Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Tuesday 29 December 2015

HAWAMTAKI MUHONGO, WALITAKA WATEULE WAO?

Profesa Sospeter Muhongo siku alipojiuzulu Januari 24, 2015

Na Daniel Mbega
UTEUZI wa Baraza la Mwaziri umepokelewa kwa hisia tofauti ambapo wapo wanaosema Rais Dk. John Magufuli amekosea kuwateua Profesa Sospeter Muhongo na Dk. Harrison Mwakyembe.
Wanaokosoa uteuzi wa mawaziri hao wawili kuwemo kwenye baraza wanawahusisha na ufisadi, hali wanayosema inaweza isilete mabadiliko ambayo yalianza kuonekana katika serikali ya awamu ya tano.

Prof. Muhongo anahusishwa na kashfa ya uchotwaji wa fedha za akaunti ya Tegeta Escrow wakati Dk. Mwakyembe anahusishwa na ununuzi wa mabehewa mabovu ya TRL kutoka India.
Lakini Prof. Muhongo, ambaye amerejeshwa kwenye Wizara ya Nishati na Madini, ndiye anayeonekana kuwaumiza vichwa wengi, kwani uteuzi wake umezua mjadala mkubwa kila mahali.
Wanaopinga uteuzi wake wanasema waziri huyo alilazimishwa kujiuzulu na Bunge kufuatia kashfa hiyo ya Escrow, katika wanashindwa kutambua kwamba, kujiuzulu kwake kulikuwa kwa uwajibikaji wa kawaida katika kutuliza hali ya hewa iliyokuwepo baina ya Bunge na Serikali.
Prof. Muhongo alijiuzulu Januari  24, 2015. Lakini kiuhalisia, hakutuhumiwa ufisadi wowote kwenye kashfa ya Escrow, bali ni kuhusishwa na uamuzi mbovu.
Kilicho dhahiri hapa ni kwamba, wanaompinga wote ‘wanasingizia’ tu kashfa ya Escrow, lakini hawataki kusema kurudi kwa Muhongo pale Nishati na Madini ni kuendelea kuiziba mianya yote ya rushwa iliyokuwa imetamalaki.
Inafahamika namna vitalu vya mafuta na gesi vilivyozua mvutano mkubwa tangu Muhongo alipoichukua wizara hiyo kutoka kwa William Ngeleja na jinsi alivyosimamia suala la ugawaja wa vitalu hivyo.
Wafanyabiashara wazawa walilalamikia msimamo wake usioyumba katika mafuta na gesi, wakapiga kelele nyingi kwamba wanabaguliwa, lakini kwa kuzingatia maslahi ya taifa, Muhongo akasema lazima utaratibu ufuatwe na siyo kugawa tu vitalu hivyo kwa sababu ya uzawa ambao hautaweza kuinufaisha nchi.
Yalifichuka mambo mengi yaliyokuwa yamefichwa, kwamba wapo wafanyabiashara wazawa ambao walitaka kujilimbikizia vitalu vya gesi na mafuta wakati uwezo wao ni mdogo, kumbe wanataka watumie umiliki huo kufanya udalali na wawekezaji wa nje.
Kama hawana uwezo, ni kwa nini basi wawe madalali? Si afadhali serikali iingie moja kwa moja mikataba na wawekezaji hao wageni wenye uwezo kuliko kuwaacha wajanja wachache waanze ‘kupiga dili’ kwa rasilimali za wananchi? Tatizo liko wapi?
Inafahamika kwamba wapo wafanyabiashara ambao wamejilimbikizia vitalu vya uchimbaji madini, lakini kwa miaka nenda rudi, hawajawahi kuchimba badala yake wanatafuta wawekezaji wageni ili waingie nao mikataba. Unafanyaje udalali kwa mali ya umma kwa sababu tu una uwezo wa kupenya na kujipatia mikataba hiyo?
