Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Wednesday, 13 May 2015

MAPINDUZI YA NKURUNZIZA KAMA YA OBOTE UGANDA 1971, WOTE WALIKUWA NJE YA NCHI

Rais Pierre Nkurunziza.

 
Wanajeshi wakipongezwa na wananchi baada ya kupindua serikali ya Burundi.
Kiongozi wa ''Mapinduzi'' ya Burundi, Meja Jenerali Godefroid Niyombare
Apollo Milton Obote
Jenerali Idi Amin Dada

Na Daniel Mbega, Mwanza
JUMATANO Mei 13, 2015 majira ya saa 9 alasiri, Meja Jenerali Godefroid Niyombare, aliongoza ‘mapinduzi’ ya kijeshi dhidi ya Rais Pierre Nkurunziza ikiwa ni hatua ya kuunga mkono nguvu ya umma kupinga kusudio la rais huyo kujiongezea muhula wa tatu wa kuwa madarakani kinyume cha katiba ya nchi hiyo.
Wakati mapinduzi hayo yakifanyika, Rais Nkurunziza mwenyewe alikuwa jijini Dar es Salaam katika kikao cha wakuu wa nchi za Afrika Mashariki waliotaka kutafuta suluhu ya kumaliza mgogoro huo ambao umeacha majeraha makubwa kwa Warundi, huku baadhi wakiwa wamepoteza maisha kufuatia kushambuliwa na polisi wakati wakifanya maandamano.
Tukio hili linanikumbusha lile la Januari 25, 1971 nchini Uganda ambalo liliongozwa na Jenerali Idi Amin Dada likiwa ni sehemu ya Vita Baridi, ambalo lilifanikiwa kumuondoa madarakani Apolo Milton Obote na kuuweka utawala wa kidikteta wa Amin.
Jenerali Amin alikuwa anaungwa mkono na Uingereza na Israel, ingawa Waisraeli nao walionja joto ya jiwe baada ya kibaraka wao huyo kuwateka raia wa Israel kabla ya vikosi vya kijasusi kutoka Mossad havijaenda kuwakomboa kwenye Uwanja wa Ndege wa Entebbe.
Kama ilivyotokea Burundi, wakati mapinduzi yakitokea kule Uganda mwaka huo, Obote alikuwa Singapore akihudhuria mkutano wa Wakuu wa Nchi za Jumuiya ya Madola, ikabidi akimbilie jijini Dar es Salaam kupata hifadhi.
Uingereza ilimuunga mkono Amin kwa sababu Obote alitaka kutaifisha biashara zote zilizokuwa zikifanywa na Waingereza, huku Amin naye akihofia kufukuzwa kazi mara baada ya Obote kurejea kwani kulikuwa na mtazamo tofauti kati ya utawala wa serikali kuu na jeshi.
Obote alirejea madarakani mwaka 1980, lakini Julai 27, 1985 akapinduliwa tena katika mapinduzi yaliyoongozwa na Brigedia Bazilio Olara-Okello. Marais wengine waliokuwa wamepinduliwa Uganda ni Yussuf Lule aliyetawala kati ya Aprili 13 ha Juni 1979 (siku 70) baada ya majeshi ya Tanzania kuung’oa utawala wa Nduli Idi Amin; Godfrey Binaisa akatawala kati ya Juni 20 1979 hadi Mei 12, 1980 (siku 327); Paulo Muwanga akatawala kwa siku 10 tu kati ya Mei 12 na Mei 22, 1980 kabla ya kujiuzulu na kuipisha Tume Maalum ya Urais kuongoza kwa siku 207 na hatimaye kumkabidhi Obote madaraka.
Kihistoria, hali ya kisiasa ya Burundi haina nafuu wala afadhali kwani kumekuwepo na Vita vya Wenyewe kwa Wenyewe kwa miaka mingi na hasa baada ya uhuru uliopatikana mwaka 1962. Hii yote ni kwa sababu ya migogoro ya kikabila baina ya Watutsi walio wachache wanaotawala na Wahutu walio wengi wanaokataa kutawaliwa.
Rekodi zinaonyesha kwamba vita vya wenyewe kwa wenyewe nchini humo vilipamba moto kati ya mwaka 1993 hadi 2005. Mgogoro ulianza mara baada ya uchaguzi mkuu wa vyama vingi nchini humo tangu ilipopata uhuru kutoka kwa Wabelgiji, na wengi walitarajia kwamba, baada ya kuapishwa kwa Pierre Nkurunziza Agosti 2005, huenda ndio ungekuwa mwisho wa yote, lakini hali imekuwa tofauti.
Kabla ya ukoloni, Burundi iliongozwa na utawala wa kifalme wa Kitutsi kama ilivyokuwa kwa Rwanda. Wabelgiji na Wajerumani waliona ni afadhali kuongoza kupitia utawala uliokuwepo ambao tayari Watutsi walikuwa wanawakandamiza Wahutu. Hii iliwajengea kiburi Watutsi na kujiona kwamba wana haki ya kutawala na siyo kutawaliwa!
Tofauti na Rwanda, Burundi iliamua kuendelea na utawala wa kifalme mara baada ya kupata uhuru, ingawa kwa miaka takriban 25 jeshi lililoongozwa na Watutsi ndilo limekuwa likitawala kwa nguvu kabla ya uchaguzi wa kidemokrasia wa Juni 27, 1993. Uchaguzi huo ulirejesha kumbukumbu za miaka 25 nyuma wakati Michel Micombero alipoongoza mapinduzi mwaka 1966 na kuuondoa ufalme na badala yake akaifanya Burundi kuwa Jamhuri.
Chini ya utawala wa Micombero, Watutsi wachache walijaa kwenye vyeo karibu vyote muhimu vya serikali. Mwaka 1972 kundi la Wahutu lililofahamika kama Umugambwe w'Abakozi b'Uburundi au Chama cha Wafanyakazi Burundi (UBU) kiliandaa na kufanya mashambulizi kadhaa dhidi ya Watutsi, kwa lengo la kulimaliza kabisa kabila hilo. Lakini jeshi la Watutsi likawashambulia Wahutu kwa silaha kali na hakuna idadi kamili ya Wahutu waliouawa iliyopata kurekodiwa ingawa makadirio yanaonyesha kwamba Warundi wote waliokufa walikuwa takriban 100,000. Warundi wengi wakakimbilia Tanzania na Rwanda, ambapo baadhi yao tayari wamekwishapewa uraia wa Tanzania.
Mapinduzi ya mwisho kabla haya ya sasa yalifanyika mwaka 1987 na kumuweka madarakani ofisa wa jeshi wa Kitutsi Meja Pierre Buyoya ambaye alijaribu kubadilisha baadhi ya mambo na kuweka mjadala wa kitaifa, lakini badala yake hali hiyo ikachochea mgogoro wa kikabila.
Mapigano yakaibuka sehemu mbalimbali ambapo makundi ya Wahuti yaliwashambulia na kuua mamia ya Watutsi, Buyoya akatuma jeshi kuwaua maelfu ya Wahutu.
