Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Tuesday 4 October 2016

SERIKALI YAENDELEA KUREKEBISHA MIUNDOMBINU KAGERA


Mkuu wa Mkoa wa Kagera Meja Jenerali Mstaafu Salum Kijuu akiongea na waandishi wa habari leo mjini Bukoba alipokuwa akitoa taarifa ya hatua zilizochukuliwa na Serikali katika kurejesha hali baada ya maafa ya tetemeko la ardhi lililoukumba mkoa huo.

Na Eleuteri Mangi, MAELEZO, Bukoba
Serikali inaendelea na juhudi za kurejesha miundombinu iliyoharibiwa na tetemeko ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma za msingi za kijamii ikiwemo shule za msingi, sekondari, barabara na vituo vya afya.

Akitoa taarifa ya urejeshwaji wa hali baada ya tetemeko la ardhi la Septemba 10 mwaka huu kwa waandishi wa habari leo mjini Bukoba, Mkuu wa Mkoa wa Kagrea Meja Jenerali Mstaafu Salum Kijuu  amesema kuwa Kamati ya Maafa tayari imetoa vifaa vya ujenzi ili kuhakikisha hali ya miundombinu inarejea na kuwahudumia wananchi.

Aidha, Watanzania walioguswa na janga tetemeko wametakiwa kuendelea kuwachangia Wanakagera ili kuwarejeshea maisha yao ya kawaida.

Katika kurejesha hali, tayari vifaa mbalimbali vimetolewa ikiwemo mabati 4,496 ya geji 30, mbao 98, misumari ya bati kilo 110 na misumari mchanganyiko kilo 558 ili kurekebisha na kujenga miundombinu kulingana na uharibifu uliotokea.

“Tumetoa kipaumbele katika kurejesha miundombinu ya huduma za kijamii kwenye halmashauri za wilaya zilizoathirika ili kamati za maafa za wilaya ziweze kukarabati miundombinu ya kutolea huduma za kijamii kama shule za sekondari na msingi, vituo vya kutolea huduma za afya vilivyoharibiwa na tetemeko ili huduma hizo muhimu ziweze kurejea mara moja na kutoa huduma kwa wananchi” amesema Meja Jenerali Mstaafu Kijuu.

Katika kuhakikisha wananchi wananchi wanapata mahitaji muhimu, Meja Jenerali Mstaafu Kijuu amesema kuwa Kamati ya Maafa imeendelea kugawa mahitaji kwa wananchi walioathirika na tetemeko kadri inavyoyapokea kutoka kwa wadau mbalimbali.

Mahitaji yaliyogawiwa kwa wananchi ni pamoja na unga wa sembe kilo 4,350, sukari mifuko 1,014, mchele kilo 103,400, maharagwe kilo 5,753, mahindi kilo 50,000 majani ya chai tani 3, maji katoni 850, mafuta ya kula lita 249, sabuni katoni 26, mashuka 90, mablanketi ya watu wazima na watoto 2,680, vyandarua 1,274, sare za wananfunzi 570, magodoro 694, mahema 127 na matrubali 5,760.

Kuhusu watu waliopata majeraha, Meja Jenerali Mstaafu Kijuu amesema wamebakia majeruhi sita, ambapo katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Kagera wamebakia majeruhi wawili, Hospitali ya Mugana majeruhi mmoja, na Hospitali ya Rufaa ya Bugando majeruhi watatu na majeruhi wote wanaendelea kupata huduma za matibabu na hali zao zinaendelea vizuri.

Mkuu huyo wa mkoa amesema kuwa awali baada ya tetemeko la ardhi kulikuwa na majeruhi 440 ambapo tayari majeruhi 434 wametibiwa na kuruhusiwa katika Hospitali ya Rufaa ya mkoa na vituo mbalimbali vya afya kwenye mkoa huo.

Kwa upande wa misaada iliyopokelewa na kamati ya maafa, Meja Jenerali Mstaafu Kijuu amesema kuwa kamati ya maafa imepokea misaada ya mahitaji mbalimbali yenye thamani ya zaidi ya shilingi 1,094,478,950 ambayo imeendelea kugawiwa kwa wananchi kadiri ilivyokuwa inaletwa na wananchi na wadau wengine.

Aidha, Mkuu huyo wa mkoa amewashukuru wananchi pamoja na wadau mbalimbali ambao wameendelea kutuchangia kwa fedha taslimu na hundi katika akaunti maafa inayojulikana kwa jina la “Kamati Maafa Kagera 0152225617300 CRDB BUKOBA.” ambapo hadi Oktoba 03 mwaka huu zimepokelewa jumla ya shilingi bilioni 3,481,069,473.43 na kuwaasa wananchi wasikatishwe tamaa kuchangia kutokana na tukio la hivi karibuni la kufunguliwa akaunti nyingine ambayo siyo halali na kuwahakikishia kuwa suala hilo limedhibitiwa na hakutakuwepo na udokozi wala matumizi mabaya ya fedha zinazochangwa wala vifaa vinavyochangiwa.

Wakati huo huo, Mkuu wa mkoa amesema kuwa mitandao ya simu ya M-pesa 0768196669, Tigo Pesa 0718069616, na Airtel Money 0682950009 hadi kufikia Oktoba 03 2016 zimepokelewa jumla ya shilingi milioni 4,750,927.

Zaidi ya hayo Meja Jenerali Mstaafu Kijuu aesema kuwa Kamati ya Maafa inaendelea kuwahudumia wananchi walioathirika na tetemeko mkoani Kagera wanaotoa malalamiko, ushauri, maoni na taarifa mbalimbali kutoka kwa wananchi waloathirika katika tetemeko.

Malalamiko yanaweza kuletwa kwa kamati kupitia za namba za simu zilizotolewa katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa 0621155777 na Ofisi ya Waziri Mkuu 0621155888 na kujibiwa au kuelekezwa wanachotakiwa kufanya ili kupata huduma ya misaada.

Kupitia namba hizo za simu kamati imepokea jumla ya simu 82 kutoka maeneo mbalimbali na wananchi kuhudumiwa na kupata misaada waliotarajia na kuwataka wananchi kuendelea kutumia simu hizo ili kutatuliwa kero zao hasa kuhusu misaada.

Mkuu wa mkoa alitumia nafasi hiyo kuwaomba wananchi wote ambao waliathirika na tetemeko la ardhi na nyumba zao kuharibiwa wahakikishe wanaanza kurejesha miundombinu ya nyumba zao kama baadhi yao walivyokwisha kufanya wasisubiri kujengewa na kuongeza kuwa Serikali inajenga miundombinu iliyoharibiwa ya kutolea huduma za jamii.

No comments:

Post a Comment