Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Mahusiano)
Moshi/Dar. Mawaziri Stephen Wassira na Mwigulu
Nchemba wamesema kuwa japo Bunge Maalumu la Katiba litaendelea na vikao
vyake kuanzia kesho mjini Dodoma, halitakuwa na uhalali wa kisiasa.
“Tunakwenda bungeni kuendelea na vikao kwa sababu
hatuvunji sheria. Kumbukeni hata walipotoka (Ukawa) wakati ule
tuliendelea na vikao kwa sababu akidi inaruhusu, japo hatutakuwa na
uhalali wa kisiasa lakini kisheria tuna uhalali,” alisema Wasira ambaye
ni Waziri wa Nchi (Ofisi ya Rais, Uratibu na Uhusiano).
Hoja hiyo ilisisitizwa na Nchemba ambaye ni Naibu
Waziri wa Fedha kuwa vikao hivyo havitakuwa na uhalali wa kisiasa japo
kisheria vina uhalali.
“Unajua kilichosababisha mkwamo huu ni kila kundi
kushikilia upande wake, kama kila kundi lingeweka masilahi ya Taifa
tusingefika huko. Tunakwenda bungeni, ingawa hakutakuwa na uhalali wa
kisiasa lakini tutaendelea kujadili mambo ya kitaifa,” alisema Mwigulu.
Viongozi hao walisema hayo baada ya mdahalo wa
Katiba uliofanyika Dar es Salam jana na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri
Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi akisema wanakwenda bungeni
kuendelea na mijadala japo katiba haitakuwa na afya... “Nawaomba Ukawa
warejee bungeni, ikishindikana sisi tutakwenda, tutajadiliana,
tutawaletea Katiba bora ila haitakuwa na afya bila Ukawa.”
Wengi waendelea kupinga Bunge
Mbali na mawaziri hao, idadi ya wajumbe wa Bunge
hilo wanaopinga vikao hivyo kuendelea bila kushirikisha wenzao wa Umoja
wa Bunge la Wananchi (Ukawa) inazidi kuongezeka.
Maoni ya wajumbe hao, baadhi yao wakiwa wabunge wa
Bunge la Jamhuri ya Muungano kutoka CCM, yanatokana na Bunge la Katiba
kugubikwa na giza nene baada ya Ukawa, kusisitiza kuwa hawatashiriki
vikao hivyo.
Maoni ya wajumbe hao, baadhi yao wakiwa wabunge wa
Bunge la Jamhuri ya Muungano kutoka CCM, yanatokana na Bunge la Katiba
kugubikwa na giza nene baada ya Ukawa, kusisitiza kuwa hawatashiriki
vikao hivyo.
Mbunge wa Ludewa (CCM), Deo Filikunjombe alisema
jana kuwa haungi mkono mpango wa wabunge wenzake wa CCM kuendelea na
Bunge la Katiba bila maridhiano.
“Pengine niwakumbushe wabunge wenzangu wa CCM kuwa
kinachoandaliwa kwenye Bunge la Katiba ni Katiba ya Watanzania wote na
si Katiba ya CCM. Hatua tuliyofikia siiungi mkono, kitendo cha wabunge
wenzangu wa CCM kuendelea na mchakato wa Katiba Mpya kwa sababu suala la
Katiba halina mshindi ni jambo la maridhiano.
“Kitendo cha sisi wabunge wa CCM kuendelea na
mchakato wa Katiba Mpya ni matumizi mabaya ya wingi wetu mle bungeni. Ni
kweli CCM ina wabunge wengi na ni kweli kwenye demokrasia wengi wape,
lakini pia demokrasia pevu na yenye tija ni ile inayoheshimu na
kuyafanyia kazi maoni ya wachache.”
Isome zaidi: http://www.mwananchi.co.tz/Katiba/Ukawa-wawatia-kiwewe-Wassira--Mwigulu--Lukuvi/-/1625946/2407610/-/4030emz/-/index.html
Isome zaidi: http://www.mwananchi.co.tz/Katiba/Ukawa-wawatia-kiwewe-Wassira--Mwigulu--Lukuvi/-/1625946/2407610/-/4030emz/-/index.html
No comments:
Post a Comment