Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Sunday 24 May 2015

UJUMBE KATIKA MUZIKI: FRANCO ANAKWAMBIA ‘LISOLO YA ADAMO NA NZAMBE’

Sikiliza kibao cha Lisolo ya Adamo Na Nzambe.
 
Ntesa Nzitani Dalienst
Franco


Na Daniel Mbega
HAPAN’SHAKA yoyote kwamba mnaendelea na majukumu yenu ya kila siku vyema kabisa huko mliko. Leo nawaletea kibao cha Lisolo ya Adamo na Nzambe, yaani ‘Mazungumzo ya Adam na Mungu’, upo hapo mwanakwetu?

Basi mwanangu, kibao hiki kiliimbwa na Ntesa Dalienst mwaka 1977 ndani ya Tout Puisant Orchestre Kinnie Jazz (T.P. O.K. Jazz) na kuimbwa naye L’Okanga La Ndju Pene Luambo Luanzo Makiadi, ukipenda unaweza kumwita Francis Makiadi, au Franco, mzaliwa wa Sona Bata katika Jimbo la Bas Congo nchini DRC mnamo Julai 6, 1938, ambaye hata hivyo alifariki dunia mjini Brussels, Ubelgiji Oktoba 12, 1989.
Jamaa huyu ndiye mtu pekee aliyeitangaza sana Afrika kupitia muziki na akawafanya Wazungu waukubali muziki wa Kiafrika badala ya kuendelea na kasumba yao ya kuziita tamaduni zetu eti za kishenzi!
Hata hivyo, leo nimeuchomoa wimbo huu wa Lisolo ya Adamo na Nzambe (yaani Mazungumzo ya Adam na Mungu) kwenye albamu yake iitwayo OK Jazz Volume 3, iliyotolewa katika ‘lebo’ ya African Sonodisc mwaka 1977, ambayo pia ilikuwa na nyimbo nyingine kama Mbongo, Lotambe, Badjekate, Tambwe Lutandila na Moleka Okoniokolo Ngai Ntina.
Basi katika kibao hiki Franco, ambaye pia ameshiriki kupiga gitaa la solo, ameshirikiana na akina Mavatiku Visi maarufu kama Michelino aliyekuwa akipiga gitaa la solo, Lutumba Massiya Simaro, Josky Kiambukuta Londa, na wengineo wengi waliokuwa wakiunda kundi zima la Tout Puisant Orchestre Kinnie – yaani TP OK Jazz, unanipata lakini? Tozali moko baninga na bandeko na ngai?
Wimbo huu umeimbwa Kilingala, lakini mimi nimeutafsiri wote ili uweze kuupata ujumbe wake. Kama unataka kuusikiliza, tafuta CD, kaseti au LP.
Yanayosemwa na Franco ni mambo ya kweli kabisa yanayotokea katika maisha ya kila siku ya mwanadamu. Anazungumzia namna binadaamu alivyogeuka na kumwacha Mungu, na sasa anafanya mambo ya ajabu yanayomkasirisha muumba.
Yeye anaanza kwa kusema; “Eva aliumbwa kutoka ubavuni mwa Adam, Adam aliliona jua kabla yake, Adam alizungumza na Mungu kabla yake, Alizungumza pia kuhusu shetani? Lakini Biblia… Sikumbuki mlango wa ngapi, Imekuwaje mwanamke awe shetani anayewaangamiza wanaume? Nani aliyetufundisha ushetani huu? Utasema Eva alikuwa wa kwanza kula tunda haramu, Nani alimpa Eva tunda hilo? Ulijifunza kwamba Malaika wa kike, Aligombana na Mungu, Ili akuumize wewe? Wanaume, ninyi ndio matatizo yenu na wanaume wenzenu…”
Umeyasikia sana hayo ndugu yangu? Basi ndivyo Franco anavyoanza kueleza. Ni kweli kabisa, wanaume ndiyo chanzo cha matatizo, hata kama tutawalaumu wanawake. Mwanamume ndiye anayeanza kumchokoza mwanamke, lakini ni nadra sana kumkuta mwanamke anamtongoza mwanamume, hasa kwa mila zetu za Kiafrika, na kama itatokea hivyo unaweza kusema kwamba mwanamke huyo ana kasoro au malaya! Siyo kweli hata hivyo kwa sababu sote tunazo hisia za kutamani, kupenda na hata kuchukia.
Lakini ushetani wa wanaume uko dhahiri, kama unabisha hebu sikiliza hapa; “Unamtazama mke wa jirani yako, Unataka kumtongoza, Unamtazama binti ya jirani yako, Unaanza kummendea, Mkeo anapoanza kutongozwa, Unakimbilia kwa majiji, Unataka wapatikane na hatia.”
