Twitter Buzz

....

....

...

...

IMETOSHA!

IMETOSHA!

Featured post

KIJANA GOZBERT BWELE ALIVYOMPAGAWISHA MAKAMU WA RAIS WA HISPANIA MJINI NANSIO

Makamu wa rais mstaafu wa Hispania, Mama Maria Teresa Fernandes De la Vega alishindwa kujizuia na kwenda kumtuza mtoto Gozbert ...

Friday 25 September 2015

MALENGO ENDELEVU (SDG): TUANZIE TULIPOISHIA MALENGO YA MILENIA

Umaskini wa kutisha umepungua kiasi kwani jamii nyingi kama Wamasai nao wanashiriki kilimo. (Picha hii ni kwa hisani ya Umaskini Tanzania Blog).
Watoto wengi wameandikishwa, lakini changamoto ya vyumba vya madarasa, madawati, vitabu na nyumba za walimu inakwamisha ubora wa elimu. 
Afya ya uzazi ina changamoto kubwa, akinamama wanalazimika kulala chini ama kuchangia kitanda kimoja wagonjwa watatu. 
Huduma ya maji nayo bado ina changamoto. 

Na Daniel Mbega
KUANZIA leo Septemba 25 hadi 27, wakuu wa nchi 193 wanachama wa Umoja wa Mataifa wanakutana jijini New York, Marekani katika mkutano muhimu uliobatizwa jina la Agenda kwa Maendeleo Endelevu kuelekea mwaka 2030 (2030 Agenda for Sustainable Development).
Katika mkutano huo, nchi wanachama wa watapitisha Agenda kwa Maendeleo Endelevu 2030, ambayo inahusisha jumla ya Malengo 17 ya Maendeleo Endelevu (SDG) ambayo ni kukomesha umaskini, kuhamasisha usawa na kupinga uonevu, na kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi kufikia mwaka 2030.
Malengo haya Endelevu, ambayo pia yanafahamika kama Malengo ya Ulimwengu, yamejikita katika Malengo nane ya Maendeleo Milenia (MDG) katika kupambana na umaskini ambayo ulimwengu uliazimia kutafikia kwa mwaka 2015.
Malengo ya Milenia ambayo yalipitishwa Septemba 2000, yalilenga katika kupunguza umaskini, njaa, maradhi, uwiano wa kijinsia, na upatikanaji wa maji safi na salama.
Mafanikio makubwa yamepatikana kupitia MDG, na kuonyesha umuhimu wa kunganisha agenda hizo baina ya malengo na matarajio, na ingawa yamesaidia kuwainua mamilioni ya wananchi kote ulimwenguni kutoka kwenye lindi la umaskini na kuwapatia unafuu, lakini bado kuna umuhimu wa kwenda mbele zaidi.
Tanzania inaelezwa kwamba ni moja ya nchi zilizofanya vizuri katika Malengo ya Maendeleo ya Milenia hata kabla ya mwaka 2015 ingawa bado inakabiliwa na changamoto katika baadhi ya maeneo kupitia kwenye program mbalimbali kama MKUKUTA, MKURABITA, uwezeshaji wa mikopo kwenye SACCOS, mipango ya elimu kama MMEM, MMES na MEMKWA, na huduma za kijamii kama Bima ya Afya, Sera ya Hifadhi Jamii, Miradi ya maji kwa kuzingatia pia Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2000-2025.
Katika kupunguza umaskini, Tanzania imefanikiwa kwa takriban asilimia 19.5 na katika kupunguza idadi ya watoto chini ya miaka mitano wenye uzito mdogo imefanikiwa kwa asilimia 14.4 tu, hivyo juhudi zaidi zinatakiwa wakati wakuu watakaporidhia malengo mapya.
Baadhi ya malengo ambayo Tanzania imefanya vizuri ni pamoja na lengo   namba mbili linalohusu fursa ya elimu ya msingi kwa watoto wote, ambapo Ripoti ya Malengo ya Milenia inaeleza kwamba, lengo hilo limefanikiwa kutoka asilimia 54.2 mwaka 1990 hadi 89.71 mwaka 2013.
Lengo la tatu ni kuondoa utofauti wa jinsia katika elimu ya msingi na sekondari ifikapo 2025 na kwa ngazi zote za elimu ifikapo 2015, nalo limefanikiwa kwa elimu ya msingi kufikia asilimia 98 mwaka 2010 na asilimia 102 mwaka 2013 na elimu ya sekondari asilimia 105 mwaka 2013.
Wanawake wameendelea kupata fursa sawa za kijinsia na kuwezeshwa, ambapo kuna ongezeko la wanawake katika vyombo vya utoaji maamuzi kama vile Bunge na Baraza la Wawakilishi, kwani kwa mara ya kwanza Bunge la 10 limeongozwa na mwanamke – kwanza akiwa Naibu Spika kwa miaka mitano na baadaye akiwa Spika kamili, na sasa kama Chama cha Mapinduzi kitafanikiwa kuingia madarakani, Tanzania itaweka rekodi mpya kwa kuwa na Makamu wa Rais mwanamke kwa mara ya kwanza.
Kumekuwa na mafanikio ya kuridhisha katika upunguzaji wa vifo vya watoto wachanga chini ya miaka mitano kwa pande zote mbili za Muungano, ingawa bado watoto wanaendelea kupoteza maisha kwa maradhi yanazulikia kama vile malaria na kuharisha. 
Kwa upane mwingine, lengo namba tano kuhusu upunguzaji wa vifo vya wanawake wajawazito bado lina changamoto nyingi zinazochangiwa na uhaba wa  wataalamu na ukosefu wa wa huduma za upasuaji wa dharura, japokuwa serikali imejitahidi kulifanyia kazi kwa kuviwezesha vituo vya afya kuvipatia vifaa na wataalam.
Kuhusu lengo la sita linalohusu huduma za afya, bado kuna changamoto nyingi hasa katika kukabiliana na maambukizi ya virusi vinavyosambabisha ugonjwa wa ukimwi, malaria na kifua kikuu, magonjwa ambayo yanagusa sehemu kubwa ya jamii, mafanikio hapa ni asilimia 6.9 tu. 
