Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Sunday, 17 May 2015

MATOKEO YA AJABU: SIMBA ILIPOITANDIKA AL AHLY MWANZA 1985

Baadhi ya wachezaji hawa wa Simba walikuwemo kwenye kikosi cha mwaka 1985 kilichoihenyesha National Al Ahly kule Mwanza.

NA DANIEL MBEGA
KLABU ya Simba ina rekodi nzuri katika michuano ya kimataifa. Hilo halina ubishi. Na linapokuja suala la kupambana na klabu za Afrika Kaskazini (The Maghreb) Simba ndio wameweza kuzionyesha ubabe, japo kwa kiasi fulani, tofauti na klabu nyingine za Tanzania.
Mwaka 1985 Simba ndio walikuwa wanaiwakilisha Tanzania kwenye michuano ya Kombe la Washindi Afrika. Katika mchezo wa kwanza wa raundi ya kwanza kwenye uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza, Simba iliitandika Eritrea SF ya Asmara, Ethiopia (wakati huo kabla Eritrea haijajitenga kutoka Ethiopia) kwa magoli 5-0. Mchezo huo ulifanyika Machi 2.
Ziliporudiana wiki mbili baadaye mjini Addis Ababa, yaani Machi 16, Simba ilifungwa goli 1-0. Hata hivyo, ilisonga mbele kwa ushindi wa magoli 5-1. Sasa ilikuwa na kibarua kigumu cha kupambana na mabingwa watetezi wa kombe hilo, National Al Ahly ya Misri katika hatua ya raundi ya pili.
Mchezo wao wa kwanza ulifanyika kwenye uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza Aprili 27, na Simba ikaushangaza ulimwengu kwa kuifunga National 2-1. Simba siku hiyo iliwakilishwa na Moses Mkandawire, Kihwelu Mussa, Athumani Maulid, Shaaban Mussa, Thobias Nkoma, Ramadhani Lenny, Sunday Juma, Mtemi Ramadhani/Ezekiel Greyson 'Juju Man', Malota Soma, Zamoyoni Mogella na Douglas Muhani/Twaha Hamidu.                      
National Al Ahly iliwakilishwa na Ekramy El-Shahat, Midhat Ramadhani, Mohamed Saleh, Hamis Abu-Radi, Rabii Yasin, Magdi Abdulghani, Said Mohamed, Mokhtar Mokhtar, Mahmoud El-Khatib, Alaah Mahboub na Mohamed Amer.
Mtangazaji wa Redio ya Misri siku hiyo alisikika akipayuka kwa Kiarabu muda mfupi kabla ya dakika ya 85 ya mchezo; "Wahed Wahed, Al Ahly Wahed, Simba Wahed....aaah, Sheitwan, gooo!!", yaani "Moja moja, Al Ahly (National) moja, Simba moja....aaaah, Shetani, gooo!!"
Lilikuwa ni goli la pili la Simba ambalo mtangazaji huyo alikuwa akililaani vikali. Baada ya matokeo hayo, wachezaji na viongozi wa National walisikika wakisema  "Cairo Four", yaani Simba ingefungwa magoli manne huko Cairo katika mchezo wa marudiano.
Katika mchezo huo, Simba ikiwa imefungwa dakika tano kabla ya mapumziko, iliweza kusawazisha katika dakika ya 44 na kujipatia goli la ushindi dakika tano kabla ya mpira kumalizika. Zamoyoni Mogella ndiye aliyeisawazishia Simba kunako dakika hiyo ya 44.
Baada ya kupasiana kati ya Kihwelu Mussa, Ramadhani Lenny na Malota Soma, mpira ulimfikia Zamoyoni Mogella ambaye aliachia shuti kati katikati ya mabeki wa National. Mpira ulimwamba wa juu na kisha kurejea ardhini kwa nyuzi 90. Lilikuwa goli safi sana la mwaka 1985.
