Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Tuesday 29 December 2015

SERIKALI MAKINI HUKUSANYA KODI!

Bandari ya Dar es Salaam ambayo kutokana na ufisadi na rushwa, watendaji wa serikali wanaikosesha mabilioni ya fedha za kodi na ushuru mbalimbali. (Picha ya mtandao).

Na Daniel Mbega
NAKUMBUKA hotuba ya Mwalimu Julius Nyerere wakati wa Mei Mosi 1995 pale kwenye Uwanja wa Sokoine, Mbeya. Alisema mambo mengi sana, yote yenye maana, lakini kubwa ninalolikumbuka leo, alisisitiza umuhimu wa kukusanya kodi.

Alisema wazi kwamba, hata hao IMF (Shirika la Fedha Duniani) na Benki ya Dunia, ambao ndio walioshinikiza tuyabinafsishe mashirika yetu ya umma, walikuwa wanahimiza tukusanye kodi.
Na hawahimizi tukusanye kodi kwa sababu nao wamechoka kutusaidia, bali ndio wajibu wa serikali yoyote makini, kwani kodi ndiyo chanzo kikuu cha mapato ya serikali.
Hata hivyo, hili haliko hivyo katika serikali yetu, serikali iliyojisahau ama kupuuza wajibu wake na kila mmoja aliye madarakani anaona kwamba jambo la msingi zaidi kwake ni kuangalia maslahi yake, siyo ya umma.
Tunashuhudia kila uchao namna ambavyo maofisa wa serikali wanavyokumbwa na kashfa mbalimbali za ufisadi, wizi na ubadhilifu katika idara wanazoziongoza.
Shirika la Viwango Tanzania (TBS) lilikumbwa na kashfa kubwa ya kutokusanya kodi kwa magari yanayoagizwa kutoka nje na badala yake watu wachache wakajinufaisha kwa mamilioni ya fedha zilizopaswa kuingia serikalini, wakatoa vibali kwa magari yasiyo na viwango.
Tumeshuhudia jinsi vigogo wa Mamlaka ya Bandari wanavyoitumia bandari yetu kama kitega uchumi chao na familia zao kwa kushindwa kutoza ushuru wa serikali, badala yake ule wanaokusanya, ambao ni kidogo, nao unaingia kwenye akaunti zao zilizofurika huko nje.
Mamlaka ya Mapato nchini (TRA) nayo imeendelea kuandamwa na zimwi la rushwa na ufisadi kwa maofisa wake kujineemesha kwa fedha za umma, wakikusanya fedha chache kupitia mlango wa nyuma huku nyingi zikiendelea kubakia kwa wafanyabiashara wenye uroho wa fisi, makupe wanaopenda kufonza mpaka waone damu imekauka.
Sekeseke lililotokea hivi karibuni la kupitishwa kwa makontena 349 bila kulipiwa ushuru ni mfano mmojawapo tu wa namna mabilioni ya kodi yanavyochotwa pale Bandari kwa ushirikiano na TRA.
Tunaipongeza serikali ya awamu hii chini ya Rais John Magufuli, ambaye ameamua kupambana kuhakikisha kodi za umma zinakusanywa na wahusika wote wanashughulikiwa.
Aliahidi kwenye kampeni na ameendelea kurudia kauli yake kwamba lazima apambane na wafanyabiashara wakubwa ‘wasioguswa’ ambao wamekuwa wakikwepa kulipa kodi, na hii ya sasa pengine ni picha ya utangulizi tu.
Katika hotuba yake ya ufunguzi wa Bunge la 11, Rais Magufuli alitamka bayana kwamba, ameamua kubana matumizi yasiyo ya lazima pamoja na kuongeza kasi ya ukusanyaji wa kodi. Amefuta safari za ng’ambo zisizo za lazima ili kubana matumizi ikiwa ni pamoja na sherehe mbalimbali ambazo zimekuwa zikigharimu mabilioni ya fedha.
Kwa zaidi ya miaka mitatu sasa ukusanyaji wa mapato umekuwa chini ya makadirio kwa sababu mbalimbali. Serikali ya Awamu ya Tano itaongeza nguvu katika upanuzi wa wigo wa kodi na kuongeza ufanisi katika ukusanyaji wa mapato. Tutahakikisha kwamba kila mtu anayestahili kulipa kodi analipa kodi stahiki.  Hatutasita kumchukulia hatua mtu yoyote atakayekwepa kulipa kodi. Tunawaomba wananchi mhakikishe mnapewa risiti kila mnaponunua bidhaa au huduma. Kodi ni kitu muhimu lazima kila mtu anayestahili kulipa kodi alipe,” alisema kwa msisitizo.
Aliahidi kwamba, serikali yake itahakikisha kila senti inayoongezeka katika mapato ya Serikali inaelekezwa katika kutoa huduma bora zaidi kwa wananchi na kwamba wataziba mianya ya upotevu wa fedha za Serikali ambayo inaipunguzia Serikali uwezo wake wa kuwahudumia wananchi. 