Oktoba 21, 1993, rais wa kwanza wa Burundi aliyechaguliwa kidemokrasia akitokea kabila la Wahutu, Melchior Ndadaye, aliuawa na waasi wa Kitutsi na kuzusha mapigano ya wenyewe kwa wenyewe ambayo yalisababisha watu kati ya 50,000 hadi 100,000 kuuawa ndani ya mwaka mmoja. Rais aliyefuata baadaye, Cyprien Ntaryamira, ambaye naye alikuwa Mhutu, aliuawa kwenye ajali ya ndege pamoja na Rais wa Rwanda, Mhutu Juvenal Habyarimana, wakati wakitokea Dar es Salaam.
Hata alipoteuliwa Sylvestre Ntibantunganya Aprili 8, 1994, hali haikuweza kutulia Burundi. Nakumbuka Mwalimu Julius Nyerere ndiye aliyeteuliwa na Umoja wa Mataifa kuwa msuluhishi wa mgogoro wa Burundi na alijitahidi sana ambapo matokeo yake ni Wahutu na Watutsi kufikia muafaka wa kuwa na serikali ya mseto mwaka 1996.
Mwaka 1996, Mtutsi Meja Pierre Buyoya akachukua madaraka akimpindua Mhutu Ndibantunganya. Mwaka 1998, Buyoya na Bunge lililoongozwa na Wahutu walikubaliana kusaini katiba ya mpito na Buyoya akaapishwa kuwa rais. Mazungumzo ya amani ya Burundi yakaanza rasmi mjini Arusha Juni 15, 1998.
Baada ya kifo cha Mwalimu Nyerere, Mzee Nelson Mandela ndiye aliyeshika mikoba ya upatanishi wa Burundi na mwaka 2000 mazungumzo yakafanyika nchini Tanzania na kufikia makubaliano ya kuunda serikali ya mpito ambapo rais na makamu wa rais wangebadilisha vyeo kila baada ya miezi 18.
Wakati ambapo serikali na vyama vitatu vya Kitutsi vilisaini makubaliano hayo, vyama viwili vikuu vya Kihutu viligoma kushiriki, na mapigano yakaendelea. Mkutano wa amani mjini Arusha Novemba 30, 2000 ulifungwa bila mafanikio.
Aprili 18, 2001, jaribu la mapinduzi lilishindika. Hata hivyo, mnamo Aprili 9, 2003 makao makuu ya Jeshi la Umoja wa Afrika nchini Burundi yalifunguliwa jijini Bujumbura chini ya Meja Jenerali Sipho Binda wa Afrika Kusini. Hadi kufikia Oktoba 18, 2003, ilielezwa kwamba jeshi hilo lilikuwa limejiimarisha zaidi likiwa na wanajeshi 1,483 kutoka Afrika Kusini, Waethiopia 820, na 232 kutoka Msumbiji.
Mnamo Julai 2003, mashambulio ya waasi yaliua watu 300 na kuwaacha watu 15,000 wakiwa hawana makazi. Lakini ni mwezi huo ambao Mhutu Domitien Ndayizeye alipotwaa madaraka ya urais katika serikali ya mpito, na Buyoya akang’atuka. Pamoja na kikundi kikuu cha waasi cha Wahutu - National Council for the Defense of Democracy–Forces for the Defense of Democracy (FDD) - Rais Ndayizeye akasaini makubaliano ya kumaliza mapigano kwenye Mkutano wa Wakuu wa Nchi za Afrika uliofanyika jijini Arusha, Tanzania mwezi Novemba 2003. Chini ya makubaliano hayo, FDD kikawa chama cha siasa, na ikaamuliwa kwamba, wanamgambo wote wa Kihutu waingizwe kwenye jeshi la nchi hiyo lililokuwa limesheheni Watutsi watupu.

