Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Wednesday, 13 May 2015

KUMBUKUMBU ZANGU: FIKE MAPUGILO ALIYEANZA NDONDI ZA KULIPWA AKIWA NA MIAKA 16!

Fike Mapugilo wakati anaingia kwenye masumbwi ya kulipwa mwaka 1991

NA DANIEL MBEGA
WENGI wanamfahamu kama Fike Wilson, lakini wakati anapanda ulingoni kwa mara ya kwanza kucheza ndondi za kulipwa kwa mara ya kwanza Jumanne Machi 19, 1991 dhidi ya Keith Mwila jijini Dar es Salaam wengi walimfahamu kwa jina la Fike Mapugilo. Hakuwa akilitumia zaidi jina la katikati la ‘Wilson’.

Lakini jina la Mapugilo ‘lilipotea’ mwaka 1997 alipoanza mashindano ya ‘Mr Tanzania’ na yeye akatwaa taji hilo jijini Dar es Salaam. 
 Fike mwenye bukta nyeusi mbele wakati akishiriki mashindano ya Mr Tanzania mwaka 1997.
Huyu alikuwa miongoni mwa mabondia wengi kutoka Kinondoni waliotamba enzi hizo na ambao walishindwa kuendelea na mchezo huo kutokana na ‘siasa’ zilizoingia baadaye pamoja na ukosefu wa udhamini kwenye masumbwi hayo ya kulipwa.
Unaweza kusema alicheza ndondi kwa miaka 15, lakini kwa hakika hakuwa akicheza mfululizo katika kipindi chote hicho, kwani rekodi zilizopo zinaonyesha kwamba alicheza mapambano 19 tu ya kulipwa akishinda 12 (8 kwa KO), akapoteza matano (matatu kwa KO) na kutoka sare mawili. Alicheza jumla ya raundi 104 na ushindi wake wa KO ni asilimia 42.11.
Fike Wilson mwenye urefu wa futi 5 na inchi 11½ (182 sentimeta), alizaliwa Oktoba 22, 1975 Mbeya na ndiyo maana mapambano yake mengi ya awali aliyechezea huko kwao.
Pambano lake la kwanza lilikuwa dhidi ya Keith Mwila kama nilivyoeleza hapo juu ambalo lilikuwa la raundi 6 na alishinda kwa pointi jijini Dar es Salaam.
Alipanda ulingoni mara ya pili Juni 15, 1991 kuzichapa na Salum Yazidu, pambano ambalo lilifanyika mjini Mbeya na akashinda kwa pointi katika raundi 8. Agosti 12, 1991 akapanda tena ulingoni mjini Mbeya kuzipiga na Sunny Mwakasala katika pambano la raundi sita na kushinda kwa pointi kabla ya kumtwanga kwa pointi Salum Yazidu kwa mara nyingi katika raundi sita Oktoba 18 mwaka huo huo mjini Kyela.
Pambano lake la kwanza dhidi ya bondia kutoka nje ya Tanzania lilifanyika mjini Mbeya Februari 18, 1992 dhidi ya Ngabo Foreman wa Zaire, ambapo alishinda kwa KO ya raundi ya 3 tu. Mwezi mmoja baadaye, yaani Machi 19, 1992 alipanda ulingoni kuzichapa na Abraham Mwitupa huko huko Mbeya na kwa mara nyingine akashinda kwa KO ya raundi ya 3. Oktoba 20, 1992 alimchapa kwa KO ya raundi ya 5 William Schula kwenye pambano lililofanyika Kyela.
Mei 12, 1993 alionja kipigo cha kwanza kutoka kwa bondia hatari wa Zambia enzi hizo, Charles Libondo ‘Mawe’ baada ya kupoteza pambano hilo la raundi 8 kwa pointi huko Mbeya.
Kwa hasira tu, alipopanda ulingoni Oktoba 25, 1993 alimchakaza kwa KO ya raundi ya 9 mpinzani wake Mnatija kwenye pambano lililokuwa la raundi 10. Baada ya hapo akapotea kwenye ulimwengu wa masumbwi na ndipo alipojikita katika mazoezi ya viungo, hasa ya utunishaji wa misuli, akiwa amefungua gym yake huko Mwananyamala na hatimaye kuanzisha mashindano ya utunishaji wa misuli, maarufu kama ‘Mr Tanzania’.