“Nitataja baadhi tu ya maeneo ambayo tutayasimamia kwa lengo la kupunguza matumizi yasiyo ya lazima na kuziba mianya ya uvujaji wa fedha za Serikali: Kwanza, safari zote zisizo za lazima nje ya nchi Serikalini tutazidhibiti na badala yake tutawatumia mabalozi wetu kutuwakilisha kwenye mikutano ya aina hiyo. Na pale inapolazimu kiongozi au mtumishi mwandamizi kusafiri tutahakikisa kwamba haandamani na msururu wa watu wengi ambao hawana umuhimu wala shughuli za kufanya katika safari hizo.
“Katika kusisitiza hili napenda niwape takwimu za fedha zilizotumika ndani ya Serikali, Mashirika ya Umma na Taasisi nyingine za Serikali kwa safari za nje kati ya mwaka 2013/14 na 2014//2015. Jumla ya shilingi bilioni 356.324 zilitumika kwa ajili ya safari za nje kama ifuatavyo: Tiketi za ndege zilitumia shilingi bilioni 183.160;Mafunzo nje ya nchi zilitumika shilingi bilioni 68.612; Posho za kujikimu (Per Diem Foreign) zilitumika shilingi bilioni 104.552,” alifafanua.
Alizitaja Wizara na Taasisi zinazoongoza kwa matumizi ya safari za nje kuwa ni pamoja na Bunge, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikano wa Kimataifa, Wizara ya Fedha, Ofisi ya Waziri Mkuu, Ofisi ya Taifa ya Ukaguzi wa Hesabu za Serikali (NAOT), Wizara ya Mambo ya Ndani, na kadhalika.
Kwa mdomo wake akasema: “Hizi fedha zingeweza kutumika vizuri kuboresha huduma za wananchi wa maisha ya chini, kama afya, maji, elimu, umeme n.k. Mfano; fedha hizi zingetosha kutengeneza kilometa 400 za barabara za lami, tujiulize zingeweza kutengeneza zahanati ngapi? nyumba za walimu ngapi?, madawati mangapi? … Tunapodhibiti safari za nje tunawaomba Waheshimiwa Wabunge na Watanzania wote mtuelewe na mtuunge mkono.”
Akabainisha kwamba, atahakikisha anadhibiti safari na ziara za mafunzo nje ya nchi zinazogharamiwa na serikali ambayo yanapatikana hapa nchini, lakini pia kudhibiti warsha, semina, makongamano, na matamasha ambayo yanatumia fedha nyingi tu za serikali lakini hayana tija na wala hayaongezi ufanisi katika utekelezaji na usimamizi wa sera na mipango ya Serikali.
Inaonekana wazi kwamba Rais Magufuli amedhamiria, kwani aliahidi pia kusimamia kwa ukamilifu Sheria ya Manunuzi ya Umma ili kuhakikisha mianya yote ya fedha za umma inayotokana na usimamizi hafifu inazibwa huku akisisitiza kusimamia na kudhibiti ukiukwaji wa maagizo na maelekezo mbalimbali yaliyokwisha kutolewa na Serikali siku za nyuma kuhusu ununuzi wa bidhaa kama samani kwa ajili ya matumizi ya Serikali.
“Samani zote kwa ajili ya matumizi ya Serikali zinatakiwa ziwe zile zinazozalishwa hapa hapa nchini,” akasema na kuongeza: “Serikali ya Awamu ya Tano itasimamia kwa karibu na kuthibiti ununuzi wa magari ya gharama kwa ajili ya Viongozi na Watumishi waandamizi wa Serikali; na tutaendelea kuchunguza na kudhibiti matumizi ya Serikali na Taasisi zake zote yasiyo na tija kwa uchumi wa taifa letu.”
Ni jambo lililo wazi kwamba, mamlaka zinazohusika na ukusanyaji wa mapato hazikuwajibika ipasavyo huko nyuma, watumishi hawakuwa waadilifu, wakageuza taasisi kama visima vya kuchota mali ya umma, matokeo yake yakaifanya serikali ikose mapato stahiki na kugeuka ombaomba kila siku kutembeza bakuli kwa wahisani ili kukidhi hata bajeti yake ya kila mwaka.
Walalahoi ndio waliobanwa na kodi kwa sababu wanakamuliwa katika kila bidhaa wanayonunua, lakini wafanyabiashara husika, wakiwemo wale wakubwa, licha ya kuwakamua walalahoi, bado wameendelea kukwepa kulipa kodi hiyo kama wanavyopaswa.
Deni la serikali linaongezeka kila siku, asilimia arobaini ya bajeti ya serikali inategemea fedha za wahisani ambao nao hutuwekea masharti ya ajabu ndipo watupatie fedha hizo. Tukishindwa kutekeleza, basi hatupati.
Mara kadhaa serikali imenyimwa fedha hizo za bajeti kutoka kwa wahisani, matokeo yake miradi mingi ya maendeleo inakwama.
