Na Daniel Mbega
WIKI iliyopita nilikuwa napitia – kwa mara
nyingine – kitabu cha Confession of an
Economic Hit Man (Ushuhuda wa Mharibifu wa Kiuchumi) ambamo John Perkins,
Mmarekani ambaye alitumia sehemu kubwa ya maisha yake kufanya ulaghai wa
kijasusi kuhujumu uchumi wa mataifa mbalimbali, hasa ya Dunia ya Tatu.
Perkins anasema katika Dibaji: “Waharibifu ama wapigaji wa kiuchumi ni
wataalamu wanaolipwa fedha nyingi kuzihadaa nchi mbalimbali ulimwenguni na
kuvuna matrilioni ya dola. Wanachukua fedha nyingi kutoka Benki ya Dunia,
Shirika la Kimataifa la Misaada la Marekani (USAID), na mashirika mengine ya
‘misaada’ ya kimataifa na kuyaingiza taasisi kubwa na mifuko ya matajiri
wanaomiliki rasilimali za dunia hii. Silaha zao ni kuangalia ripoti za kifisadi
za fedha, chaguzi zenye utata, malipo yasiyo rasmi, utesaji, ngono, na mauaji.
Wanacheza mchezo wa kale ambao umekuwa kama himaya, lakini ambao umegeuka kuwa
wa kutisha hasa katika kipindi cha utandawazi.”
Yapo mengi ambayo anayazungumza, lakini
kubwa ni mbinu wanazotumia kuzirubuni nchi zinazoendelea (hii ikiwa na maana na
Tanzania) ili kuchota rasilimali zilizopo.
Perkins, ambaye alikuwa jasusi wa Shirika
la Kijasusi la Marekani (CIA), anasema mara nyingi wanachokifanya ni kwenda
kutoa misaada na mikopo kwa nchi hizo kwa kujenga miundombinu ya barabara,
viwanda, nishati na maeneo ya maegesho.
Mara nyingi, anasema, mambo wanayoyafanya
yanakuwa yale ambayo yatawasaidia matajiri wachache na siyo wananchi walio
wengi ambao hawapati umeme wala miundombinu mingine, kwa kifupi misaada hiyo
haiwasaidii wananchi walio wengi.
Anasema, misaada na mikopo hiyo 'yenye
masharti nafuu' kwa nchi hasa zenye utajiri wa rasilimali mbalimbali ikiwemo
mafuta, inakuwa mikubwa na madeni yanazidi kiasi kwamba nchi husika inashindwa
kulipa.
Ikishafikia hatua hiyo, anasema, wanarudi
hapo na kuwashawishi viongozi wakisema: "Tazama, deni hili ni kubwa,
hamuwezi kulilipa, tuachieni tuchimbe mafuta, madini au rasilimali nyingine
muhimu kufidia deni hilo kwa malipo madogo sana".
huwezi kuwatambua waharibifu hao wa
kiuchumi, kwa sababu ama wanaweza kuja kwa mgongo mwa Mashirika Yasiyo ya
Kiserikali ama maofisa waubalozi wanaofahamika kama Mwambata wa Kiuchumi
(Economic Attache).
Katika baadhi ya mataifa, wanaposhindwa
kufanikisha malengo yao kutokana na ugumu wa viongozi, wanaweza kuwatumia
harakati za vyombo vya habari kueneza propaganda kwamba serikali fulani haifai,
au la wanaweza ‘kuwapoteza’ (kuwaua) viongozi wanaoonekana kikwazo kwa
kuwatumia wauaji ambao wanafahamika kwa jina la ‘mbweha’ (jackals) ambao nao
huwa ubalozini kama maofisa wa usalama. Ikishindikana kabisa, basi hupeleka
majeshi katika mataifa hayo.