HISTORIA YA MATUKIO KATIKA BURUNDI

Wakati wa ukoloni
1890: Wajerumani waliitwaa Ruanda na Urundi (Burundi) pamoja na Tanganyika na kuifanya koloni lao waliloliita German East Africa chini ya Carl Peters.
1919: Wajerumani walipotea Ruanda-Urundi kwa Ubelgiji chini ya Udhamini wa Ligi ya Mataifa. Wajerumani na Wabelgiji wote walitawala kupitia mfumo wa kijadi wa Watutsi ulioongozwa na Mwami.
1950: Ubelgiji iliunda serikali ya ndani kuwaandaa Wanyarwanda na Warundi kwa ajili ya kujitawala.
1950: Mtutsi Prince Louis Rwagasore alianzisha chama cha siasa katika mfumo wa vyama vingi, kilichoitwa Union for National Progress (UPRONA).

Uhuru
1962: Prince Rwagasore aliuawa, lakini chama chake cha UPRONA kiliongoza serikali ya kwanza kwa ushirikiano wa Mfalme Mwambutsa IV.
1965: Utawala wa kijadili ulianguka katika uchaguzi wa kwanza baada ya wanasiasa wa Kihutu kushinda kwa wingi na kuongoza mabunge yote. Mfalme Mwambutsa alivunja bunge kabla halijakutana na jeshi lililojaa Wahutu likaasi. Jaribu la mapinduzi la jeshi hilo lilizuiliwa na maofisa wa jeshi wa Kitutsi wakiongozwa na Michel Micombero. Mfalme Mwambutsa IV akakimbia nchi na mwanawe Ntare V akatawazwa. Micombero alimwondoa Ntare maarakani na kuamrisha mashambulizi yaliyosababisha vifo vya Wahutu 5,000.
1969: Kulikuwa na harakati nyingi za Wahutu wasomi.
1972: Idi Amin wa Uganda alimsaidia Micombero kumkamata Ntare V (ambaye baadaye alikufa akiwa gerezani nchini Burundi. Akihusisha machafuko yaliyosababisha vifo vya maofisa 2,000 wa jeshi wa Kitutsi, Micombero akaanzisha utawala wa mkono wa chuma (martial law). Wahutu wasomi ndio waliokuwa walengwa na kati ya 80,000 na 500,000 waliuawa, wakati zaidi ya Wahutu 100,000 walikimbia nchi na hawakurudi tena. Wakati huo, Ufaransa, China na Libya ziliongeza msaada wa kijeshi kwa serikali ya Burundi, na ripoti ya kadhaa zinasema kulikuwa na ukiukwaji mkubwa wa haki za binadamu kwa raia wa Kihutu.
1974: Micombero aliifanyia marekebisho katiba na kuifanya nchi ya chama kimoja chini ya UPRONA.
1975: Japokuwa Kamisheni ya Haki za Binadamu ya Umoja wa Mataifa ilifungua mashtaka dhidi ya viongozi wa Burundi kuhusu unyanyasaji dhidi ya Wahutu, baadaye kesi hiyo ilitupiliwa mbali.
1976: Micombero alipinduliwa katika mapinduzi ya kijeshi yaliyoongozwa na Kanali Jean-Baptiste Bagaza, lakini madaraka yakaendelea kubaki wa Watutsi waliojaa kwenye vyeo vya juu vya jeshi, watumishi wa umma na UPRONA.
1985: Bagaza alipanua wigo dhidi ya wapinzani wa serikali na kuliongeza Kanisa Katoliki kwenye mamlaka.
1987: Bagaza alipinduliwa na Pierre Buyoya katika mapinduzi mengine ya kijeshi.
1988: Kulikuwa na machafuko makubwa wakati jeshi lilipowaua Wahutu 25,000 kama kisasi kwa mauaji ya baadhi ya Watutsi kaskazini mwa nchi hiyo. Takriban Wahutu 60,000 walikimbilia Rwanda na wengine 100,000 wakakosa mahali pa kuishi nchini Burundi.
1991: Chama cha Mapinduzi ya Ukombozi wa Wahutu – The Revolutionary Party for the Liberation of the Hutu People (PALIPEHUTU) – kilianzisha mashambulizi zaidi, na kuanzisha mapambano mapya.
1991: Buyoya aliongeza ushiriki wa Wahutu kwenye serikali. Japokuwa Wahutu walijaa kwenye nafasi za uwaziri, mamlaka ya mwisho yalibaki kwa Kamati ya Kijeshi ya Wokovu ya Taifa iliyokuwa na Watutsi.
1992: Katiba mpya ikafungua milango kwa uchaguzi wa vyama vingi.
1993: Uchaguzi ulishindwa kufanyika wakati machafuko makubwa yalipoibuka. Karibu wakimbizi 175,000 walikimbilia Rwanda.
Februari 1995: Mkutano wa OAU kufanyika kwa mara ya kwanza kabisa jijini Bujumbura kuzungumzia hali ya wakimbizi walioko Rwanda.
1995/09/09: Mkutano wa pilia wa OAU kufanyika Bujumbura kuzungumzia tatizo la wakimbizi walioko Rwanda.
*Imeandaliwa na www.brotherdanny.com (Ukiichota usiache kuonyesha chanzo).

No comments:

Post a Comment