Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Saturday, 4 October 2014

UJANGILI NI UJAMBAZI, ASEMA OLE MEING’ATAKI!

Baadhi ya wadau wakiwa wameshikilia bango baada ya maandamano hayo.
Kaimu Mhifadhi Ruaha, Paul Banga.
Mratibu wa SPANEST, Godwell Ole Meing'ataki
Waziri Kivuli wa Maliasili na Utalii, Mchungaji Peter Msigwa (MP Chadema)
Katibu Tawala Msaidizi Mkoa wa Iringa, Adam Swai
Burudani pia zilikuwepo

Katika picha ya pamoja (Picha zote kwa hisani ya BongoLeaks Blog)

Na Daniel Mbega, Iringa
MRATIBU wa Mradi wa Kuboresha Mtandao wa Maeneneo Yaliyohifadhiwa Kusini mwa Tanzania (Spanest), Godwell Ole Meing’ataki, amesema ujangili ni ujambazi na kwamba unapaswa udhibitiwe kama ilivyo kwa uhalifu wa ujambazi ikiwa kweli kuna dhamira ya dhati ya kuutokomeza.
Akizungumza katika kilele cha maadhimisho ya Siku ya Maandamano ya Tembo na Faru duniani, ambayo kimkoa yamefanyika mjini Iringa leo hii, Ole Meing’ataki amesema ujangili wa tembo na faru haupaswi kufumbiwa macho na akatoa rai kwa vyombo vya dola na Watanzania kwa ujumla kuunganisha nguvu kuwashughulikia wahusika.
“Wahusika wa ujangili ni Watanzania wenzetu, ndugu zetu na majirani zetu, baadhi yawezekana wananchi wanawajua, hivyo ni jukumu la kila mmoja wetu kuhakikisha vitendo hivi vinakomeshwa ili maliasili hizi, ambazo ni urithi wa bure kutoka kwe Mungu, ziweze kuwanufaisha wananchi wote,” alisema.
Akaongeza: “Pembe za ndovu na faru hazipatikani mijini, haziuzwi Iringa wala Dar es Salaam, zinapatika porini – vijijini, na wahusika wote wanatumia barabara zetu, bandari zetu na hata viwanja vyetu vya ndege kusafirisha, lakini wanashirikiana na Watanzania wenzetu kwa ubinafsi tu.”
Ole Meing’ataki amesema, vijana walioko vijijini, ambao mara nyingi ndio wanaohusika na uuaji wa tembo na faru, wanapaswa kupatiwa elimu na kutambua madhara ya ujangili na kujua umuhimu wa maliasili hizi kuwanufaisha wote, hivyo Spanest kwa kushirikiana na wadau wengine wataendelea na program zao za kutoa elimu vijijini ili maliasili hizo zilindwe kwa faida ya kizazi cha sasa na kijacho.
“Tunatambua kwamba kuna tatizo la ajira nchini na duniani kwa ujumla, lakini ujangili usiwe mbadala wa ajira hizo kwa sababu kadiri wanyama hawa adhimu wanavyouawa Taifa linapoteza rasilimali na mapato kwani hatutaweza kupata wageni ambao ndio wanaotuingizia fedha za kigeni,” amesema.
Spanest ni mradi wa kuimarisha utalii nchini ambao uko chini ya udhamini wa Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP), Mfuko wa Kimataifa (GF) pamoja na Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (Tanapa) ambapo linafanya shughuli zake katika mikoa mitatu ya Nyanda za Juu Kusini mwa Tanzania – Iringa, Njombe na Mbeya.
Maandamano na maadhimisho hayo yameandaliwa na kuratibiwa na shirika binafsi la Wildlife Connection lenye makao yake makuu Tungamalenga wilayani Iringa, ambapo limeshirikisha wadau mbalimbali wa maliasili na utalii mkoani humo.
Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dk. Christine Ishengoma, amesema lengo la maandamano hayo ni kuujulisha umma juu ya tatizo la mauaji yanayowakabili wanyama hao ambao ni muhimu katika uhifadhi na utalii.
Katika hotuba yake iliyosomwa kwa niaba yake na Katibu Tawala Msaidizi, Adam Swai, Dk. Ishengoma amesema faida ya wanyamapori nchini ni kubwa hasa kupitia sekta ya utalii ambayo inachangia takriban 17% ya pato la Taifa na kuingiza zaidi ya 21% ya fedha za kigeni.
“Mkoa wa Iringa una bahati ya kuwa na hifadhi za taifa zenye tembo wengi hasa Ruaha na Udzungwa, hivyo maandamano haya yanafanyika kwa kutambua hali halisi ya ujangili katika hifadhi hizi na pia kuunga mkono jitihada zinazofanywa na wadau mbalimbali pamoja na wananchi katika kukabiliana na ujangili,” amsema.
Amewapongeza wadau wanaojishughulisha na utalii, uhifadhi na utafiti kama vile Wildlife Conservation Society, Carnivore Project, HALI Project, Southern Tanzania Elephant Research Project, WWF, PAMS Foundation, Friends of Ruaha na wengineo kwa jitihada kubwa wanazozifanya na kuwataka waendelee vivyo hivyo.
Aidha, aliwapongeza Wildlife Connection walioandaa na kuratibu maandamano hayo akisema hiyo imewapa nafasi ya kuungana na jumuiya ya kimataifa katika kupiga vita ujangili wa tembo na faru.
