Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Wednesday 16 March 2016

DENI LA TAIFA: TUNADAIWA AU TUMENYONYWA?



Na Daniel Mbega
MWISHONI mwa wiki iliyopita, Mbunge wa Kigoma Mjini (ACT Wazalendo) Zitto Kabwe, kupitia mitandao ya kijamii, alitoa taarifa kwamba Deni la Taifa la Tanzania kwa sasa limefikia Dola 15 milioni ambazo ni zaidi ya Shs. 30 trilioni.
Kutokana na ukubwa wa deni hilo, Zitto Kabwe anasema, Tanzania hulipa Huduma ya deni la taifa takriban Shs. 2.2 trilioni kila mwaka, fedha ambazo ni nyingi kuliko hata bajeti ya wizara yoyote nchini.
Lakini akasema kwamba, ndani ya madeni hayo kuna ambayo yamepatikana kwa rushwa na mengine yamechukuliwa kwa matumizi ya anasa tu, yaani ‘odious debts’.
Deni mojawapo la hovyo ni la Dola 600 milioni (Shs. 1.2 trilioni) ambalo Tanzania ilikopa kutoka Benki ya Standard ya Uingereza kupitia Hati Fungani (Bonds), mkopo ambao Taasisi ya Serious Fraud Office (SFO) ya Uingereza imebainisha kwamba umepatikana kwa rushwa huku taasisi nyingine ya Corruption Watch ya Uingereza pia ikisema kwamba Tanzania imepata hasara ya Dola 80 milioni (Shs. 160 bilioni) kwa kuchukua mkopo huo.
Alhamisi Juni 11, 2015 wakati akiwasilisha Taarifa ya Hali ya Uchumi yam waka 2014 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa mwaka 2015/2016 bungeni mjini Dodoma, aliyekuwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Mahusiano na Uratibu), Dk. Marry Nagu, alisema kwamba Deni la Taifa limekua kutoka Shs. 30.6 trilioni hadi kufikia Shs. 35.01 trilioni huku ongezeko hilo likitokana na riba, madeni mapya yaliyokopwa na Serikali kugharamia ujenzi na ukarabati wa miundombinu hasa ya usafirishaji wa nishati.
Lakini akasema licha ya deni hilo kufikia kiasi hicho, utafiti na takwimu unaonyesha kiwango cha umaskini vijijini kimepungua kwa asilimia 6.1, katika kipindi cha miaka mitano iliyopita.
Hili linatia mashaka na kuzua maswali mengi yasiyo na majibu kwa sababu kwa miaka nenda-rudi tumekuwa tukielezwa kwamba deni la taifa ninaendelea kukua – halipungui.
Wanasiasa na wanaharakati nchini Tanzania wamekuwa wakilizungumzia sana Deni la Taifa na wengine kwa miaka kadhaa sasa wamelifanya kuwa mjawao ya agenda zao wanaonadi sera za vyama vyao.
Ukiangalia ukubwa wa deni hilo, kama wanavyosema wanasiasa, kwa Watanzania milioni 45 waliopo sasa, maana yake kila mmoja anadaiwa Shs. 778,000!
Tanzania, kama zilivyo nchi nyingi za Afrika na zinazoendelea, ni mtumwa wa madeni, lakini hivi ni kweli tunadaiwa ama tumenyonywa?
Kwa sasa ni jambo la kawaida kuona kwa nchi ya Kiafrika kuwa na mfadhili, mhisani, mwekezaji ama mdai hata kama mfadhili ama mwekezaji huyo ndiye chanzo cha matatizo na umaskini kwa nchi husika.
Kinachoonekana bora zaidi ni kwa nchi hiyo tu kusifiwa kama mfano wa kuigwa wa mafanikio ya uchumi wa uliberali mamboleo na hivyo kuendelea kupokea misaada zaidi, mikopo na makubaliano mabaya katika mikataba ya ‘kimahaba’.
Na kwa kadiri inavyojikuta imebanwa katika sera za kibepari, nchi hiyo yenye madeni makubwa, tegemezi, na inayonyonywa kirahisi, itaendelea tu kuwa kipenzi cha Mataifa ya Magharibi!
Tunatambua kwamba dhana ya deni la taifa inamaanisha idadi yote ya fedha zilizokopwa na Serikali kutoka kwa wakopeshaji mbalimbali – wawe wakopeshaji wa ndani ama wa nje, wenye masharti nafuu ama masharti ya kibiashara.
