Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Thursday 3 November 2016

WATAKIWA KUJIEPUSHA NA SIASA KATIKA KUJADILI MUSWADA WA HABARI


Na Mwandishi Wetu.
Dar es Salaam.
2.Nov.2016.

WADAU wa tasnia ya habari nchini wametakiwa kujiepusha  na itikadi za kisiasa kwa kisingizio cha ufinyu wa  muda katika kujadili muswada wa sheria ya huduma za habari kwa kuwa sheria si kitabu takatifu kisichoweza kufanyiwa marekebisho. 



Hayo yamesemwa leo Jijini Dar es Salaam na Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Antony Mtaka - pichani - wakati wa mahojiano maalum na mwandishi wa habari hizi.

Mtaka alisema Muswada wa Sheria ya Huduma za Habari ni mjadala wa miaka mingi ambao kwa kipindi kirefu wadau wa habari wakiwemo Wamiliki, Wahariri, vyama vya taaluma na waandishi wa habari wamekuwa  wakilumbana na Serikali pasipo kupatikana kwa suluhu ya kudumu.

Kwa mujibu wa Mtaka alisema Tanzania haitokuwa Nchi ya kwanza duniani  kutunga sheria na kuibadilisha, hivyo aliwataka wadau wa habari kutambua kuwa Serikali ina dhamira ya dhati ya kusaidia tasnia hiyo tofauti na tafsiri mbalimbali zinatolewa na wadau hao kuhusu muswada huo.

“Wanahabari wanapoujadili muswada huu, wanapaswa kuangalia leo na kesho kwani Serikali ilitoa kipindi kirefu cha kujadili na wadau waliwasilisha maoni yao, wasiwasi unatoka wapi kuhusu muswada huu” alisema Mtaka.

Aliongeza kuwa kabla ya muswada huo kuwasilishwa kwa mara ya kwanza Bungeni, baadhi ya wamiliki na wahariri wa vyombo mbalimbali vya habari walikuwa mafundi wa kuandika makala na tahariri zilizoishutumu Serikali kuwa inachelewesha muswada huo bila sababu za msingi.

Aidha ,Mtaka aliongeza kuwa kupatikana kwa sheria mpya itayotokana na muswada itasaidia kufutwa kwa sheria mbalimbali zinazoongoza tasnia hiyo ikiwemo sheria ya magazeti ya mwaka 1976 ambayo kwa kipindi kirefu imekuwa ikilalamikiwa na wadau wa habari kuwa ni sheria kandamizi kwa ustawi wa vyombo vya habari nchini.

Akizungumzia kuhusu Ibara ya 7 ya muswada huo inayozungumzia kuhusu Wajibu wa vyombo vya habari kutangaza na kuandika habari zinazohusu maslahi ya taifa, Mtaka alisema kipengele hicho hakikusudii kuminya uhuru wa vyombo binafsi vya habari.

Alisema kwa kuzingatia kuwa vyombo vya habari ni mhimili wa nne wa dola, ni wajibu wa taasisi za habari kutangaza na kuandika habari zinazozingatia maslahi ya nchi na wananchi kwa ujumla wake.

Kuhusu uhuru wa habari kutambuliwa katika Katiba ya nchi, Mtaka alisema wahariri na waandishi wa habari wamekuwa wakiitafsiri vibaya ibara ya 18 ya Katiba na kusahau Ibara ya 31 inayoeleza mipaka inayopaswa kuzingatiwa katika kutafuta, kupokea na kusambaza taarifa.

Kuhusu kipengele cha leseni kwa waandishi wa habari, Mtaka alisema wakati umefika kwa tasnia ya habari kuwa na heshima kama zilivyo taaluma nyingine ambazo wadau wake hupewa  leseni inayowawezesha kutambulika na Bodi za kitaaluma.

Mtaka alisema utaratibu huo ni vyema ukaanzia ndani ya vyombo vya habari vyenyewe ikiwemo nafasi ya Mhariri wa gazeti/televisheni au redio ni vyema awe na leseni ya kazi, hatua itayosaidia kuongezea hadhi na sifa ya tansia hiyo.

“Ukianzisha utaratibu kama huu, utasaidia kuongeza morali ya wanahabari sasa kwenda kusoma na hiyo itasaidia kuwaongezea weledi katika taaluma” alisema Mtaka.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Nanyumbu Mkoani Mtwara, Hamis Dambaya aliwataka wadau wa habari kufanya maridhiano ya pamoja na  Serikali badala ya kupinga muswada huo.

Alisema kwa muda mrefu muswada huo ulikuwa mikononi mwa wadau wa habari, ambao kwa kipindi kirefu wamekuwa wakilalamikia kukosekana chombo cha kusimamia taaluma hiyo, ambapo muswada  umependekeza kuanzishwa Baraza huru la Habari ambalo litasimamia haki, wajibu na miiko ya tasnia hiyo.

“Wadau hawatakiwi kuweka mikwamo pasipo na kufahamu mbele kuna nini, ni vyema sasa suala hili likafikia mwisho ili sheria iweze kutungwa na hatimaye tasnia ya habari ikapata hadhi na heshima kama zilivyo taaluma nyinge” alisema Dambaya.

No comments:

Post a Comment