Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Sunday, 7 June 2015

UJUMBE KATIKA MUZIKI: ANGALIA USIMCHEZEE CHATU!

 
Hassan Rehani Bitchuka

Na Daniel Mbega
NI Jumapili nyingine wapendwa wasomaji wa blogu hii ambapo wengi wetu tunapumzika majumbani tukijiandaa kwa siku ya kesho (wale wa ofisini) kwenda kulijenga taifa.

Karibuni tukumbushane mambo mbalimbali ya kijamii yanayopatikana kwenye tungo za wanamuziki mbalimbali. Ni tungo maridhawa ambazo pamoja na kuimbwa miaka mingi iliyopita, lakini bado ujumbe wake ungali na mantiki kwa jamii yetu.
Leo nakiangalia kibao cha Chatu Mkali, cha bendi ya International Orchestra Safari Sound (IOSS) ukiwa ni utunzi wake Hassan Rehani Bitchuka ambaye aliimba akishirikiana na Muhidin Maalim Gurumo, Skassy Kasambula, Ali Akida, Dingituka Molay, Tchibanda Sony, Benno Villa Anthony, Kabeya Badu, Numbi Kileba, Mobali Jumbe, na Deus Mugunda.
Solo katika wimbo huu ilipigwa na ‘String Master’ Joseph Mulenga, rhythm alipiga Ally Makunguru na gitaa la bass likaungurumishwa na Charles John 'Ngosha', Emanuel Zagallo alipiga drums, Mbaraka Rajab alipiga tumba, Ngoie Mubenga na Ibrahim Mwinchande kwenye trumpet, Saleh Maluu, Kimeza Abdalah na Majengo Suleiman kwenye Sax (mnaweza kunisahihisha kama mahali nimesahau).
Ngoja niwarejeshe nyuma kidogo. Hii ilikuwa ni awamu ya pili ya bendi hii ambayo ilikuja kuimarishwa na Gurumo na Bitchuka pamoja na wapiga ala kama Joseph Mulenga na Charles John ‘Ngosha’ waliotokea DDC Mlimani Park Orchestra (Sikinde) mwaka 1984.
Mmiliki wa bendi hiyo, Hugo Kisima, aliamua kuwachukua wanamuziki hao kuimarisha bendi yake ambayo awali ilikuwa chini ya Maestro Freddie Ndala Kasheba aliyetamba na mtindo wa Dukuduku na kuleta upinzani dhidi ya bendi ya Marquiz du Zaire.
Gurumo alipotua hapo akaanzisha mtindo wa Ndekule na sasa ushindani ukawa baina ya Sikinde na Ndekule.
Hata utunzi wa kibao cha Chatu Mkali kinatajwa kwamba yalikuwa majibu kwa Sikinde ambao walikuwa wametoa kibao cha M.V. Mapenzi 2 kikimponda Gurumo kwa kuitosa Sikinde ‘Meli ya Wapendanao’.
Pamoja na vijembe hivyo, lakini ujumbe huu bado ungali na maana kwa jamii yetu ya sasa.
Wapo wanajamii ambao wana kawaida ya ‘kuwachokoza’ wenzao, kuwabeza na kuwafanyia mambo mengi mabaya hasa wanapowaona wakimya.
Hivi inakuwaje ukamfanyia hiyana ndugu ama jamaa yako ambaye mmeazimia kwa pamoja kufanya jambo. Mnakuwa wote katika dhiki na taabu wakati mnalianzisha, wakati mwingine unatumia hata rasilimali zako kufanikisha jambo hilo ukiamini kwamba ni lenu pamoja, lakini mara mambo yanaponyooka ndugu huyu anakudhulumu na kukutelekeza?
Semeni ukweli ndugu zangu, kama jambo hili halijakutokea wewe, basi limetokea ndugu, jamaa ama hata jirani yako.
Wanaofanya hivi wanadharau kwamba, “Aaah, hata nikimfanyia hivi, atanifanya nini?” Wanasahau kwamba, ndugu hawa nao wana mioyo ya nyama na wana nyongo. Hata kama hawataweza kulipiza, lakini kamwe hawawezi kukaa kimya, wanaweza kumlilia Mungu naye akakuadhibu kwa aibu kubwa.
Wengi ambao wamewatendea unyama wenzao mwisho wao ni mbaya.
Lakini kamwe hupaswi kuwatendea wenzio ubaya, hasa wale wakimya. Bora hata mtu anayezungumza ama kujibu mapigo papo hapo kuliko yule ambaye ni mkimya, maana anaweza ‘akakuvizia’ kama afanyavyo chatu, na kuvia kwake ni “kumshtakia Mungu…”
Narudia tena, katu usimchokoze mtu mkimya, mtu mwema na asiyependa ugomvi, kwa sababu akiamua kulipiza, utalia! Kamwe huwezi kushinda nakwambia na utaumbuka na kudhalilika mbele ya jamii inayokuheshimu.
Tazama mashairi ya kibao hiki:

Chatu mkali kwa nini wamuogopa!
Mnyama asiye kivuli hana mfupa !
Tena jabali awindapo hana pupa!
Apenda  machakani mjini hakuzoea
 (repeat x 3)

Hutega njiani usiku amekusudia
Ni mwepesi kubaini adui kumfikia  
Usimchezee ndugu utaangamia!
Ukufike mtukutu ujute kuzaliwa

(Chorus)
Usimchezee chatu ohoo! chatu ehee!
Dongo usimtupie, utaukosa ushindi! x 2
 
[Muhidin Gurumo]
Natoa onyo kwa yeyote anayechezea chatu ni hatari
Atakuwa asipate lolote la manufaa
Na ajali imkute bila ya kutegemea!
Atakuja adhirika ajute na Dunia

(Chorus)
Usimchezee chatu ohoo! chatu ehee!
Dongo usimtupie, utaukosa ushindi! x 2
 
0656-331974

No comments:

Post a Comment