Awali, Naibu Mkurugenzi wa shirika la Wildlife Connection, Julius Mbuta, alisema pamoja na jitihada zinazofanywa na serikali katika kutokomeza ujangili, lakini mapambano dhidi ya ujangili yanapaswa kuhusisha wadau wote wakiwemo wananchi wa kawaida.
“Sisi katika kupambana na ujangili tumekuwa tukiwaelimisha wananchi hasa wanaozunguka Hifadhi ya Taifa ya Ruaha kuhusu umuhimu wa kuwatunza wanyama hao ambao ni tunu kutoka kwa Mungu na wanatuletea faida kubwa kama taifa,” alisema. “Tunafanya hivyo kwa kushirikiana na uongozi wa Hifadhi ya Jamii ya Mbomipa na tumeanzisha maktaba mbili katika eneo hilo ili wanafunzi wapate fursa ya kujisomea na kujifunza umuhimu wa kuhifadhi maliasili.”
Ameongeza kwamba, katika kukabiliana na migogoro ya wananchi na wanyama, hasa tembo, wanaovamia makazi na mashamba, wameanzisha mradi wa ufugaji wa nyuki ambapo hutandaza mizinga mipakani ili kuwazuia tembo wasivamie mashamba na makazi.
“Tumeunda kikundi cha watu watano na tumeanza na mizinga 120. Kwa kuwa tembo anaogopa nyuki, tunaamini ufugaji huu wa nyuki utasaidia kuwauia tembo wasilete uharibifu kwa jamii, lakini wakati huo huo wanajamii wakipata faida katika mradi huo,” alisema.
Mbunge wa Jimbo la Iringa Mjini, Mchungaji Peter Msigwa, ambaye pia ni Waziri Kivuli wa Maliasili na Utalii, amesema suala la kulinda maliasili ni la kila Mtanzania kwa mujibu wa Katiba na akawataka wananchi wote kushiriki kikamilifu katika kupambana na kuwafichua majangili wote.
Amesema maliasili zinakuza uchumi wa taifa na kwamba mapambano dhidi ya ujangili hayapaswi kuchukuliwa kisiasa kwa kuwa yatadidimiza uchumi.
“Siasa haiwezi kutenganishwa na uchumi, maliasili hizi ndizo zinazokuza uchumi wetu kwa kuleta fedha nyingi za kigeni, leo hii kama tusingekuwa na tembo kamwe hawa Wazungu wasingeweza kuja kwetu, lazima tushikamane pamoja kuutokomeza ujangili,” alisema.
Hata hivyo, pamoja na kuunga mkono jitihada za serikali katika kupambana na ujangili, amesema nivyema elimu ikatolewa kwa Watanzania wote huku wananchi wa vijijini wakipewa kipaumbele kwani ndio wahusika na washirika wakubwa.
“Wanaoua tembo ni Watanzania wenzetu – hata kama wanatumwa na Wachina. Hakuna Mchina hata mmoja anayekwenda porini kuua tembo wetu, vijana wetu ndio wanaoshika magobore, hivyo lazima elimu ikatolewa kwao kujua umuhimu wa kuwatunza wanyama hawa,” alisema.
Aidha, aliitaka serikali kutekeleza Azimio la Kimataifa kuhusu Mpango wa Kulinda Tembo lililotolewa jijini London, Uingereza mwezi Februari 2014 ambalo liliagiza ufanyike ukaguzi wa wazi wa meno ya tembo na kutambua meno yaliyopatikana kihalali na kinyume cha sheria, kisha kuyateketeza hadharani yale yaliyopatikana kiharamu kama wanavyofanya China, Hong Kong na Vietnam.
“Iliagizwa pia kwamba, shehena zote za meno ya tembo kuanzia gramu 500 lazima zipimwe vinasaba (DNA) pindi zinapokamatwa ili kujua wapi zilikotokea na hivyo kuongeza udhibiti, jambo ambalo halijafanyika mpaka sasa,” alisema.
Naye Muikolojia wa Hifadhi ya Taifa ya Ruaha, Paul Banga, amesema Mfumo- Hifadhi ya Taifa Ruaha ni sehemu ya mfumo ikolojia wa Rungwa-Kizigo –Muhesi ambao unachukua eneo la kilometa za mraba 45,000 na hifadhi yenyewe – ambayo ndiyo kubwa zaidi Tanzania na Afrika Mashariki kwa ujumla – ina kilometa za mraba 20,226.
Hifadhi hiyo ni ya pili kwa ukubwa barani Afrika baada ya Hifadhi ya Kafue ya Zambia. Ukubwa wa Hifadhi ya Ruaha ni zaidi ya 2/3 (theluthi mbili) kwa ukubwa wa nchi ya Ubelgiji ambayo eneo lake la mraba ni kilometa za mraba 30,528! Rwanda yenye eneo la ukubwa wa kilometa za maraba 26,338 na Burundi (27,834km2) zinaizidi kidogo hifadhi hii wakati ambapo ina karibu ukubwa sawa na Jimbo la New Jersey la Marekani, ambalo eneo lake ni kiliometa za mraba 22,608.
Banga amesema idadi ya tembo katika hifadhi hiyo inaendelea kupungua kila mwaka ambapo kwa takwimu za mwaka 2013, wanyama hao wamebaki takriban 25,000 kutoka idadi ya awali ya 31,000.
“Ingawa ndiyo hifadhi ya pili Afrika kwa kuwa na tembo wengi, lakini idadi inapungua sana na hali inatisha,” alisema.

No comments:

Post a Comment