Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Sunday, 5 October 2014

BOLINGO DANSI: ZAÏKO LANGA LANGA ILIYOZAA BENDI NYINGI CONGO

Unaweza kuwatambua hawa? Kushoto kabisa mwenye gitaa ni Felix Pepe Manuaku Waku, anafuatiwa na N'Yoka Longo Mvula na kulia ni bwana mdogo Jules Shungu Wembadio Pene Kikumba 'Papa Wemba'.
N'Yoka Longo (wa pili kushoto) na Pepe Manuaku Waku wakiwa na mchezaji mahiri wa AS Vita Club na timu ya taifa ya Zaire (Les Leopards) wakati huo Emmanuel Kakoko Etepe. Kushoto ni mwandishi akiwahoji.


Na Daniel Mbega
KAMA siyo kutoka ubavuni mwake, basi bendi nyingi, kama si zote zinazotamba nchini Congo (Jamhuri ya Kidemokrasia) kwa sasa, zimeasisiwa na wanamuziki ama waliotoka ndani ya bendi hii au katika bendi zilizoanzishwa na wakali waliopata kuipigia.
Naam. Hiyo ndiyo Zaiko Langa Langa, bendi kongwe nchini Congo kwa sasa ambayo bado inaendelea kudunda licha ya wimbi kubwa la kuhamwa na wanamuziki mahiri pamoja na ushindani uliopo hivi sasa.
Kimsingi twaweza kusema Zaiko Langa Langa ni chuo cha muziki katika Congo, kwa sababu bendi nyingi zinazotamba hivi sasa, ambazo zimeanzishwa kuanzia miaka ile ya 1970, ni matunda yake.
Ukitaja wanamuziki nyota wa nchini Congo kuanzia Papa Wemba, Bozi Boziana, Dindo Yogo, Evoloko Ley Ley ‘Joker’, Defao Matumona, Koffi Olomide, na wengineo wote lazima utapata chimbuko lao kutoka kwenye shina la Zaiko Langa Langa, ambayo mpaka sasa bado ingali inaongozwa na mkongwe N’Yoka Longo Mvula.

Bendi nyingi kama Isifi Lokole, Yoka Lokole, Viva la Musica, Langa Langa Stars, Zaiko Familia Dei, Choc Stars, Le Anti Choc, Le Grand Zaiko Wawa, Quartie Latin na nyinginezo nyingi zimetoka kwenye chimbuko la Zaiko ambayo sasa inajulikana kama Zaiko Langa Langa Nkolo Mboka, yaani ‘Wakuu wa Mji’.
Siyo ajabu kuona leo hii kuna idadi kubwa ya bendi zilizotokea ubavuni mwa Zaiko Langa Langa zikijiita ‘Ukoo wa Langa Langa’ (Clan Langa Langa). Bendi hizo ni Isifi Lokole iliyoanzishwa na Papa Wemba, Bozi Boziana, Evoloko Jocker na Mavuela Somo; Yoka Lokole iliyoanzishwa na Papa Wemba, Bozi Boziana na Mavuela Somo; Grand Zaïko Wa Wa iliyoanzishwa na Felix ‘Pepe’ Manuaku Waku aliyeungana na Shimita El Diego na Djo Poster; Viva La Musica iliyoanzishwa na Papa Wemba akiwa na Emeneya Mubiala na Theodore Djangi Dindo Yogo; Choc Stars iliyoanzishwa na Bozi Boziana, Tshimpaka Roxy na kuungana na akina Ben Nyamabo, Carlito Lassa, na Defao Matumona; L'Orchestre Anti-Choc iliyoanzishwa na Bozi Boziana akiungana na Deyesse Mukangi, Jolie Detta, Dodoli, Walingonda, Fifi Mofude, na wengineo; Langa Langa Stars iliyoanzishwa na Verckys Kiamuangana Mateta, Evoloko Jocker, Bozi Boziana, Tshimpaka Roxy, Emeneya Mabiala na Djo Mali; Zaiko Langa Langa Familia Dei ya Lengi Lenga, Ilo Pablo, Bimi Ombale, Beniko Popolipo, Petit Poisson, na Djimi Yaba; Zaïko Langa Langa Nkolo Mboka yenyewe chini ya N'Yoka Longo, Meridjo, Oncle Bapius, Zamuangana, Nono Atalaku, Mbuta Matima, Malage de Lugendo, Adamo Ekula, Baroza, na Shiro Shiro; Zaiko Universel ya Meridjo na Oncle Bapius Muaka; Langa Langa Rénové ya Evoloko Jocker; Basilique Loningisa iliyoanzishwa na Bimi Ombale; Etumba na Ngwaka Aye iliyokuwa chini ya Dindo Yogo; Les Quatros de Langa Langa ukiwa ni muungano wa Papa Wemba, Evoloko, Bozi Boziana na Gina Efonge; Les Stars de Zaiko (sasa inaitwa Zaikas Kolo Mboka) ikiwa chini ya Adamo Ekula, Petit Poisson, Tshanda na Papy Cocaine; na Clan Petrole ambapo nyimbo nyingi zimerekodiwa kupitia majina ya makundi tajwa hapo juu yanayowakilisha Ukoo wa Langa Langa.

KUZALIWA KWAKE
Watu wengi wamekuwa wakikosea historia ya Zaiko Langa Langa, kwamba ilianzishwa mwaka 1970. Hii siyo kweli kabisa.
Bendi hii mwaka huu imetimiza miaka 45 tangu kuanzishwa kwake. Ilianzishwa rasmi Desemba 24, 1969 jijini Kinshasa ikijulikana kama Orchestra Zaiko, ambayo ni kifupi cha maneno ya Kilingala ya Zaire ya bankoko (Zaire ya babu zetu). Neno Langa Langa lina utata kidogo: kwenye wavuti  ya bendi linamaanisha ‘utukufu’, lakini nilipata kuongea na N’Yoka Longo jijini Dar es Salaam wakati fulani akasema maana ya Langa Langa ni ‘Maji Maji’ (kwa maana nyingine walichukua jina la Mto Zaire). Hivyo kirefu chake ama tafsiri yake halisi ni Zaire ya mababu zetu ni ya maji maji!
Wakati huo muziki wa Congo ulitawaliwa zaidi na bendi za African Jazz ya Joseph Athanase Tchamala Kabaselleh ‘Le Grand Kalle’, African Fiesta ya Nicolas Kassanda wa Mikalay maarufu kama Dk. Nico, Tout Puisant Orchestre Kinnie Jazz (TP OK Jazz) ya L’Okanga La Ndju Pene Luambo Luanzo Makiadi Franco na hata African Fiesta National ya Pascal-Emmanuel Sinamoyi Tabu, almaarufu Tabu-Rey Rochereau, aliyoianzisha baada ya kutengana na Dk. Nico na mwaka 1970 akaibadili jina na kuiita Orchestre Afrisa Intanatinale.
Waanzilishi wa Zaiko Langa Langa walikuwa wanamuziki ambao baadhi walikuwa wanapigia bendi ndogo ndogo tu za mitaani na wengine walikuwa wanafunzi. Hawa si wengine bali ni mpiga conga maarufu D.V. Moanda, ambaye jina lake halisi ni Vital Moanda-di Veta (Alifariki mwaka 1984 jijini Kinshasa), Marcelin Delo, Henry Mongombe, Olemi Eshar-Eshar dem'belina, Andre Bita, Mavuela ‘Somo’ Simeon, Evoloko Lay Lay ‘Joker’, Teddy Sukami, Oncle Bapius aliyekuwa akipiga bass, Zamuangana Enock le meilleur, baba ya wapiga solo wa kizazi kipya Congo Felix Manuaku Waku (pia alijulikana zaidi kama Pépé Fely), na N'Yoka Longo Mvula, anayelikana kama Jossart, ama Vieux Mbombas, lakini maarufu zaidi kama N’Yoka Longo, ambaye asili yake ni Angola. Hawa walikuwa wakipiga soukous. Katika upande wa pop, muziki uliokuwa ukifungua pazia katika shoo zote za bendi hiyo, kulikuwa na Bimi Ombale, Mbuta Matima Zephirin na Mashakado Mbuta.
Moanda, Mongombe, Marcelin, Waku, N’Yoka Longo na Andre Bita walitokea kwenye bendi ya mtaani iliyojulikana kama Bel Guide National. Wote hawa walikuwa wanafunzi wakitokea katika familia za matajiri jijini Kinshasa.
Baadaye mwaka huo bendi hiyo ikamchukua bwana mdogo mwenye miaka 19, ambaye alikuwa anaimba kwaya kanisani. Huyu si mwingine bali ni Jules Shungu Wembadia Pene Kikumba, maarufu kama Papa Wemba.
Itaendelea...

No comments:

Post a Comment