Malengo haya mapya yamejikita katika kutokomeza umaskini katika namna zake zote kila mahali duniani licha ya idadi ya watu wanaoishi katika umaskini wa kutupwa kupungua kwa zaidi ya nusu – kutoka watu 1.9 bilioni mwaka 1990 hadi watu 836 milioni mwaka 2015, kwani wapo wengi ambao bado wanaendelea kuhangaika kupata huduma za msingi za kibinadamu.
Ulimwenguni kote, zaidi ya watu milioni 800 wanaishi kwa kipato cha chini ya Dola 1.25 kwa siku; wengi wanakosa chakula bora, mai safi na salama. Kukua kwa uchumi kwa kasi katika nchi kama China na India kumewatoa wengi kwenye umaskini, lakini maendeleo pia yamekuwa hayana uwiano sawa. Wanawake wana uwezekano wa kuishi kwenye umaskini mkubwa kuliko wanaume kwa sababu ya kukosa fursa ya kazi yenye mshahara, elimu na rasilimali.
Mafanikio pia yamekuwa madogo katika baadhi ya maeneo, kama Asia Kusini na nchi za Kusini mwa Jangwa la Sahara, ambayo yana asilimia 80 ya idadi ya watu wote ulimwenguni wanaoishi katika umaskini mkubwa. Idadi hii inategemewa kuongezeka kutokana na mabadiliko ya hali ya hewa, migogoro na uhaba wa chakula.
Kutokomeza njaa, kufanikiwa katika usalama wa chakula na kuboresha lishe na kukuza kilimo endelevu kutasaidia kukuza uchumi na kuongeza tija katika mazao ya kilimo kama ilivyoonekana katika miongo miwili iliyopita. Nchi nyingi zinazoendelea ambazo zilikuwa zinakabiliwa na majanga ya njaa sasa zinaweza kujivunia usalama wa chakula.
Hata hivyo, zaidi ya watoto milioni 90 walio chini ya miaka mitano bado wako katika hatari ya uzito mdogo na mtu mmoja kati ya wanne anashinda na kulala na njaa barani Afrika.
Malengo Endelevu ya Maendeleo yamejikita katika kuhakikisha aina zote za njaa zinakomeshwa ifikapo mwaka 2030 na kuhakikisha watu wote hasa watoto wakipata mlo stahili.
Kwa maana nyingine, kilimo kinapaswa kuimarishwa na serikali ijayo ya Tanzania ili kiweze kukidhi matakwa ya malengo haya.
Malengo mapya pia yameikita kuhakikisha jamii inakuwa na afya bora kwa kuzingatia kwamba Malengo ya Milenia yamesaidia kupunguza vifo vya watoto, kuboresha afya ya uzazi na mapambano dhidi ya magonjwa ya Ukimwi, malaria na kifua kikuu kwa asilimia 30 tangu mwaka 2000.
Baada ya kufanikiwa kuandikisha watoto wengi shuleni, sasa ni wakati wa kujikita katika utoaji wa elimu bora. Hiyo ndiyo njia pekee ya kuwapatia unafuu wa maisha wananchi kimaendeleo badala ya kuwa na bora elimu ambapo watoto wengine wanaingia sekondari wakiwa hawajui kusoma, kuandika wala kuhesabu.
Lakini pia serikali kupitia malengo hayo mapya, zitajikita katika kuwawezesha wanawake na kuhamasisha uwiano wa kijinsia ni muhimu kwa kuchochea maendeleo, hivyo serikali zote safari hii zitajikita katika kuhakikisha zinakomesha aina zote za ubaguzi dhidi ya wanawake. Kwa sasa, inaelezwa kwamba wanawake wana asilimia 41 katika ajira za mshahara kulinganisha na asilimia 35 mwaka 1990. Bado kuna changamoto katika utumikishwaji wa wanawake katika maeneo mengi.
Uhaba wa maji unawaathiri asilimia 40 ya watu ulimwenguni kote, idadi kubwa ambayo inaweza kuongezeka kutokana na ongezeko la joto duniani na mabadiliko ya tabianchi. Japokuwa watu bilioni 2.1 wamepata maji tangu mwaka 1990, lakini changamoto ya upatikanaji wake bado ni kubwa katika maeneo mengi ulimwenguni.
Mnamo mwaka 2011, nchi 41 zilikubwa na uhaba mkubwa wa maji; kumi kati ya hizo zinakaribia kukausha hata vyanzo vyake na sasa zinategemea vyanzo visivyo rasmi. Serikali zote ulimwenguni sasa zinatakiwa kubuni mbinu ambazo zitasaidia upatikanaji wa maji safi na salama.
Suala na nishati limepewa kipaumbele katika malengo mapya ya maendeleo ambapo serikali zote zinapaswa kuhakikisha nishati ya gharama nafuu, ya uhakika, endelevu na ya kisasa inapatikana kwa wote. Kati ya mwaka 1990 na 2010, idadi ya watu wanaotumia umeme meongezeka hadi kufikia bilioni 1.7, lakini kwa kadiri idadi ya watu inavyoongezeka duniani, mahitaji nayo yatakuwa makubwa.
Tanzania bado inaendelea kuhangaikia kuhakikisha nishati ya umeme wa uhakika inapatikana na kuondokana na mgawo ambao umeathiri uchumi kwa kiasi kikubwa. Hii ndiyo sababu imetoa kipaumbele katika uzalishaji wa umeme wa gesi, mitambo ambayo tayari imekwishaunganishwa kwenye gridi ya taifa.
Kwa ujumla, malengo yote haya 17 yakipewa kipaumbele katika serikali ijayo hapa Tanzania, kuna uwezekano mkubwa wa kupiga hatua kutoka pale yalipoishia Malengo ya Milenia na kuleta maendeleo zaidi kwa jamii ya Watanzania kwa kuzingatia pia Dira ya Taifa ya Maendeleo ya miaka 25 (kutoka mwaka 2000-2025) pamoja na mikakati mingine ya kupambana na umaskini kama MKUKUTA II na MKURABITA.

