Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Tuesday 29 December 2015

SERIKALI HAIJUI AU INAZUGA UFISADI NGUZO ZA UMEME?


Na Daniel Mbega
HATUA ya Katibu Mkuu Wizara ya Viwanda, Biashara na Masoko, Uledi Mussa, kulitaka Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) kuacha kasumba ya kutumia mabilioni ya fedha kununua nguzo za umeme nje ya nchi ni sawa na serikali kujipiga kofi na kulia yenyewe.

Na kilichofanywa na mtendaji huyo wa wizara ni usanii na kuwazuga wananchi kwa kuwafanya mazezeta, kwa sababu serikali inaufahamu fika mchezo uliokuwepo kwa muda mrefu wa kukataa kununua nguzo za umeme hapa nchini, lakini inaagiza nje ya nchi nguzo zile zile zilizotoka kwenye kampuni za kizalendo ambazo zinazalisha nguzo imara.
Wakati akiwa katika ziara mkoani Njombe, Mussa aliagiza kwamba iwe mwisho kwa Tanesco kuagiza nguzo hizo nje ya nchi kwa sababu viwanda kama Tanwat alichokitembelea eneo la Kibena, vinazalisha nguzo imara ambazo alizikuta zimelundikwa zikisubiri kusafirishwa kwenda Kenya na Afrika Kusini ambako ndiko liliko soko lao kubwa.
Ni huko ambako watendaji wa serikali, hasa Tanesco, wamekuwa wakisingizia Sheria ya Ununuzi ya Umma (PPRA) kuwapa zabbuni wafanyabiashara wa nje wailetee nguzo zile ambazo zimetokea Njombe au Mafinga, wakizinunua kwa bei mbaya kuliko kama wangezinunua nchini, kwa sababu tu ama wanapata kamisheni kubwa kujaza viriba tumbo vyao au kampuni zao ndizo zinazopewa zabuni hizo.
Tanwat siyo kampuni pekee ya kizalendo inayotengeneza nguzo imara za umeme. Nenda pale Mafinga, tena barabarani kabisa, utakuta kuna kampuni inayotengeneza nguzo hizo ambayo walau kidogo imekuwa ikiiuzia Tanesco – pindi wakubwa wanapoamua ‘kuua soo’ ili waonekane wanajali hata viwanda vya ndani.
Ni hivi karibuni tu iliripotiwa kwamba Tanesco ilikuwa katika mchakato wa kuagiza nguzo 700,000 kutoka Afrika Kusini huku Mkurugenzi Mkuu wa shirika hilo, Felchesmi Mramba, akiitetea hatua hiyo kuwa inatokana na mahitaji ya Sheria ya Ununuzi wa Umma inayoweka ukomo wa zabuni kutangazwa kimataifa.
Hii siyo mara ya kwanza kwa serikali kuagiza Tanesco isiagize nguzo nje, ndiyo maana nikasema, kinachofanyika sasa ni kama kuwazuga wananchi waonekane mazezeta wasiojua kinachoendelea.
Nakumbuka mwaka 2012 wakati George Simbachawene akiwa Naibu Waziri wa Nishati na Madini alipata kuiagiza Tanesco kuacha kuagiza nguzo za umeme kutoka nje ya nchi na badala yake itumike bidhaa ya hapa nchini.
Hatua hiyo ilikuja baada ya Simbachawene kutembelea baadhi ya timba za nguzo wilayani Mafinga na kujionea hali halisi ya nguzo hizo zikikosa soko, huku Tanesco ikiagiza  bidha hizo  kutoka Kenya na Afrika Kusini.
 “Sioni sababu ya kuagiza nguzo kutoka Kenya au Afrika Kusini wakati hapa nchini tuna bidhaa hii inakosa soko, hili ni jambo la ajabu sana, hili ni swali ambalo hata ukiulizwa na mtoto mdogo unapata shida sana kulijibu,” alisema.
Akaongeza: “Haya ni maajabu makubwa, viwanda vyetu havina kazi, lakini malighafi zipo, eti tunakwenda kununu nje ya nchi, sisi tunaosimamia wizara hii, tunaambiwa na Tanesco kuwa tatizo kubwa ni nguzo za umeme, na wananchi wetu wanahangaika kupata huduma hii ya umeme kwa gharama kubwa, hapa kama kiongozi na naibu waziri nimesikitishwa sana, moja ya maamuzi ya maana na ya haraka ni kuzuia huu uagizaji wa nguzo nje ya nchi. Haiwezekani wakulima wakawa wanazalisha miti na kupata nguzo tena zenye ubora, halafu sisi tunakwenda kununua nje ya nchi, wakati hao wanaotuuzia wanazinunua kwa gharama nafuu hapa hapa nchini kwetu, hii haiwezekani.”
Aliongeza kuwa wakati sasa umefika kwa Tanesco kwa kutumia bidhaa iliyopo nchini ili kuleta tija kwa viwanda vya ndani, hatua ambayo ingepunguza mzigo wa ununuzi wa gharama kubwa kwa wananchi wanaohitaji nyumba zao kuingiziwa umeme.
