Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Saturday, 18 July 2015

KOMBE LA KAGAME: GOR MAHIA NDIO WABABE WA AFRIKA MASHARIKI WENYE MAFANIKIO ZAIDI AFRIKA

 Gor Mahia ikimenyana na watani wao wa jadi AFC Leopards katika moja ya mechi za Ligi ya Kenya miaka ya 1980. 
Mashabiki wa Gor Mahia wako kila mahali dunia kwa sasa.


Na Daniel Mbega wa www.brotherdanny.com

HAPANA shaka yoyote kwamba Gor Mahia ndiyo timu pekee ya Afrika Mashariki ambayo imepata mafanikio makubwa katika mashindano ya Afrika baada ya kutwaa Kombe la Washindi Afrika mwaka 1987, ambalo sasa limefutwa.
Mtandao wa www.brotherdanny.com unaendelea kuwaletea uchambuzi wa kihistoria katika mashindano haya ambayo mwaka 2015 yanafanyika jijini Dar es Salaam.
Katika mashindano ya Kombe la Kagame, timu hiyo inashika nafasi ya nane kwa kushinda mechi 24 kati ya 54 ilizocheza, kutoka sare 15 na kupoteza 16, lakini ikifunga jumla ya mabao 75 na kufungwa 49.
Inashiriki mara ya 14, lakini katika safari 13 ilizoshiriki imetwaa mara tatu ubingwa katika miaka ya 1980, 1981 na 1985, imeshika nafasi ya pili mara moja mwaka 1984 na kurudia nusu fainali mara nne mwaka 1975, 1982, 1991 na 1996. Miaka mingine iliposhiriki ni 1977, 1983, 1986, 1994, na 2014.
Mabingwa hao wa Kenya hawajapoteza mechi msimu huu huku wakionesha dalili za kutangaza ubingwa mapema kabisa.
Timu hiyo inajivunia hazina ya wachezaji wenye vipaji wakiwemo Khalid Aucho, George Odhiambo, Micheal Olunga, Mnyarwanda Meddie Kagere na walinda mlango Boniface Oluoch na nahodha Jerim Onyango. Pia yumo mlinzi wa Uganda Cranes Godfrey Walusimbi. Inanolewa na Mskochi Frank Nutall anayesaidiwa na mzalendo kipa wa zamani Mathew Ottamax.
Wachezaji wengine ni Kevin Oluoch, Musa Mohammed, Collins Okoth, Ronald Otieno, Timothy Otieno, Ali Abondo, Abouba Sibomana (Uganda), Abdoul Nizigiyimana (Rwanda), Dirkir Glay (Liberia), Jerry Santos, Martin Werunga, Charles Bruno, Erick Ochieng, Haron Shakava, Ernest Wendo, Khalid Aucho (Uganda), Boniface Oluoch, Israel Emuge (Uganda), Simon Pierre (Cameroon), David Juma, Bernard Odhiambo na Innocent Wafula.
Ipo katika Kundi A pamoja na Yanga, Al Khartoum ya Sudan, KMKM ya Zanzibar na Telecom ya Djibouti.

