Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Saturday, 18 July 2015

KOMBE LA KAGAME: NI MECHI YA 6 YANGA NA GOR MAHIA KAGAME


Na Daniel Mbega wa www.brotherdanny.com

MABINGWA wa soka Tanzania Bara, Yanga, leo wanafungua pazia la michuano ya Kombe la Kagame dhidi ya Gor Mahia ya Kenya, pambano ambalo linatarajiwa kuwa la kusisimua kutokana na ukongwe wa timu hizo katika historia ya kandanda Afrika Mashariki na Kati.

Hili litakuwa pambano lao la nane katika mashindano mbalimbali, lakini ni la sita katika Kombe la Kagame tangu zilipokutana mara ya kwanza mwaka 1975 kule Zanzibar.
Timu hizi ziliwahi kupambana mara mbili katika raundi ya kwanza ya Klabu Bingwa Afrika mwaka 1984 ambapo katika mchezo wa kwanza uliofanyika Dar es Salaam Aprili 7, zilitoshana nguvu kwa kufungana 1-1 na ziliporudiana mjini Nairobi Aprili 28, Yanga ikalala kwa mabao 2-1.
Hata hivyo, mechi yao ya kwanza iliiponza Yanga ikafungiwa na Shirikisho la Soka Afrika (CAF) kutoshiriki mashindano hayo kwa miaka mwili kwa madai ya kutoa rushwa kwa waamuzi kutoka Ethiopia na viongozi wake wawili, John Ketto na Julius Rutainurwa, wakafungiwa maisha kutojihusisha na soka.
Gor Mahia nayo mwaka huo ilifungiwa miaka miwili kutokana na wachezaji wake kumpiga mwamuzi wakati ilipocheza na Zamalek huko Cairo, Misri katika mchezo wa raundi ya pili ya Klabu Bingwa Afrika. Pia wachezaji sita wa Gor Mahia walifungiwa kwa mwaka mmoja, adhabu ambayo ilitambuliwa na CECAFA. Katibu Mkuu wa KFF naye alifungiwa na CAF kwa miaka miwili kutokana na kutuma teleksi kulikashfu Shirikisho hilo kwa kuiadhibu Gor Mahia.
Ukiachana na mechi hizo mbili, Yanga na Gor Mahia zimekutana mara tano kwenye mashindano haya ya Kagame, ambapo Gor imeshinda mechi tatu, kutoka sare moja na Yanga imeshinda mechi moja tu.
Zilikutana kwa mara ya kwanza katika nusu fainali mjini Zanzibar Januari 11, 1975 na Yanga ikashinda kwa mabao 2-0, ushindi ambao pia iliupata katika mechi ya fainali dhidi ya Simba.
Mwaka 1982 Yanga na Gor Mahia zilikuwa kwenye Kundi B mjini Kisumu, Kenya ambapo katika mechi ya kundi hilo, Gor ilishinda 3-1. Zilipokutana katika mechi ya kutafuta mshindi wa tatu, Gor ikashinda tena 2-1.
Mwaka 1996 timu hizo zilipangwa Kundi B mjini Mwanza. Katika mechi yao ya kwanza, zilifungana 1-1, lakini katika mechi ya kutafuta mshindi wa tatu, Gor ikashinda mabao 4-0.
Swali kwamba nani ataibuka mbabe katika mechi ya leo ndilo linalotawala na litaamuliwa na filimbi ya mwisho uwanjani.


No comments:

Post a Comment