Akasisitiza kwamba hawezi kuruhusu tena nguzo ziendelee kuletwa nchini, kwani hali hiyo inachangia kuua viwanda vidogo, inaua uchumi na ajira, na inaleta madhara makubwa kwa taifa.
Lakini muuzaji wa nguzo katika mji wa Mafinga, Awadhi Shedaffa, alisema hatua ya Tanesco kuagiza nguzo nje ya nchi inawanyima fursa wazawa kuuza bidhaa zao zenye ubora, kwani kampuni yake inao uwezo wa kuzalisha nguzo 12,000 kwa mwaka, lakini imekuwa ikiuza nguzo 700 tu kwa mwaka huku akilalamika kwamba licha ya kuomba zabuni mara kadhaa, Tanesco hawajawahi kuwapatia.
Sangito Sumari meneja wa Kiwanda cha Green Resources cha Mufindi anasema kampuni hiyo inao uwezo wa kuzalisha nguzo kati ya elfu hamsini na elfu tisini kwa mwaka, lakini kutokana na kukosa soko, wanazalisha nguzo 14,856 baada ya Tanesco kuacha kuagiza nguzo zao kutokana na deni kubwa la Shs. 2 bilioni kwa wakati huo.
Ukisimama pale Igumbilo mjini Iringa kwenye kizuizi, kila siku utaona malori mengi yakiwa yamebeba nguzo kutoka ama Njombe au Mafinga, lakini nguzo hizo haziishii Dar es Salaam, kwani ama zinaingizwa kwenye makontena kupakiwa na meli kupelekwa Afrika Kusini au malori yanapitiliza kwenda Mombasa na Nairobi, Kenya.
Lakini ukikaa Namanga au Horohoro, utashuhudia pia malori yenye nguzo yakitoka Kenya na kuingia Tanzania. Ukiuliza unaambiwa hizo ni nguzo za Tanesco wamenunua Kenya!
Inakuwaje tunajiibia kwenye mfuko mmoja na kuweka kwenye mfuko wa pili? Biashara ya kujipiga makofi na kulia wenyewe itakwisha lini hii?
Nyingi kati ya nguzo zinazozalishwa na viwanda hivi vya ndani zimethibitishwa na wataalamu kutoka nje ndiyo maana zinapata soko huko kwamba ni bora na imara, zikiwa na uwezo wa kudumu kwa miaka zaidi ya 15.
Tunaposema tunatakiwa kutengeneza ajira nyingi kwa Watanzania kupitia viwanda tutakuwa tunajidanganya wenyewe ikiwa bidhaa za viwanda hivi hatuzithamini kwa sababu matokeo yake lazima uzalishaji utashuka na viwanda hivyo kufungwa kwa sababu hakuna anayeweza kuendelea kufanya kazi kwa hasara.
Mikoa ya Iringa na Njombe ndiyo inayoongoza kwa kilimo cha miti tangu enzi za Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere. Shamba kubwa la miti la Sao Hill lina hazina ya kutosha ya kupata nguzo imara kabisa ambazo hata mataifa mengine yanazitumia.
Hata hivyo, ufisadi uliotamalaki kila idara ndio unaokwamisha maendeleo haya kiasi kwamba rasilimali zetu zinakosa thamani nchini mwetu, lakini zinapokwenda nje na kugongwa mihuri, eti zinaonekana zinafaa.
Imepata kuripoti huko nyuma kwamba, katika ufisadi huo wa ununuzi wa nguzo za Tanesco, hata baadhi ya wabunge walikuwa wakihusika kwa kutumia kampuni zao ama za jamaa zao kununua nguzo Mafinga na Njombe na kuzipeleka nje, halafu wanakula njama na watendaji wa Tanesco ili kuzirejesha tena nguzo hizo nchini kwa bei mbaya.
Siyo siri, mradi huo wa nguzo, kama ilivyo kwa mradi wa mafuta ya kuendeshea mitambo kwa Tanesco, umezingirwa na harufu ya rushwa iliyotamalaki na wabunge waliokuwepo wakati huo wanajijua ni namna gani walivyokuwa wakihusika.
Haikushangaza hata Kamati ya Bunge ya Nishati na Madini iliyokuwa chini ya January Makamba ilipovunjwa mwaka 2011 kufuatia kashfa ya rushwa hasa wakati wa kuelekea kwenye Bajeti ya Wizara ya Nishati na Madini.
Ni wakati muafaka kwa serikali, kama inataka kuziba mianya ya rushwa na kubana matumizi ya hovyo kabisa ya idara zake, kuitupia macho Tanesco na biashara hiyo ya nguzo, vinginevyo Rais John Magufuli atakuwa anaweza fedha kwenye kapu lililotoboka bila kujua.
Wasalaam.

0656-331974


No comments:

Post a Comment