Mbinu hizi hazitumiwi na na CIA peke yake,
bali mataifa mengi yanafanya ujasusi wa aina hii wa kiuchumi kwa nia na
madhubuni ya kukomba rasilimali za mataifa yanayoendelea huku wakija na
kisingizio la misaada na mikopo kwa shughuli za maendeleo ya kijamii, mara
nyingi fedha hizo huwa hazitolewi taslimu.
Nilikuwa napitia mistari mbalimbali kwenye
kitabu hiki ndipo nikakumbuka kwamba deni la taifa hadi kufikia Desemba 2014 ni
Shs. 27.04 trilioni (Shs. 20.23 trilioni ni deni la nje na Shs. 6.81 trilioni
ni deni la ndani) ambapo kwa hesabu ya haraka, kila Mtanzania kati ya watu
milioni 45, haijalishi kama ni mtoto au mzee, anadaiwa Shs. 600,000/-.
Japokuwa serikali inajipa moyo kwamba deni
hilo asilimia 28, hivyo bado inakopesheka kwa kuwa kiwango cha ukomo wa kukopa
ni asilimia 50, bado inatia mashaka kama linaweza kulipwa leo au kesho.
Tanzania ni moja ya mataifa yanayoendelea
na yenye rasilimali nyingi ambazo kwa miaka mingi zinachotwa na kupelekwa nje
huku Watanzania wakiwa hawanufaiki na wakiendelea kuogelea katika dimbwi la
umaskini.
Mashirika yasiyo ya kiserikali (NGO) nayo
ni mengi mno Tanzania, yapo yanayojishughulisha moja kwa moja na jamii, lakini
yapo mengine ambayo kazi zao ni za kiharakati zaidi na hutegea kama kuna hoja
yenye kutatiza na kutoa matamko ama kuhamasisha wananchi wapinge.
Kwa sasa Tanzania imekuwa kivutio cha
uwekezaji kwa mataifa makubwa kama Marekani, Uingereza, China, India na
kadhalika.
Ugomvi mkubwa wa uwekezaji nchini Tanzania
ni baina ya Marekani na China, ambayo inakuja kasi sana.
Marekani, ambayo ilikuwa inaongoza kwa
uwekezaji, hivi sasa inashika nafasi ya tano nyuma ya Uingereza, China, India
na Kenya.
Hadi kufikia mwaka 2012, uwekezaji wa moja
kwa moja wa Marekani nchini Tanzania ulikuwa Dola 950 milioni, wakati Uingereza
ilikuwa inaongoza kwa kuwekeza jumla ya Dola 4.7 bilioni kutokana na makampuni
ya BG Group Plc lililojikita kwenye gesi asilia na mafuta pamoja na kampuni ya
SABMiller Plc, India ilikuwa imewekeza Dola 1.8 bilioni, wakati Kenya imewekeza
Dola 1.5 na China ilikuwa imewekeza Dola 1.4 bilioni.
Lakini kwa sasa, inaonekana China
inakaribia kuipita Uingereza kwenye uwekezaji kutokana na kuingia mikataba
mingi hivi karibuni.
Kwa mujibu wa takwimu kutoka Kituo cha
Uwekezaji Tanzania, hadi kufikia Agosti 2013, kulikuwa na kampuni 300 za
Kichina zilizowekeza moja kwa moja nchini Tanzania (Foreign Direct Investment)
katika maeneo ya miundombinu, kilimo, viwanda na ujasiriamali mdogo na wa kati
(SME) zote kwa pamoja zikiwa na mtaji wa zaidi ya Dola 2.1 bilioni.
Kampuni za Kichina zimepata mikataba mingi
ya ujenzi ambapo kwa mujibu wa taarifa kutoka Wakala wa Barabara nchini
(Tanroads), katika kipindi cha miaka 10 iliyopita, kampuni 14 kutoka China
zimeingia jumla ya mikataba 58 ya ujenzi wa kilometa 3,140.85 yenye thamani ya
Dola 1.75 bilioni.