Sasa ndugu yangu umesikia hivyo? Mambo haya hayatokei kwenye jamii zetu jamani? Ni wangapi walioripotiwa na magazeti kwamba wamefumaniwa, ama na wake za watu au vibinti vya watu? Jiulize, wanawake hao, ama mabinti hao, ndio waliowatongoza wanaume hao?
Utakuta wanaume wengine hata soni hawana. Kusaidiana ni jambo la kawaida katika jamii, lakini akiombwa msaada na mke wa jirani yake, au hata binti wa jirani yake, basi yeye anataka alipwe fadhila, na si fadhila nyingine zaidi ya ngono!
Franco anasema; “Ukimuona mke wa jirani yako mwache aende…mwache aende, Ukimuona mtoto wa jirani yako mwache aende …mwache aende, kumbuka kwamba wewe pia una mke na watoto, Kumbuka kwamba hili ni tatizo la rafiki yako pia.”
Swadakta kabisa. Hiyo ndiyo kuntu nturuba haswa. Yale unayoyafanya na wenzako wanafanyiwa ama wanayafanya. Matatizo kama hayo yatakukuta na wewe pia, kwa maana nyingine, ni matatizo ya jamii nzima na mtu mwenye kuyakomesha ni wewe na mimi.
Watu wengine hawana huruma hata kidogo. Wako tayari kuwanyanyasa jirani zao bila aibu, kwa kuwa tu wao wamebahatika kuwa na hali fulani. Kwa kutumia uwezo alionao, anataka afanye ufirauni kadiri apendavyo.
“Mtoto wa jirani yako, Aliyeumbwa mamchoni pako, Mtoto wa jirani yako, Aliyekua machoni pako, Kwa kuw amatiti yake yamekua, Unamtamani na kutaka kumuoa, Huna aibu?”
Wanadamu wengine bwana, eti wakishapata mali wanataka kujibadili kama kinyonga. Wanataka wawapate wanawake wote wazuri. Wanaanza kuwadharau hata wanawake wao, ambao wamepigana pamoja mpaka kuweza kupata mali hizo.
“Wakati ulipokuwa maskini, Ulioa mwanamke mbaya, Kwa kuwa sasa ni tajiri, Unaanza kutamani wanawake warembo, Kwanza mfukuze mwanamke mbaya, ndipo uoe mwanamke mrembo… Leo unamiliki Mercedes, Unasema unataka mwanamke anayezungumza Kifaransa, Mke wako, wakati ulipomuoa, Hukujua kwamba unaweza kuwa tajiri siku moja, Tazama mambo yanavyoweza kutokea, Hatutaki hivyo..”
Lakini kwa kuwa watu hawa tunao katika jamii zetu, tunapaswa kuwaambia ukweli; “Acha unafiki wako wa kizamani, Tunakufaahamu, Mheshimu mke wa jirani yako, Acha kuwa mnafiki, Rafiki zako wanakujua, Acha kukataa… Waache wake za wale unaofanya nao kazi kampuni moja, Wote wanafahamu kwamba wewe unawatamani wake zao, Lakini waache, waache, Acha wake za rafiki zako…
“Kwako wewe, wanawake wazuri wanaweza kununuliwa kwa fedha, Rafiki zako wameoa wanawake wazuri, Wakati walipokuwa katika hali nzuri, Leo unadhani unaweza kuwaumiza watu, Kwa kuwa una fedha… Haya macho yako, unatamani wake wa wenzako, Yatang’olewa siku moja, Haya macho yako, unatamani binti za wenzako, Yatang’olewa siku moja, Jihadhari na wanawake wa wenzako, Jihadhari na binti za wenzako, Unajitafutia matatizo…”
Mwasikia sana bandugu? Kibao hiki ni kitamu sana kinachezeka katika ule mtindo wa rhumba, miziki ya bakulutu, lakini ujumbe uliomo ni mzito na unatakiwa kuzama.
Shairi ni refu sana na nimelazimika kunyofoa baadhi ya beti. Si mnamfahamu mzee mzima jinsi alivyokuwa akitunga nyimbo ndefu? Muziki ukipigwa unaweza kusinzia, ukiamka unakuta muziki unaendelea.
Tukutane tena Jumapili ijayo, ni kila Jumapili!

Mnaweza kunitumia mchango wenu kwa sms ama kunipigia kupitia kilongalonga – 0715 – 070 109, Whatsapp/Telegram 0656-331 974 au barua-pepe: brotherdanny5@gmail.com.


No comments:

Post a Comment