Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Tuesday 29 December 2015

TANZANIA YAPOTEZA, BOTSWANA NA NAMIBIA ZAVUNA MADAKTARI

Mwenyekiti wa Jumuiya ya Madaktari inayoongoza mgomo wa madaktari, Stephene Ulimboka akiuliza swali wakati Waziri Mkuu, Mizengo Pinda alipozungumza na madaktari na wauguzi wa hospitali ya taifa ya Muhimbili jijini Dar es salaam, Februari 9,2012. (Picha na Maktaba
Waziri Mkuu, Mizengo Pinda akisalimiana na Mwenyekiti wa Jumuiya ya Madaktari inayoongoza mgomo wa madaktari, Stephene Ulimboka baada ya kuzungumza na madaktari na wauguzi wa hospitali ya taifa ya Muhimbili jijini Dar es salaam, Februari 9,2012. (Picha na Maktaba) 

Na Daniel Mbega
SERIKALI ya awamu ya tano chini ya Rais Dk. John Magufuli imewaahidi Watanzania kuboresha sekta ya afya. Hili ni jambo jema.
Imeahidi kujenga hospitali za wilaya, mikoa na hospitali za rufaa pamoja na kutekeleza Sera ya Afya inayosisitiza kwamba kila kijiji kiwe na zahanati na kkila kata iwe na kituo cha afya ili kusogeza karibu huduma za afya kwa jamii.
Licha ya kuahidi pia upatikanaji wa dawa, lakini bado haijazungumzia mikakati yake ya kuhakikisha wanakuwepo watumishi wa kutosha wa afya, hususan madaktari.
Katika kipindi cha takriban miaka 10 iliyopita Tanzania imeshuhudia wimbi la madaktari likitimka nchini kwenda katika mataifa mengine kusaka mishahara minono.
Hali hiyo inatokana na mazingira duni ya kufanyia kazi hapa nchini pamoja na mishaara midogo licha ya mzigo mkubwa wa kuhudumia wagonjwa wengi huku mamlaka husika zikishindwa kusikiliza kilio cha wataalamu hao wa tiba ambao wakati mwingine wanalazimika kugoma ili kuishinikiza serikali.
Tumeshuhudia mara kadhaa migomo hiyo ya madaktari ikileta athari kubwa kwa wananchi, ikiwemo vifo vya wagonjwa wasio na hatia, lakini badala ya kutatua matatizo yaliyopo, serikali imekuwa ikiwafukuza kazi na kuwasimamisha wengine kwa migomo hiyo.
Matokeo yake Tanzania sasa imekuwa miongoni mwa nchi tisa zilizoko Kusini mwa Jangwa la Sahara ambazo zinapoteza mabilioni ya fedha kuwasomesha madaktari, lakini baadaye wanatimikia nje kusaka maisha mazuri.
Uamuzi wa kufukuza kazi au kuwasimamisha madaktari haujaleta nafuu kwa taifa, badala yake umeleta hasara kubwa huku ukizinufaisha nchi kama Botswana, Namibia na Zambia, ambako inaelezwa kwamba maslahi ni mazuri zaidi na ndiko wataalamu wetu wanakokimbilia.
Utafiti uliofanywa na Edward Millas wa Taasisi ya Global Health ya Chuo Kikuu cha Ottawa, unaonyesha kwamba Tanzania ni moja kati ya nchi tisa za Kusini mwa Jangwa la Sahara ambazo zinapoteza mabilioni ya fedha kwa kuwasomesha madaktari lakini wanatimka kwenda nchi nyingine.
Mbali ya Tanzania, nchi nyingine zinazoathirika na kuondoka kwa madaktari wake ni Ethiopia, Kenya, Malawi, Nigeria, Afrika Kusini, Uganda, Zambia na Zimbabwe.
Kwa mujibu wa utafiti huo, Afrika Kusini na Zimbabwe ndizo zinazoongoza kupoteza fedha nyingi kusomesha madaktari hao, ambao hatimaye wanatimkia nje, huku Australia, Canada, Uingereza na Marekani zikinufaika zaidi kwa kuwaajiri madaktari hao.
Utafiti huo unaeleza takwimu za namna nchi husika zinavyotumia fedha kuwasomesha madaktari na jinsi nchi nyingine zinavyookoa fedha hizo kwa kuwaajiri madaktari hao badala ya kuwasomesha wao.
