe kupitia +255756809535 aliwatumia shilingi 150,000/= wafuasi wa kundi lake,  Juliana Shonza +255756359073, Habib Mchange +255762178678, Mtela Mwampamba +255755178927, Gwakisa  Burton +255713316790, Eddo Makata +255757149043, Greyson Nyakarungu +255755023503, Deogratius Kisandu +255655025609, Adams Chagulani +255767137831, Exaud Mamuya  +255767160685, Ben Saanane +255768078523,
Baada ya hapo saa 10:32 asubuhi hiyohiyo Zitto Kabwe kupitia namba yake ya simu+255756809535 aliwatumia shilingi 200,000/= Mkumbo Kitila +255754301908 na John Shibuda +255754465597
Tarehe 26/3/2012 saa 11:12 asubuhi, Zitto Kabwe kupitia namba yake ya simu+255756809535 aliwatumia shilingi 150,000/= wafuasi wa kundi lake,  Juliana Shonza +255756359073, Habib Mchange +255762178678, Mtela Mwampamba +255755178927, Gwakisa  Burton +255713316790, Eddo Makata +255757149043, Greyson Nyakarungu +255755023503, Deogratius Kisandu +255655025609, Adams Chagulani +255767137831, Exaud Mamuya  +255767160685, Ben Saanane +255768078523, Baada ya hapo saa 11:43 asubuhi hiyohiyo Zitto Kabwe kupitia namba yake ya simu +255756809535 aliwatumia shilingi 200,000/= Mkumbo Kitila +255754301908 na John Shibuda +255754465597
Tarehe 20/4/2012 saa 09:11 asubuhi, Zitto Kabwe kupitia namba yake ya simu+255756809535 aliwatumia shilingi 150,000/= wafuasi wa kundi lake,  Juliana Shonza +255756359073, Habib Mchange +255762178678, Mtela Mwampamba +255755178927, Gwakisa  Burton +255713316790, Eddo Makata +255757149043, Greyson Nyakarungu +255755023503, Deogratius Kisandu +255655025609, Adams Chagulani +255767137831, Exaud Mamuya  +255767160685, Ben Saanane +255768078523, Baada ya hapo saa 10:30 asubuhi hiyohiyo Zitto Kabwe kupitia namba yake ya simu +255756809535 aliwatumia shilingi 200,000/= Mkumbo Kitila +255754301908 na John Shibuda +255754465597
Tarehe 22/5/2012 saa 10:15 asubuhi, Zitto Kabwe kupitia namba yake ya simu+255756809535 aliwatumia shilingi 150,000/= wafuasi wa kundi lake,  Juliana Shonza +255756359073, Habib Mchange +255762178678, Mtela Mwampamba +255755178927, Gwakisa  Burton +255713316790, Eddo Makata +255757149043, Greyson Nyakarungu +255755023503, Deogratius Kisandu +255655025609, Adams Chagulani +255767137831, Exaud Mamuya  +255767160685, Ben Saanane +255768078523, Baada ya hapo saa 11:02 asubuhi hiyohiyo Zitto Kabwe kupitia namba yake ya simu +255756809535 aliwatumia shilingi 200,000/= Mkumbo Kitila +255754301908 na John Shibuda +255754465597
Tarehe 28/6/2012 saa 13:51 mchana,  John M. Shibuda kupitia namba yake ya simu+255754465597 aliwatumia shilingi 150,000/= wafuasi wenzake,  Habib Mchange +255762178678, Mtela Mwampamba +255755178927, Gwakisa  Burton +255713316790, Eddo Makata +255757149043, Deogratius Kisandu +255655025609, Adams Chagulani +255767137831, Exaud Mamuya  +255767160685, Ben Saanane +255768078523, Greyson Nyakarungu +255755023503, Juliana Shonza +255756359073,