Mikopo hiyo hujazia kwenye pengo la bajeti na wakati mwingine serikali zinakopa baada ya hao wanaojiita wahisani kuamua kuchangia bajeti ama kutochangia kwa sababu wanazozijua wenywe, kama walivyogoma wakati wa sakata la Akaunti ya Escrow. Huwezi kwenda kuwashikia mtutu wa bunduki wakupe.
Hivi sasa Waafrika, nchi zote zilizo kusini mwa dunia na watu wote wanapigania na kulilia maisha bora, haki za kijamii, haki za kibiashara na siyo misaada ya kibiashara.
Hata hivyo, ni mara ngapi tumewahi kuketi kutafakari na kuchambua mizizi ya matatizo yetu? Tumewahi kuhusisha madeni haya makubwa na ufukara wetu? Je, tunatambua madhara ya madeni haya katika maisha yetu kisiasa, kiuchumi na kijamii?
Tumeshawahi kufanya ukaguzi wa madeni haya tunayodaiwa na kujiridhisha ni akina nani wanaotudai, wanatudai kiasi gani, kwa ajili gani na kwa masharti gani? Madeni hayo ni ya muda gani na riba yake ni kiasi gani? Nini siasa ya deni husika? Je, tunatambua ni wakati gani msaada ama ruzuku inapokuwa deni? Hivi ni kweli tunadaiwa ama tumenyonywa?
Katika miaka ya 1980 Rais wa Kwanza wa Tanzania, Mwalimu Julius Nyerere aligomea mabadiliko ya uchumi (Structural Adjustment Programme) yaliyohimizwa na Shirika la Kimataifa la Fedha (IMF) na Benki ya Dunia kwa sababu aliona kile ambacho viongozi wetu wa sasa hawakioni ama wanajifanya hawakioni.
Kwake yeye, mkakati wa IMF na WB ulikuwa kutufundisha ubepari na kanuni zake za mchezo wa kukopa na misaada. Kwa sasa wakubwa hao wanaketi wakiwa wameridhika kwamba mkakati wao umefanikiwa na hata kama vyombo hivyo vitaondoka leo, havina hofu kwa kuwa bado wanaye mrithi mwingine mbaya zaidi ambaye anaitwa Shirika la Biashara la Dunia (WTO) ambalo ndani yake mataifa yote wanachama, makubwa kwa madogo, matajiri kwa maskini, yanatazamwa kama yako sawa.
Kwa Mwalimu Nyerere, ilikuwa wazi kwamba IMF na WB ndiyo majeshi mapya ya makabaila chini ya jina jipya la utandawazi wa kibiashara, majeshi ambayo tofauti na wakati wa ukoloni yalipotumia bunduki, dhahabu, vito na serikali kumiliki maisha yetu na kuchota rasilimali zetu, sasa yanazitumia serikali zetu wenyewe na mashirika ya kimataifa pamoja na mikopo na mitaji kama silaha yao ya kutudhibiti, kutunyonya na kutukandamiza.
Wakati tunaelezwa kwamba nchi yetu ina madeni makubwa – mengine yasiyolipika – lakini ni kwa kiasi gani cha rasilimali ambacho kimechotwa isivyo halali barani Afrika, Tanzania ikiwemo, kwa miaka yote na bado wanaendelea kutaka kuchota tu rasilimali hizo.
Mabadiliko ya tabia nchi yaliyosababisha uhalibifu wa mazingira dunia nzima umefanywa na mataifa hayo hayo makubwa kutokana na uchafuzi unaofanywa na viwanda vyao vinavyotegemea rasimali zinazochotwa barani Afrika huku sisi tukipatwa na madhara hayo. Kitu gani ambacho wametulipa kwa kusababisha uharibifu wa mazingira ambao katika sehemu kubwa umetusababishia ukame na jangwa?
Hivi kwa umaskini waliotuachia kwa kuchota rasimali zetu badala ya kutuendeleza wenyewe tusimamie, na kwa madhara mengi waliyotusababishia, bado tunaendelea kusema kwamba tunadaiwa? Kwamba fedha walizotupatia kama mkopo zinapaswa kuwa fidia kwa rasilimali zetu walizozichota, wakati mwingine kwa kutumia viongozi wetu, hivyo tunaweza kusema hatudaiwi!