Historia yake
Gor Mahia, ambayo nchini Kenya inafahamika kwa majina mengi ya utani ya Kiluo kama K'Ogalo (Nyumba ya Ogalo), Mayienga (Tetemeko), Sirkal (Serikali) na Taya (Mwanga) ilianzishwa rasmi Februari 17, 1968. Inautumia Uwanja wa City wenye uwezo wa kuingiza wazamaji 15,000 pale Nairobi.
Klabu hiyo ambayo ina upinzani wa jadi (wa kikabila) na Afc Leopards (zamani ikiitwa Abaluhya FC) imepata kutwaa ubingwa wa Kenya mara 14, ikiipiku AFC Leopards kwa msimu mmoja. Pia imetwaa Kombe la Rais la KFF mara 10.
Ndiyo timu pekee kutoka ukanda wa Cecafa kutwaa taji la klabu za Afrika mpaka sasa, baada ya kushinda Kombe la Washindi Afrika mwaka 1987 ikisaidiwa sana na mabao ya vichwa vya Peter Dawo.
Kuanzishwa kwa klabu hiyo kulitokana na muungano wa klabu za Wajaluo – Luo Union na Luo Sports Club (Luo Stars) – na ilitwaa ubingwa katika msimu wake wa kwanza tu kuingia 1968.
Baadhi ya waasisi wake ni Tom Mboya na Jaramogi Oginga Odinga. Klabu hiyo ilipewa jina kumuenzi mganga wa jadi maarufu kutoka Homa Bay katika nadharia za Kiluo, ambaye jina lake la utani lilikuwa Gor Mahia ("mahia" ni neno la Kiluo ambalo maana yake ni "miujiza") kwa sababu alikuwa maarufu kwa kufanya miujiza. Jina maarufu la utani la klabu hiyo, K'Ogalo, pia linatokana na mganga wa jadi, ambaye jina lake halisi lilikuwa Gor Wuod Ogada nyakwar Ogalo (Gor mwana wa Ogada mjukuu wa Ogalo), na alikuwa akifahamika kama Gor Makogalo, au Gor K'Ogalo kwa kifupi, likimaanisha "Gor kutoka ukoo wa Ogalo".
Hata hivyo, klabu hiyo ilikuwa imeanzishwa mapema zaidi katika miaka ya 1910, na ikashiriki katika mashindano ya mitaani huko Kenya Magharibi. Makundi mbalimbali yalitumia jina la Gor Mahia kwa nyakati tofauti.
Mwaka 1976, Gor Mahia ilitwaa ubingwa bila kupoteza hata mchezo mmoja ikijivunia ‘uchawi’ wa kocha mchezaji Allan Thigo. Alikuwa anasaidiwa na nyota kama Festus Nyakota, James Ogolla na wachezaji wapya Jerry Imbo aliyesajiliwa kutoka Black Mamba na mshambuliaji mashuhuri Maurice Ochieng kutoka Polisi Kenya. Kipa George Ayuka alikuwa hafungiki msimu mzima. Maurice Ochieng alimaliza msimu akiwa amepachika mabao 20, mbele ya mkongwe William "Chege" Ouma aliyepachika mabao 16.
Kikosi cha mwaka 1976 ni moja ya vikosi imara ambacho timu hiyo imepata kuwa navyo. Kilihusisha wachezaji nyota kama Masanta Osoro, Paul "Cobra" Oduwa, Festus Nyakota, Duncan Aluko na Duncan Migan, wote walikuwa wakiichezea timu ya taifa. Waziri wa sasa wa Barabara wa Kenya, Chris Obure, pia aliichezea Gor katika miaka ya 1970.
Gor Mahia iliichapa AFC Leopards bao 1-0 kutwaa ubingwa wa ligi mwaka 1983 na mwishoni mwa mechi hiyo, Rais Daniel arap Moi akakabidhi taji kwa nahodha Peter Otieno Bassanga.
Gor Mahia ilitwaa kombe jipya la Dhahabu la Moi mwaka 1986 kwa kuichapa Bandari 1-0 kwenye fainali. Bao la dakika za majeruhi la Hezborn Omollo liliipatia ubingwa kwenye Uwanja wa Nyayo. Kikosi imara cha Bandari kikinolewa na Mohammed Kheri kilikuwa kinashiriki kwenye Ligi ya Kanda ya Pwani. Kwa kutwaa taji hilo Gor ikapata nafasi ya kushiriki kwenye Kombe la Washindi Afrika mwaka 1987.

Mafanikio:
Kombe la Washindi: Bingwa 1987

Ubingwa wa Cecafa: Mara 3
1980, 1981, 1985

Ubingwa wa Kenya: 14
1968, 1974, 1976, 1979, 1983, 1984, 1985, 1987, 1990, 1991, 1993, 1995, 2013, 2014

Kombe la Chalenji Kenya/Kombe la Dhahabu la Moi/Transparency Cup/President's Cup/Kombe la KFF/Kombe la FKL: 10
1976, 1981, 1983, 1986, 1987, 1988, 1992, 2008, 2011, 2012

Kombe Kubwa la Kenya (Super Cup): 3
2009, 2013, 2015

Kombe la Shirikisho la CAF: Imeshiriki mara 3
2009 – Raundi ya Awali
2012 – Raundi ya Awali
2013 – Raundi ya Kwanza

Klabu Bingwa Afrika: Imeshiriki mara 8
1969: Robo Fainali
1977: Raundi ya Pili
1980: Raundi ya Pili
1984: Ilivunjika katika Raundi ya Pili
1991: Raundi ya Kwanza
1992: Robo Fainali
1994: Raundi ya Kwanza
1996: Raundi ya Kwanza

Kombe la CAF: Imeshiriki mara 2
1993 – Robo Fainali
1998 – Raundi ya Kwanza

Kombe la Washindi: Imeshiriki mara 7
1979 - Fainali
1981 – Robo Fainali
1982 – Ilijitoa Raundi ya Kwanza
1983 – Raundi ya Awali
1987 - Mabingwa
1988 – Robo Fainali
1989 – Nusu Fainali


KUMBUKUMBU HIZI ZIMEANDALIWA NA MTANDAO WA www.brotherdanny.com. Tafadhali ukirejea weka chanzo cha habari.

No comments:

Post a Comment