Baada ya Shibuda kuwalipa 28/6/2012 saa 13:51 mchana,  sasa Zitto alibadili mfumo wa malipo ukawa wa TIGO PESA +255713730256 lakini viwango vilevile na mtiririko ulele.
Tarehe 22/7/2012 saa 08:17 asubuhi, Zitto Kabwe kupitia namba yake ya simu +255713730256 aliwatumia shilingi 150,000/= wafuasi wa kundi lake,  Ben Saanane +255768078523, Adams Chagulani +255767137831, Juliana Shonza +255756359073, Habib Mchange +255762178678, Mtela Mwampamba +255755178927, Gwakisa  Burton +255713316790, Eddo Makata +255757149043, Greyson Nyakarungu +255755023503, Deogratius Kisandu +255655025609, Exaud Mamuya  +255767160685, Kisha saa 09:38 asubuhi hiyohiyo Zitto Kabwe kupitia namba yake ya simu  +255713730256 aliwatumia shilingi 200,000/= Mkumbo Kitila +255754301908 na John Shibuda +255754465597
Tarehe 24/8/2012 saa 09:06 asubuhi, Zitto Kabwe kupitia ++255713730256  aliwatumia shilingi 150,000/= wafuasi wa kundi lake,  Ben Saanane +255768078523, Adams Chagulani +255767137831,Juliana Shonza +255756359073, Habib Mchange +255762178678, Mtela Mwampamba +255755178927, Gwakisa  Burton +255713316790, Eddo Makata +255757149043, Greyson Nyakarungu +255755023503, Deogratius Kisandu +255655025609, Exaud Mamuya  +255767160685, Kisha saa 09:23 asubuhi hiyohiyo Zitto Kabwe kupitia namba yake ya simu +255756809535 aliwatumia shilingi 200,000/= Mkumbo Kitila +255754301908 na John Shibuda +255754465597
Tarehe 02/09/2012 saa 09:52 asubuhi, Zitto Kabwe kupitia  +255713730256 aliwatumia shilingi 150,000/= wafuasi wa kundi lake,  Ben Saanane +255768078523, Adams Chagulani +255767137831, Juliana Shonza +255756359073, Habib Mchange +255762178678, Mtela Mwampamba +255755178927, Gwakisa  Burton +255713316790, Eddo Makata +255757149043, Greyson Nyakarungu +255755023503, Deogratius Kisandu +255655025609, Exaud Mamuya  +255767160685, Kisha saa 10:43 asubuhi hiyohiyo Zitto Kabwe kupitia namba yake ya simu +255713730256  aliwatumia shilingi 200,000/= Mkumbo Kitila +255754301908 na John Shibuda +255754465597
Tarehe 20/09/2012 saa 10:19 asubuhi, Zitto Kabwe kupitia  +255713730256 aliwatumia shilingi 150,000/= wafuasi wa kundi lake,  Ben Saanane +255768078523, Adams Chagulani +255767137831, Juliana Shonza +255756359073, Habib Mchange +255762178678, Mtela Mwampamba +255755178927, Gwakisa  Burton +255713316790, Eddo Makata +255757149043, Greyson Nyakarungu +255755023503, Deogratius Kisandu +255655025609, Exaud Mamuya  +255767160685, Baada ya hapo saa 10:53 asubuhi hiyohiyo Zitto Kabwe kupitia namba yake ya simu +255713730256  aliwatumia shilingi200,000/= Mkumbo Kitila +255754301908 na John Shibuda +255754465597
Tarehe 24/10/2012 saa 11:18 asubuhi, Zitto Kabwe kupitia  +255713730256 aliwatumia shilingi 150,000/= wafuasi wa kundi lake,  Ben Saanane +255768078523, Adams Chagulani +255767137831, Juliana Shonza +255756359073, Habib Mchange +255762178678, Mtela Mwampamba +255755178927, Gwakisa  Burton +255713316790, Eddo Makata +255757149043, Greyson Nyakarungu +255755023503, Deogratius Kisandu +255655025609, Exaud Mamuya  +255767160685, Kisha saa 11:52 asubuhi hiyohiyo Zitto Kabwe kupitia namba yake ya simu  +255713730256 aliwatumia shilingi 200,000/= Mkumbo Kitila +255754301908 na John Shibuda +255754465597
Tarehe 25/11/2012 saa 10:34 asubuhi, Zitto Kabwe kupitia +255713730256  aliwatumia shilingi 150,000/= wafuasi wa kundi lake,  Juliana Shonza +255756359073, Habib Mchange +255762178678, Mtela Mwampamba +255755178927, Gwakisa  Burton +255713316790, Eddo Makata +255757149043, Greyson Nyakarungu +255755023503, Deogratius Kisandu +255655025609, Adams Chagulani +255767137831, Exaud Mamuya  +255767160685, Baada ya hapo saa 10:56 asubuhi hiyohiyo Zitto Kabwe kupitia namba yake ya simu+255713730256  aliwatumia shilingi 200,000/= Mkumbo Kitila +255754301908 na John Shibuda +255754465597
Tarehe 29/11/2012 saa 12:12 mchana, Zitto Kabwe kupitia  +255713730256 aliwatumia shilingi 150,000/= wafuasi wa kundi lake,  Juliana Shonza +255756359073, Habib Mchange +255762178678, Mtela Mwampamba +255755178927, Gwakisa  Burton +255713316790, Eddo Makata +255757149043, Greyson Nyakarungu +255755023503, Deogratius Kisandu +255655025609, Adams Chagulani +255767137831, Exaud Mamuya  +255767160685, Baada ya hapo saa 12:32 mchana huohuo Zitto Kabwe kupitia namba yake ya simu+255713730256  aliwatumia shilingi 200,000/= Mkumbo Kitila +255754301908 na John Shibuda +255754465597
Kundi hili lilikuwa na mipango mingi sana, lakini lengo/shabaha/dhamira ilikuwa ni moja tu nayo ni kukidhohofisha Chadema kwa manufaa ya ccm. Uthibitisho wa lengo la kundi hili unabainishwa katika mawasiliano ya simu kati ya Zitto na wanakikundi hicho,  katika ujumbe wa maandishi (sms)  aliousambaza kwa wanakikundi hiki Zitto anasisitiza umakini ili wasije kujulikana na Chama, vilevile anawasisitiza kukisajili kikundi hiki ikiwa ni pamoja na kufungua akaunti ya benki ya kikundi hiki,
Ujumbe mwingine aliousambaza tarehe 30/11/2012 saa 08:21 kwa wafuasi wa kundi hili kupitia namba +255713730256,  unasema, “Ni lazima tukidhibiti hiki kibabu vile vile lazima tumng’oe Mbowe, Tunadanganyana tu kuwa chadema itaingia ikulu, kwanza simamieni harakati za kushinikiza kadi ya kibabu irudishwe ccm”.
Timu ya kijasusi imejiridhidha kuwa Ben Saanane alikuwa kwenye kundi hilo kwa kazi maalumu na ameisaidia sana timu hii ya ujasusi kupata habari muhimu za  ndani za kundi hilo la uasi lililokuwa limejipanga kwa ustadi likitumia mbinu za kuwagombanisha viongozi wa juu wa chama hasa likilenga Mwenyekiti na Katibu mkuu, huku juhudi za kumkwamisha mwenyekiti wa BAVICHA nazo zikipamba moto na kusukwa kwa ustadi mkubwa, Kikundi hiki hakikuishia hapo tu kwani kilianzisha mradi wa kuwatukana viongozi wa Chadema na familia zao, kuanzisha tuhuma za uongo na kuzisambaza kwenye mitandao ya kijamii. Lilianzisha mradi wa kuhubiri udini, ukanda na ukabila ndani ya chama kwa kutumia vyombo vya habari na mitandao ya kijamii. Likaanzisha tena harakati za kumpindua mwenyekiti kupitia kifupi cha jina PM7 (Pindua Mbowe 7) nk.