Miaka sita na nusu ikapita, hatimaye Fenruari 5, 2000 akarejea ulingoni kuzichapa na bondia Masoud Kambenga ambaye ndiyo kwanza alikuwa anaingia kwenye ndondi za kulipwa siku hiyo. Mapugilo alipoteza pambano hilo lililofanyika Dar es Salaam kwa KO ya raundi ya 3 tu.
Mei 12, 2000 akapanda ulingoni kutwangana na Meddie Serunjogi katika pambano la raundi 10 pale Diamond Jubilee jijini Dar es Salaam, lakini Mapugilo alishinda kwa KO ya raundi ya 3 na kuurejesha moto wake enzi zake katika uzani wa middle.
Akiwa ameiva kweli kimazoezi, Agosti 16, 2000 Mapugilo akamwaibisha bondia B Mwakasanga aliyeingia ngumi za kulipwa siku hiyo kwa kumtwanga kwa KO ya raundi ya 1 tu.
Hatimaye Novemba 5, 2000 akapanda ulingoni kuwania ubingwa wa taifa wa uzito wa middle unaotambuliwa na shirikisho la ndondi la TPBC akipambana na bondia mkongwe Said Yazidu, ambapo alishinda kwa pointi katika raundi 10 na kunyakua taji hilo.
Wakati sasa akiwa na miaka 26, mnamo Juni 11, 2001 Mapugilo alipambana na Abdallah Nyuki mjini Dar es Salaam katika pambano lisilo la ubingwa la raundi 10 na akashinda kwa KO ya raundi ya 8
Pambano lake la kwanza nje ya Tanzania lilifanyika Septemba 21, 2001 kwenye ukumbi wa Blue Horizon jijini Philadelphia, Pennsylvania, Marekani dhidi ya Ronald Boddie likiwa na raundi 4, ambapo Mapugilo alipigwa kwa KO katika dakika ya 1:39 ya raundi ya 3, mwamuzi akiwa Eddie Cotton.
Akarejea Dar es Salaam kwa hasira na kumtwanga kwa TKO Abdallah Nyuki katika raundi ya 8 kwenye pambano la raundi 10.
Akiwa anataka kujaribu bahati yake, Mapugilo alikwenda tena Marekani na Januari 12, 2002 alipanda ulingoni kwenye ukumbi wa Cox Pavilion jijini Las Vegas, Nevada kuzitwanga na Jeff Lacy katika pambano la raundi 6. Hata hivyo, akapoteza pambano hilo kwa TKO katika sekunde ya 50 ya raundi ya kwanza mbele ya mwamuzi Tony Weeks na majaji Robert Hoyle, Jerry Roth na Paul Smith.
Desemba 14, 2002 alipambana na Said Yazidu kuwania taji la taifa la uzani wa middle ambapo katika pambano hilo la raundi 10 lililofanyika kwenye ukumbi wa DDC Kariakoo jijini Dar es Salaam aliweza kushinda kwa pointi.
Pambano lake la mwisho kabisa kabla hajatundika glavu lilifanyika wakati wa Mwaka Mpya 2006 dhidi ya bondia Pascal Ndomba kwenye ukumbi wa New Vijana Social Hall, Dar es Salaam, likiwa la ubingwa wa super middle linalotambuliwa na TPBC, lakini mabondia hao walitoka sare.
Amewahi kuishi jijini Philadelphia, Pennsylvania, Marekani kwa miaka kadhaa kabla ya kurejea nchini, ambapo ameweza kuendelea kituo cha kuwafundisha vijana masumbwi na ukakamavu kiitwacho Fike Fitness Gym kilichoko Kinondoni, jijini Dar es Salaam.
 Fike Wilson Mapugilo alivyo hivi sasa
Hii ndiyo filamu ya Jamal

Mbali ya hayo, hivi sasa amejiingiza kwenye uigizaji wa filamu ambao filamu yake ya kwanza iliyotoka mwaka 2010 iliitwa ‘The Power of God’ na mwaka 2014 akaibuka na filamu nyingine iitwayo ‘Jamal’ ambayo ameshirikiana na mbabe mwingine Jimmy Mponda ‘Jay Plus’ na wasanii wengine kama Chrispin Kisinni, Ahmed Ulotu na wengineo.

No comments:

Post a Comment