Kwenye upande wa madini, hasa ya mkaa ya
mawe na chuma, China imeingia mkataba wa Dola 3 bilioni (takriban Shs. 6
trilioni) kupitia kampuni yake ya Sichuan Hongda ambao utadumu kwa zaidi ya
miaka 100.
Rasilimali kubwa za Tanzania ni madini na
maliasili (wanyama mwitu), lakini hivi sasa kuna suala kubwa la ugunduzi wa
mafuta na gesi.
Ukiacha madini kama dhahabu, almasi na
tanzanite ambayo yamechimbwa na kupelekwa nje kiasi cha kuacha mahandaki tele
huku wananchi wakiwa maskini, lakini kuna madini ya uranium ambayo ni muhimu
sana kiuchumi na tayari yamekwishaanza kuchimbwa na Serikali ya Urusi huko
Mkuju, wilayani Namtumbo.
Suala la mafuta na gesi linanifikirisha
sana nikirejea maelezo ya Perkins, kwani tangu mwaka 2013 tumeshuhudia mvutano
mkubwa baina ya Serikali na wawekezaji, hasa wa ndani, kuhusiana na suala la
vitalu.
Hili bado halijakaa sawa kwa sababu
serikali inashikilia msimamo wake wa kuwaalika wawekezai kutoka nje na kusema
wazawa hawana uwezo.
Kwa misingi ya mbinu za kijasusi za
waharibifu wa kiuchumi (economic hit men), suala la mafuta na gesi lina umuhimu
mkubwa kuliangalia kiusalama hasa tunapoelekea kwenye uchaguzi mkuu wa Oktoba
25, 2015.
Kama ushuhuda wa Perkins unavyosema,
Tanzania haiko salama kwa rasilimali zilizopo kwa sababu tunaamini kabisa
kwamba mataifa makubwa yanapigana vikumbo yenyewe kwa yenyewe kutaka kuwekeza
hapa.
Ni katika vikumbo hivyo ambamo wanaweza
kuwemo akina CIA, KGB na hata MI6 na wote wanapotajwa kuhusishwa na mambo
mazito kama haya, kauli mbiu yao inatofautiana kidogo, nayo ni Usikiri
Chochote, Kanusha Kila Kitu, Toa Tuhuma Nyingi (Admit Nothing, Deny Everything, Make Counter Accusations).
Mwaka 1982 ilishuhudiwa mabadiliko ya
uongozi yaliyofanyika nchini Australia ambayo yalifanikishwa zaidi na Benki ya
Nugan Hand. Hadithi yao na jinsi walivyouawa, haina nafasi leo hii hapa.
Lakini kuondolewa madarakani wa Hugo Chavez
wa Venezuela tunatambua kwamba ilikuwa ni vita ya mafuta.
Tanzania hatuwezi tukawa salama zaidi hasa
kama majasusi wa mataifa mengine watatumia harakati za uchaguzi mkuu wa mwaka
huu kutaka kupenyeza ‘watu wao’ watakaolinda maslahi yao ili wawekeze kwenye
mafuta na gesi.
Badala ya kushangilia umati mkubwa wa watu
kwenye mikutano ya Ukawa na Chama cha Mapinduzi, ni vyema vyombo vya usalama
vifanye jitihada za kuchunguza kama kuna chochote ama yeyote nyuma ya uchaguzi
huu, iwe kwa vyama ama wagombea mmoja mmoja.
Si mara moja au mara mbili tumewahi
kufutiwa madeni yetu ‘yasiyolipika’ na tukaendelea na ushirikiano na nchi
husika. Je, kuna chakula cha bure duniani au ndiyo mbinu anazozisema Perkins
kwamba wanafanya hivyo ili kuchota maliasili katika nchi zinazoendelea?
Uzalendo kwanza.
0656-331974
NB: Makala haya yalichapwa kwa mara ya kwanza na gazeti la WAJIBIKA la Septemba 14, 2015.
No comments:
Post a Comment