MAPENDEKEZO YA HATUA ZA KUCHUKUA
Baada ya kujiridhisha kuwa Zitto Zuber Kabwe Mbunge wa Chadema na Naibu Katibu Mkuu wa Chadema, ameasi Chama na ameunda kundi ndani ya chama linaloendesha vuguvugu la mapinduzi kwa viongozi halali wa chama kwa ufadhiri wa chama tawala ccm, ikiwa ni kinyume cha katiba na itifaki za chama,  Timu ya ujasusi inapendekeza yafuatayo:
Chama kijiridhishe bila ya kuacha chembe ya mashaka kutoka kwa wahusika wa kikundi hiki ambao ni Zitto na wenzake, Ikiwa watakiri kuhusika, Chama kiwaamuru wawaombe radhi wanachama.
Naibu Katibu mkuu ndugu Zitto Kabwe na Makamu Mwenyekiti wa BAVICHA ndugu Julina Shonza wapime wenyewe kama wanastahili kuendelea na nafasi zao za uongozi ndani ya Chama.
Ikiwa Chama kitaamua kuunda tume ya uchunguzi wa haya, wahusika wote hasa wenye vyeo kama Zitto Kabwe na Juliana Shonza wawekwe pembeni na shughuli za Chama ili kupisha uchunguzi huru.
Chama kiwavue uanachama Zitto Kabwe na kundi lake lote bila kusita, hii inatokana na mikakati ya kukiangamiza chama inayoendelea ndani ya CCM kwa ushirikiano wa Zitto Kabwe na viongozi waandamizi wa ccm.
Kuelekea 2015, Idara ya ujasusi ya chama iongezewe nguvu na mafunzo, ikiwezekana kiundwe kikosi maalumu nje ya timu ya kijasusi iliyopo sasa na kipewe mafunzo na vitendea kazi vya kutosha kwaajili ya ulinzi wa chama na viongozi wake.
Chama kianzishe utaratibu wa semina au mafunzo ya kipindi kifupi na kati kwa makada wake jinsi ya utumiaji wa mitandao ya kijamii.
Kiundwe kitengo cha propaganda za kisiasa chenye watu weledi wa mambo na masuala mbalimbali na kipewe uwezo ili kukabiliana na propanda za chama tawala na vyama vingine.
Chama kizidi kuchukuahatua stahiki za kimaamuzi dhidi ya viongozi au wanachama wanao dhoofisha harakati za mabadiliko kuelekea 2015 na baada ya 2015

Mwisho tunawashukuru baadhi ya maafisa wa kijasusi wa mjini Berlin Ujerumani waliosaidia kupata baadhi ya taarifa muhimu kutoka Ujerumani.

CHANZO CHA HABARI HII NI www.jamiiforums.com
  
 Zitto alitolea ufafanuzi tuhuma hizi.

No comments:

Post a Comment