Kwa upande mwingine, tangu tupate uhuru, ardhi ya Tanzania iliyopimwa, ambayo ndiyo serikali inategemea kukusanya kodi, ni asilimia moja tu! Haya ni masikhara.
Ufisadi umejaa mno katika sekta ya ardhi. Viongozi wa serikali ni washirika namba moja wa ufisadi huo ambapo tunatambua namna walivyojiuzia wenyewe nyumba za watumishi wa serikali kwa bei ya kutupia, halafu wameingia ubia na ‘wenye fedha’ kujenga mahekalu huku serikali ikihangaika kuwatafutia watumishi wapya nyumba nyingine. Wizi mtupu!
Naam, nyumba za kule Masaki, Oysterbay, Ada Estate na pale Kinondoni ambazo zilijengwa kwa ajili ya watumishi wa umma, walijiuzia vigogo wa serikali, tena kwa bei waliyoipanga wao. Wakati wanajiuzia, sote tulitegemea wangekaa huko, lakini ajabu ni kwamba, nyumba hizo kwa sasa zimepangishwa na zinaendelea kupangishwa kwa bei ya kati ya Dola 3,500 na Dola 15,000 kwa mwezi! Ni kwa mwezi, siyo kwa mwaka.
Nyumba hizi hizi walizojiuzia kwa vijisenti, zimekuwa mradi mkubwa kwa waheshimiwa hawa, huku serikali ikishindwa kukusanya kodi yake ambayo kama ingepatikana, ingeweza kuongeza pato la taifa.
Uzembe wa serikali kutokupima ardhi umefanya wananchi wengi, hasa mijini, kuishi katika maeneo yasiyopimwa, hivyo kuinyima fursa serikali ya kukusanya kodi. Matokeo yake serikali inaendeleza tabia yake ya kutembeza bakuli kwa wahisani kuomba fedha za maendeleo badala ya kutumia vyanzo tulivyonavyo!
Mwalimu Nyerere alisema; “… Serikali corrupt haikusanyi kodi…!” Naam, ndivyo ilivyo serikali yetu katika awamu tatu zilizopita, ilikuwa corrupt iliyojaa mafisadi wengi kila idara kiasi kwamba hivi sasa badala ya kuwaza namna gani tubuni na kusimamia miradi ya maendeleo, tunaanza kutumia gharama kubwa kuchunguza nani anakwiba sana fedha za umma na mambo kama hayo.
Naamini kitu kimoja. Kwamba ndani ya serikali wamekuwepo watu makini, waadilifu ambao wanaishauri vyema serikali kila siku, lakini hawakuwa wakisikilizwa. Zaidi tu ni kwamba, ukiendelea kujifanya mchokonozi watakutafutia visa, mwishowe utajikuta uko benchi bila sababu zozote. Ukihurumiwa, utahamishiwa huko ‘Tanganyika’, ambako kunywa maji yenye viluwiluwi na yaliyo machungu utadhani tunaishi jirani na Uvinza ni jambo la kawaida.
Kama serikali haikusanyi kodi na haina utamaduni huo, hivi tunawezaje kujidanganya na kudanganyika kwamba uchumi wetu umekua? Hizi takwimu za kwenye makaratasi tunazopewa na watawala wetu zina ukweli kiasi gani?
Maisha ya wananchi yako chini mno, wengi hawana hata uhakika wa mlo mmoja, huduma za jamii kama maji, afya na kadhalika siyo za kuridhisha – mwili ukichemka unapewa Dawa Mseto, ukiumwa malaria unapatiwa panadol na mambo kama hayo.
Ndiyo, serikali imejitahidi kuimarisha miundombinu ya barabara, lakini bidhaa ngapi zinazopitishwa humo ambazo zimetozwa kodi halali? Maofisa wa TRA mipakani ni mamilionea, biashara za magendo zinaingia na fedha zinakusanywa kupelekwa mfuko wa kushoto huku serikali ikikosa mapato.
Jambo baya zaidi ni kwamba, kwa ulafi wao Watanzania wanaletewa bidhaa feki, zenye sumu na zisizofaa kwa matumizi ya binadamu, halafu mwisho wa siku tunadanganywa kwamba uchumi wetu umekua! Umekua wapi wakati watu wachache ndio wamevimba matumbo huku maelfu kwa mamilioni wakiishi kwa utapiamlo?
Sekta ya kilimo, ambayo kimsingi ndiyo mkombozi wa Watanzania walio wengi, kwa muda mrefu inatumiwa kisiasa na watawala wetu wakiwahadaa wananchi kwa nyimbo nzuri, mapambio na ngonjera kwamba wataleta hiki na kile, lakini hakuna chochote kinachofanyika kivitendo.
Mwisho wa siku asilimia kubwa ya bajeti yetu inategemea wahisani na mikopo, na kwa asilimia zilizosalia tunategemea tukusanye kwenye ‘pombe na bangi’ tu! Ni aibu!
Tunataka serikali ikusanye kodi.

0656-331974

No comments:

Post a Comment