Matokeo ya utafiti huo yanaonyesha kwamba, serikali katika nchi hizo zinatumia kati ya Dola za Marekani 21,000 (kwa nchi ya Uganda) hadi Dola 59,000 (Afrika Kusini) kumsomesha daktari mmoja, ambapo kwa nchi tisa zilizofanyiwa utafiti, inaonekana zilitumia kiasi cha Dola 2 bilioni (takriban Sh 4.4 trilioni) kuwasomesha madaktari wao na hazikuweza kuwatumia.
Lakini Uingereza inaokoa karibu Dola 2.7 bilioni (Sh 6 trilioni) huku Marekani ikiokoa Dola 846 milioni (Sh 1.9 bilioni) kwa kutowasomesha madaktari wake na kuajiri wale kutoka nchi zinazoendelea.
Itakumbukwa kwamba, mara baada ya mgomo wa Januari na Juni 2012, madaktari 80, wakiwemo madaktari bingwa, kati ya 200 waliofukuzwa kazi kutokana na kushiriki mgomo waliondoka nchini kwenda Kusini mwa Afrika kati ya mwezi Januari na Juni.
Hata hivyo, kuondoka kwa madaktari hao ambao wanatafuta maslahi zaidi, kunaelezwa kumechangiwa na uzembe wa Serikali katika kutatua kero na kuboresha maslahi yao kwa miaka mingi sasa.
Taarifa zinasema, madaktari wengi wanakimbilia Botswana kwa sababu nchi hiyo inawalipa vizuri zaidi, sambamba na walimu, na kwamba ndiyo inayoongoza kwa kuwa na madaktari wengi kutoka Tanzania pamoja na wataalam wa fani nyinginezo, hasa za uhandisi.
Takwimu za Shirika la Afya Duniani za mwaka 2006, zinaonyesha kuwa, uwiano wa daktari na wagonjwa kwa nchi ya Botswana ni 1: 2,500, wakati ambapo Tanzania, ambayo inaendelea kuwapoteza madaktari kila siku, uwiano wake ulikuwa 1: 50,000.
Baada ya mgomo wa Juni 23, 2012 Serikali ilitangaza kuwafukuza kazi madaktari zaidi ya 200 waliodaiwa kushiriki mgomo kutoka Hospitali ya Rufaa Mbeya, Hospitali ya Mkoa wa Dodoma, Hospitali ya Rufaa Bugando na Hospitali ya Taifa Muhimbili.
Hata hivyo, wengi kati ya waliofukuzwa ni wale ambao walikuwa mafunzoni (interns), huku madaktari bingwa wakisimamishwa kazi kwa muda usiojulikana, hali ambayo iliwafanya wengi wao kutafuta ajira nje ya nchi.
Januari 2012, uongozi wa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) ulitangaza kuwafukuza kazi madaktari 229 waliokuwa katika mafunzo kwa njia ya vitendo kutokana na mgomo wa siku nne wakishinikiza kulipwa posho zao za mwezi mmoja, takriban Shs. 176 milioni.
Kuondoka kwa madaktari hao na watumishi wa afya kutoka katika nchi zinazoendelea kama Tanzania kukichangiwa na migomo kunazorotesha mfumo mzima wa afya, hivyo kuwa tishio katika kufikia Malengo ya Endelevu ya Dunia.
Mwaka 2010, Jukwaa la Afya la Dunia (World Health Assembly) liliridhia azimio la kwanza la kimataifa katika kuajiri wataalam wa afya kwa kutambua matatizo yanayosababishwa na kuhama kwa madaktari kutoka nchi maskini kwenda nchi tajiri, ambazo hatimaye ndizo zinazotoa misaada katika sekta ya afya.
Azimio hilo ni muhimu kwa nchi za Kusini mwa Jangwa la Sahara lenye uhaba mkubwa wa watendaji katika sekta hiyo, lakini wachunguzi wa mambo wanasema, kitendo cha serikali kupuuza madai ya madaktari na kusababisha migomo kinarudisha nyuma azma ya kutatua matatizo hayo.
Pengine ni wakati muafaka sasa kwa serikali kuboresha mazingira ya kufanyia kazi pamoja na maslahi ya watumishi wa sekta ya afya, ambayo siyo tu yatawavutia wataalamu walioko nchini kufanya kazi, bali pia kuwavutia wale waliotimka kurejea na kuwahudumia Watanzania wenzao.

0656-331974


No comments:

Post a Comment