Goli la National lililopatikana katika dakika ya 40 lilikuwa zuri na kiufundi. Baada ya pasi 14, Mahmoud El-Khatib aliachia kiki ambayo ilikwenda moja kwa moja wavuni huku Moses Mkandawire akiwa amelala upande mwingine.
Goli la ushindi kwa Simba lilifungwa na nahodha wake, Mtemi Ramadhani katika dakika ya 85 kutokana na juhudi kubwa za wachezaji wa Simba, ambao pamoja na kucheza mpira wa kiwango cha chini ukilinganisha na wenzao National walikuwa wamedhamiria kweli kuibuka na ushindi siku hiyo.
Katika mchezo wa marudiano uliofanyika uwanja wa Gamal Abdel Nasser mjini Cairo Mei 11, 1985 mbele ya mashabiki 80,000, Simba ilifungwa magoli 2-0 na National na hivyo kutolewa kwa jumla ya magoli 3-2. Goli la kwanza la National lilifungwa na Mahmoud El-Khatib ‘Bibo’ dakika ya 37 na lile la pili lilifungwa na Zakaria Nassir dakika ya 59.
Kwenye mechi ya Cairo, timu ziliwakilishwa hivi: Al Ahly: Ekram El-Shabat, Mohammed Hashis, Rabiya Yassin, Amdi Aburabi, Magdi Abdelghani/Mohammed Ameir, Zakaria Nassir, Mahmoud el Khatib 'Bibo, Mustafa Abdul, Alaa Mayhobe, Taher Abuzaid.
Simba: Moses Mkandawile, Kihwelu Mussa, Athumani Maulid 'Big Man'/Daudi Salum ‘Bruce Lee’, Thobias Nkoma, Talib Hilal, Ramadhan Lenny, Ibrahim Marekano/Abdallah Mwinyimkuu, Mtemi Ramadhan, Zamoyoni Mogella, Malota Soma, Sunday Juma.
Siku hiyo mwamuzi alikuwa K. Teeluckdhaamy aliyesaidiwa na K. Mootiem na D. Desscan.
Tukirudi katika mchezo wa kwanza mjini Mwanza, Simba siku hiyo iliweka rekodi ya kuwa timu ya pili ya Afrika (Nje ya Misri) kuifunga National katika kipindi cha kati ya mwaka 1982 hadi 1985. Tokea mwaka 1982, ni mwaka 1983 tu wakati National ilipofungwa na Asante Kotoko ya Ghana goli 1-0 mjini Kumasi katika mchezo wa fainali ya Klabu Bingwa Afrika. Kotoko ilitwaa ubingwa huo kwa goli lililofungwa na Opoku N'ti, ambaye mwaka huo alikuwa Mwanasoka Bora wa Afrika.
Vinginevyo, tokea mwaka 1982 mpaka hapo Aprili 27, 1985, National ilikuwa haijafungwa tena katika mashindano ya Afrika. Kawaida ya timu hiyo ilikuwa ni kutoka sare ama kushinda ugenini na kushindilia magoli mengi inapocheza nyumbani.
Miongoni mwa timu zilizokuwa zinaijua vizuri National ni Yanga, ambayo ilichapwa magoli 5-0 mjini Cairo na kutoka sare ya goli 1-1 Dar es Salaam mwaka 1982 katika michuano ya Klabu Bingwa Afrika.
Kadhalika katika mashindano hayo mwaka huo Nkana Red Devils ya Zambia ilifungwa 2-0 huko Cairo baada ya kutoka sare ya bila kufungana mjini Lusaka, na Asante Kotoko ilifungwa 1-0 huko Kumasi baada ya kutoka sare ya bila kufungana mjini Cairo. Goli hilo liliipa National ubingwa wa Klabu Afrika mwaka 1982, ambalo lilifungwa na Mahmoud El-Khatib, ambaye mwaka huo alikuwa Mwanasoka Bora wa Afrika (Mwaka 1983 alikuwa wa pili). Katika fainali ya Kombe la Washindi Afrika mwaka 1984, National iliifunga Canon Yaounde 1-0 huko huko Cameroon na 2-0 mjini Cairo.

NB: Tembelea www.brotherdanny.com kila siku kwa habari mbalimbali zilizotafitiwa kwa kina.

No comments:

Post a Comment