Prof. Muhongo aliguswa guswa tu kwenye kashfa ya Escrow, hakuhusika. Lakini ugumu alioupata wakati ule, na ambao kuna uwezekano atakabiliana nao sasa, ni kuwepo hata kwa maofisa wa serikali wanaotumiwa na wafanyabiashara hao kuhujumu juhudi za serikali katika sekta ya mafuta na gesi.
Watumishi hao wasio waaminifu wanaihujumu serikali kwa manufaa yao binafsi, jambo ambalo haliwezi kuleta maendeleo kwa taifa, hivyo sasa wameunganisha juhudi na ‘wapiga dili’ wanaokwenda kwa mwamvuli wa wafanyabiashara ili kumkataa Muhongo.
Prof. Muhongo siyo mwanasiasa na kimsingi amerudishwa pale ili kulinda mikataba ya gesi, mafuta, madini na dili zote za tanesco. Hajarudi kwa bahati mbaya.
Katika serikali ya Dk. Magufuli inayowataka watendaji na siyo wanasiasa wapiga dili, Muhongo ni chaguo sahihi kwa sababu licha ya utendaji wake, yeye ni mtaalamu wa mambo hayo na alidhihirisha hayo katika kipindi alichokaa wizarani hapo.
Zile dili za kuzima ovyo umeme ili watu wauze majenereta zilikufa katika kipindi chake na haukushuhudiwa mgao wa ajabu wa umeme.
Wakati alipokuwa madarakani, Mradi wa Nishati Vijijini (REA) ulikuja kwa kasi, lakini tangu alipoondoka mradi huo umezorota, hivyo kwa asilimia kubwa kurejea kwake kutawanufaisha wananchi wa vijijini wakiwemo wa kule Kamsamba wilayani Sumbawanga na kwingineko nchini ambao wanaonekana wako kisiwani kutokana na jiografia ya maeneo hayo.
Katika zama ambazo Tanzania imeshuhudia mikataba ya mibovu sana ya madini iliyohusisha kampuni kama Meremeta, Tangold, TanzaniteOne, Buzwagi na mingineyo, pamoja na kuchotwa kwa mchanga wa dhahabu na kusafirishwa Ulaya ili ukasafishwe, tunahitaji mtu kama Muhongo ambaye anaweza kuendana na kasi ya Rais Magufuli kuondoa uchafu huo.
Wale wanaolalamikia uteuzi wa Muhongo, pengine walitaka watu wao ndio washike wizara hiyo, lakini kwa staili ya Magufuli, hakuna mwanya wa kujipenyeza kwenye kufanya ‘ushawishi’ (lobbying) kama ilivyokuwa huko nyuma.
Mambo ya ‘kumshawishi’ Rais amteue fulani kwa maslahi ya wachache hata kama hana uwezo ndiyo yamesababisha utawala unayumba kwa sababu watu wamekuwa wakiangalia sura badala ya utendaji, matokeo yake tunawaweka wapiga dili watupu.
Wanaolalamika wanajua kwamba hawatakuwa na nafasi ya kumwita hoteli Prof. Muhongo ili wasaini mikataba ya kulifilisi taifa, hivyo wanaona ndoto zao zimeyeyuka.
Kuna kila dalili kwamba, mikono ya mafisadi hata sasa inaweza kutumika kukwamisha utendaji wa Muhongo, kwani hata watendaji wake wa chini wanaweza kutumika kumhujumu.
Hata hivyo, ni afadhali asiyeweza kazi, ama aliyeizowea kazi, akaondoka mwenyewe kwa sababu Tanzania ya sasa inahitaji mabadiliko chanya ya maendeleo ya kiuchumi na kijamii, ndoto ambazo zilipotezwa na tamaa ya baadhi ya watendaji waliopita.
Rais Magufuli ana makusudi yake, siyo maamuma, na tusubiri tuone kitakachotokea badala ya kulalamika na kwa wale wanaompinga Muhongo, naweza kuwaambia kwamba hawana namna zaidi kukubali matokeo kwani ‘msiyempenda kaja’!


0656-331974

No comments:

Post a Comment