Mwalimu Nyerere alisema kwamba hatudaiwi na hatupaswi kulipa. Ndiyo maana alimwambia hata Nelson Mandela asilipe deni la makaburu wakati alipoingia madarakani, siyo halali. Alimwambia pia Laurent Kabila asilipe deni la Mobutu Seseseko! Ni makossa kulipa deni haramu ambalo limewanufaisha wachache.
Wakati wa Mpango wa Kurekebishaji Uchumi (SAP) mojawapo ya masharti yaliyowekwa na wakubwa wa IMF na WB ilikuwa ni kuondoa ruzuku kwenye huduma za jamii na kilimo na ndipo gharama za uchangiaji huduma za elimu, afya na kadhalika zilipoanzishwa.
Mwalimu Nyerere hakuamini kwamba mikopo na misaada inaweza kutukomboa kiuchumi, badala yake aliona kwamba ukombozi wa Mwafrika ulikuwa kwenye mawazo yake: kama tutapatiwa elimu katika fani mbalimbali litakuwa suluhisho la kudumu hata kusimamia rasilimali zetu.
Ikiwa sisi ni maskini licha ya kuwa na rasilimali zote hizi, basi hiyo inatokana na uwezo kielimu, lakini pia kimawazo, maana tunaweza kusoma tukajaza makabati kwa shahada zetu, lakini tusipobadilika kimawazo, bado tutaendelea kuwa wajinga na mwisho wake tutaogelea katika lindi la utumwa-mamboleo.
Mataifa mengi yanakimbilia Afrika kuja kuwekeza kwa sababu yanaelewa tunazo rasilimali. Wakubwa hao wako tayari kutoa misaada hata ya vyandarua na vifaa vya kukusanyia taka kama geresha tu huku wakichuma rasilimali zetu nyingi ambazo hazina idadi.
Afrika siyo maskini, lakini imebatizwa jina la umaskini mpaka kwenye fikra zetu ili tuamini kwamba hatuwezi kufanya jambo lolote kwa sababu ‘sisi ni maskini’.
Ili kuondoka na hilo, ni vizuri viongozi wa Afrika na Waafrika kwa ujumla tuzinduke. Hao wanaokimbilia kuja kuwekeza lazima tuwabane tuone sisi kama taifa tunanufaikaje, na kama wanatupatia msaada, basi usiwe na masharti kwa sababu maendeleo waliyonayo huko yametokana na rasilimali zetu wakati wao hawakutulipa fidia.
Ni kwa msingi huo ndiyo maana ninaona kwamba sisi hatudaiwi, bali tumenyonywa vya kutosha na wakatupumbaza kwamba ‘ni maskini’ ili waendelee kutunyonya huku wakitupatia ‘peremende’ kidogo kufanikisha unyonyaji wao.
Tukatae kuitwa wadaiwa sugu kwa sababu deni hilo kimsingi hakuna anayelifahamu kwa kina na linazidi kutufanya tuwe maskini kila siku.
Tunachopaswa kukifanya ili kuepukana na ‘madeni’ hayo ni kuwajibika. Kwanza lazima serikali ya sasa iyachunguze madeni yote ambayo Tanzania inadaiwa, kama yalipatikana kihalali ama siyo kihalali, kama yalilenga kuhudumia wananchi ama kwa anasa za viongozi kama tulivyoambiwa hapo juu.
Kauli mbiu ya Rais John Magufuli katika ‘kutumbua majipu’ lazima ijikite huku kwenye deni la taifa kwa sababu linawatesa wananchi wakati kumbe inawezekana limetokana na uzembe wa viongozi au hata wamekopa kushibisha matumbo yao tu.
Kushindwa kufanya hivyo hatari yake ni kwamba hata mapato yote ya ndani yanaweza kuishia kulipa madeni na utafika wakati ambapo serikali itashindwa kuwahudumia wananchi katika elimu, afya, maji na miundombinu kwa sababu fedha zote zitakuwa zikilipa madeni ya ‘anasa’.
Baada ya hapo lazima tuweke mkazo katika kukusanya kodi, wajibu ambao ulisahauliwa na viongozi wetu kiasi kwamba wapo wafanyabiashara ambao walikuwa kwenye fungate la muda mrefu huku wakiingiza mabilioni ya fedha na serikali ikikosa mapato.

CREDIT: FIKRAPEVU


No comments:

Post a Comment