Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Saturday 27 September 2014

KATIBA MPYA: WARIOBA SASA KUTUMIA NGUVU YA UMMA

Aliyekuwa Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba

NA ROMANA MALLYA
Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba, ametangaza rasmi kuungana na umma mpana, kupinga rasimu ya Katiba Mpya inayopendekezwa na Bunge Maalum la Katiba (BMK).
 
Hatua hiyo isiyotarajiwa, inafuatia Bunge Maalum la Katiba kukamilisha rasimu hiyo Jumatano iliyopita, ikitarajiwa kupigiwa kura mapema wiki ijayo.
 
Akizungumza kwenye adhimisho la miaka 19 tangu kuanzishwa kwa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), Aidha, Jaji Warioba, alisema Bunge hilo limeondoa mambo ya msingi  yaliyopendekezwa na wananchi yakiwa ni kiini cha kupatikana kwa Katiba Mpya.
 
Adhimisho hilo lilitumika pia kumkumbuka muasisi wa LHRC, marehemu Dk. Sengondo Mvungi, ambapo kitabu kinachoelezea maisha yake, kinachoitwa ‘Sengondo Mvungi, breathing the Constitution’ ikimaanisha, ‘Sengondo Mvungi, pumzi ya Katiba’, kilizinduliwa. 
 
Kwa mujibu wa Jaji Warioba, rasimu ya Katiba inayopendekezwa na BMK ni mfano wa ile iliyopo sasa ikiwa imewekewa viraka.
 
“Bunge limeacha mawazo ya wananchi na kuingia katika mikakati na misimamo yao, walioona rasimu yetu siyo, watatoka bungeni watakutana nasi mitaani, tutatetea maoni ya wananchi na wao watoke waje  kutetea mawazo yao,” alisema.
 
Jaji Warioba, alitoa mfano wa mambo ya msingi yaliyotokana na maoni ya wananchi, yakaondolewa na BMK kuwa ni  maadili, tunu za taifa, mgawanyiko wa madaraka, miiko ya uongozi na Muungano.
 
MAADILI 
Jaji Warioba, alisema wananchi waliotoa maoni walisisitiza masuala yanayohusu maadili kwa taifa yaingizwe kwenye Katiba Mpya, lakini hali hiyo haikukubalika kwa BMK.
 
Kadhalika, alisema  tunu za Taifa ambazo ni utu, uzalendo, uadilifu, umoja, uwazi, uwajibikaji na lugha ya taifa zilizopendekezwa na wananchi, rasimu hiyo ya bunge imezipunguza na kubaki nne tu.
 
Alizitaja zilizowasilishwa na rasimu ya bunge kuwa ni lugha ya Kiswahili, muungano, utu na udugu na amani na utulivu.
 
“Tunu za taifa zilizopendekezwa na wananchi, na siyo vyama vya siasa wala tume zimeondolewa, Bunge linasema eti ni hiyo ni misingi ya utawala,” alisema.
Aliongeza, “mimi siwaelewi kabisa kusema hizo siyo tunu za kitaifa, siwaelewi kabisa,” alisema.
 
Alisema, sura ya tatu ya rasimu ya Katiba iliyopendekezwa na Tume yake, ilihusu miiko ya uongozi.
 
Jaji Warioba, alisema sura hiyo ilieleza kuwa kiongozi wa umma hapaswi kuwa na akaunti ya benki nje ya nchi na kutangaza mali na madeni yake.
Pia, ilieleza kiongozi huyo anapaswa kuwasilisha kwenye ofisi za umma zawadi anazopewa, kutotumia mali za umma kwa mambo binafsi, kukomesha rushwa na ufisadi.
 
Alisema, miiko ya uongozi ilifanikisha kukabiliana na kadhia kama Ufilipino, Kenya, Namibia na Afrika Kusini.
 
“Tunajua ufisadi na rushwa ndiyo chanzo cha hayo yote, watu wanapewa zawadi wanasaini mikataba ya hovyo, lakini tunapokuwa na miiko yeyote atakayebainika amepokea zawadi au ana akaunti nje ya nchi  atawajibishwa… kwenye haya wameniita mimi ni shida,” alisema.
 
MADARAKA YA NCHI
Jaji Warioba, alisema wananchi walipendekeza kumuondoa Mwakilishi asiyewajibika kwao, kuwapo ukomo wa ubunge  na muundo wa serikali tatu, lakini vimeondolewa na BMK.
“Wananchi walisema baadhi ya wabunge ni watalii kwenye majimbo yao, wakataka wapate mamlaka ya kuwaondoa, cha ajabu wenyewe wamejipa mamlaka ya kumfukuza mbunge asiyeshiriki kikao kimoja, na vyama vya siasa vimejipa madaraka ya kuwaondoa wabunge wao, kwa nini mwananchi anyimwe hili,” alihoji.
 
MGAWANYO WA MADARAKA
Alisema, Tume ilipendekeza kuwa kutokana na mwingiliano uliopo kati ya Bunge na Serikali, ipo haja ya kuwapo mgawanyo wa madaraka kwenye Katiba Mpya.
 
Alitoa mfano namna ushawishi wa Rais ulivyofanikishwa kurejeshwa bungeni kwa Sheria ya Mabadiliko ya Katiba baada ya kukutana na viongozi wa upinzani.
Aliongeza, “hata sasa, wakati rasimu yao inasema Katiba itaitwa ya mwaka 2014, Rais anasema haiwezi kupatikana mwaka huu hadi 2016. Huu ni muingiliano wa madaraka, ndio maana tume tuliona kila mhimili ujitegemee.” 
 
MUUNGANO
Jaji Warioba, alisema muundo wa serikali tatu ulipendekezwa na wananchi na kwamba ndani ya Tume, kila mjumbe alikuwa na maoni yake.
 
“Mfano Baregu (Profesa Mwesiga Baregu) alitaka serikali mbili, Joseph Butiku alitaka moja, Awadhi Said alikuwa muumini wa Muungano wa mkataba, mimi ni serikali mbili kwenda moja,” alisema.
 
 
AZIPONDA KURA ZA MTANDAO
Jaji Warioba, alisema pamoja na kasoro iliyopo kupigia kura ibara badala ya sura za rasimu ya Katiba inayopendekezwa, alipinga pia utaratibu wa kuruhusu wajumbe wasiokuwapo bungeni kupiga kura.
 
“Kusaka kura kwa mtandao hakuwezi kutuletea Katiba ya maridhiano na mimi nimeanza kukata  tamaa, ninachoona mchakato huu utarudiwa mara baada ya kupatikana kwa Rais mpya,” alisema na kuongeza:
 
LHRC BILA DK. MVUNGI
Mkurugenzi Mtendaji wa LHRC, Dk. Hellen Kijo-Bisimba, alisema endapo angekuwapo Dk. Mvungi, angeshangaa kuona maslahi ya taifa yanatupwa na yale ya itikadi yanapewa kipaumbele.
Pia, alisema angeshangaa kuondolewa kwa vipengele kama kuwajibishwa wabunge, ukomo wao  na jinsi mchakato ulivyokiuka maoni ya wananchi.
 
Mjane wa Dk. Mvungi, Anna Mvungi, alisema baada ya kuteuliwa katika tume, moja ya kauli zake (Dk. Mvungi) ilikuwa ni ‘nimetimiza nia yangu’.
 
Mwenyekiti wa ukoo wa Mvungi, Adrian Mvungi, aliiasa LHRC kuondokana na woga na kuendeleza mapambano ya kutetea haki za watu.
 
Mmoja wa wahariri wa kitabu hicho, Profesa Chris Maina, alisema Dk. Mvungi alikuwa ni Profesa kutokana na makala 20 alizoziandika kwa wananchi na shauri kuhusu wanyonge na matatizo wanayoyapata. Kuhusu Tume ya Warioba, alisema pamoja na `madongo’ wanayoyapa wamekuwa imara kutokana na yote waliyosimamia waliyaamini.
 
“Jinsi tunavyopata vioja vya Dodoma tunazidi kuvumbua ubora wa tume hii, wananchi wanajua mchele na pumba historia haifutwi na FFU,” alisema.
 
Mwenyekiti wa chama cha NCCR-Mageuzi James Mbatia, alisema kuna mazungumzo yanayoendelea yakivihusisha vyama vya siasa hususani vyenye wabunge, ili kuinusuru Katiba Mpya.
 
“Yapo mazungumzo yanayoendelea yanahusisha vyama vyote vyenye wawakilishi bungeni CCM, Chadema na NCCR-Mageuzi, tunataka Tanzania isifike mahali tukamwaga damu kwa sababu ya ubinafsi wa watu wachache,” alisema.
 
KITABU CHA DK. MVUNGI
Katika kitabu hicho zipo makala mbalimbali za wanataaluma, familia na wanafunzi na walimu wake, wananchi na wanahabari ambazo zimemuelezea jinsi alivyofanya kazi za utetezi wa wanyonge.
 
Kitabu hicho ambacho kimepambwa na picha 157 kina sura kumi ambazo waandishi wake wametumia lugha mbalimbali kufikisha ujumbe ambazo ni Kiswahili, Kingereza, Kijerumani na Kipare kilichokuwa lugha ya Dk. Mvungi.
CHANZO: NIPASHE

3 comments: