Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Monday 24 November 2014

TAARIFA YA HARAKA KWA VYOMBO VYA HABARI KUHUSU MGOGORO WA ARDHI LOLIONDO


Taarifa ya Haraka kwa Vyombo vya Habari Kuhusu Mgogoro wa Ardhi Loliondo

Sisi Viongozi wa Mila, Kisiasa, Wawakilishi wa Wanawake tumesikitishwa sana na Taarifa ya uongo aliyoitoa Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe. Lazaro Nyalandu juu ya ukweli wa Mgogoro wa Loliondo. Ifuatayo  ni ufafanuzi wa hali halisi kinyume na Waziri alivyodanganya Dunia kupitia BBC tarehe 19/11/2014 na Gazeti la leo la Mwananchi
  1. Kwamba eneo la Loliondo halina Wamaasai 40,000 watakaoadhirika endapo Serikali itatoa tamko Wakati  wowote sasa:
Jibu: Idadi ya wakazi katika eneo la km za mraba 1,500 ambavyo ni vijiji vya Ololosokwan, Soitsambu, Oloipiri, Arash, Maaloni, Olorien/Magaiduru, Piyaya na Malambo ambavyo vina jumla ya wakaazi 57,532. Kwa mujibu wa sensa ya Taifa ya watu na Makazi ya 2012 kama ilivyo kwenye jedwali hapa chini.
SN
Kata
Idadi ya watu
1
Arash
7,841
2
Olosoito/Maaloni
4,353
3
Oloipiri
4,114
4
Soitsambu
10,956
5
Ololosokwan
6,557
6
Piyaya
5,303
7
Malambo
8,923
8
Olorien- Magaiduru
9,485
9
Orgosorok
1,521
10
Engusero Sambu
12, 268

Jumla
71, 321

Vijiji viwili (Engusero sambu na Orgosorok) venye idadi ya watu 13,789 hawana makazi katika eneo la mgogoro lakini ni watumiaji wa eneo hilo la malisho.Hivyo tunathibitisha kuwa watu watakaoathirika eneo hili likichukuliwa ni 71,321.Hivyo Waziri kusema eneo hilo halina watu 40,000 ni uongo mtupu.
  1. Kwamba Serikali ya Tanzania haijawahi kuwa na mpango wa kuwaondoa Wamaasai katika eneo la Loliondo:
1992: Serikali ilitoa ardhi ya vijiji vya Tarafa za Loliondo na Sale kwa Mfalme wa UAE bila RIDHAA ya wananchi na kusababisha mgogoro unaoendelea mpaka sasa. Kumweka mwekezaji katika ardhi ya jamii bila ridhaa ilikua ni mpango wa muda mrefu wa kupora ardhi.
2008: Mgogoro huu umechukua sura tofauti baada ya kampuni kuweka mikakati ya kuchukua ardhi yetu kwa ajili ya uwindaji na kutengeneza mikataba iliyoridhiwa na viongozi na sio wananchi.
2009: Serikali ilitumia mikataba iliyoridhiwa na baadhi ya viongozi wa vijiji kufanya opersheni ya kijeshi ambayo iliharibu rasilimali, ilichoma makazi na kusababisha mtoto moja katika kijiji cha Arash kupotea mpaka leo. Kijana Ngodidio Rotiken alijeruhiwa kwa bomu na kupoteza jicho na madhara mengine mengi.
2010: Serikali ilitengeneza RASIMU ya mpango wa Matumizi wa Ardhi ya  Wilaya kwa ufadhili wa OBC wa shilingi 157,000,000. Mpango huo ulitengeneza rasimu ya ramani ya kutenga eneo la Kilomita za Mraba 1,500 kutoka kwenye ardhi ya vijiji. Mpango ulipingwa vikali na kukataliwa na baraza la madiwani la Halmashauri ya Wilaya Ngorongoro na jamii kwa ujumla kwa sababu ya dhana nzima ya kutenga ardhi ya vijiji bila ushiriki wa wananchi.
2011/12: Serikali kupitia kamishina wa ardhi iliagiza vijiji vya Ololosokwan na Engaresero kurudisha vyeti vya ardhi ya vijiji kwa madai kuwa vina migogoro. Madai hayo yalithibitishwa kuwa ya uongo na yenye hila ya kupora ardhi ya vijiji.
2013: Serikali kupitia Mhe. Waziri wa Maliasili na Utalii (Mhe. Khamis Kaghasheki) ilitangaza RASMI kutenga eneo la Kilomita za mraba 1,500 ya ardhi ya vijiji kuwa Pori Tengefu la Loliondo. Jambo hili lilizua taharuki kubwa ndani na nje ya Nchi na kutishia usalama kwenye jamii ya Wafugaji na hatimaye kumlazimu Waziri Mkuu kuingilia kati.
2014: Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Lazaro Nyalandu (Mb) alizuru Loliondo mara mbili kwa nia ya kuhamasisha na kushawishi madiwani na wenyeviti wa vijiji kukubali pendekezo la Serikali/OBC kutoa FIDIA ya shilingi Bilioni moja kwa vijiji endapo watakubali kuachia eneo la kilomita za mraba 1,500. Pendekezo lake halijakubaliwa hata na viongozi wachache aliyokutana nao.
Tarehe 19/11/2014 wakati wa mahojiano na mtangazaji wa BBC, Mhe. Lazaro Nyalandu alisema alikwenda Loliondo Kuhamashisha Mpango wa Matumizi Bora ya Ardhi:
Jibu: Waziri kisheria, hana mamlaka juu ya kupanga matumizi ya Ardhi ya vijiji na wala haijawahi kuzungumziwa katika mikutano ya Waziri na Baadhi ya Madiwani na wenyeviti alipokuja Loliondo. Mipango ya Matumizi bora ya ardhi za vijiji inaratibiwa na Wizara ya Ardhi na Makazi na sio Wizara ya Maliasili na Utalii…….. Ni Wizara hiyo hiyo inayoongozwa na Nyalandu iliyopinga upimaji wa vijiji uliokuwa unatekelezwa na Wizara ya Ardhi na Makazi mwaka 2013 kwa kuwarudisha ndani ya masaa 24 timu ya wataalamu wakiongozwa na mpima wa Wizara ya Ardhi Ndg. Isaa Marwa waliokuwa wameanza zoezi la upimaji. 
Katika Mahojiano na BBC tarehe 19/11/2014, Waziri Nyalandu alisema sio Wamaasai tu wanaishi katika eneo la kilomita za mraba 1500:
Jibu: Wakazi wa eneo hili ni wafugaji wa jamii ya wamaasai ambao ni zaidi ya 40,000
Katika gazeti la Mwananchi la tarehe 21/11/2014 Mhe Nyalandu alisema “yaani tunapanga kutumia askari kuwaondoa wananchi kwenye maboma yao na kuyachoma moto…..Huu ni uongo, hakuna mpango kama huo”
Jibu: Kwa kuwa Mhe Waziri Lazaro Nyalandu yaelekea hana kumbukumbu ya matukio ya Loliondo tunamrejesha kwenye tukio la mwaka 2009 lililoratibiwa na Wizara ya Maliasili na Utalii kutumia jeshi la Polisi (FFU) kuteketeza kwa moto maboma ya wafugaji ya jamii ya Kimaasai zaidi ya 300 katika eneo la Loliondo.  

  1.  Baada ya mkanganyiko huu wa Mhe Nyalandu, sisi viongozi wa Kisiasa, Kimila na Wawakilishi wa wanawake tumedhamiria kumwona tena Mhe. Waziri Mkuu ili kupata uhakika wa mpango huu wa Nyalandu, kwani hatuna imani tena na Wizara ya Maliasili na Utalii. Tumeumizwa na kusikitishwa sana na kitendo cha kushindwa kumwona japo tulipata uhakika wa muda wake wa kutuona (appointment) tarehe 19/11/14.
  2. Katika sakata hili tunatoa tena kwa mara nyingine ushauri ufuatao kwa Serikali ili kufikia suluhu ya kudumu kwa mgogoro huu:
                  I.        Waziri Mkuu kutoa agizo lenye masharti ya muda kwa Wazira ya Maliasili na Utalii kufuta kwa Maandishi Tamko lake kwa vyombo vya habari la tarehe 21, Machi 2013 kama ulivyotuahidi Sept mwaka jana.
                II.        Serikali kupitia Wizara ya Maliasili na Utalii kutengua/kufuta hadhi ya Pori Tengefu katika vijiji vya Loliondo kwa mujibu wa sheria mpya ya Wanyamapori ya mwaka 2009 na kuheshimu miliki halali za kisheria kwa ardhi yetu na mfumo wa maisha yetu usioharibu mazingira.
               III.        Waziri Mkuu kutoa TAMKO kwa umma wa Watanzania na Dunia nzima kwa maandishi kuhusu Ahadi yake ya tarehe 23/9/13 kwetu kwamba Serikali imeachana na mpango wa kupora ardhi ya Vijiji vyetu. Aidha tunamwomba Waziri Mkuu kukemea kwa uzito usumbufu huu tuanoupata watu wa Loliondo toka kwa Wizara ya Maliasili na Utalii unaojirudia kila Wakati.
              IV.        Tunaishauri Serikali kufuta uwindaji katika Ardhi yetu, kwani hauhifadhi Wanyamapori wala sio rafiki na mazingira, ufugaji na utalii wa picha. Uwindaji katika eneo la Loliondo ni mpango wa kuwamaliza wanyama katika ikolojia ya Serenegeti, Ngorongoro na Maasai Mara. Kuendelea kuruhusu uwindaji katika eneo hili, mgogoro utaendelea na kusababisha madhara endelevu kwa uhifadhi wa wanayamapori, maisha yetu na ustawi wetu.
               V.        Tunamwomba Mhe. Waziri Mkuu kutoa maelekezo ya haraka kwa Wizara ya Ardhi na Makazi iendelea na zoezi la upimaji wa vijiji lililohairishwa na Wizara ya Maliasili na Utalii mwezi August, 2013 ili kuharakisha zoezi la kuandaa mipango ya Matumizi ya bora za Ardhi.
              VI.        Tunamwomba Mhe. Waziri Mkuu kutekeleza haya kwa muda mfupi uwezekanavyo kwani tumekuheshimu kwa kuvuta subira kwa mwaka mzima kama ulivyotuelekeza kwenye Barua yako ya Mwezi Mei mwaka jana “tuwe watulivu na wavumilivu wakati ukishughulikia kilio chetu”. Kama utashindwa kutoa maelekezo hayo ya kutimiza ahadi yako kwetu, basi hatuna budi kuhamasisha dunia kupitia vyombo vya habari na kufika Dodoma ofisini kwako kwa maelfu ili utueleze hatma ya Ardhi yetu na maisha yetu. Japo tunaamini katika utatuzi wa migogoro kwa njia ya amani, hata hivyo uvumilivu umetuishia na kamwe ardhi yetu haitaporwa kwa maslahi ya kampuni ya OBC.
Imeandaliwa na:
1.Elias Ngorisa – Mwenyekiti Wa Halmashauri
2. Ibraham Sakai- Mwenyekiti wa CCM Wilaya.
3. Daniel Ngoitiko- Diwani
4. Mathew Siloma- Diwani
5. Tina Timan- Diwani
6. John Kulinja- Kiongozi wa Mila.
7. Mathew Timan- Kiongozi wa Mila
8. Loserian Minis- Mwakilishi wa Wenyeviti wa Vijiji.
9. Kooya Timan – Mwakilishi wa Wanawake
10. Manyara Karia- Mwakilishi wa Wanawake
Imetolewa leo tarehe 21/11/2014, Arusha na Wawakilishi wa Jamii toka Tarafa za Loliondo na Sale.

No comments:

Post a Comment