Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Saturday, 18 July 2015

‘USHEMEJI’ WAMPONZA MEMBE, MAADUI ZAKE 11 WASALIMIKA

 
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa na Mbunge wa Jimbo la Mtama, Bernard Membe (kushoto) akipongezwa na Waziri Mkuu mstaafu Edward Lowassa kwa kuingia kwenye 'tano bora' mjini Dodoma hivi karibuni.

Na Daniel Mbega, Dodoma
NDOTO za kachero Bernard Kamilius Membe (62) za kuwa raia namba moja wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania zimekatika ghafla.
Ni sawa na kumshtua ‘teja’ wa dawa za kulevya ambaye baada ya kujidunga sindano anasinzia akiota kujenga ghorofa linaloelea angani huku yeye akiwa na mabawa, lakini anaposhtuliwa na kujikuta yuko pale pale kijiweni, humchukia kila aliyemzunguka, hususan yule aliyemwamsha.
Naam. Julai 11, 2015 Halmashauri Kuu ya Chama cha Mapinduzi imeleta mapinduzi kwa kumwengua Bernard Membe kutwa moja tu baada ya hali ya hewa mjini hapa kubadilika kufuatia kuenguliwa kwa Edward Lowassa na kusababisha kikundi cha vijana wasiozidi 100 kufanya fujo za hapa na pale.
Kuenguliwa kwa Membe, ambaye tangu mwaka 2011 alisema alikuwa akisubiri kuoteshwa ndoto ili awanie urais, kumeleta faraja kwa makundi mengi ndani ya chama hicho na pia walau kuleta utulivu hasa baada ya kusikia kwamba walioingia tatu bora ni Dk. John Pombe Magufuli aliyeongoza kwa kupata kura 290, Balozi wa Kudumu katika Umoja wa Afrika Amina Salum Ali aiyepata kura 284 na Dk. Asha-Rose Migiro aliyepata kura 280.
Membe aliburuza mkia kwenye hatua hiyo baada ya kupata kura 120 nyuma ya January Makamba aliyepata kura 124.
Lakini duru za siasa zinasema kuenguliwa kwa Membe kumekuwa faraja kwa ‘maadui zake 11’ ambao walikuwa na hofu kwamba kama angepitishwa na CCM, basi wangetafuta mahali pa kukimbilia.
Akihojiwa katika kipindi cha Dakika 45 cha runinga ya ITV mnamo Julai 16, 2012, Membe, akiongea kwa hisia na uwazi kuhusu maisha yake ya kisiasa pamoja na mvutano uliopo kati yake na mahasimu wake, alisema ana maadui 11 na kuapa kwamba mwaka 2016 ‘wangekimbilia Kenya’, pengine akijua kwamba wakati huo yeye ndiye angekuwa rais.
Maadui wa Membe, kwa mujibu wa maelezo yake, ni wale wote wanaomzushia kashfa ambapo kati ya 11, wawili ni waandishi wa habari na kwamba ipo siku angewataja kwa majina na sura zao kwani kwa wakati huo alikuwa akikusanya taarifa za kila mmoja na kutengeneza ‘dossier’ ili hatimaye awataje hadharani.
‘Kisasi’ hicho kimetajwa kwamba huenda ni sababu mojawapo ambayo iliyomuondoa kwenye kinyang’anyiro hicho kwa maelezo kwamba CCM inaona siyo vyema kuwa na kiongozi mwenye visasi.
Hata hivyo, sababu kubwa iliyobainishwa na vyanzo vya habari kutoka ndani ya duru za siasa kwenye CCM ni ‘ushemeji’ wake na Rais Jakaya Kikwete, ambao umeelezwa kuwa ndio uliochangia akaingia kwenye ‘tano bora’.
Kikundi cha vijana waliokuwa wakiimba na kudai kwamba ni wafuasi wa Lowassa, kilieleza hisia zake kuwa “Membe ameingia tano bora kwa kubebwa kwa sababu ni shemeji wa Rais Kikwete.”
Dhana ya ‘ushemeji’ inakuja kutokana na mke wa Rais, Mama Salma Kikwete, kutoka mkoani Lindi ambako ndiko anakotokea Membe na familia namba moja imekuwa karibu na Waziri huyo wa Mambo ya Nje.
Vyanzo vya ndani ya CCM, hususan Kamati ya Maadili na Usalama pamoja na Kamati Kuu, vinadokeza kwamba kulikuwepo na kutokuelewana baina ya wajumbe kuhusu Membe, ambaye hata wazee wa chama hicho walionyesha mashaka yao ya wazi.
Inaelezwa kwamba, hiyo ndiyo sababu pia ya makada watatu wa chama hicho, Dk. Emmanuel Nchimbi, Adam Kimbisa na Sophia Simba kutangaza kujitoa kwenye Kamati Kuu wakipinga namna mambo yalivyoendeshwa.
Hata hivyo, taarifa zinasema makada hao watatu Jumamosi walifuatwa na viongozi wa juu wa Umoja wa Vijana (UVCCM) kuombwa wafute kauli yao na warejee kwa wenzao ili wakijenge chama.
Kelele zilizokuwa zikiendelea nje ya ukumbi Jumamosi kutoka kwa vijana wanaomuunga mkono Lowassa, kwamba wanakitaka chama chao au watarudisha kadi za chama na kuelekea upande mwingine, nazo zinatajwa kuwa ni sababu ya kuenguliwa kwa Membe kwa hali haikuwa nzuri, si hapa Dodoma tu, bali hata katika miji mingine.
Tangu mwaka 2014, ilielezwa kupitia mitandao ya kijamii na baadhi ya vyombo vya habari kwamba familia ya Rais Jakaya Kikwete (hasa Mama Salma na Ridhiwani) ndiyo ilikuwa nyuma ya kampeni za Membe na kwamba haikushangaza wakati jina lake lilipoingia kwenye tano bora.
Wengine waliokuwemo kwenye timu hiyo ni Lazaro Nyalandu, ambaye pamoja na kujitokeza kugombea alikuwa kama anayeweka ‘foleni’ tu ili kupunguza kura kwa baadhi ya watu.
Wamo pia Paul Makonda na Jack Steven Gotham anayedaiwa kuwa ndiye aliyekuwa akiratibu zoezi la kukusanya fedha
Miaka mitatu nyuma Membe aliripotiwa na gazeti la RAI kwamba alikuwa akilitumia vibaya jina la Rais kwa kitendo chake cha kupita katika nchi za Kiarabu kuomba fedha na magari, hususan Muungano wa Falme za Kiarabu (UAE).
Ilielezwa kwamba, Membe alikuwa akitumia wadhifa wake serikalini na uhusiano kati ya watawala wa UAE na Tanzania kufanikisha azma hiyo.
Familia ya kifalme ya nchi hiyo chini ya Sheikh Mohammed bin Al Maktoum, mbali na mahusiano ya kidiplomasia, wamekuwa wawekezaji katika sekta ya uwindaji wa kitalii nchini kwa zaidi ya miongo minne.
Pamoja na Membe kuzikanusha tuhuma hizo na nyingine nyingi, lakini bado kuna watu wanaamini hiyo ni kashfa ambayo haikuwa na nafasi ya kumpa madaraka makubwa.


 MAKALA HII ILICHAPISHWA KWA MARA YA KWANZA JULAI 13, 2015 KATIKA GAZETI LA WAJIBIKA.

No comments:

Post a Comment