Muhtasari:

Malengo ya Maendeleo ya Milenia (2000-2015)
Mwezi Septemba 2000, wakuu wa nchi wanachama wa Umoja wa Mataifa walikutana jijini New York na kupitisha Azimio la Umoja wa Mataifa la Milenia kwa kupunguza umaskini uliokithiri baada ya miaka 15.
Malengo nane yalipitishwa, ambayo ni:
1. Kupunguza umaskini uliokithiri na njaa
2. Kuhakikisha upatikanaji wa elimu ya msingi
3. Kuhamasisha usawa wa jinsia na kuwawezesha wanawake
4. Kupunguza vifo vya watoto
5. Kuboresha afya ya uzazi
6. Kupambana na Ukimwi, malaria na maradhi mengine
7. Kutunza mazingira
8. Kuendeleza ushirikiano wa kidunia kwa maendeleo

Malengo Endelevu ya Maendeleo (2015-2030)
Hii ndiyo agenda mpya ya maendeleo ya ulimwengu kwa sasa na wakuu wa mataifa zaidi ya 160 wanakutana leo hii kujadili, kupitisha na hatimaye kuridhia malengo hayo.
Paul Ladd, Mkurugenzi wa Timu ya UNDP kuelekea kwenye Agenda ya Maendeleo 2015, anasema Agenda hiyo inahusisha Malengo mapya 17 ya Maendeleo Endelevu, ambayo ndiyo yatakuwa mwongozo kwa sera na ufadhili kwa miaka mingine 15 ijayo, yakianza na ahadi ya kihistoria ya kutokomeza umaskini kila mahali duniani.
Malengo haya mapya yanapaswa kumalizika kazi ya Malengo ya Milenia ambayo yameleta mafanikio katika mataifa mengi duniani, Tanzania ikiwa miongoni mwao.
Malengo haya mapya ya maendeleo hayajawekwa kwa mataifa maskini na yanayoendelea tu, bali mataifa yote ulimwenguni, kuhamasisha amani na kushirikisha jamii, kutengeneza ajira nzuri na kupambana na mabadiliko ya tabia nchi.
Malengo hayo mapya ni:
1: Hakuna umaskini
2: Kutokomeza njaa
3: Afya bora na ustawi
4: Elimu bora
5: Uwiano wa kijinsia
6: Maji safi na salama
7: Nishati rahisi na safi
8: Kazi nzuri na ukuaji wauchumi
9: Viwanda, ubunifu, miundombinu
10: Kupunguza uwiano usio sawa
11: Miji na jamii endelevu
12: Uwajibikaji
13: Hatua za kutunza mazingira
14: Maisha chini ya maji
15: Maisha katika ardhi
16: Amani, haki na taasisi imara
17: Ushirikiano katika malengo

0656-331974